Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Nimemruhusu Yehova Aongoze Njia Yangu

Nimemruhusu Yehova Aongoze Njia Yangu

NILIPOKUWA tineja, nilijichagulia njia yangu mwenyewe, kazi niliyoipenda sana. Lakini Yehova alinialika nifuate njia tofauti, ni kana kwamba aliniambia: “Nitakupa ufahamu na kukufundisha njia unayopaswa kufuata.” (Zab. 32:8) Kumruhusu Yehova aongoze njia yangu kumenipatia fursa na baraka nyingi za kiroho, kutia ndani kutumikia miaka 52 barani Afrika.

KUTOKA KWENYE NCHI NYEUSI HADI KWENYE NCHI YENYE UCHANGAMFU YA AFRIKA

Nilizaliwa 1935 huko Darlaston, sehemu ya Nchi Nyeusi (Black Country), yaani, eneo la Uingereza lililopata jina kutokana na moshi mweusi uliojaa hewani, uliotoka kwenye karakana na viwanda mbalimbali. Nilipokuwa na umri wa miaka minne hivi, wazazi wangu walianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Katika miaka yangu ya mapema ya utineja, nilisadiki kwamba hii ndiyo kweli na nikabatizwa mwaka wa 1952, nikiwa na umri wa miaka 16.

Karibu na muda huo, nilianza kujifunza kazi katika kiwanda kikubwa kilichotengeneza vifaa na sehemu za magari. Nilianza kuzoezwa kuwa karani wa kampuni, kazi ambayo niliipenda sana.

Nilikabili uamuzi muhimu mwangalizi anayesafiri aliponiomba nianze kuongoza Funzo la Kitabu la Kutaniko katikati ya juma kwenye kutaniko la nyumbani kwetu la Willenhall. Lakini huo ulikuwa uamuzi mgumu kwangu. Wakati huo, nilikuwa nikishirikiana na makutaniko mawili. Katikati ya juma, nilikuwa nikihudhuria mikutano katika kutaniko lililokuwa karibu na sehemu niliyofanya kazi huko Bromsgrove, kilomita 32 hivi kutoka nyumbani. Na mwisho juma, nilipoenda nyumbani kwa wazazi wangu, nilihudhuria mikutano kwenye kutaniko la Willenhall.

Kwa kuwa nilitamani kuunga mkono tengenezo la Yehova, nilikubali mwaliko wa mwangalizi anayesafiri, hata ingawa ilimaanisha kuacha kazi niliyoipenda sana. Kumruhusu Yehova aongoze njia yangu wakati huo, kulinifungulia njia ambayo imenisaidia kuishi maisha ambayo sijutii kamwe.

Nilipokuwa nikihudhuria kutaniko la Bromsgrove, nilikutana na dada mrembo aliyependa mambo ya kiroho, anayeitwa Anne. Tulifunga ndoa mwaka 1957, na pamoja tumefurahia mapendeleo ya kuwa mapainia wa kawaida, mapainia wa pekee, kufanya kazi ya kusafiri, na utumishi wa Betheli. Anne amekuwa chanzo cha shangwe katika maisha yangu yote.

Mwaka wa 1966, tulisisimuka sana kuhudhuria darasa la 42 la Shule ya Gileadi. Tulipewa mgawo wa kwenda Malawi, nchi ambayo hasa inajulikana kama nchi changamfu ya Afrika kwa sababu ina watu wenye fadhili na wanaopenda wageni. Hatukutarajia kwamba hatungeishi huko kwa muda mrefu.

KUTUMIKIA WAKATI WA MISUKOSUKO NCHINI MALAWI

Gari aina ya Kaiser Jeep lililotumiwa katika kazi ya kusafiri nchini Malawi

Tuliwasili nchini Malawi Februari 1, 1967. Baada ya masomo yenye kina ya mwezi mmoja ya kujifunza lugha, tulianza kazi ya kusafiri nikiwa mwangalizi wa wilaya. Tuliendesha gari aina ya Kaiser Jeep ambalo wengi walifikiri lingepita mahali popote, hata kuvuka mito. Lakini licha ya matarajio hayo, tuliweza kuvuka tu maji yenye kina kifupi. Nyakati nyingine, tulikaa katika nyumba za udongo zilizoezekwa kwa nyasi ambazo tulihitaji kuweka turubai chini ya paa wakati wa msimu wa mvua. Ilikuwa njia ngumu ya kuanza kazi ya umishonari lakini tuliipenda!

Mwezi Aprili, nilianza kuona dalili ya matatizo kuzuka nchini. Nilisikia kwenye redio hotuba ya rais wa Malawi, Dkt. Hastings Banda. Alidai kwamba Mashahidi wa Yehova hawalipi kodi na kwamba wanaingilia mambo ya kisiasa. Bila shaka, mashtaka hayo yalikuwa ya uwongo. Sote tulijua kwamba tatizo lilikuwa msimamo wetu wa kutounga mkono upande wowote, hasa kukataa kununua kadi za chama cha kisiasa.

Mwezi Septemba, tulisoma katika magazeti kwamba rais aliwashtaki akina ndugu kuwa wanasababisha matatizo kila mahali. Kwenye mkutano fulani wa kisiasa, alitangaza kwamba serikali yake ingetekeleza upesi pendekezo la kuwapiga marufuku Mashahidi wa Yehova. Marufuku hiyo ilianza Oktoba 20, 1967. Muda mfupi baada ya hapo, maofisa wa polisi na maofisa wa uhamiaji waliwasili kwenye ofisi ya tawi ili kuifunga na kuwafukuza wamishonari nchini.

Tulipokamatwa na kufukuzwa nchini Malawi mwaka wa 1967 pamoja na wamishonari wenzetu Jack na Linda Johansson

Baada ya kukaa gerezani siku tatu, tulihamishiwa katika nchi ya Mauritius, iliyokuwa chini ya Uingereza. Hata hivyo, wenye mamlaka nchini Mauritius hawangeturuhusu kuishi nchini humo tukiwa wamishonari. Basi, tukapewa mgawo wa kwenda Rhodesia (sasa ni Zimbabwe). Tulipowasili huko, tulikutana na ofisa wa uhamiaji aliyekuwa mkali sana ambaye alituzuia kuingia nchini, akisema: “Mmepigwa marufuku kukaa nchini Malawi. Hamjaruhusiwa kukaa nchini Mauritius, na sasa mmekuja hapa kwa sababu mnafikiri ni rahisi.” Anne akaanza kulia. Ilionekana kwamba hakuna nchi iliyotutaka! Wakati huo, nilitamani kuondoka na kurudi moja kwa moja nyumbani nchini Uingereza. Mwishowe, maofisa wa uhamiaji walituruhusu tukae usiku huo katika ofisi ya tawi, na wakatuambia turipoti siku inayofuata kwenye makao yao makuu. Tulikuwa tumechoka sana, lakini tulikuwa tumeamua kuacha mambo mikononi mwa Yehova. Alasiri siku iliyofuata, bila kutarajia, tulipata kibali cha kuishi kama wageni nchini Zimbabwe. Sitasahau kamwe jinsi nilivyohisi siku hiyo, nilisadiki kwamba Yehova alikuwa akiongoza njia yetu.

MGAWO MPYA​—KUTUMIKIA MALAWI NIKIWA NCHINI ZIMBABWE

Nikiwa na Anne kwenye Betheli ya Zimbabwe, mwaka wa 1968

Kwenye ofisi ya tawi ya Zimbabwe, nilipewa mgawo katika Idara ya Utumishi, kusimamia kazi nchini Malawi na Msumbiji. Akina ndugu nchini Malawi walikuwa wakinyanyaswa vikali. Sehemu ya kazi yangu ilihusisha kutafsiri ripoti zilizotumwa na waangalizi wa mzunguko nchini Malawi. Jioni moja baada ya muda wa kazi, nilipokuwa nikikamilisha ripoti fulani, nililia kwa sababu ya ukatili ambao ndugu na dada zetu walikuwa wakitendewa. a Hata hivyo, nilitiwa moyo sana na ushikamanifu, imani, na uvumilivu wao.​—2 Kor. 6:4, 5.

Tulifanya yote tuliyoweza ili kuandaa chakula cha kiroho kwa ajili ya akina ndugu waliobaki nchini Malawi na pia wale waliokimbilia nchini Msumbiji kwa sababu ya ukatili. Kikundi cha kutafsiri Chichewa, lugha inayozungumzwa na wengi nchini Malawi, kilihamishiwa kwenye shamba kubwa la ndugu fulani nchini Zimbabwe. Kwa fadhili, aliwajengea makao na ofisi. Wakiwa huko waliendelea na kazi yao muhimu ya kutafsiri machapisho yanayotegemea Biblia.

Tulifanya mpango ili waangalizi wa mzunguko nchini Malawi wahudhurie kusanyiko la wilaya katika Chichewa nchini Zimbabwe. Wakiwa huko, walipewa mihtasari ya hotuba za kusanyiko. Walipokuwa wakirudi nchini Malawi walijitahidi kadiri walivyoweza kuwapatia akina ndugu habari hizo. Mwaka fulani walipokuja nchini Zimbabwe, tulifaulu kupanga Shule ya Huduma ya Ufalme ili kuwatia moyo waangalizi hao wa mzunguko wenye ujasiri.

Nikitoa hotuba katika lugha ya Chichewa kwenye kusanyiko la Chichewa/​Shona nchini Zimbabwe

Februari 1975, nilisafiri ili kuwatembelea Mashahidi kutoka nchini Malawi waliokuwa wakiishi katika kambi huko Msumbiji. Ndugu hao walikuwa wakienda sambamba na tengenezo la Yehova, kutia ndani mpango wa kuwa na baraza la wazee. Wazee hao wapya walikuwa wamepanga utendaji mbalimbali wa kiroho, uliotia ndani kutoa hotuba za watu wote, kuzungumzia andiko la siku na Mnara wa Mlinzi, na hata kufanya makusanyiko. Mipango katika kambi hizo ilikuwa kama mipango inayofanywa kwenye kusanyiko, kulikuwa na idara ya usafi, kusambaza chakula, na ulinzi. Ndugu hao waaminifu walikuwa wametimiza mengi sana kupitia baraka za Yehova, nami nilitiwa moyo sana.

Mwishoni mwa miaka ya 1970, ofisi ya tawi ya Zambia ilianza kusimamia kazi nchini Malawi. Lakini bado niliendelea kuwakumbuka na kusali kwa ajili ya ndugu na dada zetu nchini Malawi, kama walivyofanya wengine wengi. Katika pindi mbalimbali, nikiwa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Zimbabwe, nilikutana na wawakilishi kutoka makao makuu, kutia ndani ndugu waliosimamia kazi nchini Malawi, Afrika Kusini, na Zambia. Kila mara, tulizungumzia swali hili, “Tunaweza kuwafanyia jambo gani lingine akina ndugu nchini Malawi?”

Kadiri muda ulivyopita, mnyanyaso ulipungua. Akina ndugu waliokuwa wamekimbilia nchi nyingine sasa walikuwa wakirudi nchini Malawi, na kwa wale waliokuwa wamebaki mnyanyaso ulikuwa ukipungua hatua kwa hatua. Nchi jirani zilikuwa zikiwatambua watu wa Yehova kisheria na kuondoa vizuizi. Nchi ya Msumbiji ilifanya hivyo pia mwaka wa 1991. Lakini tulijiuliza, ‘Mashahidi wa Yehova watakuwa huru lini nchini Malawi?’

KURUDI NCHINI MALAWI

Mwishowe, hali ya kisiasa nchini Malawi ilibadilika, na mwaka wa 1993 serikali ikaondoa marufuku dhidi ya Mashahidi wa Yehova. Muda mfupi baada ya hapo, nilikuwa nikizungumza na mmishonari fulani aliyeniuliza, “Je, utarudi Malawi?” Wakati huo nilikuwa na umri wa miaka 59, basi nikajibu, “Hapana, nimezeeka sana!” Hata hivyo, siku hiyohiyo tulipokea ujumbe wa faksi kutoka kwa Baraza Linaloongoza wakituomba turudi huko.

Tuliupenda mgawo wetu nchini Zimbabwe, basi huo ulikuwa uamuzi mgumu kwetu. Tulikuwa tumezoea maisha huko na pia tulikuwa tumesitawisha urafiki wa karibu pamoja na akina ndugu na dada. Kwa fadhili, Baraza Linaloongoza lilisema kwamba hawangebadili mgawo wetu isipokuwa tufanye hivyo kwa hiari. Hivyo, ingekuwa rahisi kwetu kujichagulia njia na kubaki nchini Zimbabwe. Lakini nilikumbuka jinsi Abrahamu na Sara walivyoacha makao yao yenye kustarehesha wakiwa na umri mkubwa ili kutii mwongozo wa Yehova.​—Mwa. 12:1-5.

Tuliamua kufuata mwongozo wa tengenezo la Yehova na kurudi nchini Malawi Februari 1, 1995, miaka 28 kamili baada ya kuwasili nchini humo kwa mara ya kwanza. Halmashauri ya Tawi ilianzishwa, ambayo ilitia ndani mimi na ndugu wengine wawili, na baada ya muda mfupi tukaanza mipango ya kuanzisha tena utendaji wa Mashahidi wa Yehova.

YEHOVA AIKUZA KAZI

Ni baraka kuona Yehova akifanya kazi ikue upesi! Idadi ya wahubiri iliongezeka kutoka 30,000 mwaka wa 1993 hadi zaidi ya 42,000 mwaka wa 1998. b Baraza Linaloongoza liliidhinisha mipango ya kujenga ofisi mpya ya tawi ili kushughulikia uhitaji uliokuwa ukiongezeka shambani. Tulinunua kiwanja chenye ekari 30 huko Lilongwe na nikachaguliwa kutumikia katika halmashauri ya ujenzi.

Ndugu Guy Pierce alitoa hotuba ya wakfu kwa ajili ya majengo hayo mapya Mei 2001. Zaidi ya Mashahidi wenyeji elfu mbili walihudhuria, na wengi kati yao walikuwa wamebatizwa zaidi ya miaka 40 iliyopita. Ndugu na dada hao waaminifu walikuwa wamevumilia kwa miaka mingi mateso makali chini ya marufuku. Walikuwa maskini kimwili, lakini matajiri sana kiroho. Na sasa walifurahia kutembelea Betheli yao mpya. Kila mahali walipoenda, kulikuwa na sauti za nyimbo za Ufalme zilizoimbwa kwa mtindo wa Kiafrika, jambo lililofanya tukio hilo lote liwe jambo ambalo limenigusa moyo zaidi maishani. Ulikuwa uthibitisho ulio wazi kwamba Yehova huwabariki sana wale wanaovumilia majaribu kwa uaminifu.

Baada ya ujenzi wa ofisi ya tawi kukamilika, nilifurahi kuanza kupokea migawo ya kuweka wakfu Majumba ya Ufalme. Makutaniko nchini Malawi yalianza kunufaika na mpango wa kujenga Majumba ya Ufalme upesi kwenye nchi zenye uwezo mdogo wa kifedha. Hapo awali, baadhi ya makutaniko yalikutana katika mabanda yaliyojengwa kwa mikalitusi. Walitumia mikeka iliyosukwa kwa matete kuezeka paa, na walitumia benchi ndefu zilizotengenezwa kwa udongo. Sasa akina ndugu walichoma matofali kwa shangwe kwenye matanuru waliyotengeneza na kujenga majumba mapya maridadi. Lakini bado walipendelea benchi, kwa sababu kama wanavyosema, Sikuzote kuna nafasi ya mtu mmoja zaidi kwenye benchi!

Pia, nimesisimuka kuona Yehova akiwasaidia watu wakue kiroho. Nilifurahishwa hasa na ndugu vijana Waafrika ambao walijitoa kutumikia kwa hiari na kupata uzoefu haraka kupitia elimu ya kitheokrasi na mazoezi hususa. Walianza kutimiza majukumu makubwa zaidi Betheli na makutanikoni. Makutaniko yaliimarishwa zaidi kupitia waangalizi wapya wa mzunguko wenyeji na wengi wao walikuwa wamefunga ndoa. Wenzi hao wa ndoa walichagua kumtumikia Yehova kikamili zaidi kwa kuahirisha shangwe ya kupata watoto, licha ya mkazo kutoka kwa jamii na katika visa fulani watu wa familia zao.

NIMERIDHISHWA NA MAAMUZI YANGU

Nikiwa na Anne kwenye Betheli ya Uingereza

Baada ya kukaa barani Afrika kwa miaka 52, nilipata matatizo ya kiafya. Baraza Linaloongoza lilikubali pendekezo la Halmashauri ya Tawi kwamba tuhamie Uingereza. Tulivunjika moyo kuacha mgawo ambao tuliupenda, lakini familia ya Betheli ya Uingereza inatutunza vizuri sana katika miaka yetu ya uzeeni.

Ninasadiki kwamba kumruhusu Yehova aongoze njia yangu, ndio uamuzi bora kabisa ambao nimefanya maishani. Ikiwa ningetegemea uelewaji wangu mwenyewe, sijui kazi yangu ya kimwili ingenifikisha wapi. Sikuzote Yehova alijua kile nilichohitaji ili ‘kunyoosha vijia vyangu.’ (Met. 3:5, 6) Nilipokuwa kijana, nilifurahi sana kujifunza jinsi kazi inavyofanywa katika kampuni kubwa. Hata hivyo, tengenezo la ulimwenguni pote la Yehova lilinipatia kazi ya kiroho ambayo imeniridhisha zaidi. Kumtumikia Yehova kulikuwa na kutaendelea kuwa maisha yenye kuridhisha sana kwangu!

a Historia ya kitheokrasi ya Malawi imechapishwa katika Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 1999, uku. 148-223.

b Sasa nchi ya Malawi ina zaidi ya wahubiri 100,000.