Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Canada: Kijiji cha Wainuit wa Kangirsuk, kaskazini mwa Quebec

MATUKIO MUHIMU YA MWAKA ULIOPITA

Habari Fupi—Kutoka Sehemu Mbalimbali Ulimwenguni

Habari Fupi—Kutoka Sehemu Mbalimbali Ulimwenguni

Kuwafikia Watu Wote wa Kanada

Video yenye kichwa Kwa Nini Ujifunze Biblia? imetafsiriwa katika lugha nane za kienyeji ili kukidhi uhitaji wa watu katika eneo la ofisi ya tawi ya Kanada. Kampeni ya siku kumi iliyofanywa mwezi wa Oktoba 2014 katika eneo lenye baridi kali la Nunavik, video ya lugha ya Inuktitut ilionyeshwa karibu kila nyumba katika jamii 14 zenye jumla ya watu zaidi ya 12,000.

Meneja Alivutiwa

Katika mwezi wa Septemba 2014, kusanyiko la kimataifa lilifanywa katika Uwanja wa Michezo wa Kimataifa wa Sangam huko Seoul nchini Korea Kusini. Wahudhuriaji zaidi ya 56,000 walifurahia programu hiyo. Meneja wa uwanja huo aliwashukuru Mashahidi kwa mwenendo wao mzuri na jinsi walivyojiendesha kusanyikoni. Alisema: “Kila mtu alijiendesha kwa njia nzuri. Nilishangaa kuona wakisafisha uwanja vizuri zaidi kuliko wataalamu wetu wa usafi. Ninatamani wataalamu wetu wangekuwa na mtazamo kama huo wanapofanya kazi yao. Ikiwa tunataka kuwa wanadini wazuri, tunahitaji kuwa kama Mashahidi wa Yehova.”

South Korea: Kusanyiko la kimataifa la mwaka 2014 jijini Seoul

Yehova Aliandaa Mazoezi Tuliyohitaji

Mwezi wa Mei 2012, serikali ya Sweden ilikataa ombi la Mashahidi wa Yehova la kupata faida inayotolewa kwa mashirika ya kidini. Baraza linaloongoza liliidhinisha kibali ili kukata rufaa kwa Mahakama Kuu Zaidi ya Usimamizi.

Mahakama iliamua kusikiliza maelezo yao kabla ya kufikia uamuzi. Ndugu kutoka nchi mbalimbali walikutana ili kujadiliana jinsi ya kujibu maswali ambayo huenda wangeulizwa. Walifanya mazoezi hayo katika Jumba la Ufalme la Stockholm.

Mazoezi yalipokuwa yakiendelea, kengele ya mlango wa jumba ikaita. Ndugu alifungua mlango na kuwakuta wasichana wawili wenye umri wa miaka 13 na 14, nao wakajitambulisha. Walisema kwamba wanataka kuuliza maswali fulani kuhusu Mashahidi wa Yehova. Ndugu anakumbuka hivi: “Nilitaka kuwaambia waje siku nyingine, kwa kuwa siku hiyo tulikuwa na shughuli nyingi na tusingependa kukatizwa.”

Hata hivyo, ndugu huyo aliamua kuzungumza na wasichana hao. Walikuwa na maswali mengi sana, baadhi ya maswali yalihusu masuala ya kijamii na kupiga kura. Baadaye, ndugu huyo alirudi na kuwasimulia ndugu wengine kuhusu maswali ambayo wasichana hao waliuliza na jinsi alivyojibu.

Siku iliyofuata, ndugu walishangaa kwamba mahakama iliuliza maswali mengi sawa na yale ambayo wasichana hao waliuliza. Ndugu aliyewakilisha tengenezo alisema hivi: “Ningekuwa na wasiwasi kwa sababu ya kusimama mbele ya wanasheria mashuhuri nchini, lakini nilikuwa mtulivu sana. Nilihisi kwamba Yehova amethibitika kuwa pamoja nasi kwa kutupatia mazoezi ambayo tuliyahitaji siku iliyotangulia.”

Mahakama ilikubali ombi letu, na kesi hiyo imerudishwa tena serikalini ili kufanyiwa upya uamuzi.

Gunia la Mchele la Ken

Ken ni mvulana mwenye umri wa miaka sita, anayeishi nchini Haiti. Alifurahi sana kujua kwamba hivi karibuni kutaniko lao litajengewa Jumba la Ufalme. Hivyo aliamua kutengeneza kwa siri sanduku dogo la michango na kulificha chumbani kwake. Badala ya kutumia pesa anazopewa na wazazi wake kutumia shuleni, aliziweka katika sanduku. Aliendelea kufanya hivyo kwa uaminifu mpaka kikosi cha ujenzi wa Jumba la Ufalme kilipofika kuanza kazi. Kisha, akawapa sanduku lake la michango, ambalo lilikuwa na pesa za kutosha kununua gunia la mchele. Kwa siku nyingi, mchele wa Ken ulitumika kwa ajili ya mlo wa mchana.

Ruhusa ya Jenerali

Kati ya mambo muhimu ya mwaka uliopita, ilikuwa kupata kibali maalumu cha kuingia maeneo ya nchi ya Sierra Leone yaliyokuwa na vizuizi kwa sababu ya mlipuko wa ugonjwa wa Ebola. Kwa mfano, waangalizi wa mizunguko walihitaji kuwa na vibali vyao na vya magari ili kuingia maeneo hayo, ilikuwa hivyo kwa waliosafirisha machapisho na vitu vingine. Washiriki wa Halmashauri ya Kutoa Msaada walihitaji kupeleka vifaa vya matibabu na chakula. Inapendeza kwamba walipata vibali wakati wote walipovihitaji.

Kuna jambo moja lililoonwa linaloimarisha sana imani. Ndugu walipeleka barua ya maombi ili kupata vibali 34 na ruhusa ya kupitisha magari 11, hata hivyo, walihitaji kuonana na jenerali wa jeshi ili kuidhinisha ombi lao. Ndugu wawili kutoka ofisi ya tawi walikutana na jenerali huyo siku ambayo walitarajia kupata vibali vya kuingia. Hata hivyo, barua yao ya maombi haikupatikana. Ndugu waliambiwa waitafute wenyewe kwenye rundo la barua za maombi, lakini hawakufanikiwa. Wakati huohuo, jenerali alimwambia karani kuwa anataka kufunga ofisi yake na hatapokea ombi lolote mpaka baada ya majuma mawili. Ndugu walisali kwa bidii ili wapate msaada wa Yehova kuhusu jambo hilo. Kisha jenerali huyo aliwatazama akina ndugu na kuwauliza, “Mnahitaji vibali vingapi?” Alipojulishwa idadi, aliamka kwenye kiti na kusema kwa sauti ya juu, “Ni vingi mno!”

Ndugu walimweleza kuhusu kazi yetu na jinsi misaada ilivyowanufaisha waliokumbwa na ugonjwa wa Ebola. Jenerali huyo alitulia kidogo, kisha akamwambia karani wake, “Wape kila kitu wanachohitaji.”

Guinea and Sierra Leone: Usafi wa mikono ulizingatiwa katika Majumba ya Ufalme