Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Mungu Anawajali Wanawake?

Je, Kweli Mungu Anawajali Wanawake?

“Dhambi ilianza na mwanamke, na kwa sababu ya mwanamke lazima sote tufe.”​—KITABU CHA KIAPOKRIFA KINACHOITWA ECCLESIASTICUS, KARNE YA PILI K.W.K.

“Wewe ni lango la ibilisi: uliufunua ule mti uliokatazwa: wewe ndiye wa kwanza kuasi sheria za Mungu . . . Uliharibu kwa urahisi mfano wa Mungu, yaani, mwanamume.”​—TERTULLIAN, KATIKA KITABU ON THE APPAREL OF WOMEN, KARNE YA PILI W.K.

MANENO hayo yaliyoandikwa kale hayapatikani katika Biblia. Kwa karne nyingi, yametumiwa kutetea ubaguzi dhidi ya wanawake. Hata leo, watu fulani wenye msimamo mkali bado wananukuu maandishi ya kidini ili kutetea ukandamizaji wa wanawake, wakidai kwamba wanawake ndio chanzo cha matatizo yanayowapata wanadamu. Je, Mungu alikusudia wanawake wadharauliwe na kutendewa vibaya na wanaume? Biblia inasema nini? Acheni tuone.

Hapana. Badala yake “yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi,” ndiye ‘aliyelaaniwa’ na Mungu. (Ufunuo 12:9; Mwanzo 3:14) Mungu aliposema kwamba Adamu ‘angemtawala’ mke wake, Mungu hakuwa akimruhusu mwanamume amkandamize mwanamke. (Mwanzo 3:16) Alikuwa tu akitabiri matokeo mabaya ya dhambi ambayo yangewapata wenzi wawili wa kwanza.

Hivyo, kutendwa vibaya kwa wanawake ni matokeo ya moja kwa moja ya dhambi ambayo wanadamu walirithi, bali si mapenzi ya Mungu. Biblia haiungi mkono wazo la kwamba ni lazima wanaume wawakandamize wanawake ili kulipia ile dhambi ya kwanza.—Waroma 5:12.

Je, Mungu alimuumba mwanamke akiwa duni kuliko mwanamume?

Hapana. Andiko la Mwanzo 1:27 linasema: “Mungu akamuumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimuumba; mwanamume na mwanamke aliwaumba.” Hivyo, tangu mwanzoni, wanadamu wote—wanaume na wanawake—waliumbwa wakiwa na uwezo wa kuonyesha sifa za Mungu. Ingawa Adamu na Hawa waliumbwa kwa njia iliyotofautiana kihisia na kimwili, wote walipokea mgawo uleule na walifurahia mapendeleo yaleyale kutoka kwa Muumba wao.—Mwanzo 1:28-31.

Kabla ya kumuumba Hawa, Mungu alisema hivi: “Nitamfanyia [Adamu] msaidizi, awe kikamilisho chake.” (Mwanzo 2:18) Je, neno “kikamilisho” linamaanisha kwamba mwanamke alikuwa duni kuliko mwanaume? Hapana, kwa sababu neno hilo la Kiebrania linaweza pia kutafsiriwa kuwa “mshirika” au “msaada unaolingana na” mwanamume. Fikiria majukumu ya daktari mpasuaji na ya mtaalamu wa dawa za kupunguza maumivu wakati wa upasuaji. Je, mmoja anaweza kufanya kazi bila mwenzake? Huenda asiweze! Ingawa daktari mpasuaji ndiye hufanya upasuaji, je, yeye ni wa maana zaidi? Hatuwezi kusema hivyo. Vivyo hivyo, Mungu alimuumba mwanamume na mwanamke ili washirikiane kwa ukaribu, bali si kushindana.—Mwanzo 2:24.

Ni nini kinachoonyesha kwamba Mungu anawajali wanawake?

Huku akijua kimbele jinsi ambavyo wanaume wasio wakamilifu wangetenda, tangu zamani Mungu alionyesha kwamba alikusudia kuwalinda wanawake. Akizungumza kuhusu Sheria ya Musa ambayo ilianza kutumika katika karne ya 16 K.W.K., katika kitabu chake La Bible au féminin (Biblia Katika Jinsia ya Kike) mwandishi Laure Aynard, aliandika hivi: “Mara nyingi, agano la Sheria linawatetea wanawake linapozungumza kuwahusu.”

Kwa mfano, Sheria iliagiza Waisraeli wamheshimu baba na pia mama. (Kutoka 20:12; 21:15, 17) Vilevile, Sheria iliagiza kwamba mwanamke mwenye mimba atendewe kwa ufikirio. (Kutoka 21:22) Hata leo, ulinzi uliotolewa na sheria hizo za Mungu ni kinyume kabisa na ukosefu wa haki za kisheria ambao wanawake wengi wanakabiliana nao katika sehemu nyingi ulimwenguni. Lakini kuna mambo mengine yanayoonyesha kwamba Mungu anawajali.

Sheria Inayoonyesha Maoni ya Mungu Kuwaelekea Wanawake

Sheria ambayo Yehova Mungu aliwapa Waisraeli iliwapa wote, wanaume na wanawake, faida nyingi sana za kimwili, kiadili, na kiroho. Kama taifa hilo lingeendelea kusikiliza na kutii, lingekuwa “juu ya mataifa mengine yote ya dunia.” (Kumbukumbu la Torati 28:1, 2) Mwanamke alikuwa na daraka gani chini ya Sheria? Fikiria mambo yafuatayo.

1. Walikuwa na uhuru wa kibinafsi. Tofauti na wanawake katika mataifa mengine mengi ya zamani, wanawake Waisraeli walifurahia uhuru mwingi sana. Ingawa mume alipewa daraka la kuwa kichwa cha familia, mke, akiwa na kibali cha mume wake, ‘angefikiria shamba na kulinunua’ na ‘kupanda shamba la mizabibu.’ Ikiwa alikuwa na ujuzi wa kusokota na kufuma, angeweza hata kufanya biashara yake. (Methali 31:11, 16-19) Chini ya Sheria ya Musa, wanawake walionwa kuwa watu wenye haki za kibinafsi.

Katika Israeli la kale, wanawake walikuwa pia na uhuru wa kuwa na uhusiano wa kibinafsi pamoja na Mungu. Biblia inazungumza kumhusu Hana, ambaye alisali kwa Mungu kuhusu jambo la kibinafsi na akaweka nadhiri kisiri. (1 Samweli 1:11, 24-28) Mwanamke fulani katika jiji la Shunemu alikuwa akizungumza na nabii Elisha siku za Sabato. (2 Wafalme 4:22-25) Mungu aliwatumia wanawake, kama vile Debora na Hulda ili wamwakilishe. Inapendeza kuona kwamba wanaume wenye vyeo na makuhani walikuwa tayari kutafuta mashauri kutoka kwa wanawake hao.—Waamuzi 4:4-8; 2 Wafalme 22:14-16, 20.

2. Waliruhusiwa kupata elimu. Kwa sababu walikuwa sehemu ya agano la Sheria, wanawake walikaribishwa kusikiliza Sheria iliposomwa, na hilo liliwapa fursa za kujifunza. (Kumbukumbu la Torati 31:12; Nehemia 8:2, 8) Pia, walizoezwa kushiriki katika migawo fulani ya ibada ya hadharani. Kwa mfano, inaelekea wanawake fulani walifanya “utumishi uliopangwa” kwenye hema la kukutania, huku wengine wakishiriki katika kikundi cha waimbaji kilichokuwa pia na wanaume.—Kutoka 38:8; 1 Mambo ya Nyakati 25:5, 6.

Wanawake wengi walikuwa na ujuzi na ustadi uliohitajiwa ili kufanya biashara na kupata faida. (Methali 31:24) Kinyume na tamaduni katika mataifa mengine siku hizo, ambako baba peke yake ndiye aliyewafundisha wanawe, akina mama Waisraeli walishiriki kuwafundisha watoto wao wa kiume mpaka walipokuwa watu wazima. (Methali 31:1) Bila shaka, wanawake katika Israeli la kale walikuwa wenye elimu.

3. Walistahiwa na kuheshimiwa. Zile Amri Kumi zilisema hivi waziwazi: “Mheshimu baba yako na mama yako.” (Kutoka 20:12) Katika methali za Mfalme Solomoni mwenye hekima, tunasoma hivi: “Mwanangu, sikiliza nidhamu ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako.”—Methali 1:8.

Sheria ilitia ndani maagizo mengi kuhusu jinsi watu ambao hawajaoana walipaswa kutendeana, na hivyo kuwaheshimu wanawake. (Mambo ya Walawi 18:6, 9; Kumbukumbu la Torati 22:25, 26) Mume mzuri alipaswa kufikiria uwezo wa kimwili na kimaumbile wa mke wake.—Mambo ya Walawi 18:19.

4. Haki ya kulindwa. Katika Neno lake, Yehova anajirejelea kuwa “baba ya wavulana wasio na baba na mwamuzi wa wajane.” Kwa maneno mengine, alikuwa Mlinzi wa wale ambao haki zao hazikulindwa na baba au mume. (Zaburi 68:5; Kumbukumbu la Torati 10:17, 18) Hivyo, pindi moja mjane fulani wa nabii alipotendewa isivyo haki na mkopeshaji, Yehova aliingilia kati na kufanya muujiza ili yule mjane alipe deni lake na kudumisha heshima yake.​—2 Wafalme 4:1-7.

Kabla ya Waisraeli kuingia katika ile Nchi ya Ahadi, kichwa cha familia aliyeitwa Selofehadi alikufa bila kuacha mwana. Hivyo, binti zake watano wakamwomba Musa awape “miliki” katika Nchi ya Ahadi. Yehova alifanya mengi zaidi ya yale waliyoomba. Alimwambia hivi Musa: “Wape miliki ya urithi katikati ya ndugu za baba yao, nawe utaupitisha urithi wa baba yao kwao.” Tangu wakati huo na kuendelea, wanawake katika Israeli wangepewa urithi na baba zao na wangewaachia watoto wao urithi huo.​—Hesabu 27:1-8.

Maoni ya Mungu Kuhusu Wanawake Yapotoshwa

Chini ya Sheria ya Musa, wanawake walitendewa kwa heshima na haki zao ziliheshimiwa. Hata hivyo, kuanzia karne ya nne K.W.K., dini ya Kiyahudi ilianza kuiga tamaduni za Wagiriki, ambao waliwaona wanawake kuwa duni.​—Ona sanduku lenye kichwa “Ubaguzi Dhidi ya Wanawake Katika Maandishi ya Kale.”

Kwa mfano, mtunga-mashairi Mgiriki Hesiod (aliyeishi karne ya nane K.W.K.) aliwalaumu wanawake kwa sababu ya matatizo yote yanayowapata wanadamu. Katika shairi lake linaloitwa Theogony, alizungumza kuhusu “jamii na kabila hatari la wanawake ambao wanaishi katikati ya wanaume na kuwasababishia matatizo mengi.” Wazo hilo liliingizwa katika dini ya Kiyahudi mwanzoni mwa karne ya pili K.W.K. Talmud, ambayo ilianza kuandikwa katika karne ya pili W.K. na kuendelea, iliwaonya wanaume hivi: “Msizungumze sana na wanawake, kwa sababu hilo litawaingiza katika upotovu wa maadili.”

Kwa karne nyingi, maoni hayo yaliyopotoka yameathiri sana daraka la wanawake katika jamii ya Wayahudi. Katika siku za Yesu, tayari wanawake walikuwa wamewekewa mipaka kwenye eneo la hekalu na waliruhusiwa tu kuingia kwenye Ua wa Wanawake. Wanaume tu ndio waliopokea elimu ya kidini, na inaelekea wanawake walitengwa na wanaume kwenye masinagogi. Talmud inanukuu maneno haya ya Rabi mmoja: “Yeyote anayemfundisha binti yake Torati [Sheria] anamfundisha mambo machafu.” Kwa kupotosha maoni ya Mungu, viongozi wa kidini Wayahudi waliwafanya wanaume wengi wawadharau wanawake.

Alipokuwa duniani, Yesu aliona ubaguzi kama huo ambao ulikuwa umekita mizizi katika mapokeo. (Mathayo 15:6, 9; 26:7-11) Je, Yesu alifuata mapokeo hayo alipokuwa akishughulika na wanawake? Tunaweza kujifunza nini kutokana na tabia na mtazamo wake? Je, Ukristo wa kweli umewaletea wanawake kitulizo? Makala inayofuata itajibu maswali hayo.