Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wamishonari Watumwa ‘Kufanya Wanafunzi’

Wamishonari Watumwa ‘Kufanya Wanafunzi’

Kuhitimu kwa Darasa la 128 la Gileadi

Wamishonari Watumwa ‘Kufanya Wanafunzi’

“ILI mataifa yote yasikie habari njema, baadhi ya Wakristo walihitaji kuwa tayari kuacha familia na nyumba zao ili kwenda kuhubiri habari njema katika nchi za kigeni.” David Splane ambaye ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alisema maneno yaliyo juu ili kuwatayarisha wasikilizaji kwa ajili ya tukio lenye kufurahisha na kujenga.

Mnamo Machi 13, 2010 (13/3/2010), watu wapatao 8,000 walikusanyika kwa ajili ya kuhitimu kwa darasa la 128 la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead). Marafiki, watu wa familia, na wageni kutoka nchi 27 tofauti-tofauti walihudhuria programu hiyo.

“Wanafunzi Hawangekaa tu Nyumbani”

Akiwa mwenyekiti, Ndugu Splane alianzisha programu hiyo kwa kuzungumzia amri hii ya Yesu: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” (Mathayo 28:19, 20) Alikazia kwamba Yesu aliwatuma wanafunzi wake waende kwa watu. Ni kweli kwamba katika Pentekoste ya 33 W.K., watu kutoka Mesopotamia, Afrika Kaskazini, na sehemu nyingi za Milki ya Roma walikuja Yerusalemu na wakasikia habari njema. Hata hivyo, msemaji huyo alisema, “wanafunzi wa Yesu hawangekaa tu nyumbani na kungoja watu kutoka katika mataifa yote waje kwao. Wangehitaji kwenda mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia ili kutafuta watu.”—Matendo 1:8.

Ndugu Splane aliendelea kusema: “Yesu hakuwaambia tu wanafunzi wake mambo ya kufanya bali aliwafundisha jinsi ya kuyafanya. Hakuwaambia tu wasali; aliwafundisha jinsi ya kusali. Hakuwaambia tu wahubiri; aliwafundisha jinsi ya kuhubiri. Hakuwaambia tu wawe walimu wazuri; aliwaonyesha mbinu za kufundisha zenye matokeo.”

Mwenyekiti huyo alielekeza fikira kwa wazazi wa wanafunzi waliohitimu na kunukuu uhakikisho huu ambao Yesu aliwapa wanafunzi wake: “Tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 28:20) Ndugu Splane aliwahakikishia wasikilizaji kuwa Yesu ataendelea kuwatunza wanafunzi wanapohubiri katika nchi nyingine.

“Jisifuni”

Anthony Morris wa Baraza Linaloongoza aliwatia moyo wahitimu ‘wajisifu.’ Alisema kuwa kuna kujisifu kunakofaa na kusikofaa. Kujisifu kusikofaa kunahusisha kujiletea utukufu sisi wenyewe. Kujisifu kunakofaa ni kule kunakotajwa katika 1 Wakorintho 1:31: “Yeye anayejisifu, na ajisifu katika Yehova.” Ndugu Morris alisema: “Hilo ndilo jambo la kujivunia, yaani, kuwa na ufahamu na ujuzi kumhusu Yehova Mungu. Kwa kweli, pendeleo kubwa zaidi ya yote—langu na lako—ni kuitwa kwa jina takatifu la Mungu, yaani, kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.”—Yeremia 9:24.

Baadaye, msemaji alikazia umuhimu wa kulijulisha jina la Yehova kwa kusimulia jambo lililoonwa na mmishonari fulani huku Afrika. Ndugu huyo mmishonari pamoja na mke wake walikuwa wanasafiri kwenda kutoa hotuba ya Biblia. Walipofika katika kituo kimoja cha ukaguzi, mwanajeshi mmoja kijana alimwelekezea ndugu huyo bunduki na kumuuliza yeye ni nani. Mke wake, ambaye alikumbuka mambo aliyojifunza katika Shule ya Gileadi, alimsogea na kumnong’onezea hivi masikioni: “Mwambie kuwa wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova na unaenda kutoa hotuba ya Biblia.” Mmishonari huyo alifanya kama alivyoshauriwa na mke wake na wakaruhusiwa kwenda. Siku iliyofuata, wenzi hao wa ndoa walisikia kwenye redio kuwa rais wa nchi hiyo alikuwa amewaambia wanajeshi wawe makini, kwa sababu ya wauaji ambao walijiita wamishonari! Kwa kujitambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova badala ya kusema kwamba wao ni wamishonari, wenzi hao wa ndoa walijiepusha na matatizo mengi. Ndugu Morris alimalizia hotuba yake kwa kusema: “Mtakapofika katika nchi mnakotumwa, mjisifu. Mjivunie yote ambayo Yehova atatimiza kupitia kazi yenu kwa utukufu wake wa milele.”

“Je, Mtatimiza Kazi Yenu?”

Geoffrey Jackson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza ambaye hapo awali alikuwa mmishonari, aliwasaidia waliokuwa wakihitimu kufikiria swali lililo juu. Aliuliza, “Tunamaanisha nini tunaposema kuwa mtu fulani ni mmishonari?” Alieleza kuwa neno “mmishonari” linatokana na neno la Kilatini linalorejelea watu au kikundi cha watu wanaopokea mgawo au kazi ya pekee. Tukiwa Mashahidi wa Yehova, kazi yetu kuu ni kuhubiri habari njema na kuwasaidia wengine wamjue Yehova na kuwasaidia wakae karibu naye. Tunapofanya kazi hii tunamwiga Yesu Kristo, ambaye wakati wote alikazia akilini kazi yake kuu duniani. Yesu alimwambia hivi Gavana Mroma Pontio Pilato: “Kwa ajili ya hili nimekuja ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.”—Yohana 18:37.

Msemaji huyo aliwasaidia wahitimu kufikiria kisa cha jiji la Yeriko. Kwa siku sita, wanaume wa vita Waisraeli waliamka asubuhi na mapema, wakavaa mavazi ya silaha, wakalizunguka jiji la Yeriko, na baadaye wakarudi nyumbani. Msemaji alisema, “Kwa maoni ya kibinadamu, kazi yao ilionekana kuwa isiyo ya akili na ya kiajabu-ajabu.” Alisema kuwa huenda baadhi ya askari-jeshi waliwaza, ‘Huku ni kupoteza wakati tu!’ Hata hivyo, katika siku ya saba, Waisraeli waliagizwa kulizunguka jiji mara saba, na kisha wapige kelele za vita. Matokeo yakawa nini? Kuta za Yeriko zilianguka pu!—Yoshua 6:13-15, 20.

Ndugu Jackson alitaja mambo manne tunayojifunza kutokana na kisa cha Yeriko. (1) Utii ni muhimu sana. Tunapaswa kufanya mambo kulingana na maagizo ya Yehova, bila kuona kuwa njia yetu ni bora. (2) Ni muhimu kuwa na imani katika Yehova na kumtegemea. “Kwa imani kuta za Yeriko zilianguka.” Hazikuangushwa kwa magogo ya kubomolea. (Waebrania 11:30) (3) Tunapaswa kuwa wenye subira. Baada ya muda, baraka za Yehova ‘zitatufikia.’ (Kumbukumbu la Torati 28:2) (4) Msikate tamaa. Msisahau kamwe kazi ambayo mmepewa. Ndugu Jackson alimalizia kwa kusema, “Mkiyatafakari mambo hayo, mtatimiza huduma yenu na hivyo kumletea Yehova sifa na utukufu.”

Mambo Mengine Makuu ya Programu

“Ipende Biblia na Mtungaji Wake.” Hicho ndicho kichwa cha hotuba ya Maxwell Lloyd, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Marekani. Aliwaambia wahitimu hivi: “Neno la Mungu linapaswa liwe hai kwenu.” Kisha akawatia moyo hivi: Msiruhusu upendo wenu kwa Yehova Mungu upoe. Msitarajie kila mtu aelewe kile mnachofundisha. Jifunzeni kufanya kweli za Biblia ziwe rahisi kueleweka ili mfikie mioyo ya wanafunzi wenu. Mwe wanyenyekevu. Msiwaonyeshe watu kwamba ninyi ni bora kwa sababu ya ujuzi wenu. Fundisheni kwa kuwaonyesha mfano. Acheni wanafunzi wenu waone kuwa mnaipenda Biblia.

‘Angalieni Kunguru.’ Michael Burnett, mwalimu wa Shule ya Gileadi ambaye alikuwa mmishonari hapo awali, alitoa hotuba yenye kichwa hicho. Alisema kuwa nyakati nyingine tutakuwa na wasiwasi. Lakini tunapaswa kukumbuka shauri hili la Yesu: “Angalieni kwamba kunguru hawapandi mbegu wala hawavuni, . . . na bado Mungu huwalisha.” (Luka 12:24) Kulingana na agano la Sheria, kunguru walikuwa ndege wasio safi na ambao hawakupaswa kuliwa. Walipaswa kuonwa kuwa chukizo. (Mambo ya Walawi 11:13, 15) Lakini, ijapokuwa ndege hao walionwa hivyo, bado Yehova aliwalisha. “Kwa hiyo, ikiwa utapatwa na wasiwasi mwingi,” akaongezea Ndugu Burnett, “wafikirie kunguru. Ikiwa Mungu aliwajali ndege walioonwa kuwa chukizo na wasio safi, je, hatakujali hata zaidi wewe ambaye ni safi machoni pake?”

‘Siwatendei Kosa.’ Mark Noumair, mwalimu mwingine wa shule hiyo, aliwasaidia wahudhuriaji kuchunguza mfano wa Yesu kuwahusu wafanyakazi katika shamba la mizabibu. Kuna wale waliofanya kazi mchana kutwa. Wengine wakafanya kazi kwa saa moja tu. Lakini, wote walipata kiwango kilekile cha mshahara! Wale waliofanya kazi kwa muda mrefu wakaanza kunung’unika. Naye bwana mwenye shamba akawaambia hivi: ‘Siwatendei kosa. Tulikubaliana dinari moja, sivyo? Chukueni kilicho chenu mwende.’ (Mathayo 20:13, 14) Funzo kwetu: Tusijilinganishe na wengine. Ndugu Noumair akasema, “Kujilinganisha na wengine kusikofaa kutafanya ukose shangwe. Zaidi ya hayo, kunaweza kukufanya uache pendeleo lako lenye thamani la utumishi.” Aliwakumbusha wahitimu kuwa Yesu ndiye anayeongoza kazi ya mavuno ya kiroho katika siku zetu na hivyo anaweza kuwatendea wafuasi wake atakavyo. Yehova na Yesu wakiamua kuwapa watumishi wengine mapendeleo zaidi, hawakutendei kosa. Wahitimu walihimizwa kuikazia fikira kazi waliyopewa na Yehova na wasiruhusu “mshahara” wa wengine uwakengeushe wasiifanye.

Mambo Yaliyoonwa na Mahojiano

Ingawa wanafunzi wa Shule ya Gileadi wanatumia wakati mwingi darasani na wakitayarisha masomo yao, bado wanajiunga na makutaniko ya karibu ya Mashahidi wa Yehova katika kazi ya kuhubiri. Sam Roberson, ambaye pia ni mwalimu wa shule hiyo, aliwahoji wanafunzi kadhaa kuhusu mambo waliyoona katika utumishi wa shambani. Kwa mfano, Dada Alessandra Kirchler alisimulia jinsi alivyokutana na mwanamke fulani ambaye alikuwa na wasiwasi kuhusu mazoea ya mwana wake ya kuvuta sigara. Baadaye, Alessandra alirudi kwa mwanamke huyo akiwa na makala ya gazeti la Amkeni! ambayo inahusu uvutaji wa sigara. Ingawa hakupata mtu nyumbani aliiacha makala hiyo. Hatimaye, Alessandra alimpata mwanamke huyo nyumbani na akakaribishwa ndani. Mama huyo aliithamini makala hiyo na akasema, “Nimekuwa nikiwaza kuhusu kile ambacho Mungu anajaribu kunifundisha kwa kuniletea majaribu haya yote.” Alessandra alimwonyesha katika Biblia kuwa Mungu hasababishi mambo mabaya. (Yakobo 1:13) Sasa mwanamke huyo na mwana wake wanafurahia funzo la Biblia.

Melvin Jones wa Idara ya Utumishi aliwahoji ndugu ambao walihitimu Shule ya Gileadi hapo awali: Jon Sommerud, ambaye anatumika Albania; Mark Anderson ambaye anatumika Kenya; na James Hinderer ambaye anatumika katika Idara ya Shule za Kitheokrasi. Wote watatu walikubali kwamba Shule ya Gileadi inawafundisha wanafunzi mafundisho muhimu ya Biblia na jinsi ya kuyatumia hata iwe wametoka wapi na wametumwa katika nchi gani.

Kisha, mwanafunzi mmoja alisoma barua ya shukrani yenye kugusa moyo kutoka kwa wanafunzi. John Barr, mwenye umri wa miaka 96, na ambaye ndiye mshiriki mzee zaidi wa Baraza Linaloongoza, alimalizia programu kwa sala, na kumwomba Yehova abariki kazi ya darasa la 128 la Shule ya Gileadi.

[Chati/Ramani katika ukurasa wa 31]

TAKWIMU ZA DARASA

Nchi zilizowakilishwa 8

Wanafunzi 54

Wenzi wa ndoa 27

Wastani wa umri 35.2

Wastani wa miaka tangu kubatizwa 19.1

Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote 13.8

[Ramani]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Wahitimu walitumwa katika nchi 25 zinazoonyeshwa hapa chini:

MIGAWO YA WAMISHONARI

HONDURAS

GUATEMALA

NIKARAGUA

JAMHURI YA DOMINIKA

ARUBA

GUYANA

EKUADO

BOLIVIA

PARAGUAI

LATVIA

RUMANIA

KOSOVO

SERBIA

ALBANIA

GUINEA

LIBERIA

CÔTE D’IVOIRE

GHANA

NAMIBIA

RWANDA

MADAGASKA

MONGOLIA

TAIWAN

KAMBODIA

INDONESIA

(NCHI INAYOSIMAMIWA NA OFISI YA TAWI YA AUSTRALIA)

[Picha katika ukurasa wa 30]

Wanafunzi wa Shule ya Gileadi wakiigiza jambo moja lililoonwa walipokuwa wanahubiri

[Picha katika ukurasa wa 31]

Darasa la 128 Lililohitimu la Shule ya Gileadi

Katika orodha iliyo chini, nambari za safu zinaanza mbele kwenda nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kwenda kulia katika kila safu.

(1) Keller, E.; Ostopowich, I.; Jacobsen, S.; Arias, M.; Dieckmann, Y.; Tanaka, J.; Harada, K.

(2) Camacho, L.; Kirchler, A.; Rodríguez, S.; Ward, B.; Trenalone, K.; Victoria, V.; Oxley, F.; Nguyen, K.

(3) Oxley, O.; De Dios, A.; Lindström, C.; Allen, J.; Meads, T.; Waddington, J.; Victoria, E.

(4) Harada, H.; Lindström, A.; Orsini, E.; Logue, D.; Missud, T.; Bergeron, S.; Camacho, G.; Ward, T.

(5) Kirchler, W.; Nguyen, H.; Kremer, E.; Burgaud, C.; Titmas, N.; De Dios, C.; Rodríguez, A.; Waddington, M.

(6) Dieckmann, J.; Allen, C.; Titmas, R.; Arias, J.; Bergeron, E.; Keller, J.; Ostopowich, F.; Burgaud, F.

(7) Tanaka, K.; Kremer, J.; Jacobsen, R.; Trenalone, J.; Logue, J.; Meads, D.; Missud, D.; Orsini, A.