Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI JUU YA MAISHA YA WATU

Yehova Alinibariki Sana Kupita Vile Niliwazia

Yehova Alinibariki Sana Kupita Vile Niliwazia

‘NILIPASWA kuwa painia.’ Lakini nilikuwa ninajiuliza hivi: ‘Nitafurahia kabisa kazi ya upainia?’ Nilikuwa ninafurahia kazi yangu katika Ujerumani, kazi hiyo ilikuwa ya kutuma vyakula katika sehemu fulani za Afrika, kama vile Dar es Salaam, Elisabethville (muji wenye kuitwa sasa Lubumbashi), na Asmara. Sikujua kabisa kama siku moja nitamutumikia Yehova katika utumishi wa wakati wote katika nafasi hizo na nafasi zingine za mingi katika Afrika!

Wakati nilifikia kushinda mashaka yangu na kuanza kazi ya upainia, maisha yangu ilibadilika katika njia yenye sikuwazia. (Efe. 3:20) Lakini unaweza kujiuliza ikiwa jambo hilo lilitokea namna gani. Acha nianzie ku mwanzo.

Nilizaliwa katika muji wa Berlin, Ujerumani, mwaka wa 1939, miezi kidogo tu kisha Vita ya Pili ya Ulimwengu kuanza. Wakati vita hiyo ilikaribia kuisha katika mwaka wa 1945, ndege za maaskari zilikuwa zinapita-pita juu ya muji wa Berlin na kumwanga sana mabombe. Wakati wa shambulizi moja, nyumba za mingi ku barabara yetu zilipigwa na mabombe, na mimi na familia yangu tulikimbilia mahali fulani ili kujificha ili mabombe isituangukie. Kisha wakati fulani, ili kupata ulinzi, tulikimbilia katika muji wa Erfurt, kwenye mama yangu alizaliwa.

Pamoja na wazazi wangu na dada yangu katika Ujerumani, mwaka wa 1950 hivi

Mama yangu alitafuta kweli kwa bidii. Alisoma vitabu vya wanafilozofia na alichunguza dini mbalimbali lakini hakutosheka. Katika mwaka 1948 hivi, Mashahidi wawili wa Yehova walitutembelea ku nyumba. Mama yangu aliwakaribisha mu nyumba na aliwauliza maulizo mbalimbali. Kisha dakika fulani, aliniambia mimi na dada yangu mudogo hivi: “Nimepata kweli!” Kisha tu pale, mama yangu, dada yangu, na mimi tulianza kuhuzuria mikutano katika muji wa Erfurt.

Katika mwaka wa 1950 tulirudia katika muji wa Berlin, na tukaingia mu Kutaniko la Berlin-Kreuzberg. Kisha kuhamia katika eneo lingine la muji wa Berlin, tuliingia mu Kutaniko la Berlin-Tempelhof. Kisha wakati fulani, Mama alibatizwa, lakini mimi niliendelea kusita. Juu ya nini?

NINASHINDA HALI YANGU YA HAYA NA KUSITA-SITA

Ilikuwa nguvu kwangu kufanya maendeleo kwa sababu nilikuwa mwenye haya. Hata kama nilikuwa ninaenda katika mahubiri, nilifanya miaka mbili bila kuzungumuza na mutu. Mambo ilibadilika wakati nilipitisha wakati pamoja na ndugu na dada fulani wenye walikuwa wameonyesha uhodari na ushikamanifu wao kwa Yehova. Wamoja kati yao walikuwa wamevumilia kufungwa mu kambi za mateso za Nazi ao mu gereza za Ujerumani Mashariki. Wengine walipeleka vichapo kwa siri katika Ujerumani Mashariki, hata kama wangekamatwa na kufungwa mu gereza. Mufano wao ulinigusa moyo sana. Niliwaza hivi: ikiwa wao walitia maisha yao katika hatari na walikuwa tayari kufungwa mu gereza kwa ajili ya Yehova na ndugu na dada zao, na mimi nilipaswa kujikaza ili kushinda haya yangu.

Nilianza kushinda haya yangu wakati nilishiriki katika kampanye ya pekee ya kuhubiri katika mwaka wa 1955. Katika barua moja, yenye ilitolewa katika Informateur, * Ndugu Nathan Knorr alitangaza kama kampanye hiyo ilikuwa moja kati ya kampanye kubwa zaidi zenye tengenezo lilikuwa limekwisha kupanga. Alisema kama wahubiri wote wangeshiriki katika kampanye hiyo, “tungepitisha mwezi muzuri sana katika kazi ya kutoa ushahidi katika dunia hii.” Ile ilikuwa kweli kabisa! Kisha wakati kidogo, nilijitoa kwa Yehova, na katika mwaka wa 1956, nilibatizwa pamoja na baba yangu na dada yangu. Lakini, bila kukawia, nilipaswa tena kukamata uamuzi mwingine wa maana.

Kwa miaka mingi, nilijua kama nilipaswa kuwa painia, lakini niliendelea kuchelewesha uamuzi wangu. Kwanza, niliamua kufanya mazoezi katika muji wa Berlin juu ya namna ya kuuza ao kutuma biashara katika inchi zingine. Kisha pale, nilipenda nitumike kwa wakati fulani ili kupata uzoefu zaidi katika kazi yangu mbele nianze upainia. Kwa hiyo, katika mwaka wa 1961, nilikubali kazi moja katika Hambourg, muji wenye kuwa na bandari (mahali kwenye mashua zinaegesha) kubwa zaidi katika inchi ya Ujerumani. Kwa sababu nilipenda sana kazi yangu, niliendelea kuchelewesha uamuzi wa kuanza kazi ya upainia. Ningefanya nini?

Niko mwenye shukrani sana kuona Yehova alitumia ndugu wenye upendo ili wanisaidie nitie kazi yake pa nafasi ya kwanza. Marafiki wangu fulani walikuwa wameanza kazi ya upainia na walinionyesha mufano muzuri. Pia, Ndugu Erich Mundt, mwenye aliokoka katika kambi fulani ya mateso, alinitia moyo nimutegemee Yehova. Alisema kama katika kambi ya mateso, ndugu wenye walijitegemea wenyewe walifikia kuwa wazaifu. Lakini, wale wenye walimutegemea Yehova kabisa waliendelea kuwa waaminifu na walifikia kuwa nguzo za tengenezo.

Wakati nilianza kazi ya upainia, mwaka wa 1963

Pia, Ndugu Martin Pötzinger, mwenye alifikia kutumikia katika Baraza Lenye Kuongoza, aliendelea kutia moyo ndugu na dada kwa kusema hivi: “Uhodari njo mali ya maana sana yenye munaweza kuwa nayo!” Kisha kufikiri sana juu ya ile maneno, mwishowe niliacha kazi yangu na nikaanza upainia katika Mwezi wa 6, 1963. Huo njo uamuzi muzuri zaidi wenye nilikuwa nimefanya! Kisha miezi mbili, mbele hata nianze kutafuta kazi ingine, nilipewa mugao wa kuwa painia wa pekee. Kisha miaka kidogo, Yehova alinibariki sana kupita vile niliwazia. Nilialikwa kusoma soma la 44 la Masomo ya Gileadi.

NINAJIFUNZA JAMBO LA MAANA KU GILEADI

Jambo moja kati ya mambo ya maana yenye nilijifunza, zaidi sana kutoka kwa ndugu Nathan Knorr na Lyman Swingle ni hili: “Usiache mbiombio mugawo wako.” Walitutia moyo tubakie katika mugao wetu hata kama ni mugao wa nguvu. Ndugu Knorr alisema hivi: “Mutakaza akili juu ya mambo gani? Uchafu, vidudu, umaskini? Ao mutaona miti, maua, na nyuso za watu zenye furaha? Mujifunze kupenda watu!” Siku moja, wakati Ndugu Swingle alifasiria juu ya nini wengi wanaachaka mbiombio migao yao, alishindwa kuzuia hisia zake mupaka akaangusha machozi. Alilazimika kusimamisha hotuba yake mupaka wakati alitulia. Hilo lilinigusa moyo sana na niliazimia kama sitamuhuzunisha hata kidogo Kristo ao ndugu zake waaminifu.​—Mt. 25:40.

Mimi, Claude, na Heinrich katika mugao wetu wa umisionere katika Lubumbashi, Congo, mwaka wa 1967

Wakati tulipewa migao yetu, Wanabeteli fulani waliuliza wamoja kati yetu ikiwa walitumwa kutumikia wapi. Walitoa maelezo ya muzuri juu ya kila mugao mupaka wakati nilisema: “Congo (Kinshasa).” Walikaa kimya na kusema tu: “Ee, Congo! Yehova akuwe pamoja na wewe!” Wakati huo, kulikuwa habari za mingi juu ya watu wenye kupigana na kuuana katika Congo (Kinshasa). Lakini, niliendelea kufikiria mambo yenye nilikuwa nimejifunza. Wakati kidogo kisha kumaliza masomo katika Mwezi wa 9, 1967, mimi, Heinrich Dehnbostel, na Claude Lindsay, tulisafiri ili kuenda Kinshasa, muji mukubwa wa inchi ya Congo.

MUGAO WENYE UNATUFUNDISHA MAMBO MINGI TUKIWA WAMISIONERE

Kisha kufika Kinshasa, tulijifunza Kifaransa kwa miezi tatu. Kisha, tukasafiri kwa ndege kuenda katika muji wa Lubumbashi, wenye uliitwa zamani Elisabethville, karibu na mupaka wa Zambia kusini mwa Congo. Tulihamia mu nyumba ya wamisionere katikati ya muji.

Kwa sababu sehemu za mingi za muji wa Lubumbashi zilikuwa hazijahubiriwa, tulifurahi kuwa watu wa kwanza wa kuhubiria kweli wakaaji wengi wa muji huo. Bila kukawia, tulipata wanafunzi wengi wa Biblia lakini hatungeweza kuwafundisha wote. Pia, tulihubiria watu wa serikali na polisi. Wengi waliheshimia Neno la Mungu na kazi yetu ya kuhubiri. Kwa kawaida, watu walikuwa wanazungumuza Kiswahili, kwa hiyo, mimi na Claude Lindsay tulijifunza luga hiyo. Kisha wakati kidogo, tulitumwa katika kutaniko la Kiswahili.

Hata kama tulikuwa na mambo mingi yenye kufurahisha, tulipata pia magumu mingi. Mara mingi tulikutana na maaskari wenye kulewa wenye kuwa na silaha ao polisi wakali, wenye walikuwa wanatushitaki mambo ya uongo. Wakati fulani, kikundi cha polisi wenye walikuwa na silaha waliingia kwa kushitukia katika mukutano wetu wa kutaniko ku nyumba ya wamisionere na wakatupeleka kwenye kituo cha polisi. Walituikalisha chini kwenye udongo mupaka saa kumi hivi mangaribi mbele watuachilie.

Katika mwaka wa 1969, nilipewa mugao wa kuwa mwangalizi wa muzunguko. Katika muzunguko huo, wakati fulani nilipaswa kutembea mwendo murefu sana katika matope na majani ya murefu, mambo ya kawaida katika Afrika. Katika kijiji kimoja, kuku na vitoto vyake walikuwa wanalala usiku chini ya kitanda changu. Sitasahau hata siku moja namna makelele yao ilikuwa inatuamusha na kungali giza. Ninaendelea kukumbuka mangaribi zenye mimi na ndugu fulani tulikuwa tunakaa pembeni ya moto na kuzungumuza juu ya kweli.

Tatizo moja kati ya matatizo makubwa yenye nilipambana nayo ni kushugulikia ndugu wa uongo, wenye walikuwa wanaunga mukono kikundi cha Kitawala. * Wamoja kati yao walifikia kubatizwa na hata walifikia kuwa wazee katika makutaniko. Wengi kati ya ‘miamba [hiyo] yenye kufichwa’ hawakudanganya ndugu na dada waaminifu. (Yud. 12) Mwishowe, Yehova alisafisha makutaniko na hilo lilileta ongezeko kubwa sana.

Katika mwaka wa 1971, nilipewa mugao wa kutumikia ku biro ya tawi ya Kinshasa, kwenye nilifanya kazi mbalimbali, kama vile kushugulikia barua mbalimbali, kufanya maombi ya vichapo, na kazi mbalimbali za Idara ya Utumishi. Ku Beteli, nilijifunza kupanga kazi katika inchi kubwa kwenye mambo mingi haiko muzuri, kama vile barabara, umeme, na namna za kusafiri. Wakati fulani, vitu vyenye tulikuwa tunatuma kwa njia ya ndege vilifanya miezi mingi ili kufika katika makutaniko. Vitu hivyo vilikuwa vinapakuliwa mu ndege na kupakizwa katika boti zenye kisha zilizama kwa majuma fulani katika maua ya mu maji yenye ilikuwa kama zulia (tapis). Lakini, kazi ilikuwa inafanyika hata kama kulikuwa ile magumu na magumu ingine.

Nilishangaa kuona namna ndugu walikuwa wanapanga mikusanyiko mikubwa hata kama hawakukuwa na feza za mingi. Walijenga majukwaa kutokana na vilima vya muchwa (termitières), walitumia nyasi fulani kuwa kuta na walikunja-kunja zingine ili kutengeneza viti. Walitumia mianzi ili kujenga nguzo za majengo na mikeka ya matete ili kutengeneza sehemu za juu za jengo ao meza. Na walikata-kata miti katika vipande vya kidogo-kidogo ili kuitumia kama misumari. Sikuzote, nilishangaa kuona mawazo yote ya muzuri yenye ndugu na dada hao walikuwa wanatumia ili kushinda magumu. Nilifikia kuwapenda sana. Nilisikia mubaya sana wakati nilipaswa kuwaacha ili kuenda katika mugao mupya!

NINATUMIKIA KATIKA INCHI YA KENYA

Katika mwaka wa 1974, nilitumwa ku biro ya tawi ya Nairobi, Kenya. Tulikuwa na mambo mingi ya kufanya, kwa sababu tawi la Kenya lilikuwa linasimamia kazi ya kuhubiri katika inchi kumi za karibu-karibu, na kazi yetu ilikuwa inakatazwa katika inchi fulani kati ya hizo. Nilitumwa mara kwa mara ili kutembelea inchi hizo, zaidi sana inchi ya Etiopia, kwenye ndugu zetu walikuwa wanateswa na walikuwa wanavumilia majaribu mingi. Wengi kati yao walitendewa mubaya sana ao kutiwa mu magereza; wengine hata waliuawa. Lakini walivumilia kwa uaminifu kwa sababu walikuwa na urafiki muzuri pamoja na Yehova na kati yao wenyewe.

Katika mwaka wa 1980, jambo la muzuri lilitokea katika maisha yangu; nilimuoa Gail Matheson, muzaliwa wa inchi ya Kanada. Nilikuwa katika somo moja la Gileadi pamoja na Gail. Tuliendelea kupashana habari kupitia barua. Gail alikuwa misionere katika inchi ya Bolivia. Kisha miaka 12, tulikutana tena katika New York. Kisha wakati kidogo, tulioana katika inchi ya Kenya. Niko mwenye shukrani sana kwa Gail kwa sababu sikuzote anaona mambo namna Yehova anaiona na anatosheka na vitu vyenye iko navyo. Anaendelea kuwa rafiki yangu wa maana sana mwenye kunitegemeza na mwenye upendo.

Katika mwaka wa 1986, mimi na Gail tulitumwa katika kazi ya wilaya, na wakati uleule nilitumikia katika Halmashauri ya Tawi. Kazi ya wilaya iliomba pia kutumikia katika inchi za mingi zenye zilisimamiwa na tawi la Kenya.

Ninatoa hotuba ku mukusanyiko katika Asmara, mwaka wa 1992

Ninakumbuka kwa furaha wakati nilifanya matayarisho kwa ajili ya mukusanyiko moja katika Asmara (katika Eritrea) mwaka wa 1992 wakati kazi yetu haikukuwa inakatazwa katika eneo hilo. Jambo la kuhuzunisha ni hili: Tulipata tu jengo moja la kuwekea vyakula lenye lilikuwa linaonekana mubaya sana ndani kuliko inje. Siku ya mukusanyiko, nilishangaa wakati niliona namna ndugu na dada walikuwa wametengeneza jengo hilo ndani na kuligeuza kuwa nafasi yenye kufaa ya kumuabudia Yehova. Familia za mingi zilileta vitambaa vya mapambo na kufunika kwa ufundi kila kitu chenye hakikuwa kinaonekana muzuri. Mukusanyiko huo ulikuwa wenye kufurahisha sana, kulikuwa watu 1 279.

Katika kazi ya kusafiri, tulipaswa kujipatanisha na mabadiliko makubwa, kwa sababu kila juma tulikuwa na makao tofauti. Wakati fulani, tulikaa mu nyumba ya muzuri sana pembeni ya bahari; wakati mwingine tulikaa mu nyumba ya manjanja tu katika kambi ya wafanyakazi; choo (WC) ilikuwa kwenye umbali wa metre zaidi ya 100. Lakini, hata kama tulitumikia wapi, mambo yenye tunakumbuka zaidi ni siku zenye tulihubiri sana pamoja na mapainia na wahubiri wenye bidii. Wakati tulipata mugao mwingine, tuliachana na marafiki wengi wapendwa sana wenye tuliendelea kukumbuka sana.

TUNAPATA BARAKA KATIKA INCHI YA ETIOPIA

Kuanzia mwaka wa 1987 mupaka 1992, kazi yetu ilikubaliwa tena kisheria katika inchi za mingi zenye zilisimamiwa na tawi la Kenya. Kwa hiyo, tawi na biro za inchi ziliwekwa katika inchi hizo. Katika mwaka wa 1993, tulipewa mugao wa kutumikia ku biro ya Addis Abeba, Etiopia, kwenye kazi yetu ilitambuliwa kisheria kisha kufanywa kwa siri kwa miaka mingi.

Wakati tulikuwa katika kazi ya wilaya katika eneo moja la mashamba la inchi ya Etiopia, mwaka wa 1996

Yehova amebariki kazi yetu katika Etiopia. Ndugu na dada wengi walianza kufanya kazi ya upainia. Zaidi ya wahubiri 20 juu ya 100 wamekuwa mapainia wa kawaida kila mwaka kuanzia mwaka wa 2012. Pia, masomo ya kiteokrasi imetolea ndugu na dada mazoezi yenye wako nayo lazima, na Majumba ya Ufalme zaidi ya 120 imejengwa. Katika mwaka wa 2004, familia ya Beteli imehamia mu jengo la mupya, na Jumba la Mikusanyiko katika kiwanja kilekile limekuwa pia baraka.

Kwa miaka mingi, mimi na Gail tumefanya urafiki wa sana na ndugu na dada wa Etiopia. Tunawapenda kabisa kwa sababu ya wema na upendo wao. Hivi karibuni, tumepata matatizo ya afya yenye iliomba tutumwe ku tawi la Ulaya ya Kati. Huku, ndugu na dada wanatuhangaikia kwa upendo, lakini tunakumbuka sana marafiki wetu wapendwa wa Etiopia.

YEHOVA AMEKOMALISHA KAZI YAKE

Tumejionea namna Yehova amefanya kazi yake ikomae. (1 Ko. 3:6, 9) Kwa mufano, wakati nilihubiria kwa mara ya kwanza Wanyarwanda wenye walikuwa wanachimbua shaba katika Congo, hakuna muhubiri mwenye alikuwa anatoa ripoti katika inchi ya Rwanda. Leo kuko ndugu na dada zaidi ya 30 000 katika inchi hiyo. Katika mwaka wa 1967, Congo (Kinshasa) ilikuwa na wahubiri karibu 6 000. Leo, kuko wahubiri 230 000 hivi, na watu zaidi ya milioni moja walihuzuria Ukumbusho katika mwaka wa 2018. Katika inchi zote zenye zilikuwa zinasimamiwa na tawi la Kenya, hesabu ya wahubiri imeongezeka kufikia zaidi ya 100 000.

Katika miaka zaidi ya 50 yenye imepita, Yehova alitumia ndugu mbalimbali ili kunisaidia nianze utumishi wa wakati wote. Hata kama ningali ninapiganisha hali yangu ya kuwa mwenye haya, nimejifunza kumutegemea Yehova kabisa. Mambo yenye nilijionea katika Afrika imenisaidia nikuwe na uvumilivu na nikuwe mwenye kutosheka. Mimi na Gail tunapendezwa na ndugu na dada wenye wanaonyesha ukaribishaji wa pekee, uvumilivu, na wenye kumutegemea Yehova. Niko mwenye shukrani sana kwa ajili ya fazili zake zenye hazistahiliwe. Kwa kweli, Yehova alinibariki sana kupita vile niliwazia.​—Zb. 37:4.

^ fu. 11 Ilifikia kuitwa Huduma Yetu ya Ufalme, na sasa imebadilishwa na Utumishi na Maisha ya Mukristo​—Buku la Mukutano.

^ fu. 23 Jina “Kitawala” linatoka katika neno la Kiswahili lenye kumaanisha “kutawala, ao kuongoza.” Kusudi la kikundi hicho lilikuwa la politike, ni kusema, kutosha watu chini ya utawala wa Ubelgiji (Belgique). Vikundi vya Kitawala vilipata, vilisoma, na kueneza vichapo vya Mashahidi wa Yehova. Watu hao walipotosha mafundisho ya Biblia ili iunge mukono mawazo yao ya politike, desturi zao za uchawi, na maisha yao ya mwenendo muchafu.