Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Usiruhusu Chochote Kikuzuie Kupata Utukufu

Usiruhusu Chochote Kikuzuie Kupata Utukufu

“Yeye aliye na roho ya unyenyekevu atapata utukufu.”MET. 29:23.

1, 2. (a) Maneno ya Kiebrania yanayotafsiriwa “utukufu” yanamaanisha nini? (b) Ni maswali gani tutakayochunguza katika makala hii?

UNAPOSIKIA neno “utukufu,” wewe hufikiria nini? Je, unafikiria fahari ya uumbaji wenye kuvutia? (Zab. 19:1) Au sifa na heshima wanayoonyeshwa wanadamu wenye utajiri mwingi, hekima nyingi, au ufanisi maishani? Katika Maandiko, maneno ya Kiebrania yanayotafsiriwa “utukufu” yanatoa wazo la uzito. Katika nyakati za kale, wakati ambapo pesa zilitengenezwa kutokana na madini, sarafu yenye uzito zaidi ndiyo iliyokuwa na thamani zaidi. Maneno yaliyotumiwa kutoa wazo la uzito yalieleweka kwa njia ya mfano kumaanisha kitu kinachothaminiwa, chenye fahari, au chenye kuvutia sana.

2 Ingawa huenda tukavutiwa na uwezo, mamlaka, au sifa za mtu mwingine, Mungu hutafuta nini katika wanadamu? Kwa kweli, Maandiko yanasema kwamba Mungu huwapa wanadamu utukufu. Kwa mfano, Methali 22:4 inasema hivi: “Matokeo ya unyenyekevu na kumwogopa Yehova ni utajiri na utukufu na uzima.” Naye mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Jinyenyekezeni machoni pa Yehova, naye atawainua ninyi.” (Yak. 4:10) Yehova huwapa wanadamu utukufu wa aina gani? Ni nini kinachoweza kutuzuia kuupata? Na tunawezaje kuwasaidia wengine kupata utukufu huo?

3-5. Yehova anaweza kutuongoza kupata utukufu gani?

3 Mtunga-zaburi alikuwa na uhakika kwamba Yehova angeushika mkono wake wa kuume na kumwongoza ili apate utukufu wa kweli. (Soma Zaburi 73:23, 24.) Yehova hufanyaje hivyo? Yehova huwaongoza watumishi wake wanyenyekevu kupata utukufu kwa kuwaheshimu kwa njia mbalimbali. Yeye huwabariki kwa kuwasaidia waelewe mapenzi yake. (1 Kor. 2:7) Anawaheshimu wale wanaosikiliza Neno lake na kumtii kwa kuwaruhusu wawe na uhusiano wa karibu na wa kibinafsi pamoja naye.—Yak. 4:8.

 4 Pia, Yehova huwakabidhi watumishi wake hazina tukufu ya huduma ya Kikristo. (2 Kor. 4:1, 7) Na huduma hiyo huwaletea utukufu. Yehova anawaahidi hivi wale wanaotumia pendeleo lao la utumishi kumsifu na kuwanufaisha wengine: “Wale wanaoniheshimu nitawaheshimu.” (1 Sam. 2:30) Watu kama hao wanaheshimiwa kwa kuwa na jina zuri mbele za Yehova, na inaelekea kwamba watakuwa na sifa nzuri mbele za watumishi wengine wa Mungu.—Met. 11:16; 22:1.

5 Wale ‘wanaomtumaini Yehova na kuishika njia yake’ watafurahia hali gani wakati ujao? Wanaahidiwa hivi: “[Yehova] atakuinua uimiliki dunia. Watu waovu watakapokatiliwa mbali, wewe utaona hilo.” (Zab. 37:34) Wanatazamia kwa hamu heshima isiyo na kifani ya kupewa uzima wa milele.—Zab. 37:29.

“MIMI SIUKUBALI UTUKUFU KUTOKA KWA WANADAMU”

6, 7. Kwa nini watu wengi hawakutaka kumwamini Yesu?

6 Ni nini kinachoweza kutuzuia tusipate utukufu ambao Yehova yuko tayari kutupatia? Jambo moja ni kufuata maoni ya wale ambao hawana msimamo mzuri pamoja na Mungu. Fikiria yale aliyoandika mtume Yohana kuhusu watu fulani waliokuwa na mamlaka katika siku za Yesu: “Wengi hata kati ya watawala kwa kweli walimwamini [Yesu], lakini kwa sababu ya Mafarisayo wakawa hawamkiri, ili wasifukuzwe katika sinagogi; kwa maana waliupenda utukufu wa wanadamu kuliko hata utukufu wa Mungu.” (Yoh. 12:42, 43) Ingekuwa bora kama nini ikiwa watawala hao hawangethamini maoni ya Mafarisayo!

7 Mwanzoni mwa huduma yake, Yesu alitaja wazi sababu ambazo zingefanya watu wengi wamkatae na kukosa kumwamini. (Soma Yohana 5:39-44.) Kwa karne nyingi, taifa la Israeli lilikuwa likingoja kwa hamu kuja kwa Masihi. Yesu alipoanza kufundisha, huenda watu fulani walitambua kutokana na unabii wa Danieli kwamba wakati uliowekwa wa kutokea kwa Kristo ulikuwa umefika. Miezi kadhaa mapema wakati Yohana Mbatizaji alipokuja akihubiri, wengi walikuwa wakisema: “Je, labda yeye ndiye Kristo?” (Luka 3:15) Sasa Masihi waliyemngoja kwa muda mrefu alikuwa akifundisha katikati yao. Lakini wale walioijua vizuri Sheria hawakumkubali. Akifunua wazi sababu iliyofanya wasimwamini, Yesu aliwauliza hivi: “Mtawezaje kuamini, wakati ninyi mnakubali utukufu kutoka kwa mtu na mwenzake na hamtafuti utukufu unaotoka kwa Mungu wa pekee?”

8, 9. Ukitumia mfano wa mwangaza, eleza jinsi utukufu wa wanadamu unavyofunika utukufu unaotoka kwa Mungu.

8 Ili tuelewe jinsi utukufu wa wanadamu unavyoweza kufunika utukufu unaotoka kwa Mungu, acheni tulinganishe utukufu na nuru. Ulimwengu wetu maridadi unavutia sana. Je, unakumbuka mara ya mwisho ulipotazama anga la usiku wakati ambapo hakukuwa na mawingu na kuona maelfu ya nyota? “Utukufu wa nyota” unastaajabisha sana. (1 Kor. 15:40, 41) Hata hivyo, unapotazama angani ukiwa katika jiji lenye taa nyingi, anga hilo linaonekanaje? Taa hizo hufanya iwe vigumu sana kuona mwangaza wa nyota zilizo mbali! Je, ni kwa sababu taa zilizo barabarani, katika viwanja vya michezo, na majengo yaliyo karibu zina mwangaza mwingi sana au zinavutia zaidi kuliko mwangaza wa nyota? Hapana! Hatuoni vizuri mwangaza wa nyota kwa sababu taa za mjini ziko karibu sana na hivyo zinatuzuia kuona vizuri uumbaji wa Yehova. Ili tujionee vizuri maajabu ya anga la usiku, ni lazima tuufunike kwa njia fulani au tuuepuke mwangaza wa taa unaotuzuia kuona.

9 Vivyo hivyo, ikiwa tunapenda sana moyoni utukufu usiofaa, utukufu huo unaweza kutuzuia tusithamini na tusitafute utukufu  unaodumu ambao Yehova yuko tayari kutupatia. Watu wengi hukataa ujumbe wa Ufalme kwa sababu wanaogopa maoni ya marafiki au watu wao wa ukoo. Lakini je, tamaa ya kupata utukufu wa wanadamu inaweza kuwaathiri hata watumishi wa Mungu waliojiweka wakfu? Tuseme kwamba kijana anapewa mgawo wa kuhubiri eneo ambalo watu wengi wanamfahamu lakini hawajui kwamba yeye ni Shahidi wa Yehova. Je, ataogopa kuhubiri? Au namna gani ikiwa mtu anadhihakiwa kwa sababu anafuatilia miradi ya kiroho? Je, ataruhusu wale ambao hawathamini mambo ya kiroho waathiri maamuzi anayofanya maishani? Au pengine Mkristo amefanya dhambi nzito. Je, ataficha dhambi yake kwa sababu anaogopa kwamba hataheshimiwa tena kutanikoni au kwa sababu hataki kuumiza hisia za watu anaowapenda? Ikiwa kwa kweli Mkristo huyo anahangaikia sana kurekebisha uhusiano wake pamoja na Yehova, ‘atawaita kwake wanaume wazee wa kutaniko’ na kuwaomba wamsaidie.—Soma Yakobo 5:14-16.

10. (a) Kuhangaikia kupita kiasi maoni ya watu kutuhusu kunawezaje kuathiri maamuzi tunayofanya? (b) Tunahakikishiwa nini tukitenda kwa unyenyekevu?

10 Huenda tunafanya maendeleo ya kiroho ili kuwa Wakristo wakomavu, lakini mwamini mwenzetu anatushauri. Shauri lake la unyoofu linaweza kutusaidia ikiwa hatutajitetea kwa kiburi ili kuepuka aibu, au kushawishika kutoa visingizio. Au tuseme kwamba unafanya kazi fulani pamoja na mwamini mwenzako. Je, utashirikiana naye ili usifiwe kwa sababu ya mapendekezo yako mazuri na kazi ngumu uliyofanya? Ukijikuta katika hali kama hizo, uwe na hakika kwamba “yeye aliye na roho ya unyenyekevu atapata utukufu.”—Met. 29:23.

11. Tunapaswa kuhisije moyoni tunapopongezwa, na kwa nini?

11 Waangalizi na wale ‘wanaojitahidi kufikia’ pendeleo hilo wanapaswa pia kuwa waangalifu ili wasitafute sifa ya wanadamu. (1 Tim. 3:1; 1 The. 2:6) Ndugu anapaswa kuitikiaje anapopongezwa kwa unyoofu baada ya kutimiza mgawo vizuri? Huenda hatajisimamishia mnara wa ukumbusho, kama Mfalme Sauli alivyofanya. (1 Sam. 15:12) Hata hivyo, je, anatambua wazi kwamba alitimiza mgawo wake kwa sababu tu ya fadhili zisizostahiliwa za Yehova na kwamba hawezi kufanikiwa wakati ujao asipoendelea kutegemea baraka na msaada wa Yehova? (1 Pet. 4:11) Jinsi tunavyohisi moyoni tunaposifiwa hudhihirisha wazi aina ya utukufu tunaotafuta.—Met. 27:21.

“MNATAKA KUFANYA TAMAA ZA BABA YENU”

12. Ni nini kilichowazuia Wayahudi fulani kumsikiliza Yesu?

12 Jambo lingine linaloweza kutuzuia tusipate utukufu kutoka kwa Mungu ni tamaa zetu. Tamaa zisizofaa zinaweza kutuzuia kabisa kuisikiliza ile kweli. (Soma Yohana 8:43-47.) Yesu aliwaambia Wayahudi fulani kwamba hawakusikiliza ujumbe wake kwa sababu ‘walitaka kufanya tamaa za baba yao, Ibilisi.’

13, 14. (a) Watafiti wanasema nini kuhusu jinsi ubongo wetu unavyoitikia sauti za wanadamu? (b) Ni nini kinachoamua tutakayemsikiliza?

13 Tamaa zetu huathiri jinsi tunavyosikiliza. (2 Pet. 3:5) Yehova alituumba tukiwa na uwezo wa kipekee wa kuamua kutosikiliza sauti zinazosumbua. Hebu tua kidogo na ujaribu kusikiliza kwa makini sauti mbalimbali unazoweza kusikia sasa hivi. Inaelekea kwamba muda mfupi uliopita hata hukujua kwamba sauti hizo zipo. Sehemu ya ubongo inayoongoza hisia ilikusaidia kukazia fikira jambo moja tu na wakati huohuo kusikia sauti mbalimbali. Lakini watafiti wamegundua kwamba ni vigumu kubainisha sauti mbalimbali za wanadamu wanapoongea wakati uleule. Hilo linamaanisha kwamba unaposikia watu wawili wakiongea wakati uleule, ni lazima umkazie fikira mmoja tu. Utachagua kumsikiliza yule  unayetaka kumsikiliza. Wayahudi waliotaka kufanya tamaa za baba yao, Ibilisi, hawakumsikiliza Yesu.

14 Sisi hupata habari kutoka katika ‘nyumba ya hekima’ na katika ‘nyumba ya ujinga.’ (Met. 9:1-5, 13-17) Hekima na ujinga huendelea kutulilia kwa sauti kwa njia ya mfano, na hilo hutulazimisha kufanya uamuzi. Tutakubali kusikiliza nini? Jibu la swali hilo linategemea ni nani ambaye tunataka kufanya mapenzi yake. Kondoo wa Yesu huisikiliza sauti yake na kumfuata. (Yoh. 10:16, 27) Wako “upande wa ile kweli.” (Yoh. 18:37) “Hawaijui sauti ya wageni.” (Yoh. 10:5) Watu wanyenyekevu kama hao hupata utukufu.—Met. 3:13, 16; 8:1, 18.

“HIZI ZINAMAANISHA UTUKUFU KWENU”

15. Ni kwa njia gani dhiki za Paulo ‘zilimaanisha utukufu’ kwa wengine?

15 Ustahimilivu wetu tunapofanya mapenzi ya Yehova utawasaidia wengine kupata utukufu. Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wa kutaniko la Efeso: “Nawaomba ninyi msife moyo kwa sababu ya hizi dhiki zangu kwa ajili yenu, kwa maana hizi zinamaanisha utukufu kwenu.” (Efe. 3: 13) Dhiki za mtume Paulo ‘zilimaanisha utukufu’ kwa Waefeso katika maana gani? Utayari wa Paulo wa kuendelea kuwatumikia licha ya majaribu uliwasadikishia Waefeso kwamba mapendeleo waliyokuwa nayo wakiwa Wakristo yalikuwa mazito sana na yenye thamani kubwa sana. Kama Paulo angevunjika moyo kwa sababu ya dhiki hizo, je, jambo hilo lisingefanya waanze kufikiri kwamba uhusiano wao pamoja na Yehova, tumaini lao, na huduma yao haikuwa na thamani yoyote? Uvumilivu wa Paulo ulitukuza Ukristo na kuonyesha wazi kwamba ukiwa mwanafunzi wa Yesu, kuna faida kubwa ya kujidhabihu kwa njia yoyote ile.

16. Ni dhiki gani ambayo Paulo alikabili huko Listra?

16 Fikiria matokeo mazuri ya bidii na uvumilivu wa Paulo. Andiko la Matendo 14:19 na 20 linasema hivi: “Wayahudi wakafika kutoka Antiokia na Ikoniamu wakaushawishi umati, nao wakampiga Paulo kwa mawe na kumkokota nje ya jiji [la Listra], wakiwazia alikuwa amekufa. Hata hivyo, wanafunzi walipomzunguka, akasimama na kuingia ndani ya jiji. Na siku iliyofuata akaondoka pamoja na Barnaba kwenda Derbe.” Hebu wazia kwamba umepigwa karibu kufa, na kesho yake unasafiri umbali wa kilomita 100, bila kutumia vyombo vya kisasa vya usafiri!

17, 18. (a) Ni katika njia gani huenda Timotheo alifuata kwa ukaribu mateso ya Paulo huko Listra? (b) Uvumilivu wa Paulo ulikuwa na uvutano gani kwa Timotheo?

17 Je, Timotheo alikuwa mmoja wa “wanafunzi” waliomzunguka Paulo na kumsaidia? Kitabu cha Matendo hakisemi wazi jambo hilo, lakini inawezekana kwamba alikuwapo. Fikiria mambo ambayo Paulo aliandika  katika barua ya pili aliyomwandikia Timotheo: “Wewe umefuata kwa ukaribu fundisho langu, mwendo wangu wa maisha, . . . namna ya mambo yaliyonipata katika Antiokia [alikofukuzwa kutoka jijini], katika Ikoniamu [walikojaribu kumuua kwa kumpiga mawe], katika Listra [alikopigwa mawe], namna ya mateso ambayo nimevumilia; na bado Bwana alinikomboa mimi kutoka katika hayo yote.”—2 Tim. 3:10, 11; Mdo. 13:50; 14:5, 19.

18 Timotheo ‘alifuata kwa ukaribu’ matukio hayo na alijua vizuri uvumilivu wa Paulo. Jambo hilo lilibaki akilini mwa Timotheo. Paulo alipotembelea Listra, alimkuta Timotheo akiwa Mkristo aliyewawekea wengine mfano mzuri, ambaye “alishuhudiwa vema na akina ndugu katika Listra na Ikoniamu.” (Mdo. 16:1, 2) Baada ya muda, Timotheo alistahili kubeba madaraka mazito zaidi.—Flp. 2:19, 20; 1 Tim. 1:3.

19. Uvumilivu wetu unaweza kuwa na uvutano gani kwa wengine?

19 Uvumilivu wetu tunapofanya mapenzi ya Mungu unaweza pia kuwa na uvutano mzuri kama huo kwa wengine, hasa wachanga, ambao wengi wao watakuwa watumishi wa Mungu wenye thamani sana. Wanafunzi wapya wanapotutazama hawajifunzi tu ustadi wetu wa kuhubiri na kufundisha katika huduma ya shambani bali pia wanafaidika wanapoona jinsi tunavyokabiliana na hali ngumu maishani. Paulo ‘aliendelea kuvumilia mambo yote’ ili wote wanaoendelea kuwa waaminifu ‘wapate wokovu na utukufu wa milele.’—2 Tim. 2:10.

Wakristo wachanga huthamini uvumilivu wa Wakristo wenye umri mkubwa

20. Kwa nini tunapaswa kuendelea kuutafuta utukufu unaotoka kwa Mungu?

20 Hivyo basi, je, hatupaswi kuendelea ‘kuutafuta utukufu unaotoka kwa Mungu wa pekee’? (Yoh. 5:44; 7:18) Bila shaka tunapaswa kujitahidi kabisa kufanya hivyo! (Soma Waroma 2:6, 7.) Yehova huwapa ‘uzima wa milele wale wanaotafuta utukufu.’ Kwa kuongezea, ‘uvumilivu wetu katika kazi iliyo njema’ huwachochea wengine kuendelea kusimama imara kwa faida yao ya milele. Hivyo basi, usiruhusu chochote kikuzuie kupata utukufu unaotoka kwa Mungu.