Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tel Aradi—Eneo Linalotoa Ushuhuda

Tel Aradi—Eneo Linalotoa Ushuhuda

Tel Aradi—Eneo Linalotoa Ushuhuda

Jiji lililopotea. Hekalu lisiloeleweka. Maandishi mengi ya kale. Mambo hayo yanaweza kusikika kama msingi wa sinema yenye kusisimua. Kwa kweli, vitu hivyo vyote na vingine vingi vilikuwa vimefichwa chini ya matabaka ya mchanga kwa karne nyingi huko Tel Aradi, Israeli, hadi waakiolojia walipoanza kuchimba eneo hilo.

KWA wageni wengi leo, Aradi ya kisasa inaonekana kama mji wa kawaida wa Israeli. Likiwa na wakaaji 27,000, linapatikana katika jangwa la Yudea magharibi ya Bahari ya Chumvi. Hata hivyo, jiji la Aradi la nyakati za Israeli la kale lilikuwa kilomita nane hivi upande wa magharibi. Huko ndiko waakiolojia wameondoa kwa uangalifu matabaka ya mchanga, na kufunua majengo na maandishi mengi.

Maandishi hayo yaliandikwa kwenye vipande vya udongo vilivyotumiwa kama mabamba ya kuandikia. Ilikuwa kawaida kwa watu kuandika kwa njia hiyo katika nyakati za Biblia. Eneo lililochimbuliwa huko Tel Aradi limetokeza kile kinachofafanuliwa kuwa mkusanyo mkubwa sana wa mabamba hayo kuwahi kupatikana nchini Israeli. Lakini umuhimu wa uvumbuzi huo ni nini?

Uvumbuzi wa Tel Aradi unaonyesha kipindi kirefu cha historia ya Biblia, kuanzia siku za Waamuzi wa Israeli mpaka mashambulizi ya Wababiloni dhidi ya Yuda mnamo 607 K.W.K. Hivyo, uvumbuzi huo unasaidia kuthibitisha usahihi wa Biblia. Pia unaonyesha mifano ya jinsi watu katika Israeli la kale waliliona jina la kibinafsi la Mungu.

Aradi na Biblia

Ni kweli kwamba Biblia haisemi mengi kuhusu Aradi. Lakini wakati fulani jiji hilo lililo mahali panapofaa lilidhibiti njia kuu ya biashara. Basi haishangazi kuwa rekodi za kihistoria na uvumbuzi wa akiolojia unaonyesha kwamba eneo hilo la zamani lilishindwa, likaharibiwa, na kujengwa upya mara nyingi katika historia yake. Kujengwa upya tena na tena kwa jiji kulitokeza tell kubwa sana, au kilima.

Biblia inazungumza kuhusu Aradi mara ya kwanza inaposimulia sehemu ya mwisho ya safari ya Waisraeli ya miaka 40 nyikani. Muda mfupi baada ya kifo cha ndugu ya Musa, Haruni, watu wa Mungu walipita karibu na mpaka wa kusini wa Nchi ya Ahadi. Mfalme Mkanaani wa Aradi aliona kwamba ni rahisi kuwashinda wasafiri hao wa jangwani na hivyo akawashambulia Waisraeli. Wakitegemezwa na Yehova Mungu, Waisraeli walipigana kwa bidii, wakapata ushindi kamili, na wakateketeza jiji la Aradi kabisa, hata ingawa inaonekana watu fulani waliokoka.—Hesabu 21:1-3.

Wakanaani walijenga upya jiji hilo haraka kwani Yoshua alipofikia eneo hilo miaka kadhaa baadaye, akivamia kutoka kaskazini na kuwaondoa kwa utaratibu Wakanaani kutoka “eneo lenye milima na Negebu,” mmoja wa wapinzani wake alikuwa “mfalme wa Aradi.” (Yoshua 10:40; 12:14) Baadaye, wazao wa Hobabu Mkeni, ambaye alijiunga na kambi ya Waisraeli walipokuwa nyikani, waliishi katika eneo hilo la Negebu.—Waamuzi 1:16.

Uvumbuzi wa Akiolojia

Magofu ya Tel Aradi yanatoa uthibitisho wa kupendeza kuhusu matukio ya baadaye katika rekodi ya Biblia. Kwa mfano, wachimbuzi wa vitu vya kale wamechimbua ngome kadhaa. Baadhi ya ngome hizo zinaweza kuwa za wakati wa utawala wa Mfalme Sulemani, ambaye alijulikana kwa miradi mingi ya ujenzi wa majiji. (1 Wafalme 9:15-19) Tabaka moja la mchanga linaonyesha uthibitisho wa kuteketezwa na inakadiriwa kwamba eneo hilo liliteketezwa mwanzoni mwa karne ya kumi K.W.K. Uvumbuzi huo unapatana na uvamizi wa Shishaki Mfalme Mmisri, miaka mitano tu baada ya kifo cha Sulemani. Huko Karnaki kusini mwa Misri, mchongo katika jiwe unaonyesha uvamizi huo na unataja Aradi kati ya majiji mengi yaliyoshindwa.—2 Mambo ya Nyakati 12:1-4.

Jambo linalopendeza sana ni kwamba vingi kati ya vigae 200 hivi vilivyofukuliwa vina majina ya Kiebrania yanayopatikana pia katika Biblia, kama vile Pashuri, Meremothi, na wana wa Kora. Baadhi ya maandishi hayo yanapendeza hata zaidi kwa sababu yanatia ndani jina la kibinafsi la Mungu. Likiwa limeandikwa kwa herufi nne za Kiebrania יהוה (YHWH) ambazo mara nyingi zinaitwa Tetragramatoni, zinawakilisha jina pekee la Mungu Mweza-Yote. Baadaye, ushirikina uliwafanya watu wengi waamini kwamba kutamka au kuandika jina la Mungu ni kukufuru. Hata hivyo, uvumbuzi huko Tel Aradi, kama uvumbuzi mwingine mwingi, unathibitisha kwamba katika nyakati za Biblia jina la Mungu lilitumika sana katika maisha ya kila siku, katika salamu, na katika kubariki. Kwa mfano, maandishi fulani yanasema hivi: “Kwa bwana wangu Eliyashibu. Yahweh [Yehova] na ahangaikie hali njema yako. . . . Anakaa katika hekalu la Yahweh.”

Namna gani kuhusu hekalu lisilo la kawaida linalotajwa mwanzoni mwa habari hii? Jengo fulani huko Tel Aradi limewafanya watu wakisie-kisie kulihusu. Jengo hilo ni hekalu lenye madhabahu lililojengwa katika kipindi cha Yudea. Ingawa ni dogo, hekalu hilo linafanana sana na lile la Sulemani lililokuwa Yerusalemu. Hekalu la Aradi lilijengwa lini na kwa nini? Lilitumiwa jinsi gani? Waakiolojia na wanahistoria wanaweza tu kukisia.

Yehova alikuwa ameeleza waziwazi kwamba hekalu la Yerusalemu ndicho kituo pekee alichokikubali kwa sherehe za kila mwaka na kutoa dhabihu. (Kumbukumbu la Torati 12:5; 2 Mambo ya Nyakati 7:12) Kwa hiyo, hekalu la Aradi lilijengwa na kutumiwa kinyume cha Sheria ya Mungu, huenda katika enzi ambapo madhabahu na desturi nyingine ziliwakengeusha watu wengi kutoka kwa ibada safi. (Ezekieli 6:13) Ikiwa ni hivyo, kituo hicho cha ibada ya uwongo huenda kiliharibiwa wakati wa marekebisho makubwa ya Hezekia au Yosia katika karne za nane na saba K.W.K.—2 Mambo ya Nyakati 31:1; 34:3-5, 33.

Ni wazi kwamba historia ya Aradi ambayo imeokoka inatufunza masomo muhimu. Baada ya karne nyingi, vitu vimegunduliwa vinavyothibitisha usahihi wa Biblia, vinavyoonyesha kuinuka na kuanguka kwa ibada ya uwongo, na vinavyoonyesha jinsi jina la Yehova lilivyotumiwa kwa heshima.

[Ramani/Picha katika ukurasa wa 23]

 

YERUSALEMU

Bahari ya Chumvi

Aradi

Tel Aradi

[Hisani]

Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Maandishi yaliyochongwa kwenye ukuta huko Karnaki, Misri

[Hisani]

Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kwa sehemu maandishi haya yanasema: “Yahweh [Yehova] na ahangaikie hali njema yako”

[Hisani]

Photograph © Israel Museum, Jerusalem; courtesy of Israel Antiquities Authority

[Picha katika ukurasa wa 25]

Sehemu ya majengo ya hekalu huko Tel Aradi

[Picha katika ukurasa wa 25]

Ngome ya Tel Aradi ikiangaliwa kutoka upande wa mashariki

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 25]

Todd Bolen/Bible Places.com