Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Dunia Itaokoka?

Je, Dunia Itaokoka?

Wasomaji Wetu Wanauliza

Je, Dunia Itaokoka?

Dunia yetu haitaharibiwa na msiba wowote. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika huo? Kwa sababu Mungu anaahidi kwamba dunia “haitatikiswa mpaka wakati usio na kipimo, au milele.” (Zaburi 104:5) Hata ingawa “kizazi kimoja kinakwenda, na kizazi kimoja kinakuja,” Biblia inasema, “dunia inadumu milele.”—Mhubiri 1:4, Zaire Swahili Bible.

Kwenye andiko la Zaburi 104:5, maneno mawili ya lugha ya Kiebrania cha awali yanatilia mkazo kwamba dunia haitaharibiwa. Maneno hayo ni ʽoh·lam’ linalomaanisha “wakati usio na kipimo,” na ʽadh linalomaanisha “milele.” Huenda neno ʽoh·lam’ likatafsiriwa kuwa “miaka mingi” au “jambo lisilokwisha.” Kulingana na kamusi moja (Harkavy’s Students’ Hebrew and Chaldee Dictionary), neno ʽadh linamaanisha “kipindi chenye kudumu, chenye kuendelea kwa muda mrefu, umilele.” Maneno hayo mawili ya Kiebrania yanaonyesha kwamba hakika dunia itadumu. Hebu chunguza sababu tatu zaidi zinazotegemea Biblia za kuamini kwamba dunia itadumu milele.

Kwanza, Mungu aliiumba dunia ili ikaliwe na watu. Alitaka iwe na mimea mingi inayonawiri, paradiso ya ulimwenguni pote yenye kupendeza bali si mahali pasipokalika. Andiko la Isaya 45:18 linamfafanua Yehova kuwa “Muumba wa mbingu, Yeye Mungu wa kweli, Mfanyizaji wa dunia na Mtengenezaji wake, Yeye aliyeifanya imara, ambaye hakuiumba tu bila sababu, ambaye aliiumba ili ikaliwe na watu.”

Pili, Mungu tayari ametoa ahadi kwamba wanadamu wanaomtii wataishi kwa amani milele duniani. Andiko la Mika 4:4 linaahidi: “Wataketi, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, wala hakutakuwa na mtu yeyote anayewatetemesha; kwa maana kinywa cha Yehova wa majeshi kimesema hivyo.” Kwa hiyo, kulingana na kusudi la Mungu, dunia itakaliwa na wanadamu milele, la sivyo ahadi yake haitatimia.—Zaburi 119:90; Isaya 55:11; 1 Yohana 2:17.

Tatu, Mungu amemkabidhi mwanadamu daraka la kuitunza dunia. Neno la Mungu linasema hivi: “Mbingu ni mbingu za Yehova, bali dunia amewapa wana wa binadamu.” (Zaburi 115:16) Je, unaweza kuwazia baba mwenye upendo akimpa mtoto wake zawadi yenye kupendeza, kisha anamnyang’anya na kuiharibu? Hapana! Vivyo hivyo, Yehova hatafanya jambo kama hilo kwa dunia na wakaaji wake, kwa sababu “Mungu ni upendo.”—1 Yohana 4:8.

Yesu Kristo alitoa uhakikisho huu kuhusu maneno ya Baba yake: “Neno lako ni kweli.” (Yohana 17:17) Naye Mungu asiyeweza kusema uwongo anaahidi hivi: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”—Zaburi 37:29; Tito 1:2.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 31]

Globe: Based on NASA photo