Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mtu Anaweza Kuacha Mazoea Mabaya?

Je, Mtu Anaweza Kuacha Mazoea Mabaya?

Maoni ya Biblia

Je, Mtu Anaweza Kuacha Mazoea Mabaya?

PINDI moja mwandishi Mark Twain alisema hivi kwa mzaha: “Kuacha kuvuta sigara ndilo jambo rahisi sana ulimwenguni. Ninajua hivyo kwa sababu nimeacha mara nyingi.” Bila shaka watu wengi wana maoni kama ya Twain. Ingawa huenda wakatambua kwamba mazoea fulani ni mabaya na hata ni hatari, wanajua pia kwamba ni vigumu sana kuyaacha. Mtu anapozoea jambo fulani kwa miaka mingi, huenda ikawa vigumu sana kuliacha hata akijitahidi. Kujaribu kuzuia tamaa hizo kwaweza kuchosha na hata kuumiza.

Dakt. Anthony Daniels, anayefanya kazi katika jela fulani, anasema kwamba mara nyingi wafungwa hudai kwamba wameshindwa kabisa kuacha mazoea na tamaa zao mbaya. Wanadai kwamba mtu akiisha kuzoea kitu fulani, “ni kana kwamba analazimika kukifanya na hawezi kamwe kukiepuka.” Ikiwa ndivyo ilivyo, basi hatuwezi kuwajibika tukitenda mambo ambayo hatuwezi kuepuka. Lakini je, ni kweli kwamba hatuwezi kuzuia hisia na tamaa zetu? Au tunaweza kuacha mazoea mabaya? Ili kupata jibu lenye kutegemeka, hebu tuone yale ambayo Biblia inasema.

Tofauti Kati ya Tamaa na Matendo

Biblia inasema waziwazi kwamba Mungu atatutoza hesabu kwa ajili ya matendo yetu. (Waroma 14:12) Pia, anataka tuishi kulingana na viwango vyake vya uadilifu. (1 Petro 1:15) Kwa kuwa yeye ndiye Muumba wetu, anajua mambo yanayotufaa, na kanuni zake zinapinga mazoea mengi ambayo ni mambo ya kawaida ulimwenguni. (1 Wakorintho 6:9, 10; Wagalatia 5:19-21) Hata hivyo, ana huruma naye hatazamii wanadamu wasio wakamilifu wafanye mambo yanayopita uwezo wao.—Zaburi 78:38; 103:13, 14.

Ndiyo sababu mtunga-zaburi aliandika hivi: “Kama ungekuwa unaangalia makosa, Ee Yah, Ee Yehova, ni nani angesimama?” (Zaburi 130:3) Naam, Yehova anajua vizuri sana kwamba “mwelekeo wa moyo wa mwanadamu ni mbaya tangu ujana wake na kuendelea.” (Mwanzo 8:21) Udhaifu ambao tumerithi, na mambo yaliyotupata maishani, hufanya iwe vigumu kuepuka mazoea na tamaa zote mbaya. Kwa hiyo, kwa sababu ya upendo wake, Yehova hadai tuwe wakamilifu.—Kumbukumbu la Torati 10:12; 1 Yohana 5:3.

Hata hivyo, haimaanishi kwamba hatuna wajibu wa kuzuia tamaa mbaya. Mtume Paulo hakukata tamaa, ijapokuwa alikubali kwamba alikuwa akipambana na tamaa mbaya. (Waroma 7:21-24) Alisema, “Naupigapiga mwili wangu na kuuongoza kama mtumwa.” Kwa nini? Ili “baada ya mimi kuwahubiria wengine, mimi mwenyewe nisikataliwe kwa njia fulani.” (1 Wakorintho 9:27) Naam, kujizuia ni muhimu ili hatimaye kushinda mielekeo na mazoea mabaya.

Mtu Anaweza Kubadilika

Wanasayansi wanaochunguza tabia za watu wanasema kwamba watu huchukua wakati kujifunza na kusitawisha mazoea mabaya, kama vile wanavyojifunza na kusitawisha mazoea mazuri. Basi, mazoea mabaya yanaweza kubadilishwa! Jinsi gani? Waandishi wa kitabu kinachozungumzia jinsi ya kushughulika na mfadhaiko wanasema: “Fikiria faida utakazopata kwa kuacha mazoea ya zamani.” Kisha, “uandike orodha inayoonyesha jinsi kubadili mazoea yako kunavyoweza kuboresha maisha yako.” Kuzingatia faida za kuacha mazoea mabaya kunaweza kutuchochea tubadilike.

Fikiria jinsi Paulo anavyotuhimiza ‘tufanywe upya katika nguvu zinazoendesha akili zetu.’ (Waefeso 4:22, 23) Nguvu hizo ni uvutano wa kiakili unaotutawala. Unaweza kubadili nguvu hizo kwa kumkaribia Mungu na kwa kupendezwa zaidi na kanuni zake. Kujua kwamba unampendeza Yehova kwaweza kukuchochea kufanya mabadiliko yanayohitajiwa.—Zaburi 69:30-33; Methali 27:11; Wakolosai 1:9, 10.

Bila shaka, haitakuwa rahisi kuyaondolea mbali mazoea mabaya ambayo yametawala maisha yetu kwa miaka mingi. Tusipuuze kamwe pambano tulilo nalo. Tutajikwaa na kuanguka mara kwa mara. Lakini uwe na hakika kwamba muda si muda, mambo yatakuwa rahisi zaidi. Kadiri unavyojitahidi kubadilika, ndivyo mwenendo wako mpya utakavyozidi kuwa kawaida yako.

Bila shaka, Mungu atamtegemeza na kumbariki yule anayempenda. Paulo anaahidi hivi: “Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha ninyi mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali . . . ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kulivumilia.” (1 Wakorintho 10:13) Hivi karibuni, Yehova Mungu atauharibu ulimwengu huu mbovu pamoja na majaribu na tamaa zake zote mbovu. (2 Petro 3:9-13; 1 Yohana 2:16, 17) Mwishowe, wanadamu wote wasio wakamilifu watakaookoka tukio hilo wataponywa kabisa kutokana na madhara yote—ya kimwili, kiakili, na kihisia. Mungu anaahidi kwamba “mambo ya zamani hayatakumbukwa akilini, wala hayataingia moyoni.” (Isaya 65:17) Bila shaka, baadhi ya ‘mambo hayo ya zamani’ yanatia ndani hamu na tamaa zenye kusumbua. Je, hiyo si sababu nzuri ya kufanya yote tuwezayo leo ili kupinga na kupambana na mazoea mabaya?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 21]

JINSI YA KUSHINDA MAZOEA MABAYA

1. Tambua na ukubali kwamba una mazoea mabaya. Jiulize, ‘Je, mazoea haya yananifaidi kwa njia yoyote? Je, yanawakera watu wengine? Je, yanaathiri afya yangu, fedha zangu, masilahi yangu, familia yangu, au amani yangu ya akili? Maisha yangu yangekuwaje ikiwa singekuwa nayo?’

2. Sitawisha mazoea mazuri. Kwa mfano, je, unatumia wakati mwingi sana kwenye Internet, huenda ukitazama habari chafu? Basi panga kutumia wakati huo kusoma habari zinazofaa, kujifunza, au kufanya mazoezi ya mwili.

3. Changanua maendeleo yako. Kila siku, tumia dakika chache kuchanganua maendeleo yako. Ukirudi nyuma, tafuta ujue ni hali gani zilizokuingiza katika tatizo hilo.

4. Waombe wengine wakusaidie. Waambie rafiki na familia yako kwamba unajaribu kuacha mazoea hayo, na uwaombe wakukumbushe wakikuona ukielekea kutumbukia tena. Zungumza na wengine ambao wamefanikiwa kuacha mazoea hayo.—Methali 11:14.

5. Uwe na usawaziko wala usitarajie miujiza. Usitarajie kupata mafanikio mara moja. Mazoea fulani ambayo yamesitawi kwa muda mrefu huchukua muda mrefu kuyabadili.

6. Sali kwa Mungu. Ukimtegemea Mungu, unaweza kuacha mazoea yoyote mabaya.—Zaburi 55:22; Luka 18:27.