Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Si Vifaa vya Kuchezea Tu

Si Vifaa vya Kuchezea Tu

Si Vifaa vya Kuchezea Tu

WAMISRI walivitengeneza wakitumia vipande bapa vya mbao, Wajapani walitumia karatasi zilizokunjwa, Wajerumani walitumia udongo, na Waeskimo walitumia ngozi ya sili. Watu wazima huvikusanya. Watoto wanavipenda sana. Tunazungumzia nini? Wanasesere.

Kitabu The World Book Encyclopedia kinasema: “Vitu vingi vya kale vinavyofanana na wanasesere vilikuwa vya kichawi au vya kidini, wala havikuwa vifaa vya kuchezea.” Wamisri wa kale walibandika vitambaa maridadi kwenye vipande vidogo vya mbao na kuvipamba kwa nyuzi za shanga zilizotengenezwa kwa udongo zikiwakilisha nywele. Waliweka “wanasesere” hao ndani ya makaburi ya wapendwa wao wakiamini kwamba wangekuwa watumishi katika maisha yao baada ya kifo. Watu waliotaka kulipiza kisasi huko West Indies walidunga wanasesere wa kichawi kwa sindano wakitumaini kwamba wangewadhuru maadui wao.

Katika jamii nyingi, wanasesere walihusianishwa na sherehe za uzazi. Kwa mfano, muda mfupi kabla ya kuolewa wasichana katika nchi ya kale ya Ugiriki waliacha wanasesere wao kwenye madhabahu ya Artemi, mungu wa kike wa uzazi. Leo wanawake wa kabila la Ashanti huko Ghana, barani Afrika, hufungilia mwanasesere kiunoni wakitumaini kwamba atawasaidia kupata watoto warembo. Wasichana fulani huko Syria huning’iniza wanasesere katika madirisha yao ili kuonyesha kwamba wamefikia umri wa kuolewa.

Machi tarehe 3 kila mwaka huko Japani, wanasesere hutumiwa katika sherehe inayoitwa Hina Matsuri, au Sherehe ya Mwanasesere. Pia inaitwa sherehe ya wasichana, nayo “inatokana na desturi kadhaa zilizo tofauti,” kinasema kitabu Japan—An Illustrated Encyclopedia. “Mojawapo ya desturi hizo ni desturi ya Kichina ya utakaso iliyofanywa kandokando ya mto mwanzoni mwa mwezi wa tatu. Wakati wa enzi ya Heian (794-1185) katika siku ya tatu ya mwezi wa tatu, watumishi wa makao ya mfalme waliwaita waaguzi ili wawaondolee uchafu na kuuhamishia kwenye maumbo ya karatasi . . . , ambayo yalitupwa mtoni au baharini.”

Vifaa vya Kuchezea

Katika enzi ya Edo huko Japani (1603-1867), wanasesere waliotengenezwa hasa kwa ajili ya watoto walikuwa na maumbo ya watu halisi wakiwa na nguo tofauti-tofauti. Wanasesere wengine wangeweza kusogezwa kwa kutumia nyaya, springi, makapi, na magurudumu ya mbao. Hata mwanasesere fulani angeweza kumpelekea mgeni kikombe cha chai na kurudi na kikombe kitupu.

Katika nchi za Magharibi kabla ya miaka ya 1700, “watoto hawakuwa na maisha kama ya watoto wa leo,” yasema ensaiklopidia moja. “Watoto walionwa kuwa watu wazima wadogo, na hivyo walitarajiwa kutenda kama watu wazima.” Wanasesere walitengenezwa kwa ajili ya watu wazima na watoto pia. Hata hivyo, katika miaka ya 1800, watu walitambua umuhimu wa mchezo katika ukuzi wa mtoto. Kwa sababu hiyo, biashara ya wanasesere ilisitawi huko Ulaya.

Mapema katika mwaka wa 1824, watengenezaji wa wanasesere huko Ujerumani walibuni kifaa kilichowezesha wanasesere kusema “mama” na “baba.” Baadaye katika karne hiyo, walitengeneza wanasesere walioweza kutembea. Mbuni Mwamerika Thomas Edison, alitengeneza redio ndogo sana iliyofanya wanasesere fulani waonekane kana kwamba wanaongea. Wakati huohuo, Wafaransa walitengeneza mwanasesere aliyeitwa Bébé Gourmand, ambaye angeweza kula chakula. Wafaransa walikuwa maarufu pia kwa kutengeneza wanasesere waliouzwa wakiwa wamevishwa nguo maridadi za kimtindo. Wanunuzi wangeweza pia kuwanunulia wanasesere hao vitu kama vile vichana, fulana, feni, na fanicha.

Katika karne ya 20 utengenezaji wa wanasesere uliongezeka kuliko wakati mwingine wowote. Katika miaka ya 1940, kutumia plastiki kulifanya iwezekane kutokeza wanasesere ambao walitengenezwa kwa ustadi lakini waliouzwa kwa bei ya chini. Mwanasesere anayeitwa Barbie amekuwa maarufu sana katika biashara ya wanasesere tangu alipotengenezwa mnamo 1959. Zaidi ya wanasesere bilioni moja wa aina hiyo wameuzwa, na katika mwaka wa 1997 pekee, walichuma dola bilioni 1.8 (za Marekani).

Vifaa vya Kufundishia

Ili kuwafundisha watoto wao kuhusu miungu ya kabila lao, Wahindi wa Pueblo wanaoishi kusini-magharibi mwa Marekani walitumia wanasesere wa kachina, waliochongwa kutokana na mizizi ya dungusi au msonobari. Katika sherehe maalumu, mtu wa kabila hilo alivaa na kutenda kama mmoja wa miungu yao. Baadaye, wazazi waliwapa watoto wao wanasesere waliofanana na mungu huyo ili kadiri walivyocheza naye, wapate kumfahamu zaidi.

Wanasesere “walimsaidia mtoto kuonyesha uchungu, hasira, na hisia nyingine,” chasema kitabu The World Book Encyclopedia. “Kucheza na wanasesere kunawawezesha watoto kufanya mazoezi ya wajibu wanaotazamia kutimiza wakiwa watu wazima.” Mwanasesere mmoja aliyeonyeshwa katika Sherehe ya Siku ya Watoto inayofanywa huko Japani kila mwaka katika Mwezi wa 5, anafanana na mwanamume aliyevaa mavazi kamili ya silaha za shujaa wa jamii hiyo. Mwanasesere huyo anatumiwa kuwa kielelezo cha kuwahimiza wavulana, kulingana na tamaduni za jamii yao, watamani kuwa watu wazima wenye nguvu na wanaoheshimika katika jamii.

Kwa sababu ya uhusiano wa kihisia kati ya watoto na wanasesere wao, wazazi wenye hekima watachukua kwa uzito uvutano wa wanasesere juu ya ukuzi wa mtoto wao. Kwa mfano, wengine wanasema kwamba sura za wanasesere fulani na nguo zao nyingi zinaweza kuwa na uvutano mbaya juu ya wasichana. Mchambuzi mmoja anadai kwamba wanasesere kama hao wanaweza kuwapotosha “wasichana wachanga na kuwafanya wapendezwe na mitindo kuliko utu wao.”

Jambo lililo wazi kwa yeyote ambaye amewahi kuwaona watoto wakicheza na wanasesere, iwe wametengenezwa kwa vitambaa, karatasi, mbao, plastiki, au kitu kingine, ni kwamba mwanasesere si kifaa cha kuchezea tu. Ni rafiki, mchezaji mwenzi, na hata msiri wa mtoto katika maisha ya utotoni.

[Sanduku katika ukurasa wa 27]

Kupendezwa Tena na Wanasesere wa Zamani

Kukusanya wanasesere kumekuwa maarufu sana. Katika miaka ya 1970, watu wengi walianza kukusanya wanasesere na hivyo kutokeza biashara ya kimataifa. Wakusanyaji wanatafuta wanasesere wa plastiki walio na thamani ya dola chache tu au wanasesere wasiopatikana kwa urahisi kama wanaotengenezwa na kampuni ya Kämmer na Reinhardt. Wanasesere hao walitengenezewa Ujerumani miaka ya 1900, na mmoja wao aliuzwa katika mnada kwa dola 277,500! Jumba la Makumbusho la Kitaifa la Strong la Michezo katika jiji la Rochester, New York, Marekani lina wanasesere 12,000 hivi, mojawapo ya idadi kubwa zaidi ya wanasesere.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 28]

Wanasesere—Kwa Nini Wazazi Wahangaike

Wazazi wanaweza kuwalindaje watoto wao wasiathiriwe vibaya na wanasesere fulani? Gazeti The Washington Post lilisema hivi: “Kama tu watengenezaji wa sigara walivyokuwa wakifanya, wafanyabiashara wa burudani na watengenezaji wa vifaa vya kuchezea hawakubali kuwajibika na wasiposhinikizwa haielekei watafanya mabadiliko yoyote.” Ni wazi kwamba wazazi wanahitaji kutimiza wajibu wao.

Biblia inawaamuru wazazi wawafundishe watoto inavyofaa kila siku. (Kumbukumbu la Torati 6:6-9; Methali 22:6) Wazazi wanaweza kuwafundishaje watoto ili wasiathiriwe na wanasesere fulani? Mama mmoja alisema kwamba alimsomea binti yake 1 Timotheo 2:9 inayozungumzia kuvaa kwa kiasi na kujadiliana naye kuhusu jambo hilo. Mazungumzo yao yalikuwa kama haya:

Mama: Wanasesere hawa wanafanana na nani, mtoto au mwanamke?

Binti: Mwanamke.

Mama: Kwa nini unasema hivyo?

Binti: Kwa sababu wana miili kama ya wanawake, na nguo na viatu vyao ni kama vya wanawake.

Mama: Umesema kweli. Kulingana na yale tuliyosoma katika Biblia, unafikiri nguo ambazo wanasesere hao wamevaa zinawafaa Wakristo?

Binti: Hapana.

Mama: Kwa nini?

Binti: Kwa sababu sketi zao ni fupi sana, . . . blauzi zao hazisitiri, . . . na mavazi yao yamewabana sana.

Kwa kweli, ili watoto wako wakate kauli kama hizo jitihada zinahitajiwa kuwafundisha kanuni za kimungu. Lakini jitihada hizo zitathawabishwa. Wazazi wengi wamenufaika na msaada unaopatikana katika kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova ili kuwasaidia wazazi wakazie kanuni za Biblia kwa watoto wao.

Unaweza kupata kitabu hiki chenye picha kilicho na kurasa 256 kwa kuwaandikia Mashahidi wa Yehova, P. O. Box 21290, 00505 Nairobi, Kenya. Andika kwamba ungependa kupokea kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mwanasesere wa Japani anayewaandalia watu chai

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mwanasesere wa Ufaransa anayeitwa Bru

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 26]

Top: ©SHOBEI Tamaya IX; middle: Courtesy, Strong National Museum of Play, Rochester, New York; bottom: © Christie’s Images Ltd