Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

INDONESIA

Binti Halisi wa Sara

Titi Koetin

Binti Halisi wa Sara
  • ALIZALIWA 1928

  • ALIBATIZWA 1957

  • HISTORIA FUPI Dada aliyemsaidia mume wake mpinzani kwa busara ajifunze Biblia.—Limesimuliwa na mtoto wake, Mario Koetin.

MAMA yangu alikuwa mchangamfu, na aliipenda Biblia. Alipokutana na mmishonari Gertrud Ott, katika eneo la Manado, Sulawesi Kaskazini, alikubali kujifunza Biblia na akaikubali kweli. Lakini baba yangu, Erwin, aliyekuwa mfanyakazi maarufu wa benki na baadaye mwenyekiti wa Soko la Hisa la Jakarta, alipinga sana imani ya mama.

Siku moja, baba alimtishia mama.

Alimwambia hivi kwa hasira: “Chagua kati ya dini yako au mume!”

Mama alifikiria kwa makini jambo hilo. Kisha akajibu hivi kwa upole, “Ninataka vyote, wewe na Yehova.”

Baba hakuwa na la kusema, na hasira yake ikapoa.

Baadaye, baba akawa mwenye subira zaidi, kwa kuwa alimpenda sana mama na alithamini sana hekima na ufahamu wake.

Hata hivyo, mama alitaka mume ajiunge naye katika ibada ya kweli. Baada ya kusali kwa bidii kuhusu tamaa yake, alikumbuka kwamba baba alipenda kujifunza lugha mbalimbali. Hivyo, aliamua kubandika Maandiko ya Biblia ya Kiingereza ukutani. Mama akamwambia “Ninajaribu kuboresha Kiingereza changu.” Kwa kuwa alijua kwamba mume wake anapenda kuhutubia watu, alimwomba amsaidie kutayarisha hotuba zake za Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Baba alikubali. Kwa kuwa alijua kwamba mume wake ni mkarimu, alimwomba ikiwa wangeweza kumkaribisha mwangalizi wa mzunguko. Baba alikubali. Kwa kuwa alijua kwamba anaipenda familia yake, kwa upole alimwomba ikiwa angependa kwenda nasi kwenye kusanyiko la Kikristo. Naye akafanya hivyo.

Busara na uvumilivu wa mama ulisaidia kulainisha moyo wa baba hatua kwa hatua. Baadaye, familia yetu ilipohamia Uingereza, baba alihudhuria mikutano na akawa rafiki wa John Barr, ambaye baadaye alikuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Mwaka huohuo baba alibatizwa na hilo lilifanya mama awe na shangwe kubwa. Miaka iliyofuata, baba alizidi kuonyesha upendo zaidi kwa mama.

Maadili mazuri, heshima na hali nzuri ya kiroho ya mama iliwavutia sana watu waliomfahamu

Baadhi ya rafiki zetu walimlinganisha mama na Lidia, mwanamke Mkristo wa karne ya kwanza ambaye alikuwa mkarimu. (Mdo. 16:14, 15) Lakini mara nyingi mimi nilimlinganisha na Sara, aliyekuwa akijitiisha kwa mume wake, Abrahamu. (1 Pet. 3:4-6) Mama alikuwa na maadili mazuri, heshima, na alikuwa mwanamke wa kiroho ambaye aliwavutia sana watu waliomfahamu. Ni mfano wake mzuri uliomsaidia baba aikubali kweli. Kwa maoni yangu alikuwa kama binti halisi wa Sara.