Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Barua Kutoka Baraza Linaloongoza

Barua Kutoka Baraza Linaloongoza

Ndugu na Dada Wapendwa:

Kwa unyenyekevu, nabii Isaya aliamini kwamba Ufalme wa Yuda ulifanikiwa na kusitawi kwa sababu ya baraka za Yehova. Kama tunavyosoma kwenye Isaya 26:12, nabii huyo alisema: “Ee Yehova, . . . umetenda kazi zetu zote kwa ajili yetu.” Sisi pia tunakubaliana na maneno hayo tunapotafakari yote ambayo tulitimiza mwaka wa utumishi uliopita. Kwa kweli, Yehova anafanya “mambo ya ajabu ambayo hayajapata kuumbwa” kamwe! (Kut. 34:10) Hebu chunguza baadhi ya baraka hizo.

Tovuti yetu rasmi, jw.org, imetumiwa kwa njia kubwa. Tovuti hii inapatikana katika lugha zaidi ya 600, na machapisho yanaweza kusomwa au kupakuliwa kwa lugha zaidi ya 750. Tovuti hii imewasaidia jinsi gani watu wanyofu kujua ukweli? Fikiria mfano huu: Wenzi fulani wa ndoa walivunjika moyo baada ya kuona unafiki wa dini. Katika jitihada zao za kutafuta mwongozo wa kiroho, waliipata tovuti yetu. Walianza kusoma kwa ukawaida machapisho na kutazama video katika tovuti hiyo. Walipakua kijitabu Kuyachunguza Maandiko Kila Siku na wakaanza kusoma kila siku pamoja na binti na mwana wao. Siku ambayo Mashahidi wa Yehova waliwatembelea walikuwa wakisoma andiko la siku. Mashahidi walitambua kwamba familia hiyo ilikuwa imefanya mabadiliko makubwa kwa sababu ya yale waliyojifunza katika tovuti yetu. Hata kabla ya kukutana na Mashahidi wa Yehova, walikuwa wameondoa alama walizojichora mwilini, wakaharibu sanamu, wakaacha kusherehekea sikukuu za ulimwengu na pia kutazama sinema chafu. Habari hii ilipokuwa ikiandikwa, wenzi hao na binti yao tayari walikuwa wahubiri ambao hawajabatizwa, na wazazi wanapanga kubatizwa hivi karibuni.

Tumepokea shukrani nyingi kwa ajili ya uandalizi mwingine, yaani, JW Broadcasting. Programu hii ya kila mwezi inapatikana katika lugha zaidi ya 70, na idadi hiyo itazidi kuongezeka. Familia nyingi hutazama programu hii wakati wa Ibada ya Familia. Ndugu mmoja alisema: “Tengenezo la Yehova linaendelea kukua, hata hivyo, tunahisi tukiwa karibu zaidi na Baraza Linaloongoza!”

Makusanyiko ni nyakati za pekee kwa watu wa Yehova, na ilikuwa hivyo kwa makusanyiko yaliyofanywa katika mwaka wa utumishi wa 2015. Programu hiyo ilitia ndani jumla ya video na picha 42 na pia nyimbo za pekee sita ambazo zilichezwa kabla ya kila kipindi cha programu kuanza. Ndugu mmoja mkomavu alisema hivi kuhusu programu hiyo: “Hakuna aliyetaka kuondoka kwenye kiti programu ilipokuwa ikiendelea, ili asikose chochote.” Dada mmishonari alisema, “Video zilifanya kweli na Ufalme uwe halisi zaidi kwangu.”

Mwaka huo pia, Yehova alitubariki kwa nyimbo mpya za Ufalme. Wenzi fulani wa ndoa waliandika hivi: “Nyimbo mpya ni kama kukumbatiwa na Yehova. Zimetufariji sana wakati wa magumu.” Makusanyiko hayo yalitukumbusha upendo na jitihada zinazofanywa na kikundi cha wanamuziki cha Watchtower ili kutusaidia tumsifu Yehova.

Tunawatia moyo kumwiga Yehova kwa kuwakaribisha kwa upendo wale wote wanaorudi

Je, kutaniko lenu linahubiri hadharani kwa kutumia vigari vya kukokotwa? Njia hiyo ya kuhubiri imekuwa na matokeo mazuri! Baadhi ya watu wanaoishi kwenye majengo ambayo watu wasio wapangaji hawaruhusiwi kuingia wamehubiriwa, na watu wengine kutia ndani Mashahidi wasiotenda wamesaidiwa kiroho. Januari 2015, mwanamume fulani nchini Korea Kusini alifika kwenye kigari cha machapisho. Alieleza kwamba hivi karibuni amekuwa akifikiria sana mambo ya kiroho. Funzo la Biblia likaanzishwa. Alihudhuria mkutano wa kutaniko kwa mara ya kwanza mwezi wa Februari, na Machi akaacha kuvuta sigara. Mwezi wa Aprili, alitembelea ofisi ya tawi ya Korea Kusini na anaendelea kufanya maendeleo. Hilo ni mojawapo ya masimulizi mengi ambayo tumepokea hapa makao makuu.

Tunasali kwamba broshua tuliyopokea kusanyikoni itawachochea waliopoa kiroho wamrudie Yehova kabla haijawa kuchelewa! Tunawatia moyo kumwiga Yehova kwa kuwakaribisha kwa upendo wale wote wanaorudi.—Eze. 34:16.

Kwa kweli, Yehova amewabariki watu wake katika mwaka wa utumishi uliopita. Tunatazamia nini zaidi? Acheni tusubiri. Kwa sasa, iweni na uhakika kwamba sisi, washiriki wa Baraza Linaloongoza, tunawapenda sana na pia tunasali daima kwa ajili yenu.

Tunawatakia mema,

Ndugu zenu,

Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova