Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jihadhari na Makusudio ya Moyo

Jihadhari na Makusudio ya Moyo

Biblia inasema hivi: “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari.” (Yer. 17:9) Moyo wetu unapotamani sana kitu fulani, je, hatutafuti sababu za kutosheleza tamaa au makusudio yake?

Maandiko yanatuonya hivi: “Mawazo mabaya hutoka moyoni, mauaji, uzinzi, uasherati, wizi, ushuhuda wa uwongo, makufuru.” (Mt. 15:19) Moyo wetu wa mfano unaweza kutudanganya na kutufanya tuanze kutetea mwenendo wetu usiopatana na mapenzi ya Mungu. Huenda tukatambua jambo hilo baada ya kutenda kwa njia isiyo ya hekima. Ni nini kinachoweza kutusaidia kutambua makusudio ya moyo wetu kabla ya kufuatilia mwenendo mbaya?

UNAWEZAJE KUTAMBUA MAKUSUDIO YA MOYO WAKO?

Kuisoma Biblia kila siku kunasaidiaje moyo wetu wa mfano?

Soma Biblia kila siku na utafakari inachosema.

Mtume Paulo aliandika hivi: “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili nalo huchoma hata kufikia kugawanya nafsi na roho.” Ujumbe wa Mungu unaopatikana katika Biblia ‘unaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.’ (Ebr. 4:12) Kwa kweli, kujichunguza kwa kutumia Maandiko kunaweza kutatusaidia sana kutambua makusudio ya moyo. Kwa hiyo, ni muhimu kama nini kwamba tusome na kutafakari Neno la Mungu kila siku. Tukifanya hivyo tutaelewa mawazo na maoni ya Yehova!

Kukubali shauri la Kimaandiko na kutumia kanuni za Biblia kutakuwa na matokeo mazuri kwa dhamiri yetu, yaani, uwezo wa ndani ‘unaotoa ushahidi.’ (Rom. 9:1) Sauti ya dhamiri yetu inaweza kutuzuia kuutetea mwenendo mbaya. Kwa kuongezea, Biblia ina mifano inayoweza “kuwa onyo kwetu sisi.”  (1 Kor. 10:11) Kujifunza kutokana na mifano hiyo kunaweza kutuzuia kutenda isivyofaa. Kila mmoja wetu anapaswa kufanya nini?

Sala zetu zinatusaidia kumjua mtu wa ndani

Sali kwa Mungu akusaidie kutambua makusudio ya moyo wako.

Yehova ni “mchunguzaji wa moyo.” (1 Nya. 29:17) Yeye “ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua mambo yote.” (1 Yoh. 3:20) Mungu hawezi kudanganywa. Ikiwa tutamweleza Yehova waziwazi mahangaiko, hisia, na tamaa zetu katika sala, anaweza kutusaidia kutambua makusudio ya moyo wetu. Tunaweza hata kumwomba Mungu ‘aumbe moyo safi ndani yetu.’ (Zab. 51:10) Kwa hiyo, ili kutambua mielekeo ya moyo wetu, hatupaswi kupuuza uandalizi wa sala.

Mikutano ya Kikristo hutusaidia kutambua makusudio ya moyo wetu

Sikiliza kwa makini unapokuwa katika mikutano ya Kikristo.

Kusikiliza kwa makini katika mikutano ya Kikristo kutatusaidia kumchunguza kwa unyoofu mtu wetu wa ndani, yaani, moyo wetu. Ingawa huenda tusijifunze mambo mpya katika kila mkutano, tunapohudhuria tunapata uelewaji mzuri zaidi wa kanuni za Biblia na vilevile vikumbusho vyenye thamani vinavyotusaidia kuchanganua makusudio ya moyo. Pia, maelezo ya ndugu na dada zetu yanatusaidia sana kuboresha mtu wetu wa ndani. (Met. 27:17) Kwa hiyo, kujitenga na wengine badala ya kufurahia ushirika wa kawaida wa Kikristo katika mikutano kunaweza kutudhuru. Hilo linaweza kutufanya ‘tutafute mapendezi yetu wenyewe.’ (Met. 18:1) Kwa hiyo, ni jambo la hekima kujiuliza hivi: ‘Je, ni desturi yangu kuhudhuria mikutano yote na kufaidika kutokana nayo?’—Ebr. 10:24, 25.

MOYO WETU UTATUONGOZA WAPI?

Moyo wetu wenye hila unaweza kutuongoza vibaya katika mambo mbalimbali maishani. Acheni tuchunguze mambo manne: kufuatia vitu vya kimwili, matumizi ya pombe, marafiki tunaowachagua, na burudani tunayochagua.

Kufuatia vitu vya kimwili.

Ni jambo la kiasili kuwa na tamaa ya kutosheleza mahitaji yetu ya kimwili. Hata hivyo, Yesu alitoa mfano wenye kuonya kuhusu kukazia fikira vitu kimwili. Katika moja ya mifano yake, Yesu anataka tufikirie kisa cha mwanamume tajiri ambaye maghala yake yalijaa. Kwa sababu hiyo, hakuwa na mahali pa kuhifadhia mavuno mengine. Mwanamume huyo alikusudia kuvunja maghala yake na kujenga mengine makubwa zaidi. Alijiambia hivi: “Humo nitakusanya nafaka yangu yote na vitu vyangu vyema vyote; nami nitaiambia nafsi yangu: ‘Nafsi yangu, una vitu vyema vingi vilivyokusanywa kwa miaka mingi; starehe, ule, unywe, na kujifurahisha.’” Hata hivyo, mwanamume huyo tajiri hakufikiria jambo hili la uhakika: Angeweza kufa usiku huohuo.—Luka 12:16-20.

Kadiri tunavyozeeka, huenda tukahangaikia sana kupata vitu vya kimwili vitakavyotusaidia uzeeni na hivyo tunaweza kuanza kujitetea tunapofanya kazi ya ziada siku za mikutano au kwa njia fulani kuanza kupuuza majukumu yetu ya Kikristo. Je, hatupaswi kujilinda na mwelekeo huo? Au labda sisi ni vijana na tunajua kwamba hakuna kazi bora zaidi maishani kuliko utumishi wa wakati wote. Lakini, je, bado tunaahirisha  kufanya upainia, tukitoa kisingizio cha kwamba tunahitaji kuwa na usalama wa kifedha kwanza? Je, hatupaswi kujitahidi kabisa sasa kuwa matajiri machoni pa Mungu? Ni nani anayejua kama tutakuwa hai kesho?

Matumizi ya pombe.

Methali 23:20 inasema hivi: “Usiwe kati ya watu wanaokunywa divai mno.” Ikiwa mtu ana tamaa yenye nguvu ya kunywa pombe, huenda akatetea zoea lake la kunywa pombe kwa ukawaida. Huenda akasema kwamba anakunywa ili kustarehe wala si kulewa. Ikiwa tunahitaji kunywa pombe ili kustarehe, inaonekana tunahitaji kuchunguza kwa unyoofu mwelekeo wa moyo wetu.

Marafiki tunaowachagua.

Ni kweli kwamba hatuwezi kuwaepuka kabisa wasioamini kwa kuwa tunakutana nao shuleni, kazini, na katika huduma. Lakini, ni jambo tofauti kushirikiana nao na hata kusitawisha urafiki wa karibu pamoja nao. Je, sisi hutetea urafiki huo kwa kusema kwamba watu hao wana sifa nyingi nzuri? Biblia inaonya hivi: “Msipotoshwe. Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” (1 Kor. 15:33) Kama vile kiasi kidogo cha uchafu kinavyoweza kuchafua maji safi, urafiki pamoja na watu wasio na ujitoaji wa kimungu unaweza kuchafua hali yetu ya kiroho na kutufanya tuanze kuiga maoni, mitindo ya mavazi, usemi, na mwenendo wa kilimwengu.

Burudani tunayochagua.

Teknolojia ya kisasa inafanya iwe rahisi sana kwetu kupata kila aina ya vitumbuizo, na vitumbuizo vingi ni vyenye kutiliwa shaka au havimfai Mkristo. Mtume Paulo aliandika hivi: ‘Ukosefu wa usafi wa kila namna usitajwe hata kidogo katikati yenu.’ (Efe. 5:3) Vipi ikiwa moyo wetu unavutiwa kuangalia au kusikiliza jambo fulani chafu? Huenda tukajitetea kwamba kila mtu anahitaji kupumzika kidogo au kuwa na burudani, na aina ya burudani ambayo mtu anachagua ni jambo la kibinafsi. Lakini acheni tulichukue kwa uzito shauri la Paulo kwa kutoruhusu macho yetu kutazama au masikio yetu kusikia uchafu wowote.

TUNAWEZA KUFANYA MABADILIKO

Ikiwa tumenaswa na mielekeo ya moyo wetu wenye hila na tumezoea kutetea mwenendo wetu usiofaa, tunaweza kufanya mabadiliko. (Efe. 4:22-24) Fikiria mifano miwili ya wakati wetu.

Miguel * alihitaji kurekebisha mtazamo wake kuelekea vitu vya kimwili. Anasema hivi: “Mimi, mke wangu, na mwanangu tunatoka katika nchi ambayo watu wanathamini sana kuishi maisha ya starehe na kuwa na vifaa vya kisasa na vilivyo bora zaidi vya kiteknolojia. Wakati fulani, nilijitahidi sana kupata vyote nilivyoweza kupata ulimwenguni, nikifikiri kwamba ningeweza kufanya hivyo bila kupenda vitu vya kimwili. Punde si punde, niligundua kwamba kufuatilia vitu vya kimwili ni kama kufuata barabara isiyo na mwisho. Nikasali kwa Yehova kuhusu maoni yangu na makusudio ya moyo wangu. Nilimweleza wazi kwamba tunataka kumtumikia kikamili zaidi tukiwa familia. Tuliweza kufanya uamuzi wa kurahisisha maisha yetu na kuhamia katika eneo lililokuwa na uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri. Baada ya muda mfupi tulianza upainia. Sasa tumegundua kwamba hatuhitaji vitu vingi vya kimwili ili kuwa na maisha yenye kuridhisha na yenye furaha.”

Mfano wa Lee unaonyesha jinsi kujichunguza kwa unyoofu kulivyomsaidia kuwaacha marafiki wabaya. Anasema hivi: “Kwa sababu ya kazi yangu, nilikutana kwa ukawaida na wafanyabiashara kutoka nchi nyingine. Nilijua kwamba watu wangekunywa pombe kupita kiasi katika mikutano hiyo, lakini nilifurahia sana kuihudhuria. Mara nyingi nilikunywa karibu nilewe, lakini nilijuta baadaye. Nilihitaji kuuchunguza moyo wangu kwa unyoofu. Shauri la Neno la Mungu na mapendekezo ya wazee yalinisaidia kutambua kwamba nilifurahia sana kushirikiana na watu wasiompenda Yehova. Sasa ninafanya biashara yangu kwa kutumia simu kadiri iwezekanavyo na ninakutana mara chache sana na wafanyabiashara hao.”

Tunahitaji kuwa wanyoofu na kutambua makusudio ya moyo wetu. Tunapofanya hivyo, tunapaswa kumwomba Yehova msaada kupitia sala, huku tukikumbuka kwamba “yeye anajua siri za moyo.” (Zab. 44:21) Mungu ametupatia pia Neno lake, tunaloweza kulitumia kama kioo. (Yak. 1:22-25) Pia, mashauri na vikumbusho tunavyopata kupitia machapisho ya Kikristo na mikutano yetu ni vyenye thamani kama nini! Tukiwa na maandalizi hayo, tunaweza kuulinda moyo wetu na kuendelea kutembea katika njia za uadilifu.

^ fu. 18 Majina yamebadilishwa.