Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Usichelewe!

Usichelewe!

Usichelewe!

GAZETI USA Today linasema kwamba “kuchelewa ni tatizo kubwa miongoni mwa maafisa wakuu.” Likizungumzia uchunguzi wa maafisa wakuu 2,700, liliongezea hivi: “Wao hufika wakiwa wamechelewa katika mikutano sita kati ya 10.”

Katika biashara, kuchelewa hakuonwi tu kuwa tabia mbaya. Uchunguzi wa watu 81,000 wanaotafuta kazi ulionyesha hivi: “Saa nyingi hupotezwa kwa sababu ya kuchelewa na kutofika kazini na hilo husababisha hasara kubwa ya kiuchumi.” Bila shaka, kuchelewa hakusababishi matatizo katika biashara tu. Uchunguzi wa walimu wakuu wa shule za sekondari ulionyesha kwamba “tatizo kubwa linalotukia mara nyingi kati ya wanafunzi ni kuchelewa.”

Muumba wetu alikusudia tutunze wakati. Ili kutusaidia kupima wakati, aliweka “mianga mikubwa miwili,” jua na mwezi. (Mwanzo 1:14-16) Leo, vifaa vya kisasa hutusaidia kupima wakati kwa kutumia dakika na sekunde. Hata hivyo, licha ya tekinolojia, wengi wetu bado huchelewa kufika kazini, shuleni, au kwenye shughuli nyingine muhimu.

Je, tatizo hilo husababishwa na kukosa wakati? Ni kweli kwamba kuna shughuli nyingi kazini na katika familia. Hata hivyo, Wanda Rosseland, mama anayefanya kazi, alisema: “Niliacha kulalamika kwamba sina wakati wa kutosha nilipotambua kwamba sisi sote tuna saa 24 kwa siku. Nimefikiria kuhusu jambo hilo na kuamua kwamba katika ulimwengu wa sasa, si kwamba hatuna wakati wa kutosha, bali ni kwa sababu kuna vitu vingi vinavyoingilia shughuli zetu na kutukengeusha.”

Pia, mfikirie Renee, * mama ya watoto watano, ambaye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Anakumbuka hivi: “Watoto wangu walipokuwa wachanga, haikuwa rahisi kuwatayarisha kwa ajili ya shule na mikutano ya Kikristo. Hata hivyo, sikuwa nikichelewa. Lakini sasa baada ya wao kukua, nimesitawisha mazoea mabaya ya kuchelewa.” Je, wewe pia una mazoea hayo mabaya? Ikiwa ndivyo, unaweza kubadilika! Unaweza kufanya baadhi ya mambo yafuatayo.

● FIKIRIA MATOKEO. Huenda tatizo la kuchelewa likaonekana kuwa jambo dogo. Lakini fikiria maneno haya ya Biblia: “Nzi waliokufa ndio hufanya mafuta ya mtengenezaji wa marashi yanuke, na kutoa povu. Ndivyo upumbavu kidogo unavyomfanya mtu mwenye thamani kwa sababu ya hekima na utukufu.” (Mhubiri 10:1) Naam, “upumbavu kidogo” tu kwa kukosa kuwafikiria wengine, unaweza kukuharibia sifa mbele ya mwalimu au mwajiri.

Alipokuwa akisomea kwenye chuo kimoja, mwanamke anayeitwa Marie alitambua kwamba baadhi ya wanafunzi wenzake “hawakujali wakati,” kwani mara nyingi walikuwa wakichelewa. “Hata hivyo iliwabidi wabadilike,” anakumbuka. “Profesa wawili walizingatia sana wakati. Kwa hiyo wanafunzi walipochelewa dakika chache, walihesabiwa kuwa hawakufika. Na baada ya kutofika mara kadhaa mwanafunzi alianguka mtihani.”

Tatizo la kuchelewa linaweza kukuharibia sifa zako mbele ya marafiki. Mwanamume wa makamo anayeitwa Joseph anamkumbuka Mkristo mwenzake aliyemjua miaka mingi iliyopita. Ijapokuwa mwanamume huyo aliheshimiwa kwa sababu ya uwezo wake wa kufundisha, alikuwa na tatizo lenye kuaibisha. “Alikuwa akichelewa sikuzote,” akumbuka Joseph. “Alikuwa akichelewa kwa kila kitu! Naye hakujali hata kidogo. Watu walimtania kuhusu kuchelewa kwake.” Je, watu wameanza kukutaja kuwa mtu ambaye huchelewa kila wakati? Ikiwa ndivyo, huenda basi wasione sifa zako nzuri.

● WAFIKIRIE WENGINE. Kuchelewa ni kukosa adabu na huwakengeusha wengine. Na kunaweza kufanya watu wafikiri kwamba unajiona kuwa bora sana. Akieleza sababu zinazowafanya wasimamizi wa makampuni kuchelewa kufika mikutanoni, mfanyabiashara mmoja alikiri hivi: “Wengi wetu wana kiburi.” Tofauti na hilo, Wakristo huwaona wengine kuwa bora kuliko wao wenyewe. (Wafilipi 2:3) Wao pia hutumia ile kanuni ya kuwatendea wengine kama wanavyotaka kutendewa. (Mathayo 7:12) Je, wewe huudhika unapolazimika kuwangojea wengine? Basi usiwafanye wengine wakungojee.

● JIFUNZE JINSI YA KUTUMIA WAKATI. Je, wewe huahirisha mambo na kuharakisha dakika za mwisho-mwisho? Je, wewe hujipangia mambo mengi kupita kiasi, na kujaribu kuyafanya kwa wakati mfupi sana? Kanuni ya Mhubiri 3:1 inaweza kukusaidia: “Kuna wakati uliowekwa wa kila kitu.” Ukiwa na “wakati uliowekwa” kwa ajili ya mambo utayafanya kwa utaratibu.

Kwanza, orodhesha mambo unayohitaji kufanya. Halafu, ufuate kanuni ya Wafilipi 1:10: ‘Hakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi.’ Naam, tanguliza mambo ya maana. Ni mambo gani ambayo ni lazima yafanywe? Ni mambo gani yanayoweza kuahirishwa? Hatimaye, kadiria kiasi cha wakati unaohitaji ili kuyafanya na pindi ambayo utayafanya. Uwe na usawaziko, na uepuke kupangia mambo mengi mno kwa wakati mfupi.

Mwanamke anayeitwa Dorothy anawashukuru wazazi wake kwa kumfundisha kutochelewa. Anasema: “Ikiwa tulipaswa kuwa kwenye mkutano wa Kikristo kufikia saa 1:30 jioni, mama yangu alitutayarisha saa nzima na dakika 45 mapema. Tulihitaji kuwa na wakati wa kula chakula, kuosha vyombo, kuvaa, na kwenda mkutanoni. Tulizoea kufika kwa wakati.” Wakati mwingine ni vizuri kuruhusu wakati kwa ajili ya mambo yasiyotazamiwa. Dorothy anakumbuka: “Hivi majuzi nilihitaji kuwachukua watu kadhaa ili twende pamoja mkutanoni. Lakini nikapata panchari njiani. Gurudumu lilirekebishwa na bado sikuchelewa kuwachukua. Nyakati zote mimi hupanga wakati kwa ajili ya matatizo ya gari au msongamano wa magari.”

● PATA MAPENDEKEZO YA WENGINE. Biblia inasema hivi kwenye Methali 27:17: “Chuma hunolewa kwa chuma. Ndivyo mtu anavyounoa uso wa mwingine.” Kupatana na kanuni hiyo, zungumza na wengine walio na hali kama zako ambao hufanya mambo kwa wakati. Mara nyingi watakuwa na mapendekezo kadhaa yanayofaa.

Renee, aliyenukuliwa awali, ameazimia kubadili tabia yake ya kuchelewa. Anasema: “Nimeazimia kufanya maendeleo. Ingawa si rahisi, ninajitahidi.” Hata wewe unaweza. Ukiwa na mtazamo mzuri na jitihada unaweza kujifunza kutochelewa!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Kuchelewa kila wakati kunaweza kuwafanya waajiri wawe na maoni mabaya kumhusu mtu na kunaonyesha kutowajali wengine

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kupanga mambo vizuri kunaweza kukusaidia kuepuka kupoteza wakati