Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Australia: Video ya michoro ya vibonzo yenye kichwa Rafiki wa Kweli ni Nani?

KUHUBIRI NA KUFUNDISHA DUNIANI KOTE

Oceania

Oceania
  • IDADI YA NCHI 29

  • IDADI YA WATU 40,642,855

  • IDADI YA WAHUBIRI 98,353

  • IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 66,022

Ujasiri wa Kuwaeleza wengine

Emily ni msichana mwenye umri wa miaka 12 anayeishi nchini Australia. Siku moja mwalimu wake alikuwa akifundisha kuhusu umuhimu wa kuchagua marafiki wazuri. Jambo hilo lilimchochea Emily kumwonyesha mwalimu video ya michoro ya vibonzo yenye kichwa Rafiki wa Kweli ni Nani? Mwalimu huyo alipowaonyesha wanafunzi video hiyo, waliitazama kwa makini. Baadaye, walitumia saa nzima kuizungumzia. Pia, mwalimu aliionyesha video hiyo kwa madarasa mengine kadhaa. Kisha, Emily alimwelekeza mwalimu huyo na wanafunzi kwenye tovuti ya jw.org. Emily anasema hivi: “Yehova alinipa ujasiri wa kuwaeleza wanafunzi wengi kuhusu tovuti yetu. Kwa kweli alinibariki sana.”

Maonyesho ya Biashara Katika Eneo la Mbali

Wahubiri watano walisafiri kwa saa tisa katika barabara mbaya ya milimani ili kuweka meza ya machapisho kwenye maonyesho ya biashara huko Suai, Timor-Leste. Watu waliotembelea walishangaa kuona machapisho ya Biblia katika lugha 12 za kienyeji, kwa kuwa lugha hizo zina machapisho machache au hazina kabisa. Mwanamke mmoja alipoona kichwa cha broshua alisema hivi kwa mshangao, “Hii ni lugha yangu!” Ilikuwa mara ya kwanza kusoma chapisho kwa lugha yake ya Bunak. Kwa siku nne tu wahubiri hao waligawa machapisho 4,571 na watu wengi waliomba watembelewe nyumbani. Watu wengi waliopendezwa hawakuwahi kukutana na Mashahidi wa Yehova. Watoto waliketi kwa muda mrefu wakitazama mfululizo wa video Uwe Rafiki ya Yehova katika lugha ya Tetun Dili. Baadhi ya watoto walikumbuka maneno ya nyimbo katika mfululizo huo na waliziimba kwa shangwe.

Timor-Leste: Watoto wakifurahia kutazama mfululizo wa video Uwe Rafiki ya Yehova

“Wanafunzi Walivihitaji”

Katika kisiwa cha Palau, wamishonari Brian na Roxanne waliomba ruhusu ya kuweka kigari cha machapisho karibu na chuo. Walikutana na mkuu wa chuo na kumwonyesha video inayohusu mahubiri ya hadharani kwenye tovuti ya jw.org. Pia, walimwachia baadhi ya machapisho ambayo walipanga kuyaweka kwenye kigari hicho. Mkuu huyo aliwaambia Brian na Roxanne kwamba walihitaji kuongea na mwelekezi wa wanafunzi. Baada ya mazungumzo hayo, waliambiwa kwamba walihitaji kuwasiliana na mshauri wa wanafunzi.

Brian alisema, “Tulikubaliana na mshauri wa wanafunzi, lakini, alituambia turudi kwa mkuu wa chuo, huko tukaambiwa tuandike barua ya kuomba ruhusa ya kuweka kigari. Tulifikiri wanatuzungusha na tukavunjika moyo, hata hivyo, tuliandika barua kwa shingo upande.”

Palau: Roxanne na Brian wakizungumza na wanafunzi kando ya kigari cha machapisho karibu na chuo

Brian na Roxanne walipoenda kupata jibu la ombi lao kwa mshauri wa wanafunzi hawakuwa na uhakika ikiwa watakubaliwa. Brian anaeleza, “Tulishangaa sana mshauri huyo aliposema alisoma vitabu tulivyoacha na kwamba vilikuwa vizuri. Akasema wanafunzi walivihitaji vitabu hivyo.” Ombi letu lilikubaliwa!

Brian anaendelea kusema: “Kisha mwelekezi wa wanafunzi alitueleza kwamba kila Jumapili wanafunzi wanaokaa hosteli hupelekwa kanisa wanalopenda. ‘Ikiwa watapenda kuja kanisani kwenu tutawaleta.’ Mimi na Roxanne tulishangaa sana. Badala ya kukataa ombi letu, walikuwa tayari kuwaleta wanafunzi Jumba la Ufalme!”

Siku ya kwanza ambayo Brian na Roxanne waliweka kigari waligawa vitabu 65, magazeti 8, na broshua 11. Pia, wanafunzi waliitikia vizuri sana. Mshauri na mwelekezi wa wanafunzi waliwaomba Brian na Roxanne warudi tena.

Wateja Watazama Video Zetu

Lipson, Mwanabetheli katika Visiwa vya Solomoni alikuwa akirudi baada ya mahubiri ya asubuhi. Akiwa njiani, alisikia wimbo wa Ufalme katika duka fulani na akaamua kwenda ili kuona kinachoendelea. Alishangaa kuona umati wa watu wakubwa kwa wadogo wakitazama video ya wimbo namba 55, “Uzima wa Milele—Hatimaye,” katika mfululizo wa video Uwe Rafiki ya Yehova. Wimbo ulipoisha, mwenye duka aliwaambia, “Nina video nyingine ambayo ningependa mtazame.” Kisha, akacheza video nyingine ya vibonzo yenye kichwa Ni Vibaya Kuiba. Baada ya kumaliza kutazama video hiyo, aliwaonya wote wasimwibie.

Kwa kuwa wengine walifika video hiyo ilipokuwa ikiendelea, aliwaambia hivi, “Ningependa nyote msikilize wimbo ninaopenda sana.” Kisha akacheza tena wimbo namba 55. Baadaye aliamua kuonyesha video Kwa Nini Ujifunze Biblia? na Ni Nini Hutendeka Kwenye Funzo la Biblia? kwa lugha ya Pijini ya Visiwa vya Solomoni.

Visiwa vya Solomoni: Mwenye duka akiwaonyesha wateja video kutoka tovuti yetu ya jw.org

Kwa sababu Intaneti ni ghali na haipatikani kwa urahisi, ni watu wachache tu wa Visiwa vya Solomoni wanaweza kutumia. Lakini, mwenye duka huyo ambaye si Shahidi wa Yehova anasaidia kupanda mbegu za kweli kwa kuwaonyesha watu video zetu dukani kwake.

Apata Jina la Mungu Kwenye Kitabu

Kila Jumatatu, wenzi fulani wa ndoa hufurahia kuhubiri kwa kutumia kigari cha machapisho katika eneo la Nouméa, mji mkuu wa New Caledonia. Siku moja mwanamke fulani mwenye haya alisogelea kigari na bila kusema lolote alichukua kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Baada ya nusu saa, alirudi akiwa na kitabu mkononi. Akawauliza wenzi hao, “Je, mmeona hili?” Alifunua kitabu na kuwaonyesha jina Yehova. Akasema “Hili ndilo jina la Mungu! Nimekuwa nikifanya utafiti kwenye maktaba kwa majuma kadhaa ili kupata ukweli kumhusu Mungu. Hata hivyo, nilichukua kitabu chenu na nikaingia kwenye gari. Nilipokifungua jambo la kwanza nililoona ni jina la Mungu, Yehova. Nimekuja kuwashukuru.” Wenzi hao walifurahia kuzungumza naye na kumwonyesha kichwa “Jina la Mungu—Maana na Matumizi” katika nyongeza ya kitabu Biblia Inafundisha. Mwanamke huyo alieleza kwamba alitaka kuendelea kufanya utafiti kwanza katika maktaba, lakini sasa anajua kigari kinapokuwa kila Jumatatu!