Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutaniko la Surabaya, 1954

INDONESIA

Wamishonari Kutoka Gileadi Wawasili

Wamishonari Kutoka Gileadi Wawasili

Julai 1951, kutaniko dogo la Jakarta lilikusanyika kumpokea Peter Vanderhaegen, mmishonari wa kwanza aliyepata mazoezi ya Gileadi kuingia nchini Indonesia. Kufikia mwishoni mwa mwaka huo, wamishonari wengine 13 waliwasili nchini kutoka Australia, Ujerumani, na Uholanzi, na kufanya idadi ya wahubiri kuwa karibu mara mbili ya idadi ya awali.

“Nilifikiria jinsi ambavyo ningehubiri nyumba kwa nyumba kwa kutumia ishara za mwili,” alikumbuka Fredrika Renskers, mmishonari kutoka Uholanzi. “Hata hivyo, kwa kuwa watu wengi walizungumza Kiholanzi, mara nyingi nilihubiri kwa lugha hiyo.” Ronald Jacka, kutoka Australia, alisimulia hivi: “Baadhi yetu tulitumia kadi za ushahidi zilizokuwa na maelezo mafupi ya lugha ya Indonesia. Nilisoma kadi hiyo kabla ya kupiga hodi katika kila mlango na kujaribu kukumbuka maneno hayo.”

Kwa sababu ya bidii ya wamishonari, idadi ya wahubiri iliongezeka haraka kutoka 34 hadi 91 ndani ya mwaka mmoja. Mnamo Septemba 1, 1951, ofisi ya tawi ya Watch Tower Society ilianzishwa katika nyumba ya André Elias iliyokuwa katika mji wa Jakarta ya Kati. Ronald Jacka alipewa mgawo wa kuwa mtumishi wa tawi.

Kuyafikia Maeneo Mengine

Novemba 1951, Peter Vanderhaegen alipewa mgawo wa kwenda Manado, Sulawesi Kaskazini, ambako Theo Ratu na mke wake walikuwa wameanzisha kikundi. Wenyeji wengi wa eneo hilo walidai kuwa Wakristo na waliheshimu sana Neno la Mungu. Wengi waliwakaribisha Mashahidi na kuwauliza maswali kuhusu mafundisho ya Biblia. Mara nyingi waliongea na vikundi vya watu kumi. Baada ya dakika 15 hivi, watu karibu 50 wangekuwa wakiwasikiliza. Ndani ya saa moja, mazungumzo hayo yalihitaji eneo kubwa zaidi kwani watu 200 wangefika ili kuwasikiliza.

Mapema mwaka wa 1952, Albert na Jean Maltby walianzisha makao ya wamishonari katika jiji la Surabaya, Java Mashariki, jiji la pili kwa ukubwa nchini. Wakiwa huko, dada sita wamishonari, Gertrud Ott, Fredrika Renskers, Susie, Marian Stoove, Eveline Platte, na Mimi Harp walijiunga nao. “Wenyeji wengi walikuwa Waislamu na walikuwa wenye urafiki sana,” akasema Fredrika Renskers. “Wengi walionekana kana kwamba wanasubiri kweli, na ilikuwa rahisi kuanza kuwafundisha Biblia. Kwa miaka mitatu, kutaniko la Surabaya likawa na wahubiri 75.”

Nyumba ya wamishonari katika Surabaya, Java Mashariki

Wakati huo, mwanamume mmoja Mwislamu aliyeitwa Azis kutoka Padang, Sumatra Magharibi, aliandikia barua ofisi ya tawi ili kupata msaada wa kiroho. Azis alijifunza Biblia na mapainia kutoka Australia miaka ya 1930 lakini akapoteza mawasiliano nao wakati wa utawala wa Wajapani. Kisha aliokota kijitabu kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Aliandika hivi: “Nilipoona anwani ya Jakarta kwenye kijitabu, tamaa yangu ilichochewa upya!” Mara moja, ofisi ya tawi iliwasiliana na Frans van Vliet aliyekuwa mwangalizi wa mzunguko huko Padang. Aligundua kwamba Azis alikuwa akizungumza na jirani yake, Nazar Ris, mfanyakazi wa serikali mwenye njaa ya kiroho. Wanaume hao na familia zao walikubali kweli. Ndugu Azis akawa mzee mwaminifu. Nazar Ris akawa painia wa pekee, na watoto wake wengi ni Mashahidi wenye bidii.

Frans van Vliet na dada yake Nel

Baada ya muda, Frans van Vliet alimtembelea ndugu Mholanzi asiyetenda aliyekuwa akirekebisha kituo cha kusafisha mafuta kilichoharibiwa wakati wa vita huko Balikpapan, Kalimantan Mashariki. Frans aliandamana na ndugu huyo katika utumishi na kumtia moyo awafundishe Biblia watu wanaopendezwa. Kabla ya ndugu huyo kurudi Uholanzi, alikuwa ameanzisha kikundi kidogo huko Balikpapan.

Baadaye, dada Titi Koetin ambaye alikuwa amebatizwa hivi karibuni alienda Banjarmasin, Kalimantan Kusini. Titi aliwahubiria ndugu zake wa ukoo katika jamii ya Dayak, na kuwasaidia wengi wao kujifunza kweli. Baadhi ya wapya hao walirudi vijijini kwao Kalimantan na kuanzisha vikundi ambavyo viliimarika na kuwa makutaniko yenye nguvu.

Kuchapisha Machapisho ya Kiindonesia

Kazi ya kuhubiri ilipozidi kusonga mbele, ndugu walihitaji machapisho mengi ya lugha ya Kiindonesia. Mwaka wa 1951, kitabu “Let God Be True” kilitafsiriwa katika lugha hiyo, hata hivyo, wenye mamlaka waliboresha mfumo wa sarufi wa lugha ya Indonesia, na hivyo ofisi ya tawi ikasahihisha kitabu hicho. * Hatimaye, kitabu hicho kilipotolewa, kiliwavutia wasomaji wengi nchini Indonesia.

Mwaka wa 1953, ofisi ya tawi ilichapisha nakala 250 za gazeti la Mnara wa Mlinzi katika Kiindonesia, toleo la kwanza kutolewa katika kipindi cha miaka 12. Mwanzoni gazeti hilo lenye kurasa 12 lilikuwa na makala za funzo pekee. Miaka mitatu baadaye, liliongezwa na kuwa na kurasa 16, nakala 10,000 za gazeti hilo zilichapishwa kila mwezi na kampuni fulani ya biashara.

Toleo la kwanza la gazeti la Amkeni! katika lugha ya Indonesia lilichapishwa mwaka wa 1957. Idadi yake iliongezeka kwa kasi hadi kufikia nakala 10,000. Kwa sababu ya uhaba wa karatasi nchini, ndugu walihitaji kuomba kibali cha kununua. Ofisa wa serikali aliyepewa ombi hilo alisema hivi: “Menara Pengawal (Mnara wa Mlinzi) ni mojawapo kati ya magazeti bora nchini Indonesia, ningependa kuwasaidia mpate kibali cha kununua karatasi kwa ajili ya magazeti mapya.”

^ fu. 1 Kumekuwa na mifumo miwili ya kutamka herufi za lugha ya Kiindonesia tangu mwaka wa 1945, kwa kiasi kikubwa zimefuata mfumo wa sarufi wa Kiholanzi cha awali.