Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Ni nini kingemchochea mshiriki wa genge la vijana la Mexico linaloitwa Mashetani Wadogo abadili maisha yake na kuwa raia mnyoofu anayefanya kazi kwa bidii? Kwa nini mwanamke Mjapani mfanyabiashara mwenye mafanikio aliacha kufuatilia mali, na ana maoni gani kuhusu mabadiliko aliyofanya? Ni nini kingechochea muuzaji wa silaha Mrusi aache biashara yake yenye mafanikio lakini isiyo halali? Hebu ona yale ambayo watu hao walisema.

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU

JINA: ADRIAN PEREZ

UMRI: 30

NCHI: MEXICO

HISTORIA: MSHIRIKI WA GENGE

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilipokuwa na umri wa miaka 13, familia yetu ilihamia Ecatepec de Morelos, Jimbo la Mexico. Wakati huo eneo hilo lilikumbwa na vijana wahalifu, uharibifu wa mali za watu, na matumizi ya dawa za kulevya. Nilianza kulewa, kuharibu mali za watu, na kujihusisha katika ukosefu wa maadili.

Baadaye tulirudi San Vicente, mji nilikozaliwa. Hata hivyo, eneo hilo lilikuwa limeanza kujaa waraibu wa dawa za kulevya. Lilikuwa jambo la kawaida kuona maiti za vijana barabarani. Nilijiunga na genge lililoitwa Mashetani Wadogo. Tuliiba na kutumia dawa za kulevya, hasa gundi. Mara nyingi, sikumbuki jinsi nilivyofika nyumbani, na wakati mwingine ningelala barabarani bila fahamu zozote. Baadhi ya marafiki wangu walifungwa gerezani kwa sababu ya wizi na mauaji.

Ijapokuwa nilifanya mambo hayo yote, nilimwamini Mungu. Ili kupunguza hisia za hatia, ningeshiriki katika sherehe za kidini, kama vile Njia ya Msalaba wakati wa Juma Takatifu. Hata hivyo, baadaye sisi sote, kutia ndani mtu aliyeigiza sehemu ya Kristo, tulisherehekea kushiriki katika tukio hilo kwa kulewa.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Nilipokaribia kuwa na umri wa miaka 20, nilianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Nilitambua kwamba maisha yangu hayakuwa na kusudi halisi na kwamba kama ningeendelea na mtindo wangu wa maisha, mambo hayangeniendea vema. Nilipendezwa hasa na maneno yaliyoandikwa katika Wagalatia 6:8: “Yeye anayepanda kwa mwili wake atavuna uharibifu kutokana na mwili wake, lakini yeye anayepanda kwa roho atavuna uzima wa milele kutokana na roho.” Andiko hilo lilinisaidia kuona kwamba ikiwa nilitaka mambo yawe mazuri, nilihitaji kupanda nikifikiria wakati ujao.

Nilipojifunza Biblia, nilianza kuthamini kwamba Yehova ni Mungu aliye hai anayependezwa kibinafsi nami, na kwamba yuko tayari kunisamehe dhambi nilizokuwa nimefanya. Nilijionea kwamba yeye anasikiliza na kujibu sala.

Haikuwa rahisi kubadili maisha yangu. Ilikuwa vigumu kutoka katika genge nililoshirikiana nalo. Maeneo fulani yalikuwa yametiwa alama na ilikuwa vigumu kwangu kupita katika maeneo hayo hata ingawa sikuwa tena katika genge. Nyakati nyingine, ningejificha ili marafiki wangu wa zamani wasinione kwa sababu walitaka nirudie maisha yangu ya zamani.

Nilipoanza kuhudhuria mikutano pamoja na Mashahidi wa Yehova kwenye Jumba la Ufalme nilitambua kwamba kutaniko lilikuwa na uchangamfu na upendo. Nilipendezwa kwa kuwa watu hapo walikuwa na usadikisho wa kweli na waliishi kupatana na mambo waliyofundisha. Yalikuwa mazingira tofauti kabisa na yale niliyozoea.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova miaka kumi iliyopita. Ninajitahidi kufuata mafundisho ya Biblia katika maisha yangu. Kwa sababu hiyo, familia yangu imeanza kuniheshimu. Sasa wananitambua kama mfanyakazi mwenye bidii, na nimewasaidia kifedha. Mama yangu alianza kujifunza Biblia na sasa yeye ni Shahidi wa Yehova. Baba yangu pia anafanya mabadiliko maishani. Wengi katika familia yangu si Mashahidi wa Yehova lakini baada ya kuona mabadiliko niliyofanya maishani wanakubali kwamba Biblia inaweza kumsaidia mtu aboreshe maisha yake.

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU

JINA: YAYOI NAGATANI

UMRI: 50

NCHI: JAPANI

HISTORIA: MFANYABIASHARA MWENYE MAFANIKIO

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nililelewa katika mji mdogo wa vijijini uliokuwa na watu wenye urafiki. Baba yangu alikuwa na duka kubwa mjini lililokuwa na wafanyakazi kumi. Nyumba yetu ilikuwa karibu na duka hilo, hivyo, ingawa Baba na Mama walikuwa na kazi nyingi, sikujihisi mpweke.

Mimi ndiye wa kwanza kati ya wasichana watatu, na tangu nilipokuwa mdogo nilizoezwa kuendesha biashara ya familia. Niliolewa nikiwa na umri mdogo. Mume wangu aliacha kazi yake ya benki na kujiunga nasi katika biashara ya familia. Tulipata watoto watatu waliofuatana kwa ukaribu. Mama yangu aliwatunza watoto alipokuwa akishughulikia kazi za nyumbani huku nikifanya kazi dukani tangu asubuhi hadi usiku. Hata hivyo, bado tulipata nafasi za kuwa pamoja kama familia.

Kisha hali ya kiuchumi katika mji wetu ikawa mbaya na mapato yetu yakaanza kupungua. Ili kukabiliana na hali hiyo, tuliamua kufungua duka la vifaa vya kurekebisha nyumba kando ya barabara kuu. Siku moja kabla ya sherehe ya kuanza ujenzi, baba yangu, aliyekuwa msimamizi wa kampuni yetu alizimia kwa sababu ya tatizo la ubongo. Uwezo wake wa kuzungumza uliathiriwa vibaya, hivyo nikawa na jukumu la kusimamia duka hilo jipya. Mume wangu alibaki katika duka la zamani. Maisha yetu yakawa na shughuli nyingi sana.

Duka letu jipya lilisitawi. Nilijivunia mafanikio yetu na nililala kwa saa chache sana ili nifanye kazi. Ingawa niliwapenda watoto wangu, wakati wote nilifikiri kuhusu kazi. Sikuwa na wakati wa kuzungumza na mume wangu, na tulipozungumza tulibishana sana. Ili kukabiliana na mfadhaiko, kila usiku nilienda kunywa na marafiki na wafanyabiashara wenzangu. Maisha yangu yalihusisha tu kufanya kazi, kunywa, na kulala. Nilikuwa nimefanikiwa kifedha lakini sikuwa na furaha na sikuelewa sababu.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Nilipoanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, mistari mitatu ya Biblia ilinigusa moyo. Nililia nilipotambua maana ya Mathayo 5:3: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbinguni ni wao.” Mstari huo ulieleza ni kwa nini sikuwa na uradhi ingawa nilikuwa nimefanikiwa kifedha na niliheshimiwa na wanabiashara wenzangu. Nilielewa kwamba ni kwa kutambua uhitaji wangu wa kiroho na kuutosheleza ningepata furaha ya kweli.

Wakati huo, uchumi wa Japani ulizorota vibaya, na miongoni mwa wafanyabiashara wenzangu niliona ukweli wa 1 Timotheo 6:9: “Wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka katika jaribu na mtego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kudhuru, ambazo hutumbukiza watu katika maangamizi na uharibifu.” Nilihisi kwamba maneno ya Yesu yaliyoandikwa kwenye Mathayo 6:24, “hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri,” yalinihusu kibinafsi na hivyo nikaamua kufanya mabadiliko maishani.

Nilitambua kwamba nilikuwa nikiwapuuza wazazi wangu, mume wangu, na watoto wangu. Pia ilikuwa wazi kwamba nilikuwa nimesitawisha tabia fulani zisizofaa. Nilikuwa nimeanza kuwa na kiburi. Sikuwa na subira niliposhughulika na watu na nilikasirika haraka. Mwanzoni, nilifikiri singeweza kubadilika na kuwa Mkristo. Hata hivyo, niliwapenda sana watoto wangu na kadiri nilivyofuata mashauri ya Biblia katika familia, ndivyo uhusiano wangu na watoto wangu ulivyokuwa mzuri. Nilitumia wakati mwingi pamoja nao na kuwapeleka kwenye mikutano ya Kikristo.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Kujua kusudi la uhai, kumtumikia Mungu, na kuishi maisha yanayompendeza, kunanipa shangwe ya kweli na uradhi. Sipuuzi tena familia yangu kwa sababu ya kazi na hivyo nimeanza kujiheshimu tena.

Kuona jinsi utu wangu umebadilika na kuwa bora kadiri nilivyofuata kanuni za Biblia kumemfanya mama yangu ajifunze Biblia na kuwa Mkristo. Jambo la kupendeza ni kwamba baba yangu na mume wangu hawajapinga uamuzi wetu. Uhusiano wangu na watoto wangu umekuwa wa karibu zaidi na ninafurahia maisha ya familia yenye furaha kwelikweli.

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU

JINA: MIKHAIL ZUYEV

UMRI: 51

NCHI: URUSI

HISTORIA: MUUZAJI HARAMU WA SILAHA

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Mji wa Krasnogorsk ambako nilizaliwa, ni eneo lenye mimea yenye kupendeza. Mto Moscow unatiririka kuelekea kusini. Upande wa magharibi na kaskazini, vijiji vimezungukwa na msitu.

Nilipokuwa mdogo nilipenda kupigana ngumi na kucheza na silaha. Nilitumia wakati mwingi katika mazoezi ya kimwili. Pia nilitengeneza bunduki, risasi, na visu kwa njia isiyo halali. Baada ya muda, hiyo ikawa biashara yangu. Nilikuwa na utaratibu mzuri na nilifanikiwa sana kuwauzia wahalifu bidhaa zangu.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Mapema katika miaka ya 1990, nilikutana na Mashahidi wa Yehova lakini mwanzoni sikuwaamini. Niliona kwamba waliuliza maswali mengi sana.

Siku moja, mmoja kati yao alinisomea Waroma 14:12: “Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.” Nilijiuliza ningemwambia Mungu nini. Andiko hilo lilinichochea kuchunguza yale ambayo Mungu alitaka nifanye.

Nilijitahidi sana kufuata shauri la Biblia lililo katika Wakolosai 3:5-10: “Kwa hiyo, viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani, ambako ni ibada ya sanamu. Kwa sababu ya mambo hayo ghadhabu ya Mungu inakuja. . . . Yaondoleeni mbali mambo haya yote kutoka kwenu, ghadhabu, hasira, ubaya, matukano, na maneno machafu kutoka kinywani mwenu. Msiwe mkiambiana uwongo. Uvueni utu wa zamani pamoja na mazoea yake, na mjivike utu mpya.”

Ilikuwa vigumu sana kwangu kufanya mabadiliko kama hayo. Wateja wangu wa zamani walikuwa wakiniahidi pesa ili niwatengenezee silaha, na ilikuwa vigumu kujizuia watu waliponitukana. Hata hivyo, niliharibu silaha zangu zote zenye thamani. Kadiri nilivyojifunza upendo ambao Mungu na Kristo wamenionyesha, nilichochewa kuwapenda. Niliendelea na funzo langu la kibinafsi la Biblia, nikahudhuria mikutano katika kutaniko la karibu, na kusali ili Mungu anisaidie.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Pole kwa pole, kwa jitihada nyingi na msaada kutoka kwa ndugu zangu Wakristo, nimeboresha utu wangu. Nilipendezwa sana kuelewa kwamba Yehova Mungu anatujali sisi mmojammoja, hata anawajali waliokufa. (Matendo 24:15) Ninathamini sana unyoofu ninaoona kati ya Mashahidi wa Yehova. Na ninathamini jinsi wanavyopendezwa nami kibinafsi na jinsi walivyo washikamanifu kwa Mungu.

Mwanzoni, baadhi ya washiriki wa familia yangu na marafiki walipinga imani yangu mpya. Lakini walijiliwaza na wazo la kwamba ilikuwa afadhali kwangu kujihusisha na dini badala ya uhalifu. Ninafurahi kwamba situmii tena maisha yangu kuuza silaha za vita lakini nimejitoa kuwasaidia wengine kujifunza kumhusu Mungu wa amani.

[Picha katika ukurasa wa 27]

Nilijihusisha katika sherehe za Kikatoliki ili kuituliza dhamiri yangu

[Picha katika ukurasa wa 28]

Nilifanikiwa kifedha lakini sikuwa na furaha