Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAONI YA BIBLIA | VITA

Vita

Vita

Nyakati za kale, Waisraeli walienda vitani kwa jina la Mungu wao, Yehova. Je, hilo linamaanisha kwamba Mungu anaunga mkono vita vinavyopiganwa leo?

Kwa nini Waisraeli wa kale walienda vitani?

WATU HUSEMA NINI?

 

Waisraeli waliabudu mungu wa vita mwenye kiu ya damu.

BIBLIA INASEMA NINI?

 

Mataifa ambayo Waisraeli walipigana nayo yalikuwa yamejaa jeuri na mazoea machafu kama vile kufanya ngono na wanyama, ngono kati ya watu wa ukoo, na kudhabihu watoto. Baada ya kuwapa mamia ya miaka ili wabadili njia zao, hatimaye Mungu alisema hivi: “Kwa mambo yote hayo mataifa ninayoyafukuza kutoka mbele yenu yamejifanya yenyewe kuwa si safi.”—Mambo ya Walawi 18:21-25; Yeremia 7:31.

“Yehova anayafukuzia mbali mataifa haya kutoka mbele yako kwa sababu ya uovu wao.”—Kumbukumbu la Torati 9:5.

Je, Mungu anaunga mkono upande wowote katika vita vinavyopiganwa leo?

HUENDA UMEJIONEA HILI

 

Katika vita vingi, viongozi wa kidini wa pande zote zinazopigana hudai kwamba Mungu yuko upande wao. Kitabu The Causes of War kinasema: “Dini zimeshiriki katika vita vyote ambavyo vimepiganwa.”

BIBLIA INASEMA NINI?

 

Wakristo hawapaswi kwenda kupigana na adui zao. Mtume Paulo aliwaandikia Wakristo wenzake hivi: “Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote. . . . Msijilipizie kisasi wenyewe.”—Waroma 12:18, 19.

Yesu hakuwaagiza wafuasi wake waende vitani, badala yake aliwaambia hivi: “Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi; ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni.” (Mathayo 5:44, 45) Wakristo hawapaswi kuunga mkono upande wowote hata ikiwa nchi ambayo wanaishi inaenda vitani, kwa sababu wao “si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19) Ikiwa Mungu anatazamia waabudu wake katika mataifa yote wawapende adui zao na wasiwe sehemu ya ulimwengu, basi anawezaje kuunga mkono upande fulani katika vita vinavyopiganwa leo?

“Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, watumishi wangu wangepigana ili nisitiwe mikononi mwa Wayahudi. Lakini, kama ilivyo, ufalme wangu hautoki katika chanzo hiki.”—Yohana 18:36.

Je, vita vitakwisha?

WATU HUSEMA NINI?

 

Hatuwezi kuepuka vita. Kitabu War and Power in the 21st Century kinasema: “Vita vitaendelea kuwepo. Katika karne hii hatutarajii kuwe na amani ya kudumu ya ulimwenguni pote.”

BIBLIA INASEMA NINI?

 

Vita vitaisha wakati ambapo hakutakuwa na yeyote anayetaka kupigana. Ili kutimiza hilo, Ufalme wa Mungu, ambao ni serikali halisi inayotawala kutoka mbinguni, utaangamiza silaha zote zilizo duniani na kuwafundisha wanadamu kufuatia amani. Biblia inatuhakikishia kwamba Mungu “[atanyoosha] mambo kuhusu mataifa yenye nguvu yaliyo mbali. Nao watafua panga zao ziwe majembe na mikuki yao iwe miundu. Hawatainua upanga, taifa juu ya taifa, wala hawatajifunza vita tena.”—Mika 4:3.

Biblia inafundisha kwamba Ufalme wa Mungu utakapokuwa ukitawala, hakutakuwa na serikali zinazopigania masilahi yao binafsi, sera zenye kukandamiza zinazochochea wananchi wapinge mamlaka, au ubaguzi unaochochea ukabila. Matokeo ni kwamba, vita vitakwisha. Mungu anaahidi hivi: “Hawatasababisha madhara yoyote wala kusababisha uharibifu wowote . . . kwa maana dunia hakika itajawa na kumjua Yehova kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:9.

“Anakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia. Upinde anauvunja na kuukata mkuki vipande-vipande; magari ya kukokotwa anayateketeza motoni.”—Zaburi 46:9.