Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MATUKIO MUHIMU YA MWAKA ULIOPITA

Kuwekwa Wakfu kwa Ofisi za Tawi

Kuwekwa Wakfu kwa Ofisi za Tawi

“MOYO wangu umejawa na shangwe,” akasema dada mmoja katika programu ya kuweka wakfu ofisi ya tawi ya Madagaska, Jumamosi Januari 24, 2015. Dada huyo pamoja na wageni 583 walisisimuka kuona vyumba vipya 19 vya makao, chumba kikubwa cha kulia na chumba cha jiko kilichorekebishwa. Ofisi zilizoongezwa ukubwa ni idara ya Utumishi, Hesabu, na Idara ya Mahali ya Usanifu-Majengo na Ujenzi. Kwa kuongezea, Idara ya Kurekodi na Idara ya Lugha ya Ishara [alama] zilipata studio mpya na Idara ya Maandishi ya Vipofu ilianzishwa. Baada ya kusikiliza historia ya kazi ya kuhubiri nchini Madagaska, wahudhuriaji walifurahi kusikiliza hotuba ya wakfu iliyotolewa na Mark Sanderson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza.

Vyumba vipya 19 vya makao katika ofisi ya tawi ya Madagaska

Watu wa Yehova jijini Jakarta, Indonesia, walifarijika sana maji ya mafuriko yalipopungua siku ya kuwekwa wakfu majengo ya ofisi ya tawi Februari 14, 2015. Kwa sasa ofisi hiyo iko katika ghorofa moja kwenye jengo la ghorofa 42 na kuna ghorofa 12 katika jengo lililo jirani. Ofisi za idara mbalimbali za Betheli zipo katika majengo yaliyo jirani. Anthony Morris mshiriki wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba ya wakfu, na siku inayofuata watu 15,257 walikusanyika katika uwanja wa michezo ili kusikiliza hotuba yenye kichwa “Endeleeni Kufanya Kazi Zilizo Njema.” Programu hiyo iliunganishwa katika maeneo 41 na watu 11,189 walisikiliza, huo ulikuwa mkutano mkubwa kuliko yote iliyowahi kufanywa na watu wa Yehova nchini Indonesia. Ronald Jacka, mmishonari wa kwanza kuingia nchini humo, alisema: “Nilipowasili mwaka wa 1951, kulikuwa na wahubiri 26 nchi nzima. Hata hivyo, leo watu zaidi ya 26,000 wamehudhuria programu hii ya pekee. Kwa kweli, Yehova amewabariki watu wake nchini Indonesia!”