Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | UKWELI KUHUSU MAONO YA MBINGUNI

Maono Kuhusu Wale Wanaoishi Mbinguni

Maono Kuhusu Wale Wanaoishi Mbinguni

Biblia inataja maono yenye kustaajabisha ambayo yanatusaidia kuelewa jinsi makao ya kiroho yalivyo. Tunakutia moyo uchunguze kwa makini maono hayo. Ingawa baadhi ya mambo katika maono hayo si halisi, yatakusaidia kuwajua wale wanaoishi mbinguni na jinsi wanavyohusika maishani mwako.

YEHOVA NDIYE MKUU ZAIDI

“Kiti cha ufalme kilikuwa mahali pake mbinguni, na kuna yule aliyeketi juu ya kile kiti cha ufalme. Na yule aliyeketi, kuonekana kwake ni kama jiwe la yaspi na jiwe jekundu la thamani, na upinde wa mvua ambao kuonekana kwake ni kama zumaridi unakizunguka kile kiti cha ufalme.”​—Ufunuo 4:2, 3.

“Naye alikuwa na mwangaza kuzunguka pande zote. Kulikuwa na kitu kinachoonekana kama upinde ambao hutokea katika wingu kubwa katika siku ya mvua. Hivyo ndivyo ulivyokuwa mwangaza uliozunguka pande zote. Kulikuwa ni kuonekana kwa mfano wa utukufu wa Yehova.”​—Ezekieli 1:27, 28.

Maono hayo ya mtume Yohana na nabii Ezekieli yanaonyesha utukufu wa Mungu Mkuu Zaidi, Yehova, na tunaweza kuyaelewa kwa sababu yanataja vitu tunavyojua, kama vile, mawe ya thamani yenye kung’aa, upinde wa mvua na ukuu wa kiti cha enzi. Maono hayo yanaonyesha kwamba makao ya Yehova yanavutia na ni matulivu sana.

Ufafanuzi huo kumhusu Mungu unapatana na maneno haya ya mtunga zaburi: “Kwa maana Yehova ni mkuu na wa kusifiwa sana. Ni mwenye kuogopesha kuliko miungu mingine yote. Kwa maana miungu yote ya vikundi vya watu ni miungu isiyo na thamani; lakini Yehova, amezifanya mbingu. Utukufu na fahari ziko mbele zake; nguvu na uzuri zipo katika patakatifu pake.”—Zaburi 96:4-6.

Licha ya kwamba Yehova ni Mkuu Zaidi, anatualika tumkaribie kupitia sala na anatuhakikishia kwamba atatusikiliza. (Zaburi 65:2) Mungu anatupenda na kutujali sana hivi kwamba mtume Yohana aliandika hivi kwa unyofu: “Mungu ni upendo.”—1 Yohana 4:8.

YESU ANAISHI MBINGUNI

“[Mwanafunzi Mkristo Stefano], akiwa amejaa roho takatifu, akakaza macho mbinguni, akaona utukufu wa Mungu na wa Yesu akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume wa Mungu, naye akasema: ‘Tazameni! Ninaziona mbingu zimefunguka na Mwana wa binadamu akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume wa Mungu.’”—Matendo 7:55, 56.

Kabla ya ono hilo, Yesu alikuwa ameuawa kutokana na uchochezi wa viongozi Wayahudi ambao sasa Stefano alikuwa akizungumza nao. Ono hilo lilithibitisha kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa na kupewa cheo cha juu. Mtume Paulo alieleza hivi: ‘[Yehova] alimfufua [Yesu] kutoka kwa wafu na kumketisha kwenye mkono wake wa kuume katika mahali pa kimbingu, juu zaidi kuliko kila serikali na mamlaka na nguvu na utawala na kila jina linalotajwa, si katika mfumo huu wa mambo tu, bali pia katika ule ujao.’—Waefeso 1:20, 21.

Zaidi ya kueleza kuhusu cheo chake cha juu, Maandiko yanaonyesha kwamba, kama alivyo Yehova, Yesu anawajali sana wanadamu. Alipokuwa duniani, Yesu aliwaponya wagonjwa, walemavu, na kufufua wafu. Pia, alionyesha kwamba anampenda sana Mungu na wanadamu kwa kutoa uhai wake uwe dhabihu. (Waefeso 2:4, 5) Hivi karibuni, Yesu, akiwa kwenye mkono wa kuume wa Mungu, atatumia mamlaka yake kuwaletea wanadamu watiifu hapa duniani baraka nyingi.

MALAIKA WANAMTUMIKIA MUNGU

Nabii Danieli alisema hivi: “Nikaendelea kutazama mpaka viti vya ufalme vikawekwa na Mzee wa Siku [Yehova] akaketi. . . . Kulikuwa na maelfu elfu walioendelea kumtumikia, na elfu kumi mara elfu kumi walioendelea kusimama mbele zake.”—Danieli 7:9, 10.

Katika ono hilo, Danieli aliona maelfu ya malaika wakiwa mbinguni. Bila shaka, hilo lilikuwa ono lenye kustaajabisha sana! Malaika ni viumbe wa kiroho wenye utukufu, nguvu, na akili nyingi. Malaika hao wanatia ndani maserafi na makerubi. Biblia inawataja malaika zaidi ya mara 250.

Malaika si wanadamu walioishi duniani zamani. Mungu aliwaumba malaika muda mrefu kabla ya kuwaumba wanadamu. Dunia ilipoumbwa, malaika walipaaza sauti na kushangilia.—Ayubu 38:4-7.

Malaika waaminifu wanamtumikia Mungu kwa kushiriki katika kazi muhimu inayofanywa duniani, yaani, kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14) Katika maono, mtume Yohana aliona jinsi malaika wanavyoshiriki katika kazi ya kuhubiri, na aliandika hivi: “Nami nikamwona malaika mwingine akiruka katikati ya mbingu, naye alikuwa na habari njema ya milele ili aitangaze kuwa habari za furaha kwa wale wanaokaa duniani, na kwa kila taifa na kabila na lugha na watu.” (Ufunuo 14:6) Ingawa siku hizi malaika hawazungumzi na wanadamu kama zamani, wao huwaongoza wahubiri wa habari njema kuwahubiria watu wanyofu.

SHETANI HUPOTOSHA MAMILIONI YA WATU

“Na vita vikatokea ghafula mbinguni: Mikaeli [Yesu Kristo] na malaika zake wakapigana na yule joka mkubwa, naye joka mkubwa na malaika zake wakapigana lakini hakushinda, wala mahali hapakupatikana mbinguni kwa ajili yao tena. Kwa hiyo yule joka mkubwa akatupwa chini, yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa; akatupwa chini duniani, na malaika zake wakatupwa chini pamoja naye.”—Ufunuo 12:7-9.

Kuna wakati ambapo mbinguni hakukuwa na amani. Mwanzoni kabisa mwa historia ya wanadamu, malaika mmoja alitamani kuabudiwa na hivyo akamwasi Yehova na kuwa Shetani, jina linalomaanisha “Mpinzani.” Baadaye, malaika wengine waliasi pia nao wakawa roho waovu. Ni waovu sana, nao humpinga Yehova na wamewapotosha watu wengi wasifuate mwongozo wenye upendo wa Yehova.

Shetani na roho wake ni waovu na wakatili. Wao ni adui za wanadamu, nao husababisha mateso mengi duniani. Kwa mfano, Shetani aliwaua watumishi na mifugo ya mwanamume mwaminifu Ayubu. Kisha, akawaua watoto wote kumi wa Ayubu kwa kuleta “upepo mkubwa” ambao ulivunja nyumba walimokuwa. Mwishowe, Shetani alimpiga Ayubu kwa “majipu hatari kuanzia wayo wa mguu wake mpaka kwenye utosi wa kichwa chake.”—Ayubu 1:7-19; 2:7.

Hata hivyo, hivi karibuni Shetani ataharibiwa. Tangu alipotupwa duniani, anajua kwamba “ana kipindi kifupi cha wakati.” (Ufunuo 12:12) Ni habari njema kujua kwamba Shetani ataangamizwa!

WALE WANAOTOKA DUNIANI

‘Wewe [Yesu] ulimnunulia Mungu watu kutoka katika kila kabila na lugha na watu na taifa, nawe ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu, nao watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.’—Ufunuo 5:9, 10.

Kama vile Yesu alivyofufuliwa na kwenda mbinguni, wengine pia wanaenda mbinguni. Yesu aliwaambia hivi mitume wake waaminifu: “Ninaenda kuwatayarishia ninyi mahali. Pia, . . . nitakuja tena nami nitawapokea ninyi nyumbani kwangu mwenyewe, ili mahali nilipo mimi, ninyi pia muwe hapo.”—Yohana 14:2, 3.

Wanadamu wanaoenda mbinguni wanaenda huko kwa kusudi fulani. Wakiwa pamoja na Yesu, watafanyiza Ufalme ambao hatimaye utaitawala dunia yote na kuwaletea baraka wanadamu. Huo ndio Ufalme ambao Yesu aliwaambia wanafunzi wake wasali kuuhusu katika sala ya mfano aliposema hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”—Mathayo 6:9, 10.

MAMBO AMBAYO WALE WALIO MBINGUNI WATAFANYA

Mtume Yohana alisema hivi: “Ndipo nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha ufalme ikisema: ‘Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, . . . naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.’”—Ufunuo 21:3, 4.

Maono hayo ya kinabii yanahusu wakati ambao Ufalme wa Mungu, utakaofanyizwa na Yesu na wale waliofufuliwa kutoka duniani, utaangamiza utawala wa Shetani na kuifanya dunia iwe paradiso. Mambo ambayo yamewasababishia wanadamu maumivu mengi na huzuni hayatakuwapo tena. Hata kifo kitaondolewa.

Namna gani mabilioni ya watu waliokufa ambao hawana tumaini la kwenda kuishi mbinguni? Wakati ujao, watafufuliwa wakiwa na tumaini la kuishi milele katika Paradiso duniani.—Luka 23:43.

Maono hayo yanatuthibitishia kwamba Yehova Mungu, Mwana wake Yesu Kristo, malaika waaminifu, na wale walionunuliwa kutoka duniani, wanatujali sana na kuhangaikia hali yetu. Ili ujifunze mengi zaidi kuhusu mambo watakayofanya, tafadhali wasiliana na Mashahidi wa Yehova au tembelea tovuti ya, www.pr418.com/sw na upakue kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?