Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Ambayo Wazazi Huuliza

Maswali Ambayo Wazazi Huuliza

NYONGEZA

Maswali Ambayo Wazazi Huuliza

“Nifanye nini ili mtoto wangu azungumze nami?”

“Nimwekee mtoto wangu saa za kurudi nyumbani?”

“Ninaweza kumsaidia jinsi gani binti yangu awe na maoni yanayofaa kuhusu chakula?”

Hayo ni baadhi ya maswali 17 yanayojibiwa katika Nyongeza hii. Habari hii imegawanywa katika sehemu sita nayo inarejelea sura hususa za mabuku mawili ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1 na Buku la 2.

Soma habari hii. Ikiwezekana, izungumzie pamoja na mwenzi wako. Kisha tumia mashauri yaliyomo kuwasaidia watoto wako. Majibu yaliyo hapa yanategemeka. Hayategemei hekima ya wanadamu bali Neno la Mungu, Biblia.—2 Timotheo 3:16, 17.

290  Mazungumzo

297  Sheria

302  Uhuru

307  Ngono na Urafiki wa Kimapenzi

311  Mambo Yanayohusu Hisia

315  Hali ya Kiroho

 MAZUNGUMZO

Je, kugombana na mwenzi wangu au watoto wangu kunaweza kuwa na matokeo yoyote mabaya?

Kutoelewana hakuwezi kuepukika katika ndoa. Hata hivyo, unaweza kuchagua jinsi ya kushughulikia hali hiyo. Vijana huathiriwa sana wazazi wao wanapobishana. Hilo ni jambo zito, mnawawekea watoto wenu mfano ambao huenda watafuata ikiwa watafunga ndoa. Kwa nini msitumie pindi hiyo kuonyesha njia zinazofaa za kutatua matatizo? Jaribu mambo yafuatayo:

Sikiliza. Biblia inatuambia tuwe ‘wepesi kuhusu kusikia, si wepesi wa kusema, si wepesi wa ghadhabu.’ (Yakobo 1:19) Usiongeze kuni kwenye moto kwa ‘kulipa uovu kwa uovu.’ (Waroma 12:17) Hata ikiwa mwenzi wako hataki kusikiliza, wewe sikiliza.

Jaribu kueleza, si kuchambua. Mwambie mwenzi wako kwa utulivu jinsi mwenendo wake unavyokuathiri. (“Ninaumia unapo . . . ”) Epuka maelekeo ya kushutumu na kulaumu. (“Hunijali.” “Husikii hata kidogo.”)

Ahirisha mazungumzo. Nyakati nyingine ni afadhali kuacha mazungumzo mpaka wakati ambapo hasira zitakuwa zimepungua. Biblia inasema: “Mwanzo wa ugomvi ni kama mtu anayefungulia maji; kwa hiyo kabla mabishano hayajalipuka, jiondokee.”—Methali 17:14.

Ombaneni msamaha​—na inapofaa waombeni watoto wenu msamaha. Brianne, mwenye umri wa miaka 14, anasema: “Nyakati nyingine baada yao kugombana, wazazi wangu huniomba mimi na kaka yangu msamaha kwa sababu wanajua jinsi tunavyoathiriwa.” Jambo moja muhimu unaloweza kuwafundisha watoto wako ni unyenyekevu wa kusema, “Pole.”

Namna gani ikiwa unaogombana nao ni watoto wako? Fikiria ikiwa kwa njia fulani unaongeza kuni kwenye moto. Kwa mfano, fikiria hali inayozungumziwa katika utangulizi wa Sura ya 2 kwenye ukurasa wa 15 wa buku hili. Unaweza kuona mambo fulani ambayo mama ya Rachel alifanya, yaliyochangia ugomvi? Unaweza kuepuka kugombana na kijana wako jinsi gani? Jaribu yafuatayo:

● Epuka shutuma za jumla kama vile “Sikuzote wewe . . .” au “Hakuna siku . . .” Ukifanya hivyo, kijana wako hana budi kujitetea. Isitoshe, taarifa hizo zimetiliwa chumvi, na mtoto wako anajua hivyo. Pia, huenda mtoto wako anajua kwamba mara nyingi unapozungumza hivyo ni kwa sababu tu ya hasira, wala si kwa sababu ya kosa lake.

● Badala ya kutumia maneno yenye kuchoma yanayoanza na neno “wewe,” jaribu kueleza jinsi tabia ya mtoto wako inavyokuathiri. Kwa mfano, unaweza kusema, “Unapo . . . mimi huhisi . . .” Amini usiamini, kijana wako anapenda kujua unavyohisi. Unapomjulisha jinsi mambo anayofanya yanavyokuathiri, inakuwa rahisi zaidi kwake kushirikiana nawe. *

● Hata iwe vigumu kadiri gani, epuka kusema lolote mpaka hasira yako itakapokuwa imepoa. (Methali 29:22) Ikiwa mabishano yanazuka kwa sababu ya kazi za nyumbani, zungumza waziwazi na mtoto wako. Andika mambo anayohitaji kufanya, na ikiwezekana, mweleze waziwazi itakuwaje asipoyafanya. Sikiliza kwa subira maoni ya mtoto wako, hata ikiwa unaona kwamba maoni yake si sahihi. Vijana wengi huitikia vizuri wanaposikilizwa badala ya kukaripiwa.

● Kabla ya kukata kauli haraka-haraka kwamba kijana wako ameambukizwa na roho ya uasi, tambua kwamba mambo mengi unayojionea ni mambo ya kawaida mtoto anapokua. Anaweza kubishana ili tu akuonyeshe kwamba anakua. Jizuie usiingizwe katika mabishano. Kumbuka kwamba kijana wako anajifunza kutokana na jinsi unavyotenda unapokasirika. Onyesha subira na ustahimilivu, nawe utamwekea mwana au binti yako mfano mzuri wa kufuata.—Wagalatia 5:22, 23.

ONA BUKU LA 1, SURA YA 2, NA BUKU LA 2, SURA YA 24

Watoto wangu wanapaswa kujua habari kiasi gani kuhusu maisha yangu ya wakati uliopita?

Jiwazie katika hali hii: Mko mezani pamoja na mwenzi wako, binti yako, na marafiki. Mnapozungumza, rafiki yako anamtaja mtu fulani ambaye, kabla hujakutana na mwenzi uliye naye sasa, mlikuwa na uchumba naye kisha ukavunjika. Binti yako anashtuka, na kubaki kinywa wazi. Anauliza kwa mshangao: “Yaani ulikuwa na uchumba na mtu mwingine?” Hujawahi kumwambia binti yako jambo hilo. Sasa anataka kujua. Utafanya nini?

Kwa kawaida, ni vizuri kujibu maswali ya mtoto wako. Kila mara, anapokuuliza maswali na kusikiliza majibu yako, mnapashana habari—jambo ambalo wazazi wengi wanatamani.

Hata hivyo, mwana au binti yako anahitaji kujua kila kitu kuhusu maisha yako ya wakati uliopita? Kwa kawaida, huenda usimwambie habari zenye kuaibisha. Hata hivyo, inapofaa, kuwaambia hali ngumu ulizopitia kunaweza kuwasaidia watoto wako. Jinsi gani?

Fikiria mfano wa mtume Paulo. Pindi moja, alisema hivi juu yake mwenyewe: “Ninapotaka kufanya yaliyo sawa, yaliyo mabaya yapo pamoja nami . . . . Maskini mimi!” (Waroma 7:21-24) Yehova Mungu alitumia roho yake kuongoza maneno hayo yaandikwe na kuhifadhiwa katika Biblia kwa faida yetu. Nasi kwa kweli tunafaidika, kwa sababu sisi sote tumewahi kuhisi kama Paulo alivyohisi.

Vivyo hivyo, kusikia kuhusu maamuzi mazuri na mabaya uliyofanya kunaweza kuwasaidia watoto wako wakuelewe vizuri zaidi. Ni kweli kwamba malezi yako yalikuwa tofauti. Hata hivyo, ingawa nyakati zimebadilika, binadamu ni walewale; nazo kanuni za Kimaandiko hazibadiliki. (Zaburi 119:144) Kuzungumzia hali ngumu ambazo umepitia—na jinsi ulivyozishinda—kunaweza kuwasaidia vijana wako wanapotatua matatizo yao wenyewe. Kijana mmoja anayeitwa Cameron anasema: “Unapogundua kwamba wazazi wako wamepitia hali kama zako, unawaona kuwa watu halisi, wenye hisia kama wewe.” Anaongezea: “Utakapopata tatizo wakati ujao, utataka kujua ikiwa wazazi wako pia walipitia hali kama hiyo.”

Tahadhari: Si lazima kila mara unapowasimulia watoto wako hali fulani ulizopitia umalizie kwa kuwapa mashauri. Ni kweli kwamba huenda ukawa na wasiwasi kwamba kijana wako atakata kauli isivyofaa au hata akahisi kwamba ana haki ya kufanya makosa kama yale uliyofanya. Lakini badala ya kumwambia kile ambacho unataka ajifunze kutokana na mazungumzo yenu (Kumwambia, “Ndiyo sababu hupaswi kamwe . . . ”), mwambie kifupi tu jinsi wewe unavyohisi. (“Kila mara ninapofikiria hali hiyo, najuta kwa nini nilifanya hivi au vile, kwa sababu . . . ”) Ukifanya hivyo, kijana au binti yako anaweza kujifunza mambo muhimu kutokana na maisha yako bila kuhisi kwamba alikuwa akikaripiwa.—Waefeso 6:4.

ONA BUKU LA 1, SURA YA 1

Nifanye nini ili mtoto wangu azungumze nami?

Watoto wako walipokuwa wachanga, huenda walikuwa na mazoea ya kukuambia kila kitu. Ulipowauliza swali, walijibu bila kusita. Kwa kweli, mara nyingi hata hukuhitaji kuuliza maswali, habari zilibubujika kama chemchemi ya maji. Sasa, kuwafanya matineja wako wazungumze ni kama kujaribu kuchota maji kutoka ndani ya kisima kilichokauka. ‘Wanazungumza na marafiki wao,’ unajiambia. ‘Kwa nini hawazungumzi nami?’

Usikate kauli kwamba wamekukataa au kwamba hawataki kukuhusisha katika maisha yao kwa kuwa tu hawakuambii kinachoendelea maishani mwao. Ukweli ni kwamba, wanakuhitaji sasa kuliko wakati mwingine wowote. Isitoshe, utafiti unaonyesha kwamba vijana wengi bado wanathamini mashauri ya wazazi wao—hata kuliko mashauri ya marafiki wao au vyombo vya habari.

Ikiwa ni hivyo basi, kwa nini wanasita kukueleza yaliyo moyoni mwao? Fikiria sababu ambazo vijana fulani wanasema zinawafanya wasiwe na uhuru wa kuzungumza na wazazi wao. Kisha ujiulize maswali yanayofuata, na kusoma maandiko yaliyoonyeshwa.

“Ni vigumu kwangu kuzungumza na Baba kwa sababu ana shughuli nyingi, kazini na kutanikoni. Ni kana kwamba hana wakati wa kuzungumza nami.”—Andrew.

‘Je, inawezekana kwamba bila kujua, nimefanya ionekane nina shughuli nyingi sana hivi kwamba sina wakati wa kuzungumza na vijana wangu? Ikiwa ndivyo, ninaweza kufanya nini ili waweze kunifikia kwa uhuru? Ni wakati gani hasa ninapoweza kuzungumza na watoto wangu kwa ukawaida?’—Kumbukumbu la Torati 6:7.

“Nilimwendea mama yangu nikilia na kumweleza kuhusu ugomvi uliotokea shuleni. Nilitaka anifariji, badala yake akanikemea. Tangu wakati huo, sijazungumza naye kuhusu jambo lolote muhimu.”—Kenji.

‘Mimi hufanya nini watoto wangu wanaponijia wakiwa na tatizo? Hata ikiwa wanahitaji kusahihishwa, je, ninaweza kujifunza kunyamaza, kusikiliza, na kuelewa hisia zao kabla ya kutoa mashauri?’—Yakobo 1:19.

“Kila wakati wazazi wanaposema tunaweza kuwaambia chochote na hawatakasirika, bado wao hukasirika. Kisha unahisi kuwa umesalitiwa.”—Rachel.

‘Mtoto wangu anaponiambia jambo lenye kukasirisha, ninaweza kujizuia jinsi gani nisikasirike?’—Methali 10:19.

“Mara nyingi nilipozungumza na Mama kuhusu mambo ya siri, aliwaambia marafiki wake. Niliacha kumwamini kwa muda mrefu sana.”—Chantelle.

‘Je, mimi huwa ninamwonyesha mtoto wangu kwamba ninajali hisia zake kwa kutoeneza mambo ya siri ambayo ameniambia?’—Methali 25:9.

“Kuna mambo mengi sana ninayotaka kuwaambia wazazi wangu. Ninachohitaji tu ni waanzishe mazungumzo.”—Courtney.

‘Je, ninaweza kuchukua hatua ya kwanza kuzungumza na kijana wangu? Ni wakati gani mzuri wa kuzungumza naye?’—Mhubiri 3:7.

Ukiwa mzazi, utafaidika sana kwa kufanya kila uwezalo ili kudumisha mazungumzo kati yako na mtoto wako. Fikiria mfano wa Junko mwenye umri wa miaka 17, nchini Japani. Anasema: “Wakati mmoja, nilimwambia mama yangu kwamba najisikia huru zaidi nikiwa na wanafunzi wenzangu kuliko ninapokuwa na Wakristo wenzangu. Siku iliyofuata, mama yangu aliniachia barua juu ya dawati. Katika barua hiyo, aliniambia jinsi yeye pia hapo awali alivyohisi hakuwa na marafiki kati ya waamini wenzake. Alinikumbusha kuhusu watu fulani katika Biblia ambao walimtumikia Mungu hata wakati ambapo hawakuwa na mtu yeyote wa kuwatia moyo. Pia, alinipongeza kwa kujitahidi kuwa na marafiki wazuri. Nilishangaa kujua kwamba si mimi peke yangu niliyekuwa na tatizo hilo. Mama yangu aliwahi kuwa nalo pia, nilifurahi kujua hivyo mpaka nikalia. Nilitiwa moyo sana na mambo ambayo mama aliniambia, na nikapata nguvu ya kufanya yaliyo sawa.”

Kama mama ya Junko alivyotambua, vijana wanaweza kuzungumza kwa uhuru na wazazi ikiwa wana uhakika kwamba hawatadhihakiwa au kuchambuliwa. Lakini, utafanya nini ikiwa kijana wako anaonekana kuwa ameudhika au hata kukasirika anapozungumza na wewe? Epuka mwelekeo wa kukasirika pia. (Waroma 12:21; 1 Petro 2:23) Badala yake, hata ikionekana kuwa vigumu, zungumza na kujiendesha kwa njia ambayo unatarajia kijana wako aige.

Kumbuka: Kipindi cha kukua ili kufikia utu uzima ni kipindi cha mabadiliko kwa vijana. Wataalamu wamegundua kwamba wakati huo, mwenendo wa vijana hubadilika-badilika—pindi moja wanaweza kujiendesha kama watu wazima na wakati mwingine kama mtoto. Ikiwa kijana wako anajiendesha hivyo, unaweza kufanya nini, hasa wakati ambapo anajiendesha kama mtoto?

Usiropoke kwa hasira au kuwa na ubishi wa kitoto naye. Badala yake, zungumza na kijana wako kama vile ungezungumza na mtu mzima. (1 Wakorintho 13:11) Kwa mfano, kijana wako akitenda kitoto kwa kukuuliza, “Kwa nini kila wakati unanisumbua?” huenda ukashawishiwa kujibu kwa hasira. Lakini, ukifanya hivyo, utaonyesha kwamba umeshindwa kudhibiti mazungumzo, na yaelekea mtaanza kubishana. Kwa upande mwingine, unaweza tu kusema: “Inaonekana umekasirika sana. Tutazungumza baadaye utakapokuwa umetulia.” Kufanya hivyo kunaonyesha unaweza kujidhibiti. Sasa mnaweza kuzungumza, badala ya kubishana.

ONA BUKU LA 1, SURA YA 1 NA YA 2

 SHERIA

Je, niweke sheria ya saa za kurudi nyumbani?

Ili kujibu swali hilo, jiwazie ukiwa katika hali hii: Ni nusu saa baada ya wakati ambao mtoto wako anapaswa kurudi nyumbani unaposikia mlango ukifunguliwa polepole. ‘Anafikiri kwamba nimelala,’ unajiambia. Bila shaka hujalala. Umekuwa ukingoja mlangoni tangu wakati ambapo alipaswa kurudi. Sasa mlango uko wazi, na macho yenu yanakutana. Utasema nini? Utafanya nini?

Kuna mambo fulani unayoweza kufanya. Unaweza kulipuuza jambo hilo. Huenda ukasema moyoni, ‘Ni kawaida ya vijana.’ Au unaweza kukasirika sana na kusema, “Huo ndio mwisho wa kutoka nyumba hii!” Badala ya kutenda bila kufikiri, msikilize kwanza, ujue ikiwa kuna sababu nzuri iliyofanya achelewe. Kisha, unaweza kutumia nafasi hiyo kumfundisha jambo muhimu. Jinsi gani?

Pendekezo: Mwambie mtoto wako kwamba mtazungumzia jambo hilo siku inayofuata. Kisha, wakati unaofaa, mketi na kuzungumzia jinsi utakavyoshughulikia jambo hilo. Wazazi fulani wamejaribu njia ifuatayo: Binti au mwana wao anapochelewa kurudi nyumbani kwa wakati uliowekwa, safari inayofuata, muda wake wa kurudi unafupishwa kwa nusu saa. Kwa upande mwingine, ikiwa kwa kawaida anarudi nyumbani wakati aliowekewa na kuonyesha kwamba anategemeka, unaweza kufikiria kumpa uhuru zaidi mara kwa mara, au hata kuongeza wakati anaopaswa kurudi nyumbani. Inafaa mtoto wako aelewe vizuri ni wakati gani anaopaswa kurudi nyumbani na matokeo yatakuwa nini asiporudi kwa wakati. Kisha usikose kutekeleza ulivyosema.

Hata hivyo, kumbuka kwamba Biblia inasema: “Usawaziko wenu na ujulikane.” (Wafilipi 4:5) Kwa hiyo, kabla ya kumwekea mtoto wakati wa kurudi nyumbani, huenda ukataka kuzungumzia jambo hilo pamoja naye ukimruhusu apendekeze wakati fulani na aeleze kwa nini amechagua wakati huo. Yafikirie maoni yake. Ikiwa mtoto wako ameonyesha kwamba ni mwenye kutegemeka, unaweza kukubali mapendekezo yake ikiwa hayapiti kiasi.

Kudumisha wakati ni jambo muhimu maishani. Hivyo, mbali na kumwepusha mtoto na hatari za kuwa nje, kumwekea wakati wa kurudi nyumbani kunatimiza mengi zaidi. Unamfundisha mambo yatakayomnufaisha kwa muda mrefu hata baada ya kuondoka nyumbani.—Methali 22:6.

ONA BUKU LA 1, SURA YA 3, NA BUKU LA 2, SURA YA 22

Ninaweza kufanya nini kutoelewana kunapotokea kati yangu na watoto wangu kuhusu mavazi?

Fikiria mfano ulio mwanzoni mwa ukurasa wa 77 katika buku hili. Wazia kwamba Heather ni binti yako. Umeona kwamba vazi alilovaa linaonyesha sana sehemu za mwili, ni kana kwamba yuko uchi. Unamwambia mara moja. “Nenda ukabadili nguo hizo mara moja, la sivyo huendi popote!” Ni kweli huenda akafanya hivyo. Anajua asipofanya hivyo, ataona cha mtema kuni. Hata hivyo, unaweza kufanya nini ili abadili maoni yake badala ya kubadili mavazi tu?

● Kwanza, kumbuka hili: Lazima kijana wako atambue matokeo ya kuvaa kwa njia isiyo na kiasi, kama tu vile wewe unavyotambua. Moyoni, kijana wako hataki kuonekana kama mjinga au kuvuta uangalifu wa watu kwa njia isiyofaa. Mweleze kwa subira ni kwa nini nguo zisizo na kiasi hazivutii. * Mpendekezee mavazi mengine.

● Pili, uwe mwenye usawaziko. Jiulize, ‘Vazi hilo linavunja kanuni ya Biblia, au ni kwamba tu silipendi?’ (2 Wakorintho 1:24; 1 Timotheo 2:9, 10) Ikiwa ni mapendezi tu, je, unaweza kulegeza kidogo msimamo wako?

● Tatu, usimwambie tu kijana wako kwamba vazi lake halifai. Msaidie kutafuta mavazi yanayofaa. Kwa nini usitumie chati kwenye ukurasa wa 82 na 83 katika buku hili kukusaidia kuzungumza na mtoto wako? Wakati unaotumia na jitihada zako hazitakuwa za bure!

ONA BUKU LA 1, SURA YA 11

Nimruhusu mtoto wangu acheze michezo ya kompyuta?

Michezo ya kompyuta imebadilika sana tangu ulipokuwa kijana. Ukiwa mzazi, unaweza kumsaidia mtoto wako jinsi gani atambue na kuepuka hatari zinazoweza kutokea?

Hutapata matokeo mazuri kwa kushutumu michezo yote ya kompyuta au kwa kusema kucheza michezo ya kompyuta ni kupoteza tu wakati. Kumbuka, si michezo yote iliyo mibaya. Hata hivyo, inaweza kumfanya mtu awe na uraibu wa kuicheza. Kwa hiyo, chunguza muda ambao mtoto wako hutumia akicheza michezo hiyo. Pia, chunguza aina ya michezo inayomvutia. Hata unaweza kumwuliza maswali kama haya:

● Ni mchezo gani unaopendwa sana na wanafunzi wenzako?

● Mchezo huo unachezwa namna gani?

● Unafikiri ni kwa nini mchezo huo unapendwa sana?

Huenda ukatambua kwamba mtoto wako anajua mengi kuhusu michezo ya kompyuta kuliko unavyofikiri! Labda hata amecheza michezo ambayo wewe unaona kuwa haifai. Ikiwa ndivyo, usitende kwa hasira. Hiyo ni nafasi ya kumsaidia asitawishe nguvu za ufahamu.—Waebrania 5:14.

Mwulize mtoto wako maswali ambayo yatamsaidia atambue sababu inayomfanya avutiwe na michezo isiyofaa. Kwa mfano unaweza kumwuliza swali kama hili:

● Wewe huona kuwa umetengwa na marafiki wako usiporuhusiwa kucheza mchezo huo?

Nyakati nyingine vijana hucheza mchezo fulani ili tu wawe na mambo ya kuzungumza na wenzao. Ikiwa hiyo ndiyo sababu, huenda usishughulikie hali hiyo kama vile ambavyo ungefanya ikiwa ungegundua kuwa mtoto wako anavutiwa na michezo inayoonyesha jeuri au mambo ya ngono.—Wakolosai 4:6.

Lakini namna gani ikiwa mtoto wako anavutiwa na mambo yasiyofaa katika mchezo huo? Vijana fulani husema kwamba hawaathiriwi na michezo yenye jeuri. Wao husema, ‘Kwa kuwa tu ninafanya jambo kwenye kompyuta haimaanishi nitalifanya kihalisi.’ Ikiwa mtoto wako anahisi hivyo, mwonyeshe Zaburi 11:5. Kama maneno ya mstari huo yanavyoonyesha, kinachomchukiza Yehova si tu kuwa mjeuri bali pia kupenda jeuri. Kanuni hiyo pia inahusu ukosefu wa adili katika ngono au matendo mengine ambayo Neno la Mungu linashutumu.—Zaburi 97:10.

Ikiwa michezo ya kompyuta ni tatizo kwa mtoto wako, jaribu mambo yafuatayo:

● Usiruhusu michezo ya kompyuta ichezwe mahali pa faragha, kama vile katika chumba cha kulala.

● Weka sheria—kwa mfano, hakuna kucheza kabla ya kumaliza kazi za shule, chakula, au mambo mengine muhimu.

● Kazia kwamba ni muhimu kufanya mazoezi ya kimwili.

● Watazame watoto wako wakicheza michezo ya kompyuta, au hata, ucheze nao nyakati nyingine.

Bila shaka, ili uwaongoze watoto wako kuhusu mambo ya burudani, unahitaji kuwa na uhuru wa kusema. Kwa hiyo jiulize, ‘Mimi huwa ninatazama sinema na vipindi gani vya televisheni?’ Usijidanganye, ikiwa una nyuso mbili, watoto wako watajua!

ONA BUKU LA 2, SURA YA 30

Namna gani ikiwa mtoto wangu ni mraibu wa simu ya mkononi, kompyuta, au chombo kingine cha elektroniki?

Je, kijana wako anatumia wakati mwingi sana kwenye Intaneti, akituma na kupokea ujumbe, au anatumia wakati mwingi zaidi na kifaa chake cha kucheza MP3 kuliko anavyotumia na wewe? Ikiwa ndivyo, unaweza kufanya nini?

Unaweza kumnyang’anya kifaa hicho. Hata hivyo, usifanye ionekane kana kwamba vifaa vyote vya elektroniki havifai. Huenda, leo hii unatumia aina fulani ya kifaa ambacho hakikuwako siku za wazazi wako. Kwa hiyo, badala ya kumnyang’anya kijana wako kifaa hicho—isipokuwa iwe kuna sababu nzuri ya kufanya hivyo—kwa nini usitumie nafasi hiyo kumfunza mwana au binti yako kutumia kifaa hicho kwa hekima na kiasi? Unaweza kufanya hivyo jinsi gani?

Mketi na kuzungumzia jambo hilo. Kwanza mweleze hangaiko lako. Pili, msikilize anapozungumza. (Methali 18:13) Tatu, tafuta utatuzi unaofaa. Usiogope kuweka mipaka thabiti, lakini uwe mwenye usawaziko. Kijana anayeitwa Ellen anasema: “Nilipokuwa nikitumia muda mwingi kutuma na kupokea ujumbe, wazazi wangu hawakuninyang’anya simu; waliweka sheria. Njia yao ya kushughulikia jambo hilo imenisaidia kuwa na usawaziko, hata wakati ambapo wazazi wangu hawako.”

Namna gani mwana au binti yako akijitetea? Usikate kauli kwamba amekataa kufuata shauri lako. Badala yake, kuwa na subira na umpe wakati afikirie jambo hilo. Kuna uwezekano kwamba anakubaliana nawe na atafanya marekebisho yanayohitajiwa. Vijana wengi ni kama Hailey, ambaye alisema: “Mwanzoni nilikasirika wazazi wangu waliponiambia kwamba nina uraibu wa kutumia kompyuta. Hata hivyo, baadaye, kadiri nilivyofikiria jambo hilo, ndivyo nilivyoona kwamba wanasema kweli.”

ONA BUKU LA 1, SURA YA 36

 UHURU

Ninaweza kumpa mtoto wangu uhuru kiasi gani?

Huenda swali hilo likaonekana kuwa gumu zaidi unapofikiria suala la faragha. Kwa mfano, namna gani ikiwa mwana wako yuko katika chumba chake cha kulala, mlango umefungwa? Uingie bila kubisha? Au namna gani ikiwa binti yako amesahau simu yake alipoondoka mbiombio kwenda shuleni? Je, usome jumbe zake?

Hayo si maswali rahisi kujibu. Ukiwa mzazi, una haki ya kujua kile ambacho kijana wako anafanya na una jukumu la kumlinda. Lakini huwezi kuwa kama mwewe, kila wakati ukizunguka-zunguka na kuchunguza kila kitu anachofanya. Unaweza kuwa na usawaziko jinsi gani?

Kwanza, tambua kwamba kijana wako anapotafuta faragha, sikuzote haimaanishi kwamba anafanya jambo lolote baya. Ni jambo la kawaida kwa vijana wanaokua. Kuwa na faragha kunawazoeza vijana ‘kuruka kwa mabawa yao wenyewe’ wanapojitafutia marafiki na kujitatulia matatizo yao kwa kutumia ‘nguvu zao za kufikiri.’ (Waroma 12:1, 2) Faragha huwasaidia vijana kukuza uwezo wa kufikiri, sifa muhimu itakayowawezesha kutenda kama watu waliokomaa. Pia, inawapa nafasi ya kutafakari kabla ya kufanya maamuzi au kujibu maswali magumu.—Methali 15:28.

Pili, tambua kwamba ukijaribu kutawala kila sehemu ya maisha ya kijana wako utamfanya akuchukie na aasi. (Waefeso 6:4; Wakolosai 3:21) Je, hilo linamaanisha kwamba unapaswa kumwacha afanye anachotaka? Hapana, kwa kuwa bado wewe ndiye mzazi wake. Hata hivyo, lengo lako ni kumsaidia mtoto wako awe na dhamiri iliyozoezwa. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7; Methali 22:6) Vyovyote vile, ni afadhali kumpa mwongozo kuliko kumchunga.

Tatu, zungumzia jambo hilo pamoja na kijana wako. Sikiliza anapokuambia mambo yanayomhangaisha. Kuna nyakati unapoweza kulegeza msimamo wako kidogo? Mwache kijana wako ajue kwamba utamruhusu kuwa na faragha kwa kiasi fulani iwapo tu atajionyesha kuwa mwenye kutegemeka. Taja waziwazi matokeo ya kutotii, na uhakikishe kwamba unatekeleza mambo unayosema. Uwe na hakika kwamba unaweza kumpa kijana wako kiasi fulani cha faragha bila kupuuza jukumu lako la kuwa mzazi mwenye kujali.

ONA BUKU LA 1, SURA YA 3 NA YA 15

Mtoto wangu anapaswa kuacha shule wakati gani?

“Walimu wangu wanachosha!” “Ninapewa kazi nyingi za shule!” “Nang’ang’ana na masomo kisha napata alama za wastani​—kuna haja gani ya kujaribu?” Kwa sababu ya hali kama hizo, vijana wengine hushawishiwa kuacha shule kabla hata hawajapata ustadi wanaohitaji ili kujitegemeza. Mwana au binti yako akitaka kuacha shule, utafanya nini? Jaribu yafuatayo:

Fikiria maoni yako mwenyewe kuhusu elimu. Je, ulikuwa na maoni ya kwamba kwenda shule ni kupoteza wakati, ukihisi kana kwamba uko gerezani na unalazimika kuvumilia mpaka wakati ambapo utaweza kufuatilia miradi muhimu zaidi? Ikiwa ndivyo, huenda watoto wako wakawa na maoni kama yako kuhusu masomo. Ukweli ni kwamba, elimu nzuri itawasaidia kupata “hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri”—sifa wanazohitaji ili wafikie miradi yao.—Methali 3:21.

Mwandalie. Vijana fulani ambao wanaweza kupata alama nzuri, hawajui namna ya kujifunza—au hawako katika mazingira yanayofaa. Mahali pa kujifunzia panaweza kuwa na meza isiyo na vitu vingi, mwangaza wa kutosha, na vifaa vya utafiti. Unaweza kumsaidia mtoto wako kufanya maendeleo, yawe ya kielimu au ya kiroho, kwa kumwandalia mahali panapofaa pa kutafakari juu ya maoni na mawazo mapya.​—Linganisha 1 Timotheo 4:15.

Jihusishe. Waone walimu na washauri kuwa marafiki, si maadui. Kutana nao. Jua majina yao. Zungumza nao kuhusu miradi na matatizo ya mtoto wako. Ikiwa mtoto wako anajitahidi pasipo mafanikio yoyote kupata alama nzuri, tafuta sababu. Kwa mfano, je, mtoto wako anafikiri kwamba kufanya vizuri shuleni kutafanya achokozwe? Anakosa kuelewana na mwalimu fulani? Namna gani masomo ambayo amechagua? Masomo yanapaswa kumchochea mtoto wako bali si kumlemea. Uwezekano mwingine: Inawezekana ana tatizo fulani la kimwili, kama vile kutoona vizuri, au kutoweza kusoma?

Ukiendelea kumzoeza mtoto wako, kielimu na kiroho, atapata mafanikio.​—Zaburi 127:4, 5.

ONA BUKU LA 1, SURA YA 19

Nitajua jinsi gani kwamba mtoto wangu yuko tayari kuondoka nyumbani?

Serena, aliyetajwa katika Sura ya 7 ya buku hili, anaogopa kuondoka nyumbani. Kwa nini? Anasema: “Hata ninapotaka kununua kitu kwa kutumia pesa zangu, Baba haniruhusu. Anasema hiyo ni kazi yake. Hivyo, wazo la kulipia gharama zangu linanitia woga.” Bila shaka, baba ya Serena anamtakia mema, lakini, unafikiri anamtayarisha binti yake kujua jinsi ya kuisimamia nyumba yake mwenyewe?—Methali 31:10, 18, 27.

Je, unawalinda watoto wako kupita kiasi hivi kwamba hawajajifunza jinsi ya kuishi peke yao? Utajua jinsi gani? Ukiwa mzazi, fikiria mambo manne yafuatayo, ambayo pia yanatajwa katika Sura ya 7 chini ya kichwa “Niko Tayari?”

Matumizi ya pesa. Je, watoto wako wenye umri mkubwa wanajua jinsi ya kujaza fomu za ushuru na kulipia ushuru mbalimbali unaotozwa katika eneo lenu? (Waroma 13:7) Wanajua jinsi ya kushughulikia madeni au mikopo? (Methali 22:7) Wanaweza kupanga bajeti na kuifuata? (Luka 14:28-30) Wamejionea furaha inayotokana na kuwa na kitu ambacho wamejinunulia kwa pesa ambazo wamechuma wenyewe? Wamejionea furaha iliyo kubwa hata zaidi inayotokana na kutumia wakati na mali zao ili kuwasaidia wengine?—Matendo 20:35.

Kazi za nyumbani. Je, binti na pia wana wako wanajua kupika? Umewafundisha kufua na kupiga pasi? Ikiwa wanajua kuendesha gari, wanajua jinsi ya kurekebisha mambo madogo-madogo kama vile kubadili fyuzi, oili, au gurudumu lenye pancha?

Kushirikiana na wengine. Watoto wako wakubwa wanapokosana, je, nyakati zote unaingilia kati na kuwatatulia matatizo yao? Au umewazoeza kutatua matatizo yao kwa amani, kisha wakueleze jinsi walivyofanya?—Mathayo 5:23-25.

Ratiba ya kibinafsi ya mambo ya kiroho. Je, wewe huwaambia watoto wako mambo wanayopaswa kuamini, au unawasadikisha kuyaamini? (2 Timotheo 3:14, 15) Badala ya kuwajibu maswali yao kuhusu dini na maadili kila wakati, je, unawafundisha kusitawisha “uwezo wa kufikiri”? (Methali 1:4) Unaona kwamba mazoea yako ya kujifunza si mazuri na hungependa watoto wako wakuige, badala yake wawe na mazoea mazuri zaidi ya kujifunza Biblia? *

Bila shaka, kuwazoeza watoto mambo hayo kunahitaji wakati na jitihada nyingi. Lakini jitihada hizo huwa na faida kubwa watakapoondoka nyumbani.

ONA BUKU LA 1, SURA YA 7

 NGONO NA URAFIKI WA KIMAPENZI

Je, nizungumze na mtoto wangu kuhusu ngono?

Watoto huanza kuambiwa kuhusu ngono wakiwa na umri mdogo sana. Biblia ilitabiri kwamba “siku za mwisho” zingekuwa “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” kwa kuwa watu wangekuwa “wasiojizuia” na “wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.” (2 Timotheo 3:1, 3, 4) Tabia ya kufanya ngono bila kuwajibika, ni moja ya mambo yanayoonyesha kwamba unabii huo ni wa kweli.

Ulimwengu wa leo ni tofauti kabisa na ulimwengu wa siku zako. Hata hivyo, matatizo ni yaleyale. Kwa hiyo, usishangazwe wala kuogopeshwa na uvutano mbaya unaowazunguka watoto wako. Badala yake, azimia kuwasaidia kufanya kama mtume Paulo alivyowasihi Wakristo miaka 2,000 hivi iliyopita: “Vaeni mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu ili mweze kusimama imara kupinga hila za Ibilisi.” (Waefeso 6:11) Ukweli ni kwamba, vijana Wakristo wanajitahidi sana kufanya yaliyo sawa ingawa kuna uvutano usiofaa unaowazunguka. Unaweza kuwasaidia jinsi gani watoto wako wafanye hivyo pia?

Njia moja ni kuanzisha mazungumzo, ukitumia sura zilizo katika Sehemu ya 4 ya kitabu hiki na Sehemu ya 1 na ya 7 katika Buku la 2. Sura hizo zina maandiko yanayochochea fikira. Maandiko fulani yanazungumzia mifano ya watu halisi ambao walichukua msimamo kwa ajili ya lililo sawa na baraka walizopata, na pia wale waliopuuza sheria za Mungu na kupatwa na madhara. Maandiko mengine yana kanuni zinazoweza kuwasaidia watoto wako kutambua kwamba ni pendeleo kubwa kwao na kwako pia kuishi kulingana na sheria za Mungu. Kwa nini msichunguze habari hiyo pamoja nao?

ONA BUKU LA 1, SURA YA 23, 25, NA 32, NA  , NA  , NA  , NA BUKU LA 2, SURA YA 4-6, 28, NA 29

Je, nimruhusu mtoto wangu aanze urafiki wa kimapenzi?

Iwe ni sasa au wakati ujao, watoto wenu watashawishiwa kuwa na urafiki wa kimapenzi. “Hata sihitajiwi kufanya lolote!” anasema Phillip. “Wasichana huniomba tuwe na urafiki, nami huwaza moyoni, ‘Nitafanya nini sasa?’ Ni vigumu kukataa kwa sababu wengine wao ni warembo sana!”

Jambo bora zaidi mnaloweza kufanya mkiwa wazazi ni kuzungumza na kijana wenu kuhusu uzito wa kuwa na urafiki wa kimapenzi, labda mkitumia Sura ya 1 katika Buku la 2 kama msingi wa mazungumzo yenu. Jaribuni kujua maoni ya mwana au binti yenu kuhusu matatizo anayopata shuleni na hata katika kutaniko la Kikristo. Nyakati nyingine mnaweza kuwa na mazungumzo hayo katika vikao visivyo rasmi, kama vile “unapoketi katika nyumba yako na unapotembea barabarani.” (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Haidhuru kikao chenyewe, kumbuka kuwa “mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema.”—Yakobo 1:19.

Usishtuke mwana au binti yako akisema anapendezwa na mtu wa jinsia tofauti. “Baba yangu alipogundua nina mpenzi alikasirika sana!” asema msichana mmoja. “Alijaribu kunitisha kwa kuniuliza maswali mengi kama vile, ikiwa niko tayari kufunga ndoa, jambo ambalo ukiwa kijana linafanya utake kuendeleza urafiki huo kwa muda mrefu ili kuwathibitishia wazazi wako kwamba wamekosea!”

Ikiwa kijana wako anajua kwamba hupendi kusikia chochote kuhusu urafiki kama huo, ni hatari. Anaweza kuazimia kuendeleza urafiki huo kisiri. Msichana mmoja anasema: “Wazazi wanapoudhika kupita kiasi, watoto huficha urafiki huo hata zaidi. Hawaukatishi. Wanachofanya ni kuwa wasiri hata zaidi.”

Utapata matokeo mazuri zaidi mkizungumza mambo waziwazi. Brittany mwenye umri wa miaka 20 anasema: “Nyakati zote wazazi wamezungumza waziwazi kuhusu uzito wa kuwa na urafiki wa kimapenzi. Ni muhimu wajue mtu ninayependezwa naye, na ninafikiri ni sawa hivyo! Baba yangu ataongea naye. Ikiwa wazazi wangu wana wasiwasi wowote kumhusu, wananiambia. Kwa kawaida mimi hukata kauli kwamba sipendezwi na mtu fulani hata kabla hatujaanza kuwa marafiki wa karibu.”

Hata hivyo, baada ya kusoma Sura ya 2 katika Buku la 2, huenda ukajiuliza, ‘Je, mwana au binti yangu anaweza kuwa na urafiki wa kimapenzi ambao sijui?’ Ona mambo ambayo vijana fulani wanasema yanafanya wawe na urafiki wa kimapenzi kisiri, kisha ufikirie maswali yanayotajwa.

“Vijana wengine hawana starehe nyumbani, kwa hiyo, wanaamua kuwa na mpenzi.”—Wendy.

Ukiwa mzazi, unaweza kuhakikisha jinsi gani kwamba mahitaji ya kihisia ya watoto wako yanatoshelezwa? Kuna mabadiliko unayoweza kufanya kuhusiana na jambo hilo? Ikiwa ndivyo, ni mabadiliko gani?

“Nilipokuwa na umri wa miaka 14, mwanafunzi kutoka nchi ya kigeni aliniomba niwe rafiki yake. Nilikubali. Nilifikiri kwamba ni jambo zuri kuwa na mvulana anayenikumbatia.”—Diane.

Kama Diane angekuwa binti yako, ungefanya nini?

“Simu za mkononi zinafanya iwe rahisi kuwa na urafiki wa kimapenzi kisiri. Wazazi hawajui kinachoendelea!”—Annette.

Unaweza kuchukua hatua gani ikiwa watoto wako wanatumia simu za mkononi?

“Ni rahisi kuendeleza urafiki wa kimapenzi kisiri iwapo wazazi hawajui watoto wao wanafanya nini na wanashirikiana na nani.”—Thomas.

Kuna njia ambazo unaweza kujihusisha katika maisha ya kijana wako huku ukimruhusu awe na uhuru zaidi?

“Mara nyingi wazazi hawawi nyumbani pamoja na watoto wao. Au wanawaruhusu watoto wao kwenda sehemu mbalimbali pamoja na watu wengine.”—Nicholas.

Mfikirie rafiki wa karibu wa mtoto wako. Je, kweli unajua mambo wanayofanya wanapokuwa pamoja?

“Urafiki wa kimapenzi unaweza kuendelezwa kisiri iwapo wazazi ni wakali sana.”—Paul.

Bila kuvunja sheria na kanuni za Biblia, unaweza kufanya nini ili ‘usawaziko wako ujulikane’?—Wafilipi 4:5.

“Nilipokuwa tineja, nilihisi sifai na nilitamani kupendwa. Nilianza kumtumia kijana katika kutaniko jirani barua-pepe na nikaanza kumpenda. Alinifanya nihisi kuwa mtu wa pekee.” —Linda.

Unaweza kufikiria njia zinazofaa ambazo zingetumiwa kutosheleza mahitaji ya Linda nyumbani?

Unaweza kutumia Sura ya 2 katika Buku la 2 na pia sehemu hii ya Nyongeza kama msingi wa mazungumzo pamoja na mwana au binti yako. Njia bora ya kushughulikia mambo yanayofanywa kisiri ni kuwa na mazungumzo yaliyo wazi yanayotoka moyoni.—Methali 20:5.

ONA BUKU LA 2, SURA YA 1-3

 MAMBO YANAYOHUSU HISIA

Nifanye nini ikiwa mtoto wangu anataka kujiua?

Katika sehemu fulani za ulimwengu, vijana wengi sana hujiua. Kwa mfano, nchini Marekani, kujiua ndicho kisababishi cha tatu kikuu cha vifo kati ya vijana wenye umri wa miaka 15 hadi 25. Katika miaka 20 iliyopita, visa vya kujiua kati ya vijana wenye umri wa miaka 10 hadi 14 vimeongezeka mara mbili. Walio hatarini zaidi ni wale walio na matatizo ya akili, wale ambao watu wao wa ukoo wamejiua, na wale ambao wamewahi kujaribu kujiua. Ishara zinazoonyesha kwamba kijana anataka kujiua zinatia ndani zifuatazo:

● Kujitenga na familia na marafiki

● Kubadili mazoea ya kula na kulala

● Kuacha kupendezwa na mambo aliyopenda zamani

● Mabadiliko makubwa ya utu

● Matumizi mabaya ya dawa za kulevya au pombe

● Kupeana vitu anavyothamini sana

● Kuzungumzia sana kifo au kupendezwa kupita kiasi na mambo yanayohusiana na kifo

Mojawapo ya makosa makubwa ambayo wazazi wanaweza kufanya ni kupuuza ishara hizo. Kila mara kijana anapotishia kufanya jambo fulani, lichukue tishio hilo kwa uzito. Usikate kauli kwamba ni jambo la kupita tu.

Pia usiaibike kumtafutia mwana au binti yako msaada ikiwa ana tatizo kubwa la kushuka moyo au ugonjwa mwingine wa akili. Na ukishuku kwamba kijana wako anataka kujiua, muulize. Si kweli kwamba kuzungumza kuhusu kifo kutamchochea ajiue. Vijana wengi hujihisi huru kuzungumza wazazi wanapoanzisha mazungumzo. Hivyo, kijana wako akikubali kwamba amewahi kufikiria kujiua, jaribu kujua ikiwa tayari alikuwa amepanga, na ikiwa ndivyo, amefanya mipango gani. Kadiri mipango ilivyokamilika, ndivyo unavyohitaji kuchukua hatua haraka zaidi ili kumsaidia.

Usifikiri kwamba ikiwa ameshuka moyo, muda si muda atarudia hali yake. Na hata ikionekana kana kwamba anarudia hali yake, usifikiri kwamba ndio mwisho wa tatizo. Huenda huo ukawa wakati hatari zaidi. Kwa nini? Kwa sababu kijana ambaye ameshuka moyo sana huenda asiwe na nguvu za kufanya lolote. Hata hivyo, hisia za kushuka moyo zinapoanza kuondoka, huenda akapata nguvu za kuchukua hatua.

Inasikitisha sana kwamba kwa sababu ya kushuka moyo, vijana fulani hufikiria kujiua. Kwa kuwa macho kuona ishara na kuchukua hatua, wazazi na watu wengine wazima wanaojali wanaweza kusema “kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika” na kuwa kimbilio kwa vijana.—1 Wathesalonike 5:14.

ONA BUKU LA 1, SURA YA 13 NA 14, NA BUKU LA 2, SURA YA 26

Je, niwafiche watoto wangu huzuni yangu?

Ni jambo linaloumiza sana kumpoteza mwenzi wa ndoa. Huenda amekufa wakati ambapo kijana wako anahitaji msaada wako. Unaweza kumsaidia jinsi gani apambane na huzuni yake, na wakati uleule usipuuze hisia zako mwenyewe? Jaribu mambo yafuatayo:

Usifiche hisia zako. Mtoto wako amejifunza mambo mengi muhimu zaidi maishani kwa kukutazama. Anaweza pia kujifunza jinsi ya kupambana na huzuni kwa kukutazama. Kwa hiyo, usione kwamba unapaswa kuficha hisia zako kwa faida ya mtoto wako. Ukifanya hivyo unamfundisha mtoto wako kuficha hisia zake pia. Tofauti na hilo, unapoonyesha hisia zako, atajifunza kwamba ni afadhali kuonyesha hisia badala ya kuzificha na kwamba ni jambo la kawaida kuhuzunika, kukata tamaa, au hata kukasirika.

Mtie moyo kijana wako azungumze. Bila kumshinikiza mtoto wako, mtie moyo akueleze yaliyo moyoni. Ikiwa anasitasita, kwa nini msizungumzie Sura ya 16 katika buku hili? Pia, zungumza kuhusu pindi ulizofurahia pamoja na mwenzi wako aliyekufa. Mweleze jinsi itakavyokuwa vigumu kwako kuvumilia. Kijana wako anaposikia ukizungumza kuhusu hisia zako itakuwa rahisi kwake kufanya hivyo pia.

Tambua mipaka yako. Inaeleweka kwamba ungependa kumtegemeza mtoto wako katika pindi hii ngumu. Lakini kumbuka, umeathiriwa sana na kifo cha mwenzi wako mpendwa. Kwa hiyo, huenda hisia zako zimeathiriwa, na huenda nguvu zako za kiakili na za kimwili zimepungua kwa kadiri fulani. (Methali 24:10) Kwa hiyo, huenda ukahitaji msaada wa watu wengine wa familia na marafiki wakomavu. Kuomba msaada ni ishara ya ukomavu. Methali 11:2 inasema: “Wenye kiasi wana hekima.”

Msaada bora zaidi unaoweza kupata unatoka kwa Yehova Mungu, ambaye anawaahidi hivi waabudu wake: “Mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika mkono wako wa kuume, Mwenye kukuambia, ‘Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.’”—Isaya 41:13.

ONA BUKU LA 1, SURA YA 16

Ninaweza kumsaidia jinsi gani binti yangu awe na usawaziko kuhusu mazoea ya kula?

Unaweza kufanya nini ikiwa binti yako ana tatizo la kula? * Kwanza, jaribu kuelewa ni kwa nini ameamua kuwa na tabia hiyo.

Imeonekana kwamba wengi kati ya wale walio na matatizo ya kula, wanajidharau nao hutarajia ukamilifu, na hivyo huwa wanajiwekea viwango vya juu kupita kiasi. Hakikisha kwamba humfanyi binti yako awe na tabia hizo. Mjenge binti yako.—1 Wathesalonike 5:11.

Pia, chunguza mtazamo wako kuhusu chakula na uzito wa mwili. Je, yawezekana kwamba bila kujua umekazia mambo hayo kupita kiasi, iwe kwa maneno au kwa matendo yako? Kumbuka, vijana huhangaikia sana jinsi wanavyoonekana. Hata kufanya mzaha kuhusu “ubonge wa kitoto” au kawaida ya vijana wanaobalehe, kunaweza kumhangaisha sana kijana.

Baada ya kufikiria kwa makini na kusali kuhusu jambo hilo, zungumza na binti yako kwa upendo. Ili ufanye hivyo, jaribu yafuatayo:

● Fikiria kwa makini mambo utakayosema na wakati wa kuyasema.

● Mweleze waziwazi kinachokuhangaisha na kwamba unataka kumsaidia.

● Usishangae ikiwa ataanza kwa kujitetea.

● Sikiliza kwa subira.

Jambo muhimu zaidi ni kujitahidi kumsaidia binti yako ashinde tatizo lake. Husisha familia nzima katika jitihada za kumsaidia!

ONA BUKU LA 1, SURA YA 10, NA BUKU LA 2, SURA YA 7

  HALI YA KIROHO

Ninawezaje kuendelea kuwafundisha watoto wangu mambo ya kiroho wanapoendelea kukua?

Biblia inasema kwamba Timotheo alipewa mazoezi ya kiroho “tangu utoto mchanga.” Huenda wewe pia umewapa watoto wako mazoezi kama hayo. (2 Timotheo 3:15) Hata hivyo, watoto wako wanapobalehe, huenda ukahitaji kubadili njia unazotumia kuwafundisha. Watoto wako wanaanza kuelewa mambo magumu na yasiyo wazi, ambayo hawangeweza kuelewa walipokuwa wachanga. Sasa kuliko wakati mwingine wowote, utahitaji kuchochea ‘nguvu zao za kufikiri.’—Waroma 12:1.

Alipokuwa akimwandikia Timotheo, Paulo alitaja mambo ambayo Timotheo alikuwa ‘amejifunza na kushawishiwa kuamini.’ (2 Timotheo 3:14) Huenda sasa vijana wako wakahitaji ‘kushawishiwa kuamini’ kweli za Biblia ambazo wamejifunza tangu utotoni. Ili kufikia mioyo yao, unahitaji kufanya mengi zaidi kuliko kuwaambia tu wanayopaswa kufanya au kuamini. Wanahitaji kujifunza wenyewe. Unaweza kuwasaidia jinsi gani? Anza kwa kuwapa wakati wa kutosha kufikiria na kuzungumzia maswali kama haya:

● Ni nini kinachonisadikisha kwamba kuna Mungu?—Waroma 1:20.

● Ninaweza kujua jinsi gani kwamba mambo ninayofundishwa na wazazi wangu kutoka katika Biblia ni ya kweli?—Matendo 17:11.

● Ni nini kinachonisadikisha kwamba kufuata kanuni za Biblia ni kwa faida yangu? —Isaya 48:17, 18.

● Ni nini kinachonihakikishia kwamba unabii wa Biblia utatimia?—Yoshua 23:14.

● Ni nini kinachonisadikisha kwamba hakuna kitu katika ulimwengu huu kinacholingana na “thamani bora zaidi ya kumjua Kristo Yesu”?—Wafilipi 3:8.

● Dhabihu ya fidia ya Kristo inamaanisha nini kwangu?2 Wakorintho 5:14, 15; Wagalatia 2:20.

Huenda ukasita kuwauliza vijana wako maswali kama hayo, ukiona kwamba hawataweza kuyajibu. Lakini kufanya hivyo, ni kama kusita kuangalia iwapo tangi ya gari lako lina mafuta, ukiogopa kwamba huenda likawa tupu. Ni afadhali kuchunguza mapema ili ujue la kufanya! Vivyo hivyo, sasa—vijana wako wakiwa wangali nyumbani—ndio wakati wa kuwasaidia kuchunguza mambo yanayohusu imani ili ‘washawishiwe kuamini.’ *

Kumbuka, hakuna ubaya mwana au binti yako kuuliza, “Kwa nini ninaamini?” Diane, mwenye umri wa miaka 22 anakumbuka akiuliza swali hilo alipokuwa tineja. Anasema: “Nilitaka kuwa na uhakika kuhusu imani yangu. Kupata majibu thabiti yaliyo wazi kulinisaidia kutambua kwamba ninataka kuwa Shahidi wa Yehova! Nilipoulizwa ni kwa nini sifanyi jambo fulani, badala ya kusema, ‘Ni kinyume cha dini yangu,’ nilisema, ‘Mimi sioni ni sawa kufanya hivyo.’ Yaani, nilifanya maoni ya Biblia yawe maoni yangu.”

Pendekezo: Ili kuelewa nguvu za kufikiri za kijana wako kuhusiana na kanuni za Biblia, mwache aigize kama mzazi wakati tatizo linapotokea. Kwa mfano, tuseme binti yako ameomba ruhusu kwenda kwenye karamu fulani ambayo unajua (na labda hata yeye pia anajua) haifai. Badala ya kusema tu hapana, unaweza kusema: ‘Ningependa ujiweke katika hali yangu. Fikiria karamu hiyo, fanya utafiti (labda katika Sura ya 37 ya kitabu hiki na Sura ya 32 katika Buku la 2), kisha uje uzungumze nami kesho. Nitachukua sehemu yako na nitakuomba ruhusa kwenda kwenye karamu hiyo, na unapoigiza kama mzazi, utaniambia ikiwa ni sawa au si sawa.’

ONA BUKU LA 1, SURA YA 38, NA  , NA  , NA BUKU LA 2, SURA YA 34-36

Kijana wetu hapendezwi tena na mambo ya kiroho. Tufanye nini?

Kwanza, usikate kauli kwamba kijana wako ameikataa imani yako. Mara nyingi, huenda kukawa na sababu nyingine. Kwa mfano, huenda kijana wako

● Anashinikizwa na marafiki na anaogopa kuonwa kuwa tofauti kwa sababu ya kufuata kanuni za Biblia

● Anawaona vijana wengine (hata ndugu au dada zake) wakiwa na hali nzuri ya kiroho na anaona kwamba haiwezekani kuwa kama wao

● Anatamani kuwa na marafiki lakini anajihisi kuwa mpweke au hafai kati ya waamini wenzake

● Anawaona vijana wengine “Wakristo” wakiishi maisha ya unafiki

● Anajaribu kujielewa, na kwa hiyo, anaona kwamba lazima ajichunguzie mwenyewe kanuni unazopenda wewe

● Anaona wanafunzi wenzake wakijiingiza katika mambo mabaya lakini hawapatwi na mabaya

● Anataka kukubaliwa na mzazi ambaye si mwamini

Kumbuka kwamba, mambo kama haya hayahusiani na mafundisho ya imani yako. Kwa sasa, yanahusiana sana na hali zinazofanya iwe vigumu kujizoeza imani. Hivyo basi, unaweza kufanya nini ili kumtia moyo kijana wako?

Onyesha ufikirio pasipo kulegeza msimamo. Jaribu kuelewa ni kwa nini kijana wako amevunjika moyo, na ufanye mabadiliko fulani ili mtoto wako awe na mazingira mazuri ya kukua kiroho. (Methali 16:20) Kwa mfano, chati yenye kichwa “Kukabiliana na Mkazo” katika ukurasa wa 132 na 133 katika Buku la 2 inaweza kumpa mtoto wako ujasiri wa kusimama imara dhidi ya wanafunzi wenzake. Au ikiwa kijana wako ni mpweke, huenda ukahitaji kumsaidia sana kupata marafiki.

Tafuta mnasihi. Nyakati nyingine vijana wananufaika wanapotiwa moyo na mtu mzima asiye wa familia yao. Unamfahamu yeyote ambaye hali yake ya kiroho inaweza kumchochea kijana wako? Kwa nini usipange atumie wakati pamoja na mwana au binti yako? Kusudi si kupuuza daraka lako. Lakini mfikirie Timotheo. Alinufaika sana kutokana na mfano wa Paulo, naye Paulo akanufaika sana kwa kuandamana na Timotheo.—Wafilipi 2:20, 22.

Maadamu kijana wako anaishi na wewe, una haki ya kutazamia afuate ratiba yako ya kiroho. Hata hivyo, lengo lako ni kumsaidia kijana wako ampende Mungu kutoka moyoni, wala si kijuujuu tu. Ili kumsaidia kijana wako akubali dini ya kweli, mwekee mfano wa kuiga. Uwe na usawaziko kuhusu yale unayotazamia kutoka kwake. Mtafutie mtu anayeweza kumwiga na pia marafiki wenye kujenga. Huenda siku moja kijana wako ataweza kusema, kama alivyosema mtunga-zaburi, “Yehova ni mwamba wangu na ngome yangu na Mwokoaji wangu.”Zaburi 18:2.

ONA BUKU LA 1, SURA YA 39, NA  , NA BUKU LA 2, SURA YA 37 NA 38

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 23 Unapojitahidi kufanya hivyo, epuka kumfanya kijana wako ahisi kuwa na hatia ukidhani unamchochea kubadilika.

^ fu. 64 Huenda kijana wako anahangaikia sana sura yake na umbo lake, kwa hiyo, uwe mwangalifu usiseme jambo litakalofanya afikiri kwamba ana kasoro fulani.

^ fu. 168 Ili kurahisisha mambo, tunarejelea mtoto wa kike. Hata hivyo, kanuni zinazozungumziwa zinahusu watoto wa kiume pia.

^ fu. 188 Sura ya 36 katika Buku la 2 inaweza kuwasaidia vijana kutumia nguvu zao za kufikiri ili wawe na usadikisho kwamba kuna Mungu.