Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuhubiri katika soko la Jakarta

INDONESIA

Kazi Yapamba Moto

Kazi Yapamba Moto

Viongozi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo walisikitika sana waliposikia kwamba Mashahidi wa Yehova wamepewa uhuru wa kuabudu. Makasisi zaidi ya 700 na viongozi saba wa Kiprotestanti walifanya mkutano jijini Jakarta ili kuishinikiza serikali irudishe tena marufuku. Hata hivyo, serikali haikukubali.

Habari zilipoenea nchini kwamba marufuku imeondolewa, watu wengi wanaopendezwa waliandikia ofisi ya tawi kuomba machapisho au funzo la Biblia. Mwaka wa 2003, watu zaidi ya 42,000 walihudhuria Ukumbusho, idadi ambayo ni mara mbili ya wahubiri wote nchini. Watu karibu 10,000 walihudhuria kusanyiko jijini Jakarta, akiwemo ofisa wa cheo cha juu wa Idara ya Mambo ya Dini. Ofisa huyo alishangaa kuona wahudhuriaji wote, wadogo kwa wakubwa wakisoma maandiko kwenye Biblia. Aliwahakikishia akina ndugu kwamba atasahihisha habari za uwongo kuwahusu Mashahidi wa Yehova.

Marufuku ilipoondolewa wamishonari walirudi nchini Indonesia. Wamishonari wa kwanza kurudi walikuwa Josef na Herawati Neuhardt * (kutoka Visiwa vya Solomoni), Esa na Wilhelmina Tarhonen (kutoka Taiwan), Rainer na Felomena Teichmann (kutoka Taiwan), pia Bill na Nena Perrie (kutoka Japani). Walifuatiwa na wamishonari wengine wapya kutoka Gileadi waliopewa migawo ya kwenda Sumatra Kaskazini, Kalimantan, Sulawesi Kaskazini, na maeneo mengine ya vijijini.

“Nilifurahia sana kuwasaidia wanafunzi kuboresha uwezo wa kufundisha na kuzungumza kwa ufasaha.”—Julianus Benig

Mwaka wa 2005, ofisi ya tawi ilipanga madarasa kwa ajili ya shule mbili mpya za kitheokrasi. Julianus Benig, mwalimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma (sasa inaitwa Shule ya Waeneza Injili wa Ufalme), alieleza hivi: “Nilifurahia sana kuwasaidia wanafunzi kuboresha uwezo wa kufundisha na ufasaha na ili wawe tayari kutumiwa zaidi na tengenezo.” Wahitimu wengi wa shule hii wanatumikia wakiwa mapainia wa pekee au waangalizi wa mizunguko. Ndugu wengi waliohudhuria darasa la kwanza la Shule ya Waangalizi wa Mzunguko, * awali walizoezwa wakati wa marufuku. Shule hiyo mpya iliwasaidia kufanya kazi yao vizuri marufuku ilipoondolewa. Ponco Pracoyo, aliyehudhuria darasa la kwanza, alisema hivi: “Shule ilinisaidia kuboresha sifa ya huruma na kutimiza kazi yangu ya kuzunguka kwa njia bora. Niliburudishwa na kuchochewa sana!”

Uhitaji wa Haraka Watoshelezwa

Katika kipindi cha miaka 25 ya marufuku, makutaniko mengi nchini Indonesia yalifanya mikutano kwenye nyumba za watu. Makutaniko machache yaliweza kujenga Jumba la Ufalme, na ilikuwa vigumu kupata kibali cha kujenga mahali pa ibada. Makutaniko yalipoongezeka haraka, ofisi ya tawi ilianzisha Dawati la Ujenzi wa Majumba ya Ufalme (sasa inaitwa Idara ya Mahali ya Usanifu-Majengo na Ujenzi) ili kushughulikia uhitaji huo wa haraka.

Eneo la kwanza kufaidika na mpango huo mpya wa ujenzi ni Kisiwa cha Nias huko Sumatra Kaskazini. Haogo’aro Gea ndugu wa muda mrefu wa kutaniko la Gunungsitoli anasema hivi: “Tuliposikia kwamba tutajengewa Jumba jipya la Ufalme tulifurahi sana. Ofisi ya tawi ilituma wajitoleaji saba wa ujenzi ili kusimamia ujenzi huo. Jumba lilikamilika mwaka wa 2001.” Faonasökhi Laoli, mshiriki wa halmashauri ya ujenzi ya eneo hilo alisema hivi: “Mwanzoni tulifanya mikutano katika nyumba ndogo na watu waliwadharau Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, baada ya kujenga Jumba la Ufalme, wastani wa hudhurio la mikutano uliongezeka kutoka 20 hadi 40. Ndani ya miezi 12, kulikuwa na ongezeko la asilimia zaidi ya 500. Mahali petu pa ibada ndiyo mahali bora zaidi katika eneo letu, sasa watu wanawaheshimu Mashahidi wa Yehova.”

Jumba la Ufalme la Bandung

Mwaka wa 2006, katika jiji la Bandung, Java Magharibi, ndugu walianza kutafuta eneo la kujenga Jumba la Ufalme la kwanza jijini humo. Singap Panjaitan mzee aliyetumikia katika halmashauri ya ujenzi anasema hivi: “Ilichukua miezi 12 kupata kiwanja kizuri. Hata hivyo, tulihitaji kupata idhini ya majirani 60 ambao si Mashahidi kabla ya kupata kibali cha wenye mamlaka. Majirani 77 waliunga mkono mradi huo, kutia ndani mwanamke mwenye ushawishi mkubwa ambaye mwanzoni alitupinga. Jumba lilipokamilika, tuliwaalika majirani na meya wa jiji la Bandung ili kutazama jengo letu. Meya huyo alisema hivi: ‘Mahali hapa pa ibada ni safi na maridadi, ni mfano wa kuigwa na makanisa yote.’” Jumba hilo la Ufalme lenye ghorofa moja liliwekwa wakfu mwaka wa 2010.

Tangu mwaka wa 2001, Majumba ya Ufalme zaidi ya 100 yamejengwa nchini Indonesia, hata hivyo, bado kuna uhitaji zaidi.

^ fu. 3 Simulizi la maisha la Herawati Neuhardt lilichapishwa katika gazeti Amkeni! la Februari 2011.

^ fu. 1 Sasa inaitwa Shule ya Waangalizi wa Mzunguko na Wake Zao.