Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Brazili: Valdira akijifunza kupitia simu ya mkononi huku akitumia mwanga wa mshumaa

KUHUBIRI NA KUFUNDISHA DUNIANI KOTE

Amerika

Amerika
  • IDADI YA NCHI 57

  • IDADI YA WATU 982,501,976

  • IDADI YA WAHUBIRI 4,102,272

  • IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 4,345,532

Kujifunza kwa Kutumia Mwanga wa Mshumaa

Wenzi wa ndoa ambao ni mapainia wa pekee nchini Brazili walikuwa wakihubiri eneo la mbali, walipopata habari kuhusu mwanamke anayeitwa Valdira, aliyewahi kujifunza Biblia miaka 13 iliyopita. Baada ya kusafiri katika barabara mbovu na yenye vumbi na kuvuka mito hatari, mapainia hao walifanikiwa kumkuta Valdira, ambaye alitamani kuendelea kujifunza Biblia. Kwa sababu aliishi kijijini, walihitaji kufanya mipango ya pekee. Ingawa Valdira alikuwa na simu ya mkononi, angeweza tu kupata mtandao katika shamba lililokuwa mbali na nyumba yake. Zaidi ya hilo, Valdira angeweza kujifunza tu kuanzia saa tatu usiku. Hebu wazia: Mwanamke huyo akiwa peke yake usiku akijifunza Biblia kupitia simu kwa kutumia mwanga wa mshumaa.

Pia, Valdira husikiliza mikutano ya Jumapili kupitia simu yake. Huenda shambani akiwa na Biblia, gazeti la Mnara wa Mlinzi, na kitabu cha nyimbo. Kunapokuwa na mvua, anaenda na mwavuli.

Mwezi wa Machi, Valdira alisafiri kilometa 96 kwenda Jumba la Ufalme kusikiliza mkutano wa pekee ambapo Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kireno ilitolewa. Alifurahi sana kupata Biblia mpya. Alipopongezwa kwa jitihada zake za kujifunza Biblia, Valdira alisema hivi, “Aah, si vigumu sana!”

“Nilijua Kwamba Siku Moja Mtakuja”

Yukpa ni jamii ya watu wenye asili ya Amerika na India waishio nchini Kolombia. Kabla ya kutembelea moja ya jamii hizo, Frank painia wa pekee, alionywa kuhusu chifu wa eneo hilo, anayeitwa John Jairo, ambaye aliwafukuza wahubiri wa dini mbalimbali walioenda kuhubiri huko. Siku moja, John alipomkuta mhudumu wa dini yao akikusanya sadaka, alimfukuza kwa kufyatua risasi hewani.

kolombia: Frank, painia wa pekee, akiwafundisha Biblia watu ya jamii ya Yukpa

Frank anakumbuka hivi: “Tulipofika katika jamii hiyo, mtu wa kwanza kutusikiliza alikuwa binti ya John Jairo! Baada ya kumwonyesha kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? mara moja akasema, ‘Hii ndiyo dini ambayo ninataka kujiunga nayo!’ Kisha, alikimbia kwenda nyumbani kumwambia baba yake. Mara moja, baba yake alituita kwake. Tulikuwa na wasiwasi tulipokutana naye. Hata hivyo, kabla hatujasema lolote, alisema: ‘Ninajua kwamba dini yenu ni ya kweli. Miaka nane iliyopita niliokota nakala ya kitabu mlichompatia binti yangu kwenye dampo la takataka huko Becerril. Nilikisoma, na tangu wakati huo nimekuwa nikisubiri mje. Nilijua kwamba siku moja mtakuja. Ninaomba mtufundishe Biblia, mimi, familia yangu, na watu wa jamii yetu. Tunawakaribisha kwa moyo mweupe.’

“Maneno hayo yalifanya tutokwe na machozi. Jamii nzima ilikusanyika kutusikiliza, na John Jairo alitafsiri kwa lugha yao. Tulipokuwa tunaondoka, John, alituazima punda wa kubeba mizigo yetu. Sasa tunaongoza mafunzo ya Biblia 47 ya watu 120 wa jamii mbalimbali za Yukpa, kutia ndani John Jairo na binti yake.”

Mtesaji Abadili Mwenendo Wake

José anayeishi nchini Ekuado alikuwa Mkatoliki mwenye bidii. Aliandika hivi: “Niliwachukia sana Mashahidi wa Yehova. Niliwatesa kwa miaka kumi. Ningekusanya kikundi cha watu ili kuwatesa Mashahidi na kuwashtaki kwa uwongo kwamba ni wezi. Kisha, tulipokuwa kituo cha polisi, nilisisitiza kwamba wafungwe gerezani. Wakati fulani, tuliharibu gari la Shahidi. Na wakati mwingine, tulitupa pikipiki yao kwenye shimo.

“Kisha, mwaka wa 2010, niliugua ugonjwa wa homa ya nguruwe. Daktari wangu alinishauri niondoke eneo la juu la Andes na kuhamia eneo la pwani lenye joto ili kupata nafuu. Nilihamia eneo la pwani katika shamba dogo la ndugu yangu, nikiwa huko niliishi na kutunza shamba peke yangu. Kwa kuwa nilikuwa mpweke, nilitamani kuzungumza na mtu yoyote. Ni nani angekuja shambani? Mashahidi wa Yehova! Kwa sababu ya upweke, nilizungumza nao, na nilishangaa jinsi walivyoitumia Biblia vizuri. Kisha, nikakubali kujifunza Biblia. Baada ya kujifunza kwa miezi sita, nilihudhuria mkutano kwa mara ya kwanza. Nilivutiwa sana jinsi walivyonionyesha upendo na fadhili, hivi kwamba nikajiambia hivi, ‘Huenda hawa ni watumishi wa Mungu wa kweli!’ Nilifanya maendeleo na kisha kubatizwa Aprili 2014.

“Ninajuta kwa sababu niliwatesa Mashahidi. Hata hivyo, Yehova amenipa fursa ya kufanya mabadiliko kwa kiasi fulani. Kwenye kusanyiko la mzunguko Oktoba 4, 2014, nilihojiwa kuhusu mwenendo wangu wa zamani na kuulizwa hivi: ‘Ikiwa ungepata fursa ya kumwomba msamaha yeyote kati ya watu uliowatesa, ungemwomba nani?’ Mara moja nikajibu kwamba ningependa kumwomba msamaha ndugu Edmundo, lakini sijui jinsi ambavyo ningekutana naye. Bila kutarajia, mwangalizi wa mzunguko alimwomba Edmundo aje jukwaani. Wahudhuriaji waliguswa moyo na kutokwa na machozi, tulipokumbatiana na Edmundo jukwaani na kulia kwa pamoja.”

“Tafadhali Yehova, Watume Mashahidi Wako Wanitembelee”

Paraguai: Mwanamke akizungumza na Mashahidi wa Yehova

Katika majira ya joto na jua kali, kikundi cha wahubiri huko Asunción nchini Paraguai, kilikuwa kimemaliza kuhubiri eneo lao. Hata hivyo, waliamua kuendelea kuhubiri nyumba chache za jirani. Dada mmoja kati ya hao alisema hivi, “Huenda kuna mtu anayetoa sala katika eneo hili.” Katika nyumba moja, mwanamke kijana aliwasalimu kwa uchangamfu na kuwauliza ikiwa wao ni Mashahidi wa Yehova. Kisha akawaeleza kuwa kwa sababu ya kazi yake alihamia nchini Paraguai kutoka Bolivia. Alikuwa akijifunza Biblia huko Bolivia kabla ya kuhama. Lakini, hakuna jirani yake hata mmoja aliyeweza kumsaidia kuwapata Mashahidi, kwa hiyo alisali hivi, “Tafadhali Yehova, watume Mashahidi wako wanitembelee.” Siku hiyohiyo, dada walimtembelea na kufanya mipango ya kujifunza naye Biblia.