Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kupata Furaha

Jinsi ya Kupata Furaha

Tunayojifunza Kutoka kwa Yesu

Jinsi ya Kupata Furaha

Siri ya kupata furaha ni nini?

▪ Yesu alitaja furaha katika maneno yake ya kwanza ya mahubiri yake yanayojulikana sana. Alisema: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Alimaanisha nini? Uhitaji wetu wa kiroho ni nini?

Ili tuendelee kuishi tunahitaji kupumua, kula, na kunywa, kama tu wanyama wanavyofanya. Lakini ili tuwe na furaha, tuna uhitaji ambao wanyama hawana, yaani, uhitaji wa kuelewa kusudi la maisha. Muumba tu ndiye aliye na uwezo wa kutosheleza uhitaji huo. Hivyo, Yesu alisema: “Mwanadamu ataishi, si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.” (Mathayo 4:4) Wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho wana furaha kwa kuwa wanamkaribia Yehova, “Mungu mwenye furaha,” anayewapatia tumaini, ambalo ni muhimu ili kupata furaha.—1 Timotheo 1:11.

Jinsi ambavyo Yesu aliwapa watu tumaini

▪ Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.” (Mathayo 5:5) Yesu aliwapa wanadamu tumaini kwa kuwaponya wagonjwa na kuwafufua watu. Pia, alileta ujumbe wa tumaini. Alieleza hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Watu wanaomtii Mungu watafurahia uzima wa milele duniani. Je, unaweza kuwazia ukiishi na watu wenye tabia-pole bila kuzeeka? Ndio sababu Neno la Mungu linasema: “Shangilieni katika tumaini.” (Waroma 12:12) Yesu alizungumzia pia jinsi ya kupata furaha sasa.

Yesu alifundisha kuhusu njia gani ya kupata furaha maishani?

▪ Yesu alitoa mashauri mazuri kuhusu marafiki, ndoa, unyenyekevu, na maoni yanayofaa kuelekea vitu vya kimwili. (Mathayo 5:21-32; 6:1-5, 19-34) Kufuata mashauri ya Yesu kutakusaidia kupata furaha.

Ukarimu huleta furaha. (Matendo 20:35) Kwa mfano, Yesu alisema hivi: “Lakini unapoandaa karamu, alika maskini, viwete, vilema, vipofu; nawe utakuwa mwenye furaha, kwa sababu hao hawana kitu cha kukulipa.” (Luka 14:13, 14) Furaha hutokana na kuwasaidia wengine wawe na furaha, na si kwa kufikiria tu furaha yetu wenyewe.

Chanzo kikuu cha furaha ni nini?

▪ Kuwasaidia watu wengine huleta furaha, lakini kufanya mambo yanayompendeza Mungu hutufanya tuwe na furaha hata zaidi. Hata furaha ya wazazi ambao watoto wao wanafanya vizuri maishani haiwezi kulinganishwa na furaha hiyo. Jambo hilo lilionekana wazi katika pindi moja Yesu alipokuwa akifundisha hadharani. “Mwanamke fulani katika umati akainua sauti yake akamwambia: ‘Lenye furaha ni tumbo la uzazi lililokuchukua wewe na maziwa uliyonyonya!’ Lakini akasema: ‘Hapana, badala yake, Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!’”—Luka 11:27, 28.

Yesu mwenyewe alipata uradhi na furaha kwa kufanya mapenzi ya Baba yake wa mbinguni. Mapenzi ya Mungu ni kwamba watu wasikie kuhusu tumaini la uzima wa milele. Yesu alimwambia hivi mtu mmoja baada ya kumweleza kuhusu tumaini hilo: “Chakula changu ni mimi kufanya mapenzi yake aliyenituma.” (Yohana 4:13, 14, 34) Wewe pia unaweza kupata furaha inayotokana na kufanya mambo yanayompendeza Mungu kwa kuwaeleza wengine kuhusu kweli za Biblia.

Kwa habari zaidi, ona sura ya 1 ya kitabu hiki, Biblia Inafundisha nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Furaha ya kweli inatokana na kutosheleza uhitaji wetu wa kuelewa kusudi la maisha