Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mashahidi wa Yehova katika Semarang, Java (karibu mwaka wa 1937)

INDONESIA

Ningependa Nianzie Hapa!

Ningependa Nianzie Hapa!

Alexander MacGillivray, mtumishi wa ofisi ya tawi ya Australia, alitembeatembea ofisini mwake akiwa na mawazo mengi. Kwa siku kadhaa alihangaishwa na jambo fulani lakini sasa alikuwa amepata suluhisho. Alihitaji kuzungumza na Frank Rice.

Frank, kolpota (painia) mwenye miaka 28, aliwasili katika ofisi ya tawi kwa majuma kadhaa. Alijifunza kweli akiwa tineja na muda mfupi baadaye akawa kolpota. Baadaye, kwa zaidi ya miaka kumi alihubiri sehemu kubwa ya Australia kwa kutumia farasi, baiskeli, pikipiki, au gari la kukokotwa. Baada ya kuwa Betheli kwa muda mfupi, Frank alikuwa tayari kuanza mgawo mwingine.

Ndugu MacGillivray alimwita Frank ofisini kwake na kumwonyesha ramani ya visiwa vilivyo kaskazini mwa Australia. Kisha alimuuliza hivi: “Frank, unaonaje kwenda kuhubiri maeneo haya? Hakuna ndugu hata mmoja katika visiwa hivi!”

Frank alivutiwa na visiwa vilivyong’aa kama lulu katika Bahari ya Hindi, yaani, Netherlands East Indies (ambayo sasa ni Indonesia). * Mamilioni ya watu katika visiwa hivyo hawakuwa wamehubiriwa habari njema za Ufalme wa Mungu. Akionyesha kwa kidole mji mkuu, Batavia (sasa Jakarta), Frank alisema hivi: “Ningependa nianzie hapa!”

Kuhubiri Kisiwa cha Java

Mwaka wa 1931, Frank Rice alifika Jakarta, jiji kubwa lenye shughuli nyingi katika kisiwa cha Java. Alipanga chumba karibu na jiji na kukijaza machapisho ya Biblia, jambo hilo lilimshangaza mwenye nyumba.

Frank Rice na Clem Deschamp wakiwa Jakarta

Frank anasema hivi: “Mwanzoni nilihisi upweke na nilitamani kurudi nyumbani. Wenyeji walivalia nguo nyeupe na kofia za jua, huku mimi nikiteseka kwa joto kali kutokana na mavazi mazito ya Australia. Sikujua hata neno moja la Kiholanzi au Kiindonesia. Nilimwomba Yehova mwongozo, nikiamini kwamba lazima kuna watu wanaozungumza Kiingereza katika eneo la biashara. Nilianza kuhubiri hapo, na kukawa na matokeo mazuri sana!

Kwa kuwa wakazi wengi wa Jakarta walizungumza Kiholanzi, Frank alijifunza kwa bidii lugha hiyo, kisha akaanza kuhubiri nyumba kwa nyumba. Pia, alianza kujifunza Kiindonesia na hatua kwa hatua akakijua vizuri. Frank anasema hivi: “Tatizo ni kwamba sikuwa na machapisho ya Kiindonesia. Hata hivyo, Yehova alinielekeza kwa mwalimu Mwindonesia, aliyependezwa na kweli naye alikubali kutafsiri kijitabu Where Are the Dead? Tulipata vijitabu vingi na watu wengi wanaozungumza Kiindonesia walianza kupendezwa na kweli.”

Mnamo Novemba 1931, mapainia wengine wawili kutoka Australia, Clem Deschamp, mwenye umri wa miaka 25 na Bill Hunter mwenye miaka 19 walihamia Jakarta. Clem na Bill walikuwa na gari lililotumika kama nyumba, gari la aina hiyo lilikuwa la kwanza nchini Indonesia. Baada ya kujifunza maneno machache ya Kiholanzi, walianza kuhubiri katika majiji makubwa ya Java.

Charles Harris akiwa amesimama kando ya baiskeli na gari lililotumiwa kama nyumba

Painia mwingine mwenye bidii kutoka Australia aliyefuata hatua za Clem na Bill ni Charles Harris. Kuanzia mwaka wa 1935, Charles alihubiri maeneo mengi ya Java kwa kutumia baiskeli au gari lililotumika kama nyumba na kuwaachia watu machapisho katika lugha tano, yaani, Kiarabu, Kichina, Kiholanzi, Kiingereza na Kiindonesia. Kwa miaka kadhaa alisambaza machapisho ya Biblia karibu 17,000.

Machapisho mengi ambayo Charles aligawanya yaliwafanya watu wengi waanze kusikiliza kweli. Ofisa fulani alimuuliza Clem Deschamp hivi: “Unahubiri na watu wangapi huko Java Mashariki?”

Ndugu Deschamp akajibu: “Peke yangu.”

Ofisa huyo akamfokea: “Unanidanganya? Ni lazima mna wafanyakazi wengi sana, ukilinganisha na idadi ya machapisho ambayo yamesambazwa kila mahali!”

Mapainia wa zamani walijitahidi kuwahubiria watu wengi iwezekanavyo. Bill Hunter anasema hivi: “Tulihubiri kila mahali katika kisiwa hicho, ni mara chache sana ambazo tulimhubiria mtu mara ya pili.” Njiani walipanda mbegu nyingi za kiroho ambazo baadaye zilizaa sana.—Mhu. 11:6; 1 Kor. 3:6.

Habari Njema Zahubiriwa Sumatra

Mwaka wa 1936 hivi, mapainia waliokuwa Java walizungumzia jinsi ambavyo wangeanza kuhubiri Sumatra, kisiwa cha sita kwa ukubwa duniani. Kisiwa hicho chenye mawe kiko kwenye ikweta na kinafanyizwa na majiji makubwa, mashamba, maeneo mengi yenye vinamasi na misitu ya mvua.

Mapainia hao walikubaliana kumtuma Frank Rice, hivyo walichanga pesa kidogo walizokuwa nazo ili kumlipia nauli. Muda mfupi baadaye, Frank aliwasili Medan, Sumatra Kaskazini, akiwa na mabegi mawili ya mahubiri, katoni 40 za machapisho, na pesa kidogo mfukoni. Frank alikuwa na imani yenye nguvu. Alianza kuhubiri mara moja, akiwa na uhakika kwamba Yehova angemtegemeza kupata mahitaji yake ili atimize mgawo wake.—Mt. 6:33.

Juma la mwisho kuhubiri huko Medan, Frank alikaribishwa nyumbani na mwanamume Mholanzi mwenye urafiki. Frank alimweleza kwamba alihitaji gari ili ahubiri habari njema kisiwa chote. Akimwonyesha gari lilokuwa limeharibika katika bustani, mwanamume huyo alimwambia: “Ukilirekebisha, nitakuuzia kwa gilda 100.” *

Frank akamjibu: “Sina gilda 100.”

Mwanamume huyo alimkazia macho Frank na kumuuliza: “Una uhakika kwamba unataka kuhubiri kisiwa chote cha Sumatra?”

Frank akamjibu, “Ndiyo.”

Mwanamume huyo akamwambia: “Kama unaweza kulirekebisha lichukue. Utalipa ukipata pesa.”

Frank alilirekebisha. Baadaye alisema hivi: “Nikajaza machapisho, nikaweka petroli, na nikiwa na moyo wenye imani, nilianza safari ya kwenda kuhubiri Sumatra.

Henry Cockman pamoja na Jean na Clem Deschamp wakiwa Sumatra, 1940

Frank alirudi Jakarta mwaka mmoja baadaye akiwa amemaliza kuhubiri kisiwa chote cha Sumatra. Akiwa huko, aliuza gari kwa gilda 100 na kumtumia pesa yule mwanamume Mholanzi wa Medan.

Majuma kadhaa baadaye, Frank alipokea barua ya mgawo mpya wa upainia kutoka Australia. Bila kukawia, alifunga mabegi yake na kuondoka ili akaanzishe kazi ya kuhubiri eneo la Indochina (ambayo sasa ni Kambodia, Laos, na Vietnam).

^ fu. 4 Pia, ilijulikana kama Dutch East Indies. Waholanzi walifika huko miaka 300 hivi mapema na kuanzisha koloni hasa kwa ajili ya biashara ya viungo. Katika simulizi hili tutatumia majina ya maeneo yanayotumika sasa.

^ fu. 3 Sawa na dola 1,100 hivi za Marekani.