Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

INDONESIA

Wamishonari Zaidi Wawasili

Wamishonari Zaidi Wawasili

Mnamo Julai 9, 1964, Idara ya Sheria nchini Indonesia iliandikisha rasmi Bible Students Association, kuwa shirika halali linalotumiwa na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, kabla ya ndugu kufurahia uhuru huo wa ibada walihitaji kuandikishwa na Idara ya Mambo ya Kidini. Wizara hii ilipata maagizo kutoka kwa Halmashauri ya Mambo ya Wakristo, iliyosimamiwa na viongozi wa Kiprotestanti waliowachukia Mashahidi wa Yehova.

Siku moja ndugu alikwenda kwa ofisa mkuu aliyefanya kazi kwa ukaribu na Waziri wa Mambo ya Kidini. Waligundua kwamba wote wawili wanatoka kijiji kimoja, hivyo wakawa na mazungumzo ya kirafiki kwa lugha ya asili. Ndugu huyo alipomweleza tatizo wanalokabili kutoka kwa Halmashauri ya Mambo ya Wakristo, ofisa huyo akapanga ndugu watatu wakazungumze moja kwa moja na waziri, Mwislamu mwenye urafiki na huruma. Mei 11, 1968, waziri alitangaza kwamba Mashahidi wa Yehova wanatambuliwa kisheria na wana haki ya kuendelea na shughuli zao za kidini nchini Indonesia.

Pia, ofisa huyo alijitolea kupeleka ombi katika Halmashauri ya Mambo ya Wakristo ili Mashahidi wageni waweze kupata viza za umishonari. Kwa msaada wa ofisa huyo, wamishonari 64 walikubaliwa kuingia nchini Indonesia miaka michache tu iliyofuata.

Kufikia mwaka wa 1968, karibu wamishonari na mapainia wa pekee 300 na wahubiri zaidi ya 1,200 walikuwa wakihubiri kotekote nchini Indonesia. Ndugu wenyeji walipata mazoezi mazuri kutoka kwa wamishonari. Hilo lilichochea maendeleo yao ya kiroho. Mazoezi hayo yalikuwa ya wakati unaofaa kwani mnyanyaso mkali ulikuwa karibu.

“Zawadi ya Krismasi” kwa Makasisi

Mwaka wa 1974, Halmashauri ya Mambo ya Wakristo ilianza tena kampeni yake ya muda mrefu ya kuwapiga marufuku Mashahidi wa Yehova. Mkurugenzi wa idara hiyo aliziandikia barua ofisi zote za mikoa za Idara ya Mambo ya Kidini, akidai kwa uwongo kwamba Mashahidi wa Yehova hawatambuliwi kisheria. Aliwaagiza maofisa wawachukulie hatua Mashahidi wa Yehova kwa sababu yoyote ile, maadamu walipata fursa ya kufanya hivyo. Maofisa wengi walipuuza maelekezo hayo. Hata hivyo, wengine walitumia fursa hiyo kupiga marufuku mikutano na kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba.

Gazeti la habari lilitangaza kupigwa marufuku Mashahidi wa Yehova nchini Indonesia, Desemba 1976

Wakati huohuo, Baraza la Makanisa Ulimwenguni (WCC) lilipanga mkutano wa kimataifa huko Jakarta. Waislamu waliliona jambo hilo kuwa ni uchokozi na uvunjifu wa amani. Kwa kuwa mvutano wa dini ulikuwa unaongezeka, WCC liliahirisha mkutano. Hata hivyo, suala kubwa lilikuwa kuenea kwa Ukristo, jambo lililofanya wanasiasa wengi kuwa na wasiwasi. Kwa hiyo, makasisi walijaribu kuwalaumu waziwazi Mashahidi wa Yehova kuhusu kazi yao ya kuhubiri. Jambo hilo liliwafanya maofisa wengi wawe na maoni mabaya kuhusu Mashahidi.

Desemba 1975, chuki ya kidini ikiwa bado inazidi kuongezeka, Indonesia ilishambulia Timor Mashariki (ambayo ni Timor-Leste), koloni la zamani la Ureno. Miezi saba baadaye, Timor Mashariki ilijitenga, hilo likachangia machafuko makubwa sana nchini. Akina ndugu hawakuunga mkono upande wowote na walikataa kushiriki katika utumishi wa kijeshi na kusalimu bendera, jambo ambalo lilichochea hasira ya makamanda wakuu wa jeshi. (Mt. 4:10; Yoh. 18:36) Ili kuwatokomeza kabisa, makasisi waliiomba serikali iwapige marufuku Mashahidi. Mwishowe, katikati ya Desemba 1976, makasisi walipokea “Zawadi ya Krismasi,” yaani, serikali ilipotangaza kwamba Mashahidi wa Yehova wamepigwa marufuku.