Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tanzania: Wapita njia wakifurahia machapisho kwenye vigari jijini Dar es Salaam

MATUKIO MUHIMU YA MWAKA ULIOPITA

Kuwafikia Watu Wasiofikiwa

Kuwafikia Watu Wasiofikiwa

INGAWA mahubiri ya nyumba kwa nyumba yanaendelea kuwa njia kuu ambayo Mashahidi wa Yehova hutumia kueneza kweli ya Biblia, kutumia meza na vigari vya machapisho kumethibitika kuwa njia yenye matokeo ya kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mt. 24:14) Wahubiri wa Ufalme wametumia vigari, meza na vibanda kuwafikia watu katika maeneo ya umma. Kwa kuongezea, vigari vya machapisho 250,000 viligawanywa katika makutaniko duniani kote. Kumekuwa na matokeo gani?

Katika jiji la Dar es Salaam nchini Tanzania, watu karibu 700 wameomba funzo la Biblia tangu mpango huo wa pekee wa kuhubiri hadharani ulipoanza mwaka 2014. Watu wengi wanaopendezwa wanahudhuria mikutano na wanajitahidi kumkaribia Mungu. Kwa mwaka mmoja, watu kutoka Afrika na maeneo mengine wamechukua nakala zaidi ya 250,000 kutoka kwenye vigari vya machapisho.

Katika Visiwa vya Solomoni, wahubiri wanaokaribia 2,000 wanahubiri eneo kubwa sana lenye visiwa zaidi ya 300. Mahubiri ya pekee ya hadharani yamekuwa njia bora sana ya kueneza mbegu za kweli. Katika mji mkuu wa Honiara, ndugu waligawa magazeti zaidi ya 104,000 na broshua zaidi ya 23,600, na watu wengi waliopata machapisho walitoka katika visiwa na vijiji vya mbali ambako hakuna Mashahidi. Alasiri moja pekee, waligawa nakala 400 za kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? na watu 60 waliomba funzo la Biblia.

Asubuhi moja, mapainia wa kawaida wawili Michael na Linda waliweka kigari cha machapisho karibu na ufukwe wa bahari wa Visiwa vya Margarita nchini Venezuela. Mwanaume mmoja anayeitwa Aníbal alikaribia kigari na kuchukua kitabu Biblia Inafundisha. Aliwaeleza mapainia hao kuwa baba yake alikufa ufukweni hapo miaka saba iliyopita, na tangu wakati huo mama yake ameugua mshuko wa moyo. Juma lililofuata Aníbal alirudi na kuwaambia Michael na Linda kwamba siku hiyo ni kumbukumbu ya kifo cha baba yake. Aníbal alichukua simu na kumpigia mama yake, na akamwomba Michael amfariji. Michael alikubali. Tangu wakati huo mama ya Aníbal huwapigia simu Michael na Linda, nao humfariji kwa maandiko. Katika ujumbe wa simu, mama ya Aníbal aliandika, “Leo ninajihisi vizuri zaidi kwa sababu mmenifariji na kunisaidia kuimarisha imani yangu.”

Mahubiri ya pekee ya hadharani yamepangwa katika maeneo 127 ndani ya miji 14 nchini Marekani. Kwa kipindi cha miezi saba ya kwanza ya mwaka wa utumishi wa 2015, mafunzo ya Biblia 8,445 yalianzishwa! Njia hii ya kutoa ushahidi imewasaidia wengi walioacha kushirikiana nasi warudie ibada ya kweli. Kwa mfano, mwanaume anayeitwa Terry alikuwa akitazama machapisho kwenye kigari huko Los Angeles, California, kwa hiyo, wenzi wa ndoa Mashahidi walimuuliza ikiwa amewahi kusoma machapisho yetu. Aliwajibu kwamba yeye ni Shahidi wa Yehova, lakini aliacha kutenda kwa karibu miaka minne. Wenzi hao walisoma na kuzungumzia andiko la Ezekieli 34:11, ambalo Yehova anasema hivi: “Mimi mwenyewe, nami nitawatafuta kondoo zangu na kuwatunza.” Walimweleza kuhusu tovuti yetu na JW Broadcasting. Asubuhi ya siku iliyofuata, Terry alimwandikia barua pepe ndugu na kumweleza kwamba kabla ya kuona kigari cha machapisho, alikuwa amesali kwa Yehova amsamehe kwa sababu aliacha kuhudhuria mikutano. Pia, alikuwa amesali ili aweze kumkaribia Yehova. Terry alisema hivi “Kisha mkanisalimu kwa uchangamfu. Mkanisomea andiko zuri na kunisaidia kupata habari nilizohitaji ili kurudi katika tengenezo la Yehova. Sala yangu ilijibiwa.”

Katika mji wa Addis Ababa nchini Ethiopia, kuna maeneo manne ambayo mahubiri ya hadharani ya pekee hufanywa. Kwa miezi mitatu ndugu waligawa machapisho 37,275, na watu 629 waliomba kutembelewa na Mashahidi. Miongoni mwa watu waliochukua kitabu Biblia Inafundisha ni mwanaume mmoja mzee aliyeanza kukisoma mara moja. Aliwahi kusoma katika seminari ya kidini, na alikuwa na maswali mengi kuhusu Yesu na Ufalme wa Mungu. Hivyo, siku iliyofuata, alienda kwenye kigari cha machapisho ili kujibiwa maswali yake. Baadaye, akakubali kujifunza Biblia, na mwishoni mwa juma hilo alihudhuria mkutano kwa mara ya kwanza. Sasa anahudhuria mikutano yetu kwa ukawaida na anafanya maendeleo mazuri.

Ethiopia: Machapisho ya lugha ya Kiamhara kwenye kigari cha machapisho jijini Addis Ababa

Mwanaume Myahudi nchini Mexico alikaribia kigari cha machapisho na kuwauliza ndugu wawili ikiwa wana chapisho lolote linalozungumzia kifo. Walimjibu kwamba wameishiwa magazeti yanayozungumzia kifo, hata hivyo, walimpatia chapisho linaloeleza kuhusu wakati ujao. Mwanaume huyo akaushika mkono wa ndugu, na kusema: “Mimi sitaki kujua kuhusu wakati ujao. Ninataka kujiua.” Kisha akaanza kulia. Ndugu walitaka kujua kilichosababisha ahisi hivyo. Akawajibu kwa huzuni:“Nimefiwa na mtoto wangu.” Hivyo, wakamwonyesha sura ya 7 ya kitabu Biblia Inafundisha. Wakamsomea mafungu mawili ya kwanza chini ya kichwa kidogo “Mpendwa Wetu Anapokufa” na pia mwishoni mwa sura hiyo ambapo tumaini la ufufuo limefafanuliwa. Akiwa ameguswa moyo sana aliushika tena mkono wa ndugu na kumwuliza, “Je, mambo haya ni kweli?” Ndugu walimhakikishia kwamba Yehova atatimiza ahadi hiyo. Akauliza:“Ninapaswa kufanya nini ili nije kumwona tena mtoto wangu?” Ndugu wakapanga kumtembelea mwanaume huyo nyumbani kwake. Walipomtembelea, alikuwa akiwasubiri kwa hamu ili aanze kujifunza Biblia.

Mwangalizi mmoja anayesimamia mahubiri ya pekee ya hadharani katika jiji la New York alisema, “Yehova ameubariki sana mpango huu!” Kisha, akaongeza hivi: “Zaidi ya kuwa njia yenye matokeo ya kuwahubiria maelfu ya watu, imetuwezesha kuwapata watu wengi wasiotenda au wale waliotengwa, yaani, ‘kondoo waliopotea’ ambao sasa wanasaidiwa kurudi kundini.”—Ezekieli 34:15, 16.