Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MASIMULIZI KUHUSU MAISHA YA WATU

Kumutegemea Yehova Kunaleta Baraka Nyingi

Kumutegemea Yehova Kunaleta Baraka Nyingi

Maisha ni magumu na mara nyingi hatujue yatakuwa namna gani wakati ujao. Lakini Yehova anawabariki wale wanaomutegemea, kuliko kutegemea akili yao wenyewe. Hayo ndiyo mambo ambayo mimi na bibi yangu tumejionea kwa muda wa maisha yetu marefu na yenye kujaa baraka. Acheni tueleze machache.

BABA na mama yangu walifahamiana katika 1919 kwenye mukusanyiko wa Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa huko Cedar Point, Ohio, Amerika. Walioana baadaye mwaka huohuo. Nilizaliwa katika 1922, na ndugu yangu, Paul, alizaliwa miaka miwili baadaye. Bibi yangu, Grace, alizaliwa katika 1930. Wazazi wake, Roy na Ruth Howell, walikomalia katika kweli, na tate ao kambo zake walikuwa Wanafunzi wa Biblia na marafiki wa Ndugu Charles Taze Russell.

Nilifahamiana na Grace katika 1947, na tulioana tarehe 16 Mwezi wa 7, 1949. Mbele ya kuoana, tulizungumuzia waziwazi miradi yetu. Tuliamua kufanya utumishi wa wakati wote na kutokuzaa watoto. Tarehe 1 Mwezi wa 10, 1950, tulianza kazi ya upainia pamoja. Kisha, katika 1952, tuliombwa kufanya kazi ya muzunguko.

KAZI YA MUZUNGUKO NA MASOMO YA GILEADI

Sisi wawili tulitambua kwamba tulihitaji musaada mwingi ili kutimiza mugawo wetu mupya. Nilijifunza kutokana na ndugu wenye uzoefu, na nilitafuta pia musaada kwa ajili ya Grace. Nilimuendea ndugu Marvin Holien, rafiki wa muda murefu wa familia yetu ambaye alikuwa na uzoefu katika kazi ya kusafiri, na nilimuuliza hivi: “Grace ni kijana na hana uzoefu. Je, unaweza kunionyesha mutu fulani anayeweza kutumika naye kwa muda muchache ili apate mazoezi fulani?” Alijibu hivi: “Ndiyo, painia mwenye uzoefu mwingi anayeweza kumusaidia sana ni dada Edna Winkle.” Baadaye, Grace alisema hivi kuhusu Edna: “Alinifanya nijisikie vizuri katika mahubiri ya nyumba kwa nyumba, alijua namna ya kushinda vizuri vizuia-mazungumuzo, na alinifundisha kusikiliza kwanza musikilizaji ili kujua yale ambayo ninapaswa kusema. Alikuwa musaada ambao nilihitaji kabisa!”

Kuanzia kushoto: Nathan Knorr, Malcolm Allen, Fred Rusk, Lyle Reusch, Andrew Wagner

Grace na mimi tulitumikia katika mizunguko miwili katika jimbo la Iowa, kutia ndani maeneo fulani ya majimbo ya Minnesota na Dakota Kusini. Kisha tulitumwa katika Muzunguko wa 1 wa New York, ambao ulitia ndani vijiji vilivyo pembeni ya miji ya Brooklyn na Queens. Hatutasahau hata kidogo namna tulivyojisikia kuwa wasio na uzoefu katika mugawo huo. Muzunguko ulitia ndani Kutaniko la Brooklyn Heights, ambalo lilifanya mikutano yake katika Jumba la Ufalme lililo kwenye Beteli na lililokuwa na Wanabeteli wengi wenye uzoefu. Kisha kutoa hotuba yangu ya kwanza ya utumishi katika kutaniko hilo, Ndugu Nathan Knorr alikuja mbele yangu na kuniambia hivi: “Malcolm, umetutolea mashauri fulani ambayo tunapaswa kutumia, na yalikuwa mashauri yenye kufaa. Usisahau jambo hili: Ikiwa hautusaidie kwa kututolea mashauri mazuri, hauko wa maana sana katika tengenezo hili. Usiache kufanya kazi hiyo nzuri.” Kisha mikutano, nilimuambia Grace maneno hayo. Baadaye tulienda katika chumba ambamo tulipangishwa kwenye Beteli. Na kwa sababu ya wasiwasi, tulilia.

“Ikiwa hautusaidie kwa kututolea mashauri mazuri, hauko wa maana sana katika tengenezo hili. Usiache kufanya kazi hiyo nzuri”

Kisha miezi michache, tulipokea barua ya kutualika kuhuzuria darasa la 24 la Masomo ya Gileadi, ambalo lingemalizika katika Mwezi wa 2, 1955. Tuliambiwa mbele ya kuenda kwenye masomo kwamba mazoezi yetu hayakuwa tu na kusudi la kututayarisha tuwe wamisionere. Lakini, yangetutolea pia mazoezi tunayohitaji ili kufanya vizuri zaidi kazi ya kusafiri. Kuhuzuria masomo hayo kulikuwa jambo zuri sana na lililotufundisha kuwa wanyenyekevu.

Juu: Fern na George Couch pamoja na Grace na mimi kwenye Masomo ya Gileadi, katika 1954

Tulipomaliza masomo, tulitumwa katika kazi ya wilaya. Wilaya yetu ilitia ndani majimbo ya Indiana, Michigan, na Ohio. Kisha, katika Mwezi wa 12, 1955, tulishangaa tulipopokea barua kutoka kwa Ndugu Knorr iliyosema hivi: “Museme waziwazi kabisa na muniambie mawazo yenu. Ikiwa munataka kuja kwenye Beteli na kubaki hapa . . . ao ikiwa munataka kuenda kutumikia katika inchi ya kigeni kisha kutumikia Beteli kwa muda kidogo, munijulishe. Ikiwa munapendelea kazi ya wilaya na ya muzunguko, nitafurahi kujua jambo hilo.” Tulijibu kwamba tungefurahi kutimiza mugawo wowote ambao tungepewa. Mara moja, tuliombwa tufike kwenye Beteli!

MIAKA YENYE KUFURAHISHA KWENYE BETELI

Nilipokuwa nikitumikia kwa furaha kwenye Beteli, migawo yangu ilitia ndani kutoa hotuba katika makutaniko, mikusanyiko ya Amerika yote. Nilishiriki katika kuzoeza na kusaidia vijana wengi ambao baadaye walipewa madaraka makubwa katika tengenezo la Yehova. Wakati huo, nilikuwa mwandishi wa Ndugu Knorr katika biro ambayo ilisimamia kazi ya kuhubiri ulimwenguni.

Chini: Nilipokuwa nikifanya kazi katika Biro ya Utumishi, katika 1956

Nilifurahia zaidi sana miaka ambayo nilipitisha katika Biro ya Utumishi. Huko nilitumika pamoja na T. J. (Bud) Sullivan. Alikuwa amesimamia biro hiyo kwa miaka mingi. Lakini, kulikuwa ndugu wengine walionifundisha mambo mengi. Fred Rusk, aliyepewa mugawo wa kunizoeza, alikuwa mumoja wao. Ninakumbuka kwa furaha wakati nilimuuliza hivi: “Fred, sababu gani unatia masahihisho mengi katika barua zangu?” Alicheka, lakini akasema maneno haya yaliyonifanya nifikiri: “Malcolm, unaposema jambo fulani kwa mudomo, unaweza kutumia maneno mengi, lakini unapoandika jambo fulani, zaidi sana jambo ambalo linatoka hapa, unapaswa kuandika vizuri na kwa usahihi kadiri inavyowezekana.” Kisha alisema hivi kwa upole: “Usiogope​—tayari unafanya maendeleo mazuri, na katika siku zinazokuja, mambo yatakuwa mazuri zaidi.”

Kwa miaka mingi ya utumishi wetu kwenye Beteli, Grace alipewa migawo mbalimbali, kutia ndani kusafisha na kutunza vyumba vya kulala. Alifurahia sana kazi hizo. Mupaka leo, wakati fulani tunapokutana na ndugu ambao walikuwa vijana kwenye Beteli miaka hiyo, wanamuambia Grace hivi kwa furaha: “Ulinifundisha kabisa namna ya kutandika kitanda, na ninaweza kukuambia kwamba mama yangu alifurahia jambo ambalo ulifanya.” Grace alifurahia pia kutumika katika Biro ya Magazeti, na Biro Inayoshugulikia Maulizo ya Wasomaji, na Biro ya Utengenezaji wa Kaseti. Kutumika katika migawo hiyo mbalimbali kulimusaidia kutambua kwamba jambo lolote tunalofanya ao mahali popote tunapotumikia katika tengenezo la Yehova ni pendeleo na baraka. Amekuwa na maoni hayo mupaka leo.

MABADILIKO AMBAYO TUMEFANYA

Katikati ya miaka ya 1970, tulianza kutambua kwamba wazazi wetu waliokuwa wakizeeka walihitaji musaada wetu. Kwa hiyo, tulipaswa kuchukua uamuzi muzito. Hatukuwa na nia ya kuacha Beteli na kuacha watumishi wa Yehova ambao tulikuwa tumependa sana. Lakini, nilitambua kwamba nilikuwa na daraka la kutunza wazazi wetu. Kwa hiyo, kisha muda fulani tuliacha Beteli, lakini tulikuwa na tumaini kwamba tungerudi huko wakati hali ingebadilika.

Ili tupate mahitaji ya kimwili, nilianza kutumika katika kompanyi ya bima ao asiranse. Kazi yangu ilikuwa kuwatembelea watu na kuwaonyesha namna wanavyoweza kulinda mali yao ikiwa musiba unatokea. Siwezi kusahau maneno ambayo mukubwa mumoja wa kompanyi hiyo aliniambia nilipokuwa nikipata mazoezi: “Kazi hii inaomba kuwatembelea watu mangaribi. Huo ndio wakati unaweza kuona watu. Hakuna jambo la maana zaidi kuliko kupatikana mangaribi, ukiwatembelea watu.” Nilimujibu hivi: “Najua unasema hivyo kwa sababu umefanya kazi hii kwa miaka mingi, na ninaheshimu maoni yako. Lakini nina pia madaraka mengine ya kiroho ambayo sijazarau hata kidogo, na sitaki kuanza kuyazarau sasa. Nitawatembelea watu mangaribi, lakini kila mangaribi ya Siku ya Pili na Siku ya Ine, ninapaswa kuhuzuria mikutano ya maana sana.” Yehova alinibariki kabisa kwa sababu sikukosa mikutano ili kufanya kazi ya kimwili.

Tulikuwa kwenye kitanda cha mama wakati alikufa katika nyumba moja ya matunzo katika Mwezi wa 7, 1987. Muganga mukubwa alikuja mbele ya Grace na kusema hivi: “Bibi ya Allen, rudi nyumbani na upumuzike. Kila mutu anajua namna ulivyokuwa hapa kila wakati ili kumutunza mama-mukwe wako. Tulia na usisumbuke sana.”

Katika Mwezi wa 12, 1987, tulijaza fomu ili kutumikia tena mahali ambapo tulipenda, ni kusema, kwenye Beteli. Lakini kisha tu siku chache, Grace alivumbuliwa na ugonjwa wa kansa ya utumbotumbo munene. Kisha upasuaji na kupona vizuri, aliambiwa kwamba hana tena ugonjwa huo. Lakini, wakati huohuo tulipokea barua kutoka kwenye Beteli iliyotuambia tuendelee kutumikia katika kutaniko letu. Kwa hiyo, tuliazimia kuendelea kufanya kazi yetu ya kuhubiri.

Baadaye, nilipata kazi huko Texas. Tuliona kwamba eneo hilo lenye joto litafaa kwetu, na imekuwa hivyo. Hapa Texas, tumezungukwa kwa miaka 25 hivi na ndugu na dada wanaotuhangaikia ambao wamekuwa marafiki wetu wa karibu.

MAMBO AMBAYO TUMEJIFUNZA

Grace amekwisha kusumbuliwa na ugonjwa wa kansa ya utumbotumbo munene na ugonjwa wa koo, na hivi karibuni kansa ya matiti ao maziba. Lakini hajanungunika hata kidogo kuhusu matatizo yake ao hajakosa kujitiisha kwangu na kunitegemeza. Mara nyingi watu wamemuuliza, “Mumefanya nini ili kuwa na familia nzuri na yenye furaha?” Grace anawatolea sababu hizi ine: “Sisi ni marafiki sana. Tunazungumuza kwa ukawaida kila siku. Tunapenda kupitisha wakati pamoja kila siku. Na hatujaenda kulala hata siku moja tukiwa tumekasirikiana.” Kwa kweli, tunakoseana wakati fulani, lakini tunasameheana na kusahau​—na hilo linatusaidia sana.

“Mutegemee Yehova kila siku na ukubali mambo ambayo anaruhusu yatokee”

Katika majaribu yote ambayo tumekutana nayo, kuna mambo mengi mazuri ambayo tumejifunza:

  1. Usitegemee hata kidogo akili yako mwenyewe.​—Met. 3:5, 6; Yer. 17:7.

  2. Kumutii Yehova na kutii sheria zake ni jambo la maana sana. Kila mutu anapaswa kuamua ikiwa atamutii Yehova ao hapana.​—Rom. 6:16; Ebr. 4:12.

  3. Tia kazi yake pa nafasi ya kwanza, wala si kutafuta vitu vya kimwili.​—Met. 28:20; Mhu. 7:1; Mt. 6:33, 34.

  4. Kazia uangalifu yale unayoweza kufanya, wala si yale ambayo hauwezi kufanya.​—Mt. 22:37; 2 Tim. 4:2.

  5.  

Mimi na Grace, kila mumoja wetu amemutumikia Yehova kwa miaka zaidi ya 75, na tangu tulioana tumemutumikia kwa miaka karibu 65. Kwa miaka hiyo yote tumefurahia maisha mazuri pamoja katika kazi ya Yehova. Tunapenda na tunasali ndugu na dada zetu wote wajionee pia namna kumutegemea Yehova kunavyoleta baraka nyingi.