Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Korongo

Mambo Tunayojifunza Kutokana na Ndege wa Mbinguni

Mambo Tunayojifunza Kutokana na Ndege wa Mbinguni

“Tafadhali uliza . . . viumbe vya mbinguni vyenye mabawa, navyo vitakuambia. Ni nani kati ya hao wote ambaye hajui vema kwamba ni mkono wa Yehova ambao umefanya haya?”—Ayubu 12:7, 9.

ZAIDI ya miaka 3,000 iliyopita, mwanamume mwaminifu Ayubu alitambua kwamba tunaweza kujifunza mengi kuhusu uumbaji wa Mungu kupitia ndege. Tabia za ndege hufanya watumiwe katika mifano na vielelezo. Katika Biblia, kuna habari nyingi kuhusu ndege ambazo zinatufundisha kuhusu maisha na uhusiano wetu pamoja na Mungu. Acheni tuchunguze mifano michache.

MAHALI AMBAPO MBAYUWAYU HUJENGA VIOTA

Mbayuwayu

Wakazi wa Yerusalemu waliwafahamu vizuri mbayuwayu, ambao kwa kawaida hujenga viota vyao chini ya paa za nyumba. Baadhi yao walijenga viota kwenye hekalu la Sulemani. Inaelekea kwamba, mbayuwayu ambao kila mwaka walijenga viota vyao hekaluni waliona mahali hapo kuwa salama, na wangeweza kulea makinda yao bila kusumbuliwa.

Mwandikaji wa Zaburi ya 84, mmoja wa wana wa Kora, ambaye alitumikia hekaluni kwa juma moja kila baada ya miezi sita aliona viota hivyo. Alitamani kuwa kama mbayuwayu ambao walikuwa na makao ya kudumu katika nyumba ya Yehova. Alisema hivi: “Jinsi ilivyo nzuri maskani yako kuu, Ee Yehova wa majeshi! Nafsi yangu imetamani sana na pia imedhoofika kwa kutamani nyua za Yehova. Hata ndege amepata nyumba, na mbayuwayu amepata kiota chake, ambapo ameweka vifaranga vyake—Madhabahu yako kuu, Ee Yehova wa majeshi, Mfalme wangu na Mungu wangu!” (Zaburi 84:1-3) Je, sisi pamoja na watoto wetu, tuna tamaa hiyohiyo na tunathamini kushirikiana kwa ukawaida na kutaniko la watu wa Mungu?—Zaburi 26:8, 12.

KORONGO ANAJUA MAJIRA YAKE

Nabii Yeremia aliandika, ‘Korongo wa mbinguni anajua nyakati zake.’ Bila shaka, Yeremia alielewa vizuri jinsi korongo wanavyohamahama na kupita katika Nchi ya Ahadi. Katika majira ya kuchipua, korongo weupe zaidi ya 300,000 husafiri kutoka Afrika kuelekea Ulaya Kaskazini kupitia Bonde la Yordani. Uwezo wao wa asili huwawezesha kutambua majira ya kiangazi na hivyo kurudi eneo lao la kutagia mayai. Kama ndege wengine wanaohamahama, korongo “huangalia vema wakati wa kila mmoja wao kuingia.”—Yeremia 8:7.

Kitabu Collins Atlas of Bird Migration kinasema hivi: “Kinachostaajabisha ni kwamba kuhama kwa ndege hao ni jambo la kisilika.” Yehova Mungu amewapa ndege hekima ya kisilika kutambua majira ya kuhama, lakini amewapa wanadamu uwezo wa kutambua wakati na majira. (Luka 12:54-56) Tofauti na hekima ya kisilika ya korongo, ujuzi kutoka kwa Mungu huwawezesha wanadamu kutambua maana ya matukio ya sasa. Waisraeli wa siku za Yeremia hawakutambua ishara katika siku zao. Mungu alieleza sababu iliyowafanya watende hivyo aliposema hivi: “Wamelikataa neno la Yehova, nao wana hekima gani?”—Yeremia 8:9.

Leo, kuna mambo mengi yanayothibitisha kwamba tunaishi katika kipindi ambacho Biblia inakiita “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5) Je, utamwiga korongo kwa kutambua ‘majira?’

TAI HUONA MBALI SANA

Tai

Tai wametajwa mara nyingi katika Biblia, nao walionekana kwa ukawaida katika Nchi ya Ahadi. Akiwa kwenye kiota chake juu ya mwamba, tai “hutafuta chakula; Macho yake huendelea kutazama mbali sana.” (Ayubu 39:27-29) Uwezo wa kuona wa tai ni wa pekee sana, hivi kwamba anaweza kumwona sungura akiwa umbali wa kilometa moja.

Kama vile tai anavyoweza “kutazama mbali sana,” Yehova ana uwezo wa kuona mambo ya wakati ujao. Yehova alisema hivi: “Yeye anayetangaza tangu mwanzo ule mwisho, na kutoka zamani za kale mambo ambayo hayajafanywa.” (Isaya 46:10) Kwa kutii mashauri ya Yehova, tunaweza kunufaika na hekima yake nyingi na uwezo wa kuona mambo kimbele.—Isaya 48:17, 18.

Pia, Biblia inalinganisha wale wanaomtumaini Mungu na tai kwa kusema: “Wale wanaomtumaini Yehova watapata nguvu mpya. Wataruka juu kwa mabawa kama tai.” (Isaya 40:31) Hewa yenye joto humwezesha tai kuruka kwa urahisi. Mara tu anapoifikia, tai hutanua mabawa yake na kuzunguka ndani ya mkondo huo wa hewa, na hivyo kupaa juu zaidi na zaidi. Kwa hiyo, tai hategemei nguvu zake kuruka na kupaa. Kama tai, wale wanaomtumaini Yehova wanaweza kumtegemea kwa kuwa ameahidi kwamba atawapa “nguvu zinazopita zile za kawaida.”—2 Wakorintho 4:7, 8.

“KAMA VILE KUKU ANAVYOKUSANYA VIFARANGA VYAKE”

Kuku na vifaranga

Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alisimama na kutazama jiji kuu la Wayahudi. Kisha, akasema hivi kwa uchungu: “Yerusalemu, Yerusalemu, muuaji wa manabii na ambaye huwapiga kwa mawe wale waliotumwa kwake, ni mara ngapi nilitaka kuwakusanya watoto wako, kama vile kuku anavyokusanya vifaranga vyake chini ya mabawa yake! Lakini hamkutaka.”—Mathayo 23:37.

Kwa kawaida ndege hujitahidi sana kulinda makinda yao. Ndege wanaojenga viota vyao ardhini, kama vile kuku, lazima wawe macho dhidi ya hatari. Kuku anapomwona mwewe angani hutoa sauti ya kuonya, na mara moja vifaranga hukimbilia chini ya mabawa yake, mahali salama. Pia, vifaranga wanaweza kujificha humo ili wasiathiriwe na mvua au jua kali. Vivyo hivyo, Yesu alitaka kuandaa makao na ulinzi wa kiroho kwa wakazi wa Yerusalemu. Leo, Yesu anatualika tupate burudisho na ulinzi ili tusilemewe na mizigo na mahangaiko ya maisha.—Mathayo 11:28, 29.

Kwa kweli, kuna mengi tunayoweza kujifunza kutoka kwa ndege. Unapochunguza tabia zao, kumbuka mifano ya Kimaandiko kuhusu viumbe hao. Mbayuwayu hutukumbusha kwamba tunapaswa kuthamini nyumba ya Yehova ya ibada. Mtegemee Mungu ili uwe na tumaini litakalokuwezesha kupaa kama tai. Mfuate Yesu na kupata kweli za kiroho zitakazokulinda kama kuku anavyolinda vifaranga wake. Mfano wa korongo na ukusaidie kuwa macho na kuelewa maana ya matukio ya ulimwengu katika kipindi tunachoishi.