Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuna Matumaini Yoyote kwa Dunia?

Je, Kuna Matumaini Yoyote kwa Dunia?

Je, Kuna Matumaini Yoyote kwa Dunia?

Ungechagua jibu gani kwa swali lifuatalo?

Hivi karibuni, je hali za dunia

(a) zitakuwa bora?

(b) zitabaki vilevile?

(c) zitakuwa mbaya zaidi?

JE, UNA mtazamo mzuri kuhusu wakati ujao? Kuna faida nyingi za kufanya hivyo. Uchunguzi unaonyesha kwamba watu walio na mtazamo mzuri wanafaulu katika masomo na wanakuwa na afya nzuri. Uchunguzi mmoja uliofanywa kwa muda mrefu unaonyesha kwamba si rahisi kwa watu walio na mtazamo mzuri kuwa na magonjwa ya moyo wakilinganishwa na watu wasio na mtazamo mzuri. Matokeo ya uchunguzi huo yanapatana na maneno haya yaliyoandikwa katika Biblia karne nyingi zilizopita: “Moyo wenye shangwe ni dawa nzuri, lakini roho iliyopondeka huikausha mifupa.”—Methali 17:22.

Hata hivyo, kwa sababu ya mambo ambayo wanasayansi wanatabiri kuhusu wakati ujao wa Dunia, watu wengi wanaona kwamba ni vigumu kuwa na mtazamo mzuri na wenye uchangamfu. Hebu fikiria baadhi ya mambo mabaya yanayotabiriwa kwenye vyombo vya habari.

Sayari Hatarini

Mnamo 2002 Taasisi ya Mazingira ya Stockholm inayoheshimiwa ilionya kwamba wanadamu wasipozuiwa kuiharibu dunia kwa sababu ya shughuli zao za kibiashara, hilo lingeanzisha “matukio ambayo yanaweza kugeuza sana hali ya hewa ya sayari yetu na mifumo ya ikolojia.” Ripoti hiyo iliendelea kusema kwamba umaskini ulimwenguni, ukosefu wa usawa, na kutumiwa sana kwa maliasili kunaweza kufanya wanadamu wakabiliane na “matatizo mbalimbali ya kimazingira, kijamii, na usalama.”

Katika 2005, shirika la Umoja wa Mataifa lilitoa ripoti ya uchunguzi wa miaka minne ya mazingira ya Dunia iliyoitwa Ukaguzi wa Milenia wa Mifumo ya Ikolojia. Uchunguzi huo wa kina ulihusisha wataalamu zaidi ya 1,360 kutoka nchi 95. Ulitoa onyo hili kali: “Shughuli za wanadamu zinalemea sana utendaji wa asili wa Dunia hivi kwamba hatuwezi kutarajia mifumo ya ikolojia iendelee kutegemeza uhai wa vizazi vijavyo.” Ripoti hiyo inaendelea kusema kwamba ili kuepuka msiba kunahitajiwa “mabadiliko makubwa katika sera, taasisi, na mazoea. Mabadiliko hayo hayapo kwa sasa.”

Anna Tibaijuka msimamizi mkuu wa Mradi wa Umoja wa Mataifa Unaoshughulikia Makao, anasema kile ambacho watafiti wengi wanaamini. Anasema hivi: “Tukiendelea kufanya mambo kama kawaida, tutakuwa na wakati ujao mbaya.”

Sababu ya Kuwa na Mtazamo Mzuri

Mashahidi wa Yehova, ambao ni wachapishaji wa gazeti hili, wanaamini kwamba hivi karibuni kutakuwa na matukio makubwa yenye kubadili mambo duniani. Hata hivyo, wanasadiki kwamba badala ya kusababisha wakati ujao mbaya, matukio hayo yatawezesha kuwe na hali nzuri zaidi kuwahi kuonekana duniani. Kwa nini wana mtazamo mzuri hivyo? Kwa sababu wana uhakika katika ahadi zinazotolewa katika Neno la Mungu, Biblia. Hebu ona mojawapo ya ahadi hizo: “Bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena; nawe hakika utapaangalia mahali pake, naye hatakuwapo. Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Zaburi 37:10, 11.

Je, tumaini hilo ni ndoto tu? Kabla ya kujibu swali hilo, fikiria jambo hili: Maelfu ya miaka iliyopita, Biblia ilitabiri kwa usahihi matatizo mengi makubwa tunayoona yakiathiri dunia na wanadamu. Tafadhali soma maandiko yanayotajwa katika habari inayofuata na ulinganishe maandiko hayo na mambo unayoona yakitendeka ulimwenguni. Unapofanya hivyo, utazidi kuwa na uhakika kwamba Biblia inatabiri kwa usahihi matukio ya wakati ujao.