Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Israeli: Kutumia kompyuta ya mkononi ili Kuhubiri Ujumbe wa Ufalme

KUHUBIRI NA KUFUNDUSHA DUNIANI KOTE

Asia na Mashariki ya Kati

Asia na Mashariki ya Kati
  • IDADI YA NCHI 49

  • IDADI YA WATU 4,409,131,383

  • IDADI YA WAHUBIRI 718,716

  • IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 766,364

Saa Mia Moja kwa Ajili ya Miaka Mia Moja

Katika nchi moja ya Asia, mwanamitindo na mwigizaji maarufu wa kike alikubali kujifunza Biblia. Mara moja alianza kutumia yale aliyojifunza na akaharibu vitabu vya kishirikina na sanamu za dini ya Budha.

Rafiki yake mmoja alimsihi hivi: “Kwa nini usiache kujifunza angalau kwa miaka mitatu tu ili ukazie fikira zaidi kazi yako? Baadaye, unaweza kuendelea kujifunza tena.”

Mwanamke huyo alijibu hivi: “Nimengoja kwa miaka 24 ili kumjua Yehova. Kwa nini niache kuendelea kujifunza miaka mingine mitatu?”

Juma ambalo alijiunga na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, kampuni ya kuandaa filamu iliwasiliana naye. Walimpa fursa ya kufanya kazi ya mshahara mnono kwa miaka minne, ikiwa angekubali kuigiza sehemu yoyote katika filamu. Alikataa kazi hiyo. Mnamo Mei 2014, alistahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, na mwezi wa Agosti ulipokaribia, aliamua kuhubiri saa 100 mwezi huo. Alipoulizwa kwa nini ameamua kufanya hivyo, alijibu, “Ninataka kusherehekea miaka 100 ya utawala wa Yesu kwa kuhubiri saa moja kwa kila mwaka aliotawala!” Alifanikiwa kutimiza lengo lake. Mwezi wa Januari 2015, alibatizwa, na sasa anatumikia akiwa painia msaidizi.

Kuutumia Usiku kwa Hekima Tukiwa Gerezani

Nchini Sri Lanka, dada wanne walisafiri kwa basi ili wakahubiri eneo ambalo halijahubiriwa lililo na Wabudha wengi. Siku ya pili walipokuwa wakihubiri, mtawa wa kiume na dereva wa teksi waliwasimamisha dada hao. Ghafla kikundi cha watu 30 wenye hasira kiliwavamia. Polisi walifika na kuwachukua dada hao mpaka kituo cha polisi, na kuwaweka seli ingawa hawakuwa na hatia yoyote. Waliwekwa pamoja na wahalifu sugu, walitukanwa, hata hivyo, kuwa gerezani kuliwapa fursa ya kutoa ushahidi. Dada mmoja alisema hivi: “Niliwekwa pamoja na wauaji, hata hivyo, nilizungumza nao kuhusu kweli. Walishangaa kwa nini nilikuwa humo na wakauliza maswali mengi kuhusu imani yangu. Mmoja wao aliniuliza hivi, ‘Kwa nini wewe ni mwenye furaha?’”

Sri Lanka: Dada wanne walisafiri kwa Basi ili kuhubiri eneo lisilohubiriwa

Mahakama Kuu ya Sri Lanka imekubali ombi la madai yetu kuhusu haki za msingi dhidi ya polisi kuwafunga watu bila uthibitisho wa kosa. Kesi hiyo bado haijasikilizwa.

Msaada kwa Mwanamke Mgonjwa

Michiko, dada ambaye ni painia nchini Japani, alikuwa anamfundisha Biblia kwa lugha ya ishara mwanamke mzee aliyekuwa hospitalini. Dada huyo aliwaomba wasimamizi ruhusa ya kuongea na wagonjwa wengine. Baadaye, Michiko alikutana na Kazumi, anayeweza kusikia lakini hawezi kuongea. Kazumi hatoki kitandani kwa sababu alilemaa kutokana na aksidenti ya gari akiwa na umri wa miaka 23 na hawezi kumeza chakula wala maji. Alikuwa na maswali mengi na akakubali kujifunza Biblia.

Japani: Kazumi akiandika barua za kitia moyo

Michiko aliuliza maswali na kisha Kazumi alionyesha jibu kwenye fungu kwa kidole au kuandika. Kazumi alipopata simu ya mkononi, Michiko alifaulu kuzungumzia andiko la siku pamoja naye kila asubuhi. Ingawa Kazumi alidhoofika kimwili, aliimarika kiroho kiasi kwamba alitamani kuwa Shahidi wa Yehova. Akiwa na umri wa miaka 61, baada ya kujifunza kwa miaka 13, Kazumi akawa mhubiri ambaye hajabatizwa.

Kwa kuwa, Kazumi hatoki kitandani, kutaniko lilifanya mipango ili aweze kusikiliza mikutano yote na programu za makusanyiko. Mikutanoni, dada mbalimbali husoma maelezo yaliyotayarishwa na Kazumi.

Kazumi humwandikia barua nzuri kila mwanafunzi wa Biblia anayehudhuria mikutano. Huwahubiria wahudumu wa hospitali na wote wanaomtembelea. Kazumi huwaambia hivi, “Ukijifunza Biblia, utakuwa mwenye furaha.”

Mtawa Ajifunza Kweli

Katika nchi iliyo Kusini mashariki mwa Asia, dada mmoja alikutana na mtawa wa kiume alipokwenda hospitali kumwona daktari wa macho. Alimuuliza hivi, “Je, ungependa kuwa na afya nzuri na kuishi milele katika mazingira maridadi?” Akaanzisha mazungumzo ya kirafiki na kumpatia broshua Msikilize Mungu. Mtawa huyo alimpatia namba ya simu, kisha dada akampatia ndugu kutanikoni. Baada ya siku chache, ndugu aliwasiliana na mwanaume huyo na kumwalika ahudhurie hotuba ya pekee. Mwanaume huyo alifurahia sana mikutano, hasa kusikiliza nyimbo za Ufalme, na alivutiwa sana kuona kila mtu akimkaribisha kwa uchangamfu.

Mtawa huyo alipouliza ikiwa Mashahidi wana vyuo vikuu au seminari, ndugu alimjibu kwamba kuna mpango wa kuwafundisha watu Biblia na akafanya mpango wa kujifunza naye. Baada ya juma moja, mtawa huyo alimaliza kujifunza sura ya 1 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Aliendelea kujifunza, akaanza kuhudhuria mikutano na kutoa maelezo katika funzo la Mnara wa Mlinzi.

Mwanaume huyo alipohudhuria kusanyiko la mzunguko, mwakilishi wa ofisi ya tawi alimwalika kutembelea Betheli. Juma lililofuata mwanaume huyo alisafiri kwa saa kumi ili kutembelea Betheli, na huko alikaribishwa kwa uchangamfu. Mwishoni mwa Februari 2015, aliacha maisha ya utawa na kuendelea kujifunza Biblia na kushiriki katika mikutano ya Kikristo.

Aliyepotea, Apatikana

Hivi karibuni, mapainia walitumwa kaskazini-mashariki mwa India, ambako habari njema haijahubiriwa kwa miaka mingi. Mapainia hao walipata watu wengi wenye kupendezwa na walianza kutafuta mahali kwa ajili ya mikutano. Walipokuwa wanaenda kwenye funzo la Biblia, waliona nyumba ikijengwa ambayo walifikiria kuulizia. Ingawa walikuwa wameipita nyumba hiyo, waliamua kurudi tena. Jirani na nyumba hiyo, walikutana na mwanamke mzee na wakajitambulisha kwamba wao ni Mashahidi wa Yehova. Mwanamke huyo akatabasamu. Kisha akasema “Mimi pia ni Shahidi wa Yehova,” na kuwakaribisha kwa uchangamfu nyumbani. Halafu akawaonyesha machapisho ya kuanzia mwaka wa 1970 hadi 1980. Aliwahi kujifunza na mapainia miaka 30 iliyopita na alihudhuria baadhi ya mikutano licha ya kupingwa na mume wake. Aliamini kwamba amepata kweli, hata hivyo, alipoteza mawasiliano na tengenezo mapainia walipoondoka eneo hilo. Watoto wake wote walijiunga na dini mbalimbali, hata hivyo, yeye alikataa kushirikiana na dini hizo.

India: Mwanamke anayependezwa akionyesha machapisho ya kuanzia mwaka wa 1970 hadi 1980

Hivi karibuni, watoto wake walimshawishi ajiunge na Kanisa Katoliki ili atakapokufa azikwe na Wakatoliki. Mdogo wake wa kike alisisitiza kumpeleka katika kanisa Katoliki ili ajiunge, hata hivyo, walipokuwa njiani, kulikuwa na foleni ndefu ya magari hivyo wakaamua kurudi. Mdogo wake alimwambia kwamba wataenda siku inayofuata, lakini aliugua. Siku hiyohiyo mchana mapainia walikutana na mwanamke huyo anayependezwa! Sasa anajifunza Biblia, anahudhuria mikutano, na pia anawachochea watoto na wajukuu wake wajifunze.