Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kusanyiko lililofanywa wakati wa marufuku, baadhi ya wasikilizaji wakiwa kwenye boti

INDONESIA

Waliazimia Kusonga Mbele

Waliazimia Kusonga Mbele

Ofisi ya tawi ilipojua kuhusu marufuku, ilichukua hatua. Ronald Jacka anasema hivi: “Tulihamisha rekodi zetu muhimu, machapisho, pesa, na kuzificha katika maeneo mengine salama jijini Jakarta. Kisha, tulihamishia ofisi ya tawi mahali pengine pa siri, na tukauza majengo ya ofisi ya awali kwa siri.”

Ndugu wengi wenyeji waliendelea kutenda bila woga. Kwa kuwa walikuwa wamevumilia mateso mengi kabla ya marufuku waliendelea kumtegemea Yehova. Hata hivyo, baadhi ya ndugu hawakusimama imara. Kwa sababu ya woga wazee wachache walitia sahihi kiapo cha kuacha kuhubiri. Wengine hata walitaja majina ya washiriki wa kutaniko. Ofisi ya tawi ilituma ndugu wakomavu ili kuyaimarisha makutano na kuwasaidia walioshindwa kusimama imara. Pia, John Booth, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitembelea nchini Indonesia na kuwatia moyo zaidi.

Kwa kweli, Yehova, yule Mchungaji Mkuu, aliwafariji na kuwaimarisha watu wake. (Eze. 34:15) Wazee walianza kuongeza bidii katika kuongoza mambo ya kiroho na wahubiri wakapata mbinu mpya za busara za kuhubiri. (Mt. 10:16) Ndugu wengi walinunua nakala za Biblia ya kisasa ya bei nafuu kutoka Chama cha Biblia cha Indonesia na kuwapatia wenye nyumba, na ilipowezekana walihubiri ujumbe wa Ufalme kwa busara. Wengine waliondoa ukurasa ulio na anwani kwenye machapisho yetu na kuwapatia watu wanaopendezwa. Mapainia wengi waliendelea kuhubiri nyumba kwa nyumba kwa kujifanya wachuuzi, mbinu iliyotumiwa na watangulizi wao wakati wa utawala wa Wajapani.

Margarete na Norbert Häusler

Kisha, mwaka wa 1977, Idara ya Mambo ya Kidini ilianzisha mbinu nyingine ya kuwakandamiza Mashahidi kwa kukataa kuongeza muda wa viza za wamishonari. Wamishonari wengi walihamishiwa nchi nyingine. * Norbert Häusler, mmishonari ambaye alitumikia pamoja na mke wake Margarete, huko Manado, Sulawesi Kaskazini alisema hivi: “Mamia ya ndugu na dada walikuja uwanja wa ndege kutuaga. Tulipanda ngazi na kugeuka nyuma kuwatazama. Tuliona mikono mingi ikitupungia, pia tulisikia sauti iliyoenea uwanja mzima ikisema: ‘Asanteni sana. Asanteni kwa kuwa pamoja nasi.’ Tuliingia ndani ya ndege na kuanza kulia.”

Machafuko Huko Sumba

Habari kuhusu marufuku zilipoenea katika visiwa vingine, Ushirika wa Makanisa ya Indonesia uliwachochea waumini wake waripoti utendaji wowote wa Mashahidi kwa wenye mamlaka. Hilo lilifanya Mashahidi wengi katika visiwa vingi wakamatwe na kuhojiwa.

Huko Waingapu, kisiwani Sumba, kamanda wa jeshi wa wilaya aliwaita ndugu 23 kwenye uwanja wa kambi ya jeshi na kuwaamuru watie sahihi kiapo cha kukana imani yao. Ndugu hao walipokataa, kamanda huyo aliwaagiza warudi kambini siku inayofuata, umbali wa kilometa 14 kwa safari ya miguu.

Asubuhi na mapema kesho yake, ndugu hao walipofika kwa kamanda, waliitwa mmoja baada ya mwingine na kuamriwa kutia sahihi kiapo. Ndugu alipokataa kutia sahihi, wanajeshi walimpiga kwa fimbo zenye miiba. Kwa hasira wanajeshi waliwapiga hivi kwamba baadhi ya ndugu walizimia. Wakati huo, ndugu wengine walikuwa wakisubiri zamu yao. Mwishowe, ndugu mmoja kijana anayeitwa Mone Kele alijitokeza na kuandika kwenye kiapo. Ndugu walihuzunika, lakini kamanda alichanganyikiwa. Mone aliandika hivi: “Nimeazimia kuwa Shahidi wa Yehova milele!” Mone alipigwa kikatili hivi kwamba alipelekwa hospitali, hata hivyo, aliendelea kuwa imara kiroho.

Kwa siku 11 kamanda huyo alijaribu kuvunja utimilifu wa ndugu hao. Aliagiza wasimame siku nzima kwenye jua kali la kitropiki. Aliwalazimisha watambae kwa mikono na magoti kilometa kadhaa na kisha wakimbie umbali mrefu wakiwa wamebeba mizigo mizito. Waliwekewa visu shingoni, na kisha kuamriwa kuisalimu bendera; hata hivyo, walikataa. Kwa hiyo, akaagiza wapigwe zaidi.

Kila asubuhi ndugu walipoenda kambini hawakujua mateso yaliyowangoja. Wakiwa njiani walisali pamoja na kutiana moyo waendelee kuwa waaminifu. Kila usiku walirudi nyumbani wakiwa na damu na majeraha, hata hivyo, walikuwa na shangwe kwa sababu walidumisha uaminifu kwa Yehova.

Ofisi ya tawi ilipojua kwamba ndugu wanatendewa isivyo haki, walituma ujumbe mara moja kuhusu hali hiyo kwa kamanda wa huko Waingapu, kamanda wa jeshi wa mkoa wa Timor, kamanda wa wilaya wa Bali, kamanda mkuu wa jeshi wa Jakarta, na viongozi wengine wa serikali. Akiwa ameaibika kwamba matendo yake maovu yalijulikana kotekote nchini Indonesia, kamanda wa jeshi wa Waingapu aliacha kuwatesa akina ndugu.

“Mashahidi wa Yehova ni Kama Msumari”

Miaka iliyofuata, Mashahidi wengi nchini Indonesia walifungwa, kuhojiwa, na kuteswa. Mmishonari anayeitwa Bill Perrie alisema hivi: “Katika eneo moja ndugu wengi waling’olewa meno ya mbele. Hivyo basi, walipokutana na ndugu aliye na meno ya mbele, kwa utani walimwuliza hivi: ‘Wewe ni mpya? Au ulikana imani?’ Licha ya minyanyaso, wale walioteswa hawakupoteza shangwe na bidii ya kumtumikia Yehova.”

“Kufungwa kumenifundisha kumtegemea Yehova zaidi, kwa kweli, kumeniimarisha sana kiroho”

Katika kipindi cha miaka 13, Mashahidi 93 walipelekwa gerezani kwa kipindi cha miezi miwili hadi miaka minne. Mateso waliyokabili yaliimarisha azimio lao la kubaki waaminifu kwa Yehova. Baada ya kutumikia kifungo cha miezi nane gerezani, Musa Rade aliwatembelea ndugu katika eneo la kwao ili kuwatia moyo waendelee kuhubiri. Aliwaambia hivi: “Kufungwa kumenifundisha kumtegemea Yehova zaidi, kwa kweli, kumeniimarisha sana kiroho.” Haishangazi kwamba baadhi ya watu waliojionea mambo hayo walisema hivi: “Mashahidi wa Yehova ni kama msumari. Kadiri unavyogonga ndivyo wanavyozama zaidi.”

Wahubiri wakielekea kuhubiri Ambon, Maluku

^ fu. 1 Wamishonari wa muda mrefu kama vile Peter Vanderhaegen na Len Davis walikuwa wamepita umri wa kustaafu na Marian Tambunan (zamani Stoove) aliolewa na Mwindonesia, kwa hiyo waliruhusiwa wabaki nchini. Wote watatu waliendelea kuwa hai kiroho nao wakapata matokeo mazuri katika huduma licha ya marufuku.