Ona video zinazopatikana

“Uko na Lazima ya Amri ya Biblia mu Kila Hali?”

“Uko na Lazima ya Amri ya Biblia mu Kila Hali?”

“Uko na Lazima ya Amri ya Biblia mu Kila Hali?”

WAKATI ulikuwaka mutoto, inawezekana wazazi wako walikuwaka nakutilia sheria za mingi. Wakati ulikomala, ulielewa kama walikuwa nafanya vile juu walikupenda na walitaka kukulinda. Sasa ulishakuwa mutu muzima, na pengine ungali nafuata kanuni fulani zenye walikufundishaka hata kama hauko tena chini ya mamlaka yao.

Yehova, Baba yetu wa mbinguni, anatupatia amri za mingi zenye kuonyesha waziwazi mambo yenye tunapaswa kufanya na mambo yenye tunapaswa kuepuka. Kwa mufano, anakataza kuabudu sanamu, kufanya uasherati, kufanya uzinifu, na kuiba. (Kutoka 20:1-17; Matendo 15:28, 29) Wakati ‘tunaendelea kukomaa katika mambo yote,’ ni kusema kukomaa kiroho, tunatambua kama Yehova anatupatia zile amri zote juu anatupenda na anataka kutulinda.​—Waefeso 4:15; Isaya 48:17, 18; 54:13.

Lakini, Biblia haituambie mambo yenye tunapaswa kufanya mu kila hali. Ile inafanya watu fulani wawaze kama wako huru kufanya mambo yote yenye wanapenda. Wanasema kama ikiwa Mungu angeona ni lazima, angetupatia amri yenye iko wazi, na yenye inaonyesha mambo ya kufanya.

Mara mingi, wale wenye wanawazaka vile wanakamataka maamuzi ya mubaya na kisha wanaanza kuhuzunika. Wanasahau kama mu Biblia hamuna tu sheria, lakini muko pia mambo yenye inatusaidia kujua mawazo ya Mungu. Wakati tunajifunza Biblia na kujua namna Yehova anaonaka mambo mbalimbali, tunakuwa na zamiri yenye kutumika muzuri na tunakuwa na uwezo wa kukamata maamuzi yenye inapatana na namna yake ya kuona mambo. Wakati tunafanya vile, tunafurahisha moyo wake na tunakamata maamuzi ya muzuri yenye inatuletea furaha.​—Waefeso 5:1.

Watu Wenye Walituachia Mufano Muzuri

Biblia inazungumuzia watumishi wa Mungu wa zamani, wenye walikamata maamuzi ya muzuri hata kama hawakukuwa na sheria yenye inaonyesha waziwazi mambo ya kufanya. Fikiria mufano wa Yosefu. Wakati bibi ya Potifa alijaribu kumuchochea afanye naye ngono, Yehova alikuwa hayatoa amri yenye kuonyesha kama ni mubaya kufanya uzinifu. Hata kama hakukukuwa amri yenye ilikataza uzinifu, Yosefu alielewa kama kufanya uzinifu ni ‘kumutendea Mungu zambi’ na pia kutendea zamiri yake zambi. (Mwanzo 39:9) Inawezekana Yosefu alijua kuwa Yehova aliambia Adamu na Eva kama bibi ao bwana anapaswa kushikamana na mwenzake.​—Mwanzo 2:24.

Fikiria mufano ingine. Matendo 16:3 inaonyesha kama, mbele Paulo amuruhusu Timoteo amusindikize mu safari zake za umisionere, alimutahiri. Mustari wa 4 unaonyesha kama kisha pale, Paulo na Timoteo walisafiri mu miji mbalimbali juu ya kutolea Wakristo “maagizo yenye yalikuwa yameamuliwa na mitume na wazee wenye walikuwa Yerusalemu.” Kati ya ile maagizo, kulikuwa uamuzi wenye ulionyesha kama haikukuwa tena lazima Wakristo watahiriwe! (Matendo 15:5, 6, 28, 29) Sasa, juu ya nini Paulo alimutahiri Timoteo? “Kwa sababu ya Wayahudi wenye walikuwa katika sehemu hizo, kwa maana wote walijua kwamba baba [ya Timoteo] alikuwa Mugiriki.” Paulo hakutaka kuwakwaza ao kuwakasirikisha. Alipenda Wakristo waendelee ‘kujipendekeza kwa kila zamiri ya mwanadamu mbele ya macho ya Mungu.’​—2 Wakorinto 4:2; 1 Wakorinto 9:19-23.

Ni vile Paulo na Timoteo walizoea kufanya. Wakati tunasoma Waroma 14:15, 20, 21 na 1 Wakorinto 8:9-13; 10:23-33, tunaona namna Paulo alihangaikia sana hali ya kiroho ya wengine. Alihangaikia zaidi sana zamiri ya wale wenye wangeweza kukwazika juu ya jambo fulani, hata kama ile jambo haikukuwa kosa. Na Paulo aliandika hivi kuhusu Timoteo: “Kwa maana sina mutu mwingine mwenye kuwa na muelekeo kama wake mwenye atajali kabisa mahangaiko yenu. Kwa maana wengine wote wanatafuta faida zao wenyewe, hapana faida za Yesu Kristo. Lakini ninyi munajua uhakikisho wenye alitoa juu yake mwenyewe, kwamba kama mutoto na baba yake alitumika pamoja na mimi ili kuendeleza habari njema.” (Wafilipi 2:20-22) Kwa kweli, wale Wakristo wawili walituachia mufano muzuri! Wakati hakukukuwa amri yenye kuonyesha waziwazi mambo ya kufanya, Paulo na Timoteo hawakufanya tu mambo yenye wanapenda. Lakini waliiga upendo wa Yehova na Yesu kwa kujiuliza ikiwa maamuzi yao itakuwa na matokeo gani juu ya wengine.

Tufikirie pia Yesu Kristo, mwenye alituachia mufano muzuri zaidi. Mu mahubiri yake ya ku mulima, alionyesha kama tunapaswa kufanya mambo mingi zaidi tu ya kutii sheria za Mungu. Tunapaswa kutafuta kujua juu ya nini Yehova anatupatia sheria fulani. Ile itatusaidia tukamate maamuzi ya muzuri kama tunajikuta mu hali yenye inafanana ile. (Matayo 5:21, 22, 27, 28) Yesu, Paulo, Timoteo, na Yosefu hawakuwaza kama mutu anapaswa kufanya mambo yenye anapenda juu tu hakuna amri yenye inaonyesha waziwazi mambo ya kufanya. Walijua kama amri mbili zenye kuwa kubwa zaidi ni kumupenda Mungu na kupenda wengine. Kwa hiyo, walikamata maamuzi yenye ilionyesha kama wanatii zile amri.​—Matayo 22:36-40.

Tuseme Nini Juu ya Wakristo Leo?

Hatupaswe kuona Biblia sawa vile kitabu ya sheria yenye inaonyesha waziwazi kila kitu yenye mutu anapaswa kufanya. Tunamufurahisha sana Yehova wakati tunaamua kufanya mambo yenye inapatana na namna yake ya kuona mambo, hata kama hakuna amri yenye inaonyesha waziwazi mambo ya kufanya. Kuliko kutafuta kila wakati amri yenye inaonyesha mambo yenye Mungu anapenda tufanye, tunapaswa kujikaza ‘kujua mapenzi ya Yehova’ ni nini. (Waefeso 5:17; Waroma 12:2) Juu ya nini kufanya vile kunamufurahisha Yehova? Juu ile inaonyesha kama hatutafute tu kufanya mambo yenye tunapenda, lakini nia yetu kubwa ni kumufurahisha Yehova. Tunaonyesha pia kama tuko wenye shukrani juu ya upendo wenye ametuonyesha na tunapenda kumuiga kwa kuonyesha wengine upendo. (Mezali 23:15; 27:11) Tena, wakati tunatumikisha kanuni za Biblia mu maisha yetu, tunakuwa na hali ya muzuri ya kiroho, na mara mingi ile inatusaidia tukuwe na afya ya muzuri.

Tuone sasa namna tunaweza kufanya vile mu mambo ya kipekee.

Mambo ya Kujifurahisha

Kwa mufano, tuseme kijana fulani mwanaume anapenda kuuza albumu fulani ya muziki. Amesikia kama mu ile albumu muko nyimbo zenye ziko na mudundo muzuri, lakini ku sehemu ya nyuma ya ile albumu inaonyeshwa kama miziki yenye iko mule, iko na maneno yenye kuzungumuzia ngono na maneno ya matusi. Tena, anajua kama mwenye aliimba zile nyimbo anazoeaka kutumia maneno makali na yenye kuchochea jeuri. Juu ule kijana anamupenda Yehova, anajiuliza ikiwa Yehova iko na mawazo gani juu ya ile jambo. Nini njo itamusaidia kujua mawazo ya Yehova?

Mu barua yenye Paulo aliandikia Wagalatia, anataya matendo ya mwili na tunda la roho ya Mungu. Kama vile unajua, sehemu za tunda la roho ya Mungu ni: upendo, furaha, amani, uvumilivu, fazili, wema, imani, upole, kujizuia. Lakini, matendo ya mwili ni gani? Paulo aliandika hivi: “Sasa matendo ya mwili yanaonekana wazi, nayo ni uasherati, uchafu, mwenendo mupotovu wa bila haya, ibada ya sanamu, kupashana habari na pepo wachafu, uadui, mizozo, wivu, milipuko ya kasirani, magomvi, migawanyiko, mazehebu, kutamani, ulevi, karamu za kupitisha mipaka, na mambo kama hayo. Ninawaonya mbele ya wakati juu ya mambo hayo, kama vile nimekwisha kuwaonya, kwamba wale wenye wanazoea kufanya mambo kama hayo hawatariti Ufalme wa Mungu.”​—Wagalatia 5:19-23.

Uliona maneno yenye alitia ku mwisho ya ile liste? Alisema: “Mambo kama hayo.” Paulo hakutaya liste ya mambo yote yenye inaweza kuonwa kuwa matendo ya mwili. Kwa hiyo, haiko jambo ya hekima kuwaza hivi: ‘Juu tendo fulani haiko kati ya matendo ya mwili yenye Paulo alitaya, ninaweza kuifanya.’ Lakini, tunapaswa kutumia uwezo wetu wa kufikiri juu ya kujua matendo yenye pengine haiko kati ya mambo yenye Paulo alitaya lakini iko kati ya mambo “kama hayo.” Kama mutu anafanya mambo “kama hayo,” ni kusema mambo yenye inafanana na mambo yenye Paulo alitaya na kisha hatubu, ule mutu hatariti ufalme wa Mungu.

Njo maana tunapaswa kujikaza kujua mambo yenye Yehova anachukia. Ni nguvu kufanya vile? Tuseme munganga anakuambia ukuwe nakula matunda mingi na mboga-mboga, lakini uepuke mandazi, biscuits na vitu vya kufanana vile. Ni nguvu kujua kama keke iko mu liste gani? Tufikirie tena tunda la roho ya Mungu na matendo ya mwili. Ile albumu ya muziki yenye tulishataya, iko mu liste gani? Ni wazi kama haichochee watu wakuwe na upendo, wema, kujizuia, ao wakuwe na sifa zingine za tunda la roho ya Mungu. Kwa hiyo, mutu hana lazima ya amri juu afikie kuona kama muziki ya vile haipatane na mawazo ya Mungu. Tunaweza kutumia zilezile kanuni wakati tunachagula vitabu vya kusoma, filme, vipindi vya televizyo, michezo ya video, site za Enternete, na mambo ingine ya kujifurahisha.

Namna Yetu ya Kuvala na Kujipamba

Mu Biblia muko pia kanuni zenye zinazungumuzia namna ya kuvala na namna ya kujipamba. Zile kanuni zinasaidiaka kila Mukristo avale na kujipamba mu njia yenye kufaa na yenye kupendeza. Wakati mutu mwenye anamupenda Yehova iko nachagula namna atavala na kujipamba, hatafutake tu kujipendeza. Lakini nia yake kubwa inakuwaka kumufurahisha Yehova, Baba yake wa mbinguni. Vile tuliona, kama Yehova hatoe amri yenye kuwa wazi kuhusu mambo ya kufanya, ile haimaanishe kama kila mutu anaweza kufanya vile anapenda. Kila fasi, watu wako na namna yao ya kuvala, na namna ya kuvala inabadilikaka kadiri wakati inapita. Lakini, Yehova anatoa kanuni za musingi zenye zinapaswa kuongoza watu wake, hata wanaishi wapi ao wanaishi mu kipindi gani.

Kwa mufano, 1 Timoteo 2:9, 10 inasema hivi: “Vilevile, wanamuke wajipambe kwa nguo zenye kufaa, kwa kiasi na akili ya muzuri, hapana kwa namna za kusuka nywele, kwa zahabu ao lulu, ao nguo za bei sana, lakini kwa njia yenye kufaa wanamuke wenye ­wanasema kama wanashikamana na Mungu, ni kusema, kupitia matendo ya muzuri.” Kwa hiyo, wanaume na wanamuke Wakristo wanapaswa kujiuliza hivi: Fasi kwenye ninaishi, watu wanaonaka kama mutu mwenye anasema kuwa “anashikamana na Mungu” anapaswa kuvala na kujipamba namna gani? Ni jambo ya maana sana Mukristo ajiulize ikiwa namna yake ya kuvala na kujipamba inaweza kufanya watu wakubali ujumbe wa Biblia ao hapana. (2 Wakorinto 6:3) Mukristo mwenye anapenda kuwekea wengine mufano muzuri, hapaswe kukazia tu kama iko na haki ya kuamua namna atavala na kujipamba. Lakini, anapaswa kuepuka kuvala na kujipamba mu njia yenye itakwaza wengine ao kuwakengeusha akili.​—Matayo 18:6; Wafilipi 1:10.

Kama Mukristo anaona kama namna yake ya kuvala na kujipamba iko nakwaza wengine, anapaswa kuiga mufano wa mutume Paulo, ni kusema hapaswe tu kujifikiria. Lakini anapaswa kufikiria mawazo ya wengine. Paulo alisema hivi: “Mukuwe waigaji wangu, kama vile mimi niko muigaji wa Kristo.” (1 Wakorinto 11:1) Na alisema hivi kuhusu Yesu: “Kwa maana hata Kristo hakujipendeza mwenyewe.” Paulo alipatia Wakristo wote hii maagizo yenye kuwa wazi: “Basi, sisi wenye tuko na nguvu tunapaswa kubeba uzaifu wa wale wenye hawana nguvu, na tusikuwe tunajipendeza wenyewe. Kila mumoja wetu amupendeze jirani yake kwa faida yake, ili kumujenga.”​—Waroma 15:1-3.

Tukomalishe Nguvu Zetu za Utambuzi

Namna gani tunaweza kukomalisha nguvu zetu za utambuzi, ili tujue namna ya kumufurahisha Yehova hata wakati hakuna amri yenye inaonyesha waziwazi mambo ya kufanya? Nguvu zetu za utambuzi zitakomala kama tunakuwa nasoma na kujifunza Biblia kila siku na kutafakari juu ya mambo yenye tuko nasoma. Inaomba wakati juu mutu akomalisha nguvu zake za utambuzi. Inaombaka wakati juu mutoto akamale. Vilevile, inaombaka wakati juu mutu akomale kiroho. Kwa hiyo, inaomba kuwa wavumilivu. Hatupaswe kuvunjika moyo kama tunaona kuwa nguvu zetu za utambuzi hazikomale mbiombio. Lakini haiko kusema kama nguvu zetu za utambuzi zitakomala juu tu wakati mingi inapita. Tunapaswa kutumia ile wakati juu ya kujifunza Biblia kwa bidii, na kufanya mambo yenye Yehova anapenda.​—Waebrania 5:14.

Wakati Yehova anatupatia sheria na kisha tunaitumikisha, tunaonyesha kama tunapenda kumutii. Lakini wakati tunakamata maamuzi ya muzuri, hata kama hakuna sheria yenye inaonyesha waziwazi mambo ya kufanya, tunaonyesha kama tunamupenda sana Yehova na tunataka kumufurahisha. Kadiri tutaendelea kukomaa kiroho, ni vile tutapenda sana kumuiga Yehova na mwana wake. Tutakuwa tayari kuchunguza kanuni za Biblia juu zitusaidie kukamata maamuzi yenye itamufurahisha Mungu. Na wakati tunamufurahisha Baba yetu wa mbinguni mu mambo yote yenye tunafanya, na siye tutakuwa na furaha zaidi.

[Picha]

Kila fasi, watu wako na namna yao ya kuvala, lakini kanuni za Biblia njo zinapaswa kutusaidia kuchagula manguo yenye tutavala