Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Dunia Itakuwa Paradiso?

Je, Dunia Itakuwa Paradiso?

Maoni ya Biblia

Je, Dunia Itakuwa Paradiso?

JAMII nyingi za wanadamu zina hekaya kuhusu enzi bora, wakati ambapo mwanadamu hakuwa na dhambi, alikuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu, na hakukabili magonjwa na kifo. Baadhi ya jamii hizo ni Wamexico, Wamisri, Waperu, na Watibet. Hekaya hizo pia zinazungumzia jinsi dhambi ilivyoingia duniani.

Ijapokuwa zimepotoshwa na kutiliwa chumvi, hekaya hizo zinafanana sana hivi kwamba haiwezekani kuwa zilitungwa tu. Hilo limewafanya wengi wakate kauli kwamba zilitokana na matukio halisi ya kihistoria. Kwa kweli, mawazo makuu ya hekaya hizo yanafanana sana na masimulizi ya sura za kwanza za kitabu cha Biblia cha Mwanzo. Hata hivyo, masimulizi hayo hayana habari za kijuu-juu tu ambazo hupatikana katika hekaya, bali yana habari hususa ya historia sahihi.—2 Timotheo 3:16.

Mwanzo Mkamilifu

Kitabu cha Mwanzo kinatuambia kwamba Mungu alipowaumba wanadamu wa kwanza—Adamu na Hawa—aliwaweka kwenye bustani iliyonyweshwa maji vizuri ambayo iliitwa Bustani ya Edeni. Walikuwa na afya kamilifu na tarajio la kuishi milele. Kifo kilikuwa adhabu ya dhambi. (Mwanzo 2:8-17; Waroma 5:12) Adamu na Hawa ‘wangezaa wawe wengi, waijaze dunia na kuitiisha.’ (Mwanzo 1:28) Hilo lingefanya dunia yote iwe paradiso iliyojaa wanadamu wakamilifu wanaojitiisha chini ya Mungu, akiwa Mtawala wao.

Kwa kusikitisha, Adamu na Hawa walikosa kumtii Mungu, na hivyo wakapoteza fursa ya kutimiza kusudi la Muumba wao na tarajio lao la kuishi milele. Hata hivyo, Yehova Mungu atatimiza kusudi lake kwa dunia. “Neno langu linalotoka katika kinywa changu . . . halitarudi kwangu bila matokeo,” Yehova alisema, bali “hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.” (Isaya 55:11) Kwa kweli, kusudi la Yehova la kuifanya dunia kuwa makao ya kiparadiso kwa ajili ya wanadamu walio na sifa kama zake ni mojawapo ya habari muhimu iliyo katika Biblia.—Waroma 8:19-21.

“Utakuwa Pamoja Nami Katika Paradiso”

Punde baada ya Adamu na Hawa kufanya dhambi, Mungu aliahidi kutokeza “uzao,” au mbegu, ambayo hatimaye ingemwangamiza “yule nyoka wa zamani,” Shetani Ibilisi, na kuvunja kazi zake mbovu. (Mwanzo 3:15; Ufunuo 12:9; 1 Yohana 3:8) Yesu Kristo ndiye aliyekuja kuwa sehemu ya msingi ya “uzao” huo. (Wagalatia 3:16) Isitoshe, Mungu alimweka rasmi awe Mfalme wa Ufalme au serikali ya kimbingu, ambayo itatawala juu ya dunia.—Danieli 7:13, 14; Ufunuo 11:15.

Kristo atatimiza kikamili kile ambacho Adamu alishindwa kutimiza. Kwa kweli, Biblia inamwita Yesu “Adamu wa mwisho.” (1 Wakorintho 15:45) Zaidi ya hilo, katika sala yake ya kielelezo, Yesu alihusianisha wakati ujao wa dunia na Ufalme wa Mungu, aliposema hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”—Mathayo 6:10.

Yesu alipokuwa duniani, yeye—akiwa Mfalme ambaye angetawala dunia wakati ujao—kwa kufaa angeweza kumwambia hivi mtenda-maovu aliyetundikwa kando yake: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.” (Luka 23:43) Paradiso ambayo Yesu alikuwa akizungumzia ingekuwa hapa duniani, kama Mungu alivyokuwa amekusudia hapo awali. Hilo linaungwa mkono kabisa na Biblia. Fikiria maandiko yafuatayo.

“Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” (Zaburi 37:29) “Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani; juu ya milima kutakuwa na mafuriko.” (Zaburi 72:16) “Wanyoofu ndio watakaokaa duniani, na wasio na lawama ndio watakaobaki ndani yake.” (Methali 2:21) “[Wasio na lawama] hawatasababisha madhara yoyote wala kusababisha uharibifu wowote katika mlima wangu wote mtakatifu; kwa maana dunia hakika itajawa na kumjua Yehova kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:9.

Kupatana na taarifa hizo, katika Mahubiri yake ya Mlimani yaliyo maarufu, Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.” (Mathayo 5:5) Baadaye, mtume Yohana aliandika hivi: “Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu . . . Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:3, 4) Kwa wazi, maandiko hayo ya Biblia hayazungumzii “paradiso” ya kimbingu bali paradiso halisi hapa duniani.

Yale Ambayo Wasomi wa Biblia Wamesema

Wasomi wengi wa Biblia wanaamini kwamba chini ya Ufalme wa Kristo, dunia itakuwa paradiso. Mwanatheolojia Joseph A. Seiss alisema hivi: “Hatimaye lazima dunia yote chini ya Masihi iwe . . . kile ambacho . . . ingekuwa iwapo Adamu hangefanya dhambi.” Katika kitabu The New Testament for English Readers, Henry Alford aliandika hivi: “Ufalme huo wa Mungu . . . utaendelea kufanya kazi mpaka utakapokuwa ufalme juu ya dunia hii, na raia wake watairithi dunia . . . , ikiwa hatimaye katika hali yake mpya na iliyobarikiwa milele.”—Italiki ni zake.

Hali kadhalika, Isaac Newton, mwanasayansi maarufu aliyejifunza Biblia kwa bidii aliandika: “Dunia itaendelea kukaliwa na wanadamu baada ya siku ya hukumu na si kwa miaka 1000 tu, bali milele.”

Kwa kuwa dunia itakuja kuwa chini ya utawala wa Yesu Kristo, uovu hautatokea tena. (Isaya 11:1-5, 9) Naam, dunia yote itakuwa paradiso, na hivyo kumletea Muumba wake sifa milele.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Ni nini lililokuwa kusudi la Mungu la awali kwa wanadamu na dunia?—Mwanzo 1:28.

▪ Ufalme wa Mungu utatimiza nini?—Mathayo 6:10.

▪ Kwa nini uovu hautatokea tena?—Isaya 11:1-5, 9.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

“Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.”—Mathayo 5:5