Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Je, Dunia Itaharibiwa?

Je, Dunia Itaharibiwa?

▪ Watu fulani waliamini kwamba dunia ingeharibiwa Oktoba 21, 2011, lakini haikuharibiwa. Kwa hiyo, unabii wa Harold Camping, mtangazaji wa redio nchini Marekani, uliambulia patupu. Alikuwa ametabiri kwamba Siku ya Hukumu ingefika Mei 21, 2011 na tetemeko kubwa la ardhi lingeikumba dunia yote, na miezi mitano baadaye, mnamo Oktoba 21, dunia ingeangamizwa.

Hata hivyo, dunia haitaharibiwa kamwe. Muumba wa dunia hawezi kuruhusu iharibiwe. Neno lake linasema hivi: “Umeiweka dunia imara, ili ipate kuendelea kusimama.”​—Zaburi 119:90.

Hata hivyo, huenda wasomaji fulani wa Biblia wakapinga jambo hilo na kusema kwamba dunia itaharibiwa kwa moto. Ili kuunga mkono maoni yao, wanataja andiko la 2 Petro 3:7, 10 linalosema: “Kwa neno hilohilo mbingu na dunia za sasa zimewekwa akiba kwa ajili ya moto nazo zinahifadhiwa mpaka ile siku ya hukumu na ya kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu. . . . Lakini siku ya Yehova itakuja kama mwizi, ambayo katika hiyo mbingu zitapitilia mbali kwa kelele ya kuvuma, lakini vitu vyake vya msingi vikiwa moto sana vitayeyushwa, na dunia na kazi zilizo ndani yake zitafunuliwa.” Je, maneno ya mtume Petro yanapaswa kueleweka kihalisi?

La, hasha. Kwa nini? Kwa sababu ufafanuzi wa mistari hiyo unapaswa kupatana na muktadha wa barua ya Petro na sehemu nyingine zote za Biblia. Kihalisi, maneno hayo yanaweza kumaanisha kwamba mbingu, au ulimwengu—unaotia ndani mabilioni ya mabilioni ya nyota na sayari nyingine—utateketezwa kwa moto kwa sababu tu sehemu moja ndogo sana ya ulimwengu huo mkubwa inakaliwa na wanadamu waovu. Je, ungeharibu eneo kubwa la mchanga kwenye ufuo wa bahari kwa sababu tu chembe moja ya mchanga huo ni mbaya? Huo ungekuwa upumbavu! Kwa hiyo, Yehova hataharibu ulimwengu wote aliouumba kwa sababu tu uasi ulitokea katika sehemu moja ya uumbaji wake.

Isitoshe, maoni kama hayo yanapingana moja kwa moja na maneno ya Yesu Kristo aliyesema: “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.” (Mathayo 5:5; Zaburi 37:29) Je, baba mwenye upendo anaweza kujenga nyumba nzuri kwa ajili ya familia yake, kisha aiteketeze? (Zaburi 115:16) Hilo ni jambo lisilopatana na akili! Kwa kuwa Yehova ni Muumba na pia Baba mwenye upendo.​—Zaburi 103:13; 1 Yohana 4:8.

Petro anatumia neno “dunia” kwa njia ya mfano, akirejelea jamii ya wanadamu—yaani, wanadamu waovu. Ona kwamba Petro analinganisha uharibifu huo na Gharika ya siku za Noa. (2 Petro 3:5, 6) Wakati huo, wanadamu waovu tu ndio walioharibiwa; lakini dunia yenyewe, na Noa aliyekuwa mwadilifu pamoja na familia yake, hawakuharibiwa. Pia, Petro anatumia neno “mbingu” kwa njia ya mfano. Katika andiko hilo, “mbingu” zinarejelea utawala wa wanadamu juu ya watu wasiomwogopa Mungu. Hivyo, waovu wasiotaka kubadilika watatoweka. Pia, serikali zote mbovu zitayeyushwa na mahali pake pachukuliwe na utawala wa mbinguni, au Ufalme wa Mungu.​—Danieli 2:44.

Kwa hiyo, je, dunia itaharibiwa? Hapana. Dunia ya mfano ndiyo itakayoharibiwa, yaani, jamii wa wanadamu waovu. Dunia yenyewe itadumu milele, kutia ndani wanadamu wenye kumwogopa Mungu.​—Methali 2:21, 22.