Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uingereza: Ndugu na dada wakiwakaribisha wajumbe kwenye kusanyiko la kimataifa

KUHUBIRI NA KUFUNDISHA DUNIANI KOTE

Ulaya

Ulaya
  • IDADI YA NCHI 47

  • IDADI YA WATU 743,421,605

  • IDADI YA WAHUBIRI 1,614,244

  • IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 842,091

Aliyedhaniwa Kuwa Shahidi Aanza Kujifunza Biblia

Kusanyiko la kimataifa lililofanywa London, Uingereza, liliwasisimua sana Mashahidi wageni na wenyeji. Andrew na Elizabeth walitembelea hoteli moja ya jijini London ili kuwasalimia baadhi ya wajumbe. Elizabeth alipomwona mwanamke aliyevalia vizuri eneo la mapokezi, alimsalimia kwa shauku akidhani kuwa ni mjumbe. Mwanamke huyo alishangaa, hivyo Elizabeth akamwomba msamaha akisema: “Samahani, nilidhani wewe pia ni mjumbe!”

Mwanamke huyo akauliza “Mjumbe wa nini?”

Elizabeth akamwonyesha ishara ya kuwakaribisha Mashahidi wa Yehova iliyokuwa kwenye meza ya mapokezi. Alishangaa sana jinsi alivyoitikia. Mwanamke huyo akasema “Safi sana! Je, ninafanana na Mashahidi?”

Kisha, mwanamke huyo alimwambia Elizabeth kwamba anaitwa Vivien, kutoka Nigeria, na alikuwa anaishi jirani na anapoishi Elizabeth. Vivien alikubali kujifunza Biblia na akataka pia watoto wake wajifunze. Andrew na Elizabeth walimtembelea Vivien nyumbani, nao pia walikaribishwa kwa uchangamfu. Vivien alifurahia sana fursa ya kukutana nao jijini London. Wenzi hao walimwonyesha Vivien kitabu Biblia Inafundisha, na walishangaa kujua ana kitabu hicho na amekuwa akisoma na watoto wake wanne. Walipomwambia kwamba kitabu hicho hutumiwa kujifunza Biblia, Vivien alisema hivi kwa shauku, “Nipo tayari kuanza sasa hivi!”

Barua Kutoka kwa Ndugu Mromani

Novemba 2014, kutaniko la kwanza la lugha ya Kiromani lilianzishwa nchini Slovakia. Kwenye kusanyiko la mzunguko la hivi karibuni, wahubiri 21 wanaozungumza Kiromani walibatizwa. Wote walitoka kijiji kimoja. Watu 495 walihudhuria Ukumbusho katika kutaniko la Kiromani. Ndugu mmoja aliyebatizwa hivi karibuni aliandika:

Slovakia: Wahubiri wa Ufalme wakimhubiria kwa shangwe mwanamke Mromani

“Mimi ni Mromani kutoka Žehra, Slovakia. Ninakoishi, watu weupe hutuona kuwa wazururaji, wachafu, waongo, na wezi. Siku moja, nilipoenda kanisani, muumini mmoja aliniambia kwamba sistahili kuwa hapo na nilipaswa kuondoka. Baada ya kufanyiwa hivyo, unaweza kuwazia jinsi nilivyohisi kuhusu watu weupe. Baadaye Mashahidi wa Yehova walinialika Jumba la Ufalme. Nilihofia kuvunjwa moyo tena. Nilishangaa kuona kwamba hata kabla ya kuingia Jumba la Ufalme, mtu mweupe alinisalimu kwa shauku. Hotuba ya watu wote ilipokuwa ikiendelea sikusikiliza kwa makini. Nilifikiria, ‘Inawezekanaje kila mtu ananisalimia kwa shauku?’

“Usiku sikupata usingizi, niliwaza tu yale niliyojionea kwenye Jumba la Ufalme. Hivyo, niliamua kwenda tena ili kuthibitisha ikiwa uchangamfu ule ulikuwa wa muda tu. Siku hiyo watu walikuwa wachangamfu zaidi na walinitendea kama rafiki yao wa muda mrefu. Sikuacha kuhudhuria mikutano, na hatimaye nikabatizwa. Hata baada ya kubatizwa, ukarimu wa akina ndugu haujabadilika, wanaendelea kunithamini. Nyakati nyingine wao hunipa chakula kizuri kuliko wanachokula! Nitaendelea kuwa sehemu ya ushirika huu, na Yehova ni Mungu ambaye ninapenda kumtumikia milele.”

Ombi la Kupata Mtu wa Kumhubiria Lajibiwa

Dada anayeitwa Aysel alikuwa akisafiri kwa basi kutoka mji wa Ganja kwenda Baku nchini Azerbaijan. Alisali kwa Yehova ili aweze kuzungumza na mtu kuhusu Biblia. Ingawa alipata mahali pa kuketi, mwanamke fulani alisisitiza akae jirani naye. Walianza kuzungumza, na baadaye, Aysel alielekeza mazungumzo hayo kwenye Biblia. Mwanamke huyo alisema kwamba anampenda Yesu na angependa kujua mengi kumhusu. Walipeana namba za simu na wakapanga kukutana tena. Mwanamke huyo alimwomba Aysel amletee Biblia.

Baada ya Aysel kurudi Ganja, alimtembelea mwanamke huyo kazini kwake. Mwanamke huyo alisema kwamba ana “kitabu cha sala” naye hukisoma kila siku. Aysel alishangaa kuona kitabu hicho ni Kuyachunguza Maandiko Kila Siku cha mwaka 2013! Walianza kujifunza Biblia na Aysel alifurahia sana kwamba Yehova alimpa ujasiri wa kuhubiri isivyo rasmi.

Barua ya Shukrani Kutoka kwa Mfungwa

Barua ifuatayo ilitoka nchini Hispania:

“Kwanza kabisa, Ningependa kuwashukuru kwa jitihada zenu za kuwapelekea ujumbe wa Biblia watu wa namna zote.

“Nilikutana na Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza jijini Tiranë, Albania miaka 15 iliyopita. Tukiwa kundi la vijana kumi wahalifu, nilishangaa kwamba Shahidi alizungumza nasi kwa ujasiri. Watu waliogopa kuzungumza nasi, hata hivyo, licha ya kwamba tulikuwa na silaha ndugu huyo alizungumza nasi. Kwa ujasiri aliongea nasi kuhusu Biblia. Nilivutiwa sana na ujasiri wake.

“Miaka minne iliyopita, nikiwa gerezani nchini Hispania nilitembelewa na Shahidi aliyependekeza nijifunze Biblia. Nilikubali, na tangu wakati huo nimefanya mabadiliko. Sasa sifanyi fujo wala jeuri. Nimefaulu kushinda tabia hizo kwa miaka kadhaa. Nimemjua Yehova, na hilo limenipa kusudi maishani. Ninajitahidi kuishi kwa amani na wengine, na nimekuwa mhubiri ambaye hajabatizwa kwa zaidi ya mwaka mmoja.

“Ingawa nimekuwa gerezani kwa miaka 12, kwa kipindi cha miaka minne kufikia sasa, nimekuwa mwenye furaha na amani ya akili kuliko wakati mwingine wowote. Ninamshukuru Yehova kila siku kwa jambo hilo.

“Majuma kadhaa yaliyopita nilitazama baadhi ya video katika tovuti ya jw.org. Niliguswa sana moyo nilipomwona ndugu aliyekuwa gerezani nchini Marekani. Mimi si mwenye hisia nyingi, lakini nilitokwa na machozi nilipoona mabadiliko aliyofanya maishani.

“Yehova na aendelee kubariki jitihada zenu za kuwafikishia habari njema watu wa namna zote kwa kutafsiri katika lugha mbalimbali na pia kututembelea tulio magerezani.

“Asanteni sana.”

“Hatimaye Nimepata Amani ya Akili”

“Mara zote nilijihisi sifai na mpweke maishani, nilitamani sana kuwa na amani,” akasema Felicity, mwenye umri wa miaka 68 anayeishi nchini Sweden. Kwa kuwa hakuridhika na imani yake ya Kikatoliki, alianza kuchunguza imani mbalimbali na hatimaye alijihusisha mno na waganga wa kienyeji na waaguzi.

Kwa sababu ya kukosa kusudi la maisha, alivunjika sana moyo hata alifikiria kujiua. “Huku nikitiririkwa na machozi, nilimwomba Mungu kwa sauti kubwa anijulishe cha kufanya. Majuma mawili baadaye, kijana fulani alinitembelea. Kijana huyo mchangamfu aliniuliza ikiwa ningependa kusikiliza Neno la Mungu. Moyoni niliwaza hivi, ‘Hapana, sikumaanisha Mashahidi wa Yehova!’”

Ingawa alifikiria kufunga mlango, aliamua kusikiliza na akakubali kujifunza Biblia kwa kutumia kitabu Biblia Inafundisha.. Felicity alisema, “Kilinisaidia kuilewa vizuri Biblia.” Alibatizwa katika kusanyiko la eneo nchini Sweden mwaka wa 2014. Sasa anasema hivi: “Hili ndilo jambo ambalo nimetafuta katika maisha yangu yote. Hatimaye nimepata amani ya akili.”