Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilikuwa Kamanda wa Jeshi Sasa Mimi Ni “Askari-Jeshi wa Kristo”

Nilikuwa Kamanda wa Jeshi Sasa Mimi Ni “Askari-Jeshi wa Kristo”

Nilikuwa Kamanda wa Jeshi Sasa Mimi Ni “Askari-Jeshi wa Kristo”

Limesimuliwa na Mark Lewis

“Hujambo, Mheshimiwa.” “Habari za alasiri, Mtukufu?” “Habari za jioni, Waziri Mkuu?” Hizo ni baadhi za salamu nilizotumia nikiwa rubani na Kamanda Mkuu wa Jeshi la Angani la Australia. Niliwasafirisha kwa ndege wakuu wa serikali na watu wenye vyeo vya juu katika serikali kotekote nchini Australia na ulimwenguni pote. Lakini sasa, ninafanya jambo linaloridhisha zaidi. Acheni niwaeleze.

NILIZALIWA huko Perth, Magharibi ya Australia, mnamo 1951 na baba yangu alikuwa mwanajeshi. Nilipokuwa na umri wa miaka 15, nilijiunga na chama cha wanyiririkaji. Tangu wakati huo nimependa sana kuruka angani.

Muda mfupi baada ya hapo, wazazi wangu waliachana, na familia yetu ikasambaratika. Ofisa mkuu wa kikosi fulani cha Jeshi la Angani pamoja na familia yake, walinichukua niishi nao huku nikimaliza shule ya sekondari. Uvutano wake ulinichochea niwe mwanafunzi katika Chuo cha Jeshi la Angani la Australia.

Napokea “Mabawa” Yangu

Miaka sita hivi baadaye, nilihitimu kama ofisa wa Jeshi la Angani nikiwa na digrii ya sayansi na urubani. Kazi yangu ya kwanza ilitia ndani kusafirisha vitu mbalimbali kotekote nchini Australia, katika maeneo ya Pasifiki Kusini, na Kusini-mashariki mwa Asia. Mara nyingi tuliruka juu ya milima mirefu na mabonde yenye kina kirefu ambako tungetua kwenye wa uwanja wa ndege uliofunikwa na nyasi. Ilikuwa kazi hatari sana. Kikosi chetu kilipoteza ndege na watu kadhaa wenye ustadi katika miaka hiyo. Lakini lengo letu lilikuwa kuwasaidia watu walioishi maeneo ya mbali. Tulisafirisha vifaa vya kujenga madaraja, matingatinga yanayotumiwa kujenga barabara, vyakula vya wakati wa dharura, na hata madaktari. Pia tuliwasafirisha wagonjwa au watu walioumia wakati wa dharura.

Mnamo 1978, nilitimiza matakwa ya kuwa mwalimu wa urubani na nikarudi kwenye Chuo cha Jeshi la Angani ili nifundishe. Nikiwa hapo nilifahamiana zaidi na Diane, mjane aliyekuwa na binti wa miaka mitatu. Nilisoma na mume wa Diane katika Chuo cha Jeshi la Angani lakini alikufa baadaye katika msiba wa angani. Nilipomwomba tuoane, aliniambia nimpe muda afikirie jambo hilo. Hakuwa na hakika ikiwa angependa kuolewa na rubani mwingine.

Wakati huohuo, nilikubali kuwa msaidizi wa karibu wa Gavana Mkuu wa Australia kwa miezi 12. Maisha katika nyumba ya Gavana Mkuu huko Canberra, yalinifanya nielewe jinsi mambo ya kisiasa yanavyoendeshwa na yalitia ndani kushirikiana kwa ukaribu na wenye mamlaka katika jamii, jeshi, na dini. Muda wangu wa kufanya kazi huko ulipokwisha, niliendelea na kazi ya kufundisha urubani. Muda mfupi baadaye, mnamo 1980, tulioana na Diane.

Mnamo 1982, nilipewa mazoezi ya miaka miwili katika Jeshi la Angani la Marekani nikiwa ofisa anayeshughulika na usalama wa ndege na mchunguzi wa misiba ya ndege. Kazi hiyo ilinifanya nisafiri kotekote nchini Marekani na hata maeneo ya mbali kama Ireland Kaskazini. Ilitia ndani kuchunguza misiba ya ndege na kuchunguza muundo wa ndege na jinsi inavyofanya kazi ili kuimarisha usalama.

Narudi Australia

Baada ya kurudi Australia, familia yetu iliongezeka binti yetu Kerry alipozaliwa, tukawa watu wanne katika familia. Kwa sababu ya kazi yangu, Diane alikuwa mama na baba, na maisha yetu ya familia yalizorota. Miaka mitatu baadaye, kwa mara ya kwanza nilipata cheo cha juu katika kikosi cha Jeshi la Angani cha kusafirisha wakuu wa serikali, kama nilivyotaja awali. Vita vya Ghuba ya Uajemi vilipoanza mnamo 1991, kikosi chetu kilitegemeza Umoja wa Mataifa huko na katika shughuli nyingine huko Pakistan, Afghanistan, Afrika, na Israeli.

Mnamo 1992, niliwekwa kuwa ofisa msaidizi wa Mkuu wa Kikosi cha Ulinzi. Nikiwa msaidizi wa kamanda mkuu zaidi wa jeshi la Australia niliweza kuona vizuri uhusiano kati ya jeshi, siasa, na UM. Nilikata kauli kwamba UM lina kasoro nyingi. Hata hivyo, bado shirika hilo lilionekana kuwa tumaini pekee la kuleta ulimwengu bora. Lakini mambo fulani yaliyotendeka nyumbani yalinifanya nibadili maoni yangu.

Maswali ya Diane Yajibiwa

Baada ya mume wake wa kwanza kufa, Diane, ambaye alikuwa Mkatoliki, alitafuta majibu kwa maswali yake lakini hakufua dafu. Hata hivyo, mambo yalikuwa mabaya zaidi binti yetu mkubwa, Renee, alipovutiwa na mizungu. Diane alipokuwa katika nyumba ya rafiki yake, aliona gazeti la Amkeni! ambalo lilikuwa na tangazo lililosema kwamba gazeti linalofuata litakuwa na makala kuhusu Ushetani. * Kabla ya hapo, hakuwa ameona Amkeni! Alipokuwa akirudi nyumbani alijiuliza, ‘Nitapata wapi gazeti hilo?’

Siku tatu baadaye, Mashahidi wa Yehova walikuja kwetu, na Diane akapata gazeti alilotaka. Baadaye alikubali kujifunza Biblia na kisha akaanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Nilifurahi kwamba alikuwa akijifunza na hata nilienda pamoja naye kwenye mikutano kadhaa, lakini sikuhisi ninahitaji kujifunza Biblia. Sikujiona kuwa mtu wa kidini. Nilimwamini Mungu lakini nilikuwa nimeona unafiki mwingi sana hivi kwamba sikuchukulia dini kwa uzito. Kwa mfano, sikuelewa ni kwa nini viongozi wa kidini katika jeshi walihubiri upendo na amani huku wakiunga mkono vita.

Diane aliacha magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ili niyasome. Nilisoma baadhi ya magazeti hayo, kisha nikayarudisha kwa uangalifu mahali yalipokuwa. Sikutaka afikiri kwamba ninapendezwa. Nilipoendelea kupata ujuzi wa Biblia, maandiko mawili yalinihangaisha. Andiko moja lilikuwa la Ufunuo 19:17, 18, linalozungumzia kuhusu ndege kula sehemu za nyama za “viongozi wa kijeshi.” Andiko lingine lilikuwa Ufunuo 17:3, linalomtaja “mnyama-mwitu mwenye rangi nyekundu.” Mashahidi walisema kwamba mnyama huyo anawakilisha Umoja wa Mataifa, maoni ambayo yalipingana na mawazo yangu kuhusu shirika hilo. * Lakini nilijaribu kupuuza maswali hayo.

Mnamo 1993, Diane aliniomba nihudhurie ubatizo wake. Sikutarajia ombi kama hilo. Nilimuuliza, “Ikiwa ungehitaji kuchagua, ungemchagua nani? Yehova au mimi?” Alinijibu: “Yehova. Lakini si lazima nichague. Ninawataka nyote maishani mwangu.” Hilo lilinifanya nitambue kwamba ninahitaji kujifunza mengi zaidi kumhusu mtu huyu mwingine aliyependwa na Diane. Mzee wa Kikristo katika ujirani wetu alisema kwamba anaweza kujifunza nami Biblia, na nikakubali.

Nilipendezwa sana na unabii wa Biblia, hasa jinsi unavyohusiana na historia ya kijeshi na ya kisiasa. Kwa mfano, katika masomo yangu katika Jeshi la Angani, nilijifunza kuhusu shughuli za kijeshi za Wagiriki wa kale. Sasa nilijifunza kwamba historia hiyo ilikuwa imeandikwa karne nyingi kabla katika sura ya 8 ya Danieli. Polepole, unabii huo na mwingine ulinisadikisha kwamba Biblia imeongozwa na roho ya Mungu.

Pia nilichunguza shirika la UM kwa uangalifu. Nilijua kwamba jeshi haliwezi kutatua matatizo ya wanadamu, amani ya kweli haiwezi kutokana na tisho la vita, na shirika la UM haliwezi kuondoa migawanyiko ya kisiasa, kidini, na kijamii inayosababisha vita. Nilianza kuona kwamba ni Mungu tu anayeweza kutatua matatizo ya wanadamu. Kwa kweli, ilionekana kwamba tayari alikuwa ameanza kusuluhisha mambo kupitia undugu wa ulimwenguni pote wa Mashahidi wa Yehova. (Zaburi 133:1; Isaya 2:2-4) Nilijiuliza, ‘Lakini kweli ninaweza kuacha kazi ya kijeshi ili nimtumikie Mungu?’

Kuchukua Msimamo Upande wa Kweli za Biblia

Mambo yalibadilika mnamo 1994 nilipohudhuria kusanyiko la wilaya la Mashahidi wa Yehova huko Sydney. Programu ilitia ndani drama ya Biblia iliyozungumza kuhusu uamuzi ambao taifa la Israeli lilihitaji kufanya. Walihitaji kuamua ikiwa watamtumikia Yehova au Baali, mungu wa Wakanaani. Nabii wa Mungu Eliya aliwaambia Waisraeli: “Mtayumba-yumba juu ya maoni mawili tofauti mpaka wakati gani? Ikiwa Yehova ndiye Mungu wa kweli, mfuateni yeye; lakini ikiwa ni Baali, mfuateni yeye.” (1 Wafalme 18:21) Maneno hayo yalinigusa moyo. Kama Waisraeli, nilikuwa ninayumba-yumba. Nilihitaji kuchagua: Je, nitamtumikia Yehova au nitaendelea na kazi ya kijeshi?

Tulipokuwa tukielekea nyumbani jioni hiyo, nilimwambia Diane kwamba nitaacha kazi katika Jeshi la Angani ili niwe Shahidi wa Yehova. Alishangaa kwamba nilifanya uamuzi huo ghafula lakini alinitegemeza kabisa. Baada ya siku chache uamuzi wangu ulikuwa uleule, kwa hiyo nilijiuzulu.

Wakati huo, nilikuwa Kamanda wa Chuo cha Kijeshi huko Canberra, jiji kuu la Australia. Nilisimamia masomo ya kijeshi na ya chuo ya watu 1,300 katika Jeshi la Nchi Kavu, Jeshi la Majini, na Jeshi la Angani na pia nilisimamia wafanyakazi wengine. Siku ya mwisho ya muhula wa chuo, niliwaambia watu 400 wenye vyeo na wafanyakazi wengine waliokuwa wamekusanyika kwamba ninaacha kazi ya jeshi ili niende nyumba kwa nyumba kuwafundisha watu Biblia nikiwa mhudumu wa kujitolea wa Kikristo. Tangazo hilo lilifanya kuwe na mazungumzo yenye kupendeza.

Kuwa Mtumishi wa Wakati Wote

Nilianza kuhubiri siku moja baada ya kujiuzulu rasmi. Miezi mitatu baadaye, mnamo Aprili 1995 nilibatizwa. Mara tu nilipopata fursa nikawa painia wa kawaida, jambo ambalo lilimaanisha kutumia wakati wangu wote katika utumishi wa hadharani.

Nilihitaji kufanya mabadiliko mengi ili niwe “askari-jeshi wa Kristo” badala ya kuwa kamanda wa jeshi. (2 Timotheo 2:3) Mojawapo ya migawo yangu ya kwanza ilikuwa kushughulikia vikuza-sauti katika mikutano ya Kikristo. Badala ya kutoa maagizo, nilihitaji kujifunza kuomba mambo yafanywe. Ufikirio na upendo ukaja kuwa muhimu kuliko kufanya kazi kwa njia bora zaidi, ingawa bado najaribu kuwa na usawaziko katika sifa hizo. Kwa sababu mshahara wangu ulipungua, familia yetu ilihitaji kurahisisha maisha.

Nilifurahia sana kazi ya kuhubiri na bado naifurahia. Siku moja nilipokuwa nikihubiri na binti yetu mwenye umri wa miaka tisa anayeitwa Kerry, nilimwomba atazame jinsi ambavyo wenye nyumba wangeitikia. Baada ya muda tuliona kwamba watu wengi hawakupendezwa lakini wengine walikuwa wazuri na hata walipendezwa. Jambo hilo lilitutia moyo. Binti yetu mwingine alijifunza Biblia kwa muda fulani lakini kwa sasa ameamua asimtumikie Yehova.

Mimi na Diane tulimtia moyo Kerry ajaribu utumishi wa wakati wote. Hivi karibuni, nilisisimuka sana kuhudhuria Shule ya Utumishi wa Painia pamoja naye. Ilikuwa mara yake ya kwanza kuhudhuria na mara yangu ya pili. Ni furaha isiyo na kifani kumwona yeye pamoja na vijana wengine wakifanya maendeleo ya kiroho na kufuatilia huduma ya Kikristo!—Zaburi 110:3.

Baraka kwa Wingi

Nikiangalia nyuma, ninaona mambo fulani yanayolingana na mambo fulani yanayotofautiana kati ya kuwa mwanajeshi na kuwa askari-jeshi wa Kristo. Majukumu yote mawili yanahitaji ushikamanifu, utii, unyoofu, nidhamu, na kujidhabihu. Ingawa wengi katika jeshi wanaweza kuwa tayari kufa kwa ajili ya nchi yao na marafiki wao, Wakristo wa kweli wanaambiwa wawapende hata maadui wao. (Mathayo 5:43-48) Na ingawa washindi katika jeshi wanaweza kupewa tuzo kwa sababu ya tendo moja tu la ujasiri, Wakristo wa kweli wanapata kibali cha Mungu kwa kuvumilia kwa uaminifu katika utumishi. Huenda hilo likamaanisha kuonyesha ujasiri tunaponyanyaswa, tunapodhihakiwa, na tunapopatwa na majaribu mengine mwaka baada ya mwaka. (Waebrania 10:36-39) Wakristo wenzangu ndio watu bora zaidi ninaowajua.

Badala ya salamu nilizotaja mwanzoni, siku hizi salamu zangu ni “Habari za asubuhi, Dada?” au “Habari za jioni, Ndugu?” Inafurahisha kama nini kutumikia katika huduma ya Kikristo pamoja na watu wanaompenda Mungu kikweli! Lakini heshima kubwa zaidi ni kumtumikia Aliye Juu Zaidi, Yehova, mwenyewe! Nisingeweza kufikiria njia yenye kuthawabisha zaidi ya kutumia maisha yangu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Lilichapishwa kwenye Amkeni! la Septemba 8, 1990, ukurasa wa 10-18.

^ fu. 17 Ona ukurasa wa 240-243 katika kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu! kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 14]

Wengi katika jeshi wanaweza kuwa tayari kufa kwa ajili ya nchi yao na marafiki wao, Wakristo wa kweli wanaambiwa wawapende hata maadui wao

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Kuruka na ndege ya Jeshi la Angani juu ya Jengo la Bunge huko Canberra

[Picha katika ukurasa wa 15]

Drama ya Biblia katika kusanyiko la wilaya la 1994 huko Sydney, Australia

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nikiwa na Kerry katika Shule ya Utumishi wa Painia

[Picha katika ukurasa wa 15]

Picha ya karibuni nikiwa na Diane na Kerry