Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 5

Umuhimu wa Mwongozo wa Watu Wazima

Umuhimu wa Mwongozo wa Watu Wazima

MWONGOZO HUO UNAHUSISHA NINI?

Watoto wanahitaji ushauri na mwongozo kutoka kwa watu wazima. Ukiwa mzazi, una nafasi kubwa ya kutimiza daraka hilo, na kimsingi, hilo ni jukumu lako. Hata hivyo, watu wengine wenye umri mkubwa wanaweza pia kuwashauri na kuwasaidia watoto wako.

KWA NINI MWONGOZO WA WATU WAZIMA NI MUHIMU?

Katika nchi nyingi, vijana hushirikiana mara chache sana na watu wenye umri mkubwa. Hebu fikiria:

  • Watoto hutumia muda mwingi shuleni, mahali ambapo walimu na watu wengine wenye umri mkubwa ni wachache ukilinganisha na idadi ya wanafunzi.

  • Wakitoka shuleni, watoto wengi hukaa wenyewe tu nyumbani kwa sababu wazazi wao wapo kazini.

  • Utafiti fulani ulionyesha kwamba, nchini Marekani, watoto walio na umri kati ya miaka 8 hadi 12 hutumia kwa wastani saa sita kila siku wakicheza michezo ya video, wakitazama televisheni, na kusikiliza muziki. *

Kitabu Hold On to Your Kids kinasema: “Siku hizi vijana hawaigi au kutafuta ushauri na mwongozo kutoka kwa mama, baba, walimu, au watu wengine wenye umri mkubwa, bali kwa . . . vijana wenzao.”

JINSI YA KUTOA MWONGOZO

Tenga wakati wa kuwa na mtoto wako

KANUNI YA BIBLIA: “Mzoeze mtoto njia anayopaswa kuifuata; hata atakapozeeka hataiacha.”​—Methali 22:6, maelezo ya chini.

Kwa kawaida, watoto hutazamia kupata mwongozo kutoka kwa wazazi wao. Isitoshe, wataalamu wanasema kwamba hata watoto wanapoanza kubalehe, bado wao huthamini ushauri wa wazazi wao kuliko wa vijana wenzao. Dakt. Laurence Steinberg aliandika hivi kwenye kitabu You and Your Adolescent: “Vijana walio katika kipindi cha kubalehe hadi wale wanaoanza kuwa watu wazima bado huwa na mwelekeo mkubwa wa kufuata mtazamo na tabia za wazazi wao.” Anaongezea kusema: “Vijana wanaobalehe hupenda kujua unachofikiria na wao husikiliza unachosema, hata ikiwa nyakati nyingine hawakwambii au kukubaliana na maoni yako.”

Mtoto wako ana tamaa ya kupata mwongozo wako, hivyo tumia fursa hiyo vizuri. Tenga wakati wa kuwa naye na umweleze maoni yako, kanuni unazofuata, na mambo uliyopitia maishani.

Mtafutie mtu anayeweza kuwa akimshauri.

KANUNI YA BIBLIA: “Anayetembea na wenye hekima atakuwa na hekima.”​—Methali 13:20.

Je, kuna mtu yeyote mwenye umri mkubwa ambaye ungependa mtoto wako aige mfano wake? Je, unaweza kufanya mipango ili mtu huyo na mtoto wako wapate nafasi za kuwa pamoja? Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba utatelekeza jukumu lako ukiwa mzazi. Lakini mtoto wako atanufaika kutokana na mchango wa mtu mwingine mwenye umri mkubwa pamoja na mambo ambayo unamfundisha. Timotheo, anayetajwa kwenye Biblia, alinufaika sana kwa kushirikiana na mtume Paulo hata baada ya kuwa mtu mzima, na Paulo alinufaika kwa kushirikiana na Timotheo.​—Wafilipi 2:20, 22.

Katika miaka 100 iliyopita, familia nyingi zimetawanyika; bibi na babu, wajomba, shangazi, na washiriki wengine wa familia wanaweza kuwa wanaishi nchi tofauti-tofauti. Ikiwa hali ya familia yenu iko hivyo, jitahidi kuandaa fursa za mtoto wako kushirikiana na watu wengine wenye umri mkubwa walio na sifa ambazo ungependa asitawishe.

^ fu. 9 Utafiti huo ulionyesha kwamba, vijana wenye umri wa kati ya miaka 13 hadi 19 hutumia kwa wastani karibu saa tisa kila siku wakicheza michezo ya video, wakitazama televisheni, na kusikiliza muziki. Muda unaotajwa kwenye takwimu hizi mbili, hautii ndani muda wanaotumia kwenye mtandao wakiwa shuleni au wakifanya kazi za shule.