Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuna ubaya gani kutumia matusi?

Kuna ubaya gani kutumia matusi?

Vijana Huuliza

Kuna ubaya gani kutumia matusi?

“Nilitaka kukubaliwa na wanafunzi wenzangu. Nafikiri hiyo ndiyo sababu nilianza kutumia matusi.”—Melanie. *

“Sikuona ubaya wowote wa kutumia matusi. Watu nyumbani na shuleni walitumia matusi kila wakati.”—David.

KWA nini inaonekana sawa kwa watu wazima kutumia matusi, ilhali vijana wanapofanya hivyo linakuwa jambo lenye kushtua? Je, umri wa mtu ndio unaoamua ikiwa ni sawa kutumia matusi au la? Kwa kuwa watu wengi sana hutumia lugha chafu na inaonekana kwamba ni sawa kwa watu wazima kutumia matusi lakini si sawa kwa vijana, huenda ukauliza, “Kuna ubaya gani kutumia matusi?”

Jinsi Ambavyo Mtu Huanza Kutumia Lugha Chafu

Hakuna shaka kwamba matusi hutumiwa kotekote. Vijana wengine wanaweza kusema kwamba ikiwa wangepewa dola moja kwa kila neno chafu walilosikia shuleni, wangekuwa na pesa nyingi sana hivi kwamba hawangehitaji kufanya kazi kamwe na hata wazazi wao wangestaafu. Eve, mwenye umri wa miaka 15 anasema: “Wanashule wenzangu hutamka matusi katika kila sentensi katika mazungumzo ya kawaida. Unaposikia matusi kila mara, ni vigumu sana kuepuka kuyatumia.”

Kama Eve, je, wewe pia umezungukwa na watu wanaotumia matusi? Je, umekuwa na zoea la kutumia matusi? * Ikiwa ndiyo, tua na uchunguze ni nini hasa hufanya utumie matusi. Ukijua kisababishi, itakuwa rahisi kwako kuacha zoea hilo.

Ili ujue ni nini hufanya utumie matusi, jaribu kujibu maswali yafuatayo.

Mara nyingi, kwa nini wewe hutumia matusi?

□ Kuonyesha nimekasirika au nimeudhika

□ Ili niwavutie wengine

□ Ili nikubaliwe na marafiki wangu

□ Ili nionekane kuwa mtu mwenye nguvu

□ Ili kuasi sheria

□ Sababu nyingine ․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․

Yaelekea utatumia matusi ukiwa katika hali gani?

□ Shuleni

□ Kazini

□ Ninapotuma barua-pepe au ujumbe mfupi kupitia simu ya mkononi

□ Nikiwa peke yangu

Wewe hutoa visingizio gani unapotumia matusi?

□ Marafiki huyatumia

□ Wazazi huyatumia

□ Walimu huyatumia

□ Burudani zimejaa matusi

□ Hakuna ubaya wowote—ni maneno tu

□ Mimi hutumia matusi ninapokuwa na watu ambao hilo haliwaudhi

□ Sababu nyingine ․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․

Kwa nini ujitahidi kuacha zoea hilo? Je, kweli ni vibaya kutumia matusi? Fikiria mambo yafuatayo.

Si maneno tu. Yesu alisema: “Kinywa cha mutu kinasema maneno yanayojaza moyo wake.” (Luka 6:45, Zaire Swahili Bible) Ona kwamba yale tunayosema hayaonyeshi aina ya mtu tunayetaka kuwa, yanaonyesha sisi ni watu wa aina gani. Hata kama unatumia lugha chafu kwa sababu tu wengine wanaitumia, kuiga mfano wao kunaonyesha kwamba ‘unaufuata umati’ na kwamba huna msimamo.—Kutoka 23:2.

Lakini si hayo tu. Mtaalamu wa lugha, James V. O’Connor, anasema: “Mara nyingi, watu wanaotumia matusi hawapendi kusuluhisha mambo, ni wachambuzi, wadhihaki, wana hasira, wabishi, na walalamishi wasio na furaha.” Kwa mfano, watu ambao hutumia matusi mambo yanapoenda mrama, huamini kwamba ni lazima kila kitu kitendeke vile wanavyotaka. Ni kana kwamba hawawezi kukubali kwamba wao hukosea. Kwa upande mwingine, O’Connor anasema kwamba watu ambao hawatumii matusi “mara nyingi huwa watu watulivu, . . . waliokomaa ambao [wanaweza] kukabiliana na mambo yenye kuudhi yanayotukia kila siku.” Wewe ungependa kuwa mtu wa aina gani?

Matusi yanakuharibia sifa. Kama vijana wengi, huenda wewe huhangaikia sana sura yako. Unataka watu wakupende. Lakini je, ulijua kwamba jinsi unavyozungumza huathiri sana maoni ya watu kukuhusu kuliko sura yako? Kwa kweli, usemi wako unaweza kuamua

□ Ni nani watakaovutiwa kuwa rafiki wako.

□ Ikiwa utaajiriwa kazi au la.

□ Kiasi cha heshima utakachopewa.

Ni kweli kwamba maoni ya watu kutuhusu hubadilika mara tu tunapoanza kuzungumza. O’Connor anasema hivi: “Huwezi kujua ni fursa ngapi za kuwa na rafiki mpya ambazo huenda ulipoteza, au ni mara ngapi ulifanya watu wajitenge nawe au wakose kukuheshimu kwa sababu ya kutumia lugha chafu bila kujali.” Hilo linakufunza nini? Ukitumia lugha chafu, unajiumiza wewe mwenyewe.

Kutumia lugha chafu kunamvunjia heshima Mwanzilishi wa usemi. Wazia kwamba umempa rafiki yako nguo kama zawadi. Ungehisije ikiwa ungemwona akitumia nguo hiyo kama zulia la kufutia miguu mlangoni? Hebu wazia jinsi ambavyo Muumba wetu huhisi tunapotumia vibaya zawadi ya usemi. Si ajabu kwamba Neno la Mungu linasema: “Uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu pamoja na ubaya wote.”—Waefeso 4:31.

Kama unavyoona, kuna sababu nzuri za kuacha kutumia matusi. Hata hivyo unaweza kushindaje zoea hilo ikiwa limekita mizizi?

Kwanza: Tambua kwamba unahitaji kubadilika. Yaelekea hutaacha kutumia matusi usipojua faida za kubadili usemi wako. Ni mambo gani yaliyotajwa hapa chini ambayo yatakuchochea uache kutumia matusi?

□ Kumpendeza Mwanzilishi wa usemi

□ Kuheshimiwa zaidi na wengine

□ Kuongeza msamiati wangu

□ Kuboresha utu wangu

Pili: Chunguza ni nini hukufanya utumie matusi. Melanie anasema: “Kutumia matusi hunifanya nijihisi jasiri kwa njia fulani. Sikutaka watu wanionee. Nilitaka kuwadhibiti watu, kuwakemea kama marafiki wangu wote walivyofanya.”

Namna gani wewe? Kuelewa ni kwa nini wewe hutumia matusi kutakusaidia kujua jinsi utakavyotatua tatizo hilo. Kwa mfano, ikiwa wewe hutumia matusi kwa sababu tu kila mtu anafanya hivyo, unahitaji kuwa na uhakika zaidi na sifa zako nzuri. Kujivunia ifaavyo msimamo wako ni sehemu muhimu ya ukuzi na kutakusaidia sana kushinda zoea la kutumia matusi.

Tatu: Tafuta njia nyingine za kujieleza. Hutaacha zoea la kutumia lugha chafu kwa kuzuia tu ulimi wako. Unapaswa kuvaa “utu mpya.” (Waefeso 4:22-24) Kufanya hivyo kutakusaidia ujizuie na kujiheshimu zaidi na pia uwaheshimu wengine.

Maandiko yafuatayo yatakusaidia kuvaa na kudumisha utu mpya.

Wakolosai 3:2: “Endeleeni kukaza akili zenu juu ya mambo yaliyo juu.”

Matumizi: Zoeza akili yako kuthamini mambo yaliyo manyoofu. Mawazo yako huathiri jinsi unavyozungumza.

Methali 13:20: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.”

Matumizi: Usemi wa marafiki wako unaweza kukuathiri.

Zaburi 19:14: “Maneno ya kinywa changu na kutafakari kwa moyo wangu na yawe yenye kupendeza mbele zako, Ee Yehova.”

Matumizi: Yehova huona jinsi tunavyotumia zawadi ya usemi.

Bado unahitaji msaada zaidi? Mbona usitumie chati iliyo hapa juu kuchunguza maendeleo yako na kuandika mara ambazo umetumia matusi? Utashangaa kuona jinsi unavyoweza kuboresha lugha yako!

MAMBO YA KUFIKIRIA

Kutumia matusi kunaweza kuamuaje

▪ ni nani watakaokuwa marafiki wako?

▪ ikiwa utaajiriwa kazi au la?

▪ jinsi watu wengine watakavyokuona?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina katika makala haya yamebadilishwa.

^ fu. 8 Wakristo wana sababu yenye nguvu ya kuepuka lugha chafu, kwa kuwa Biblia inasema: “Neno lililooza na lisitoke kinywani mwenu.” “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yenye kukolezwa chumvi.”—Waefeso 4:29; Wakolosai 4:6.

[Chati katika ukurasa wa 21]

CHUNGUZA MAENDELEO YAKO

Jumatatu Jumanne Jumatano Alhamisi Ijumaa Jumamosi Jumapili

Juma la 1 ․․․․․․ ․․․․․․․ ․․․․․․․․․ ․․․․․․․․ ․․․․․․ ․․․․․․․․ ․․․․․․

Juma la 2 ․․․․․․ ․․․․․․․ ․․․․․․․․․ ․․․․․․․․ ․․․․․․ ․․․․․․․․ ․․․․․․

Juma la 3 ․․․․․․ ․․․․․․․ ․․․․․․․․․ ․․․․․․․․ ․․․․․․ ․․․․․․․․ ․․․․․․

Juma la 4 ․․․․․․ ․․․․․․․ ․․․․․․․․․ ․․․․․․․․ ․․․․․․ ․․․․․․․․ ․․․․․․

[Picha katika ukurasa wa 20]

Huwezi kutumia vibaya zawadi unayothamini. Kwa nini utumie vibaya zawadi ya usemi?