Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 29

Je, Karamu Zote Zinampendeza Mungu?

Je, Karamu Zote Zinampendeza Mungu?

Kwa nini Mungu alipendezwa na karamu hii?

JE, UNAPENDA kuhudhuria karamu?— Hizo zinaweza kufurahisha sana. Unafikiri Mwalimu Mkuu angependa tuhudhurie karamu?— Yeye alihudhuria karamu ya harusi fulani akiwa na baadhi ya wanafunzi wake. Yehova ni “Mungu mwenye furaha,” kwa hiyo yeye anafurahi tunapofurahia karamu nzuri.—1 Timotheo 1:11; Yohana 2:1-11.

Ukurasa wa 29 wa kitabu hiki unatuonyesha kwamba Yehova aliyagawanya maji ya Bahari Nyekundu na kuwaruhusu Waisraeli kupita. Je, unakumbuka ukisoma habari hiyo?— Baadaye, watu waliimba, wakacheza dansi na kumshukuru Yehova. Hiyo ilikuwa kama karamu. Watu walifurahi sana na tuna hakika Mungu alifurahia pia.—Kutoka 15:1, 20, 21.

Miaka 40 hivi baadaye, Waisraeli wakawa na karamu nyingine kubwa. Wakati huu wale waliowaalika hata hawakuwa waabudu wa Yehova. Watu hao waliowaalika hata waliabudu miungu mingine na kufanya ngono na watu ambao si waume wao wala wake zao. Unafikiri ilikuwa sawa kuhudhuria karamu kama hiyo?— Yehova hakufurahi, na basi akawaadhibu Waisraeli.—Hesabu 25:1-9; 1 Wakorintho 10:8.

Biblia inataja pia karamu mbili za kusherehekea siku ya kuzaliwa. Je, moja ya karamu hizo ilikuwa ya kusherehekea siku ya kuzaliwa kwa Mwalimu Mkuu?— La. Karamu hizo zilikuwa za watu ambao hawakumwabudu Yehova. Moja ilikuwa karamu ya siku ya kuzaliwa kwa Mfalme Herode Antipa. Alikuwa mtawala wa wilaya ya Galilaya wakati Yesu alipokuwa anaishi huko.

Mfalme Herode alifanya mambo mengi mabaya. Alimchukua mke wa ndugu yake awe wake. Mwanamke huyo anaitwa Herodia. Mtumishi wa Mungu, Yohana Mbatizaji, akamwambia Herode kwamba ni kosa kufanya hivyo. Herode hakufurahi kuambiwa hivyo. Kwa hiyo akaamuru Yohana afungwe gerezani.—Luka 3:19, 20.

Yohana akiwa bado gerezani, siku ilifika ya kusherehekea siku ya kuzaliwa kwake Herode. Herode akaandaa karamu kubwa. Akawaalika watu wengi mashuhuri. Wote wakala na kunywa na kufurahi. Kisha binti ya Herodia akaingia na kuwachezea dansi. Kila mtu alifurahia sana dansi yake hivi kwamba Mfalme Herode akaahidi kumpa zawadi ya pekee. Akamwambia: “Chochote utakachoniomba, nitakupa hicho, hata nusu ya ufalme wangu.”

Angeomba nini? Je, angeomba pesa? nguo maridadi-maridadi? au ufalme wake mwenyewe? Msichana huyo akashindwa kusema. Basi akamwendea mamaye, Herodia, na kumwuliza: “Niombe nini?”

Kumbuka kwamba Herodia anamchukia sana Yohana Mbatizaji. Basi akamwambia bintiye aombe kichwa cha Yohana. Msichana huyo akaenda kwa mfalme na kusema hivi: “Nataka unipe sasa hivi kwenye sahani kichwa cha Yohana Mbatizaji.”

Mfalme Herode hakutaka kumwua Yohana kwa sababu alijua Yohana ni mtu mzuri. Lakini Herode alikuwa ametoa ahadi, naye akaogopa namna watu waliokuwa wamehudhuria hiyo karamu wangemfikiria iwapo angebadili maoni yake. Basi akamtuma mtu gerezani aende akate kichwa cha Yohana. Baada ya muda mfupi mtu huyo akarudi akiwa amebeba kichwa cha Yohana katika sinia, akampa huyo msichana. Kisha msichana naye akampa mamaye.—Marko 6:17-29.

Ile karamu nyingine inayotajwa katika Biblia haikuwa nzuri pia. Ilikuwa karamu ya mfalme wa Misri. Wakati wa karamu hiyo pia, mfalme aliamuru mtu mwingine akatwe kichwa. Kisha baada ya hayo akamtundika juu ya mti ili aliwe na ndege! (Mwanzo 40:19-22) Unafikiri Mungu alizikubali karamu hizo mbili?— Je, ungalifurahia kuzihudhuria?—

Tunajua kwamba yote yaliyoandikwa katika Biblia yameandikwa kwa kusudi fulani. Biblia inataja karamu mbili tu za siku ya kuzaliwa. Na katika karamu hizo, mambo mabaya yalifanywa. Kwa hiyo, unafikiri Mungu anatuambia nini kuhusu karamu za siku ya kuzaliwa? Je, Mungu anataka tusherehekee siku ya kuzaliwa?—

Ni kweli kwamba siku hizi katika karamu hizo mtu hakatwi kichwa. Lakini kule kusherehekea siku za kuzaliwa kulianzishwa na watu ambao hawakumwabudu Mungu wa kweli. Kitabu kinachoitwa The Catholic Encyclopedia kinasema hivi kuhusu sherehe hizo zinazotajwa katika Biblia: “Wenye dhambi tu ndio wanaosherehekea siku walizozaliwa.” Je, tunataka kuwa kama wao?—

Ni nini kilichotendeka katika karamu ya siku ya kuzaliwa kwa Herode?

Vipi Mwalimu Mkuu? Je, yeye alisherehekea siku aliyozaliwa?— La, Biblia haisemi kama Yesu alisherehekea siku ya kuzaliwa. Kwa hakika, wafuasi wa Yesu wa mapema hawakusherehekea siku yake ya kuzaliwa. Unajua ni kwa nini baadaye watu waliamua kusherehekea Desemba 25 kama siku ya kuzaliwa kwa Yesu?—

Kulingana na kitabu kinachoitwa The World Book Encyclopedia, tarehe hiyo ilichaguliwa kwa sababu “watu wa Roma tayari waliiadhimisha kuwa Sikukuu ya Saturn, wakisherehekea siku ya kuzaliwa kwa jua.” Kwa hiyo watu wakachagua kusherehekea siku ya kuzaliwa kwa Yesu, tarehe ambayo tayari ilikuwa sikukuu ya wapagani!

Je, unajua ni kwa nini haiwezekani kwamba Yesu alizaliwa Desemba?— Kwa sababu Biblia inasema Yesu alizaliwa wakati ambapo wachungaji walikuwa nje usiku. (Luka 2:8-12) Nao hawangeweza kuwa nje mwezi wa Desemba kwa sababu ya baridi na mvua nyingi.

Kwa Nini haiwezekani kwamba Yesu alizaliwa Desemba 25?

Watu wengi wanajua kwamba Krismasi si siku ya kuzaliwa kwa Yesu. Hata wanajua kwamba siku hiyo wapagani walikuwa na sherehe ambayo haikumfurahisha Mungu. Hata hivyo watu wengi wanasherehekea Krismasi. Wanajishughulisha sana na karamu kuliko kufikiria maoni ya Mungu kuihusu. Lakini sisi tunataka kumfurahisha Yehova, sivyo?—

Kwa hiyo tunapokuwa na karamu, tuhakikishe kwamba ni nzuri na inakubaliwa na Yehova. Tunaweza kuwa na karamu wakati wowote mwakani. Hatuhitaji kungoja mpaka siku fulani ya pekee. Tunaweza kula chakula kizuri na kufurahia michezo. Je, ungependa kufanya hivyo?— Unaweza kuongea na wazazi wako ili wakusaidie kupanga karamu. Hilo litakuwa jambo zuri, sivyo?— Lakini kabla ya kupanga, hakikisha kwamba karamu hiyo itampendeza Mungu.

Tunawezaje kuhakikisha kwamba karamu zetu zinampendeza Mungu?

Umuhimu wa kufanya kila wakati mambo ambayo Mungu anakubali unaonyeshwa kwenye Mithali 12:2; Yohana 8:29; Waroma 12:2; na 1 Yohana 3:22.