Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Tumutumikie Yehova Kama Watumwa’

‘Tumutumikie Yehova Kama Watumwa’

‘Musicheze​-cheze katika shuguli yenu. Mumutumikie Yehova kama watumwa.’​—ROM. 12:11, NW-bi7 SW.

1. Watu wengi wana maoni gani juu ya utumwa, lakini andiko la Waroma 12:11 linatutia moyo kufanya nini?

 WATU wengi wanafikiri kwamba mutumwa ni mutu anayetendewa kinyama, anayeteswa, na kuonewa. Lakini, kuwa mutumwa wa Mungu ni tofauti sana. Neno la Mungu linaonyesha kwamba mutu anaweza kuchagua ikiwa atamutumikia Bwana wetu mwenye upendo, Yehova Mungu. Zaidi ya hilo, mutume Paulo alipowaambia Wakristo wa kwanza​-kwanza ‘wamutumikie Yehova kama watumwa,’ alikuwa akiwatia moyo wamutumikie Mungu kwa kupenda. (Rom. 12:11) Huo ni utumwa wa aina gani? Namna gani tunaweza kuepuka kuwa watumwa wa Shetani na ulimwengu wake? Na tutapata baraka gani ikiwa tunamutumikia Yehova kwa uaminifu kama watumwa?

‘NAMUPENDA BWANA WANGU KWELIKWELI’

2. (a) Ni jambo gani ambalo lingemufanya mutumwa Mwisraeli aendelee kumutumikia bwana wake? (b) Kutoboa sikio la mutumwa kulionyesha nini?

2 Sheria ambayo Mungu aliwatolea Waisraeli inatusaidia kujua ikiwa Yehova anataka tuwe watumwa wa aina gani. Mutumwa Mwebrania alipaswa kuachwa huru kisha kutumikia bwana wake miaka saba. (Kut. 21:2) Lakini, ikiwa mutumwa fulani alimupenda sana bwana wake na alitaka kuendelea kumutumikia, Yehova alionyesha jambo ambalo lilipaswa kufanywa. Bwana wake alipaswa kumuleta kwenye mulango ao nguzo ya mulango na kulitoboa sikio lake kwa shindano. (Kut. 21:5, 6) Sababu gani alipaswa kufanya hivyo? Katika luga ya Kiebrania, neno linalotumiwa ili kumaanisha utii linahusiana sana na kusikia na kusikiliza. Kwa hiyo, kwa kukubali sikio lake litobolewe, mutumwa huyo alionyesha kwamba alitaka aendelee kumutumikia bwana wake na kumutii. Jambo hili linatuonyesha maana ya kujitoa kwetu kwa Yehova. Tunapojitoa kwa Yehova tunaonyesha kwamba tuko tayari kumutii kwa sababu tunamupenda.

3. Ni nini inayotuchochea tujitoe kwa Mungu?

3 Mbele ya kubatizwa, tulikuwa tayari tumeamua kwamba tutamutumikia Yehova, tutakuwa watumwa wake. Tulijitoa kwa Yehova kwa sababu tulitaka kumutii na kufanya mapenzi yake. Hakuna mutu aliyetulazimisha tufanye hivyo. Bila shaka, hata watoto wanapaswa kwanza kujitoa kwa Yehova mbele ya kubatizwa, na hawafanye hivyo kwa sababu tu wanataka kuwafurahisha wazazi wao. Upendo ndio unaotuchochea tujitoe kwa Bwana wetu wa mbinguni, Yehova. Mutume Yohana aliandika hivi: ‘Kwa maana kumupenda Mungu kunamaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake.’​—1 Yoh. 5:3.

SISI NI WATUMWA LAKINI TUNA UHURU

4. Tunapaswa kufanya nini ili kuwa “watumwa wa uadilifu”?

4 Bila shaka, tunamushukuru sana Yehova kwa kutuwezesha kuwa watumwa wake! Imani yetu katika zabihu ya ukombozi ya Kristo inatukomboa kutoka katika utumwa wa zambi. Hata ikiwa hatujakamilika, tumeamua kujitiisha chini ya mamlaka ya Yehova na Yesu. Mutume Paulo alionyesha jambo hilo waziwazi alipoandika hivi: ‘Mujihesabu wenyewe kuwa wafu kwelikweli kuhusiana na zambi lakini walio hai kuhusiana na Mungu kwa njia ya Kristo Yesu.’ Kisha alitoa onyo hili: ‘Je, hamujui kwamba ikiwa munaendelea kujitoa wenyewe kwa yeyote kuwa watumwa ili kumutii yeye, ninyi ni watumwa wake kwa sababu munamutii yeye, ama watumwa wa zambi kwa kutazamia kifo ama wa utii kwa kutazamia uadilifu? Lakini ni shukrani kwa Mungu kwamba mulikuwa watumwa wa zambi lakini kutoka moyoni mukawa wenye kutii namna ile ya fundisho ambayo muliwekwa chini yake. Ndiyo, kwa kuwa muliwekwa huru kutoka katika zambi, mulikuja kuwa watumwa wa uadilifu.’ (Rom. 6:11, 16-18) Ona kwamba mutume Paulo alionyesha kwamba tunapaswa kutii “kutoka moyoni.” Kwa hiyo, tunapojitoa kwa Yehova, tunakuwa “watumwa wa uadilifu.”

5. Sisi wote tunapambana na jambo gani katika mwili wetu, na sababu gani?

5 Kwa upande mwingine, tunapaswa kupambana na mambo fulani ili kuendelea kuishi kulingana na ahadi yetu ya kumutumikia Mungu. Tunapambana na mambo mawili. Kwanza, tunapambana na jambo ambalo Paulo alipambana nalo. Aliandika hivi: ‘Kwa kweli naipenda sheria ya Mungu kulingana na mutu niliye kwa ndani, lakini mimi naona ndani ya viungo vyangu sheria nyingine ikipigana na sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya zambi iliyo ndani ya viungo vyangu.’ (Rom. 7:22, 23) Sisi pia tumeriti hali ya kutokukamilika. Kwa hiyo, kila siku tunapaswa kupambana na tamaa za mwili. Mutume Petro alitushauri hivi: “Iweni kama watu huru, lakini muwe na uhuru wenu, si kama kifuniko cha ubaya, bali kama watumwa wa Mungu.”​—1 Pet. 2:16.

6, 7. Namna gani Shetani anafanya ulimwengu huu uonekane kuwa wenye kuvutia?

6 Pili, tunapambana na ulimwengu huu unaoongozwa na mashetani. Shetani, anayetawala ulimwengu huu, anafanya yote anayoweza ili kuvunja ushikamanifu wetu kwa Yehova na Yesu. Anapenda kutufanya tuwe watumwa wake kwa kutuchochea tufuate uongozi wake mubaya. (Soma Waefeso 6:11, 12.) Njia moja ambayo Shetani anatumia ili kutunasa ni kufanya ulimwengu wake uonekane kuwa wenye kuvutia. Mutume Yohana alionya hivi: ‘Yeyote akiupenda ulimwengu, kumupenda Baba hakumo ndani yake; kwa sababu kila kitu kilicho katika ulimwengu​—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mutu kujionyesha mali yake maishani​—hakitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu.’​—1 Yoh. 2:15, 16.

7 Tamaa ya kuwa tajiri imeenea sana katika ulimwengu. Shetani anawafanya watu wafikiri kwamba furaha inatokana na kuwa na feza nyingi. Maduka makubwa​-makubwa yanapatikana mahali pengi. Matangazo ya biashara yanawafanya watu wafikiri kwamba jambo la maana zaidi maishani ni kuwa na vitu vingi na kujifurahisha. Kompanyi za usafirishaji zinatoa nafasi ya kusafirisha mutu ili aone mahali mbalimbali penye kupendeza na mara nyingi safari hizo zinafanywa pamoja na watu walio na maoni ya ulimwengu. Bila shaka, ulimwengu unatutia moyo tufanye maisha yetu kuwa mazuri zaidi, lakini mara nyingi ni kulingana na kanuni za ulimwengu.

8, 9. Kuna hatari gani mbele yetu, na sababu gani hiyo ni hatari kubwa sana?

8 Alipokuwa akizungumuzia Wakristo wa kwanza​-kwanza waliokuwa wameanza kufikiri kama watu wa ulimwengu, mutume Petro alionya hivi: ‘Wao wanayaona maisha ya anasa wakati wa muchana kuwa raha. Wao ni madoa na dosari, wakijitia mno katika kupendezwa kusikozuiwa katika mafundisho yao ya udanganyifu huku wakila karamu pamoja nanyi. Kwa maana wao wanasema maneno ya kujigamba yasiyo na faida, na kwa tamaa za mwili na tabia zenye upotovu wao wanashawishi wale wanaotoka tu kuponyoka kutoka kwa watu ambao wanajiendesha kwa njia ya makosa. Huku wakiwaahidia uhuru, wao wenyewe ni watumwa wa uharibifu. Kwa maana yeyote anayeshindwa na mwingine hufanywa mutumwa na huyu.’​—2 Pet. 2:13, 18, 19.

9 Kutosheleza “tamaa ya macho” hakumufanye mutu kuwa huru. Lakini, kutosheleza tamaa hiyo, kunamufanya mutu kuwa mutumwa wa mutawala asiyeonekana wa ulimwengu huu, Shetani Ibilisi. (1 Yoh. 5:19) Kufuatia vitu vya kimwili ni hatari kubwa sana iliyo mbele yetu leo kwa sababu si rahisi kutoka katika utumwa huo.

KAZI INAYOLETA FURAHA MAISHANI

10, 11. Ni nani ambao Shetani anawinda zaidi leo, na elimu ya ulimwengu inatokeza tatizo gani?

10 Kama alivyofanya katika shamba la Edeni, leo pia Shetani anavizia kwanza wale wasiokuwa na uzoefu. Anawawinda zaidi sana vijana. Shetani hafurahi wakati kijana, ao mutu yeyote, anaamua kumutumikia Yehova kama mutumwa. Adui huyo wa Mungu anataka watu wote ambao wamejitoa kwa Yehova wavunje ushikamanifu wao kwake.

11 Acheni tuzungumuzie tena mufano wa mutumwa aliyekubali sikio lake litobolewe. Mutumwa huyo alisikia maumivu kwa muda; lakini maumivu hayo hayakuendelea, na alama ilibaki kwenye sikio lake ambayo ilionyesha kwamba yeye ni mutumwa. Vivyo hivyo, kuchukua uamuzi ulio tofauti na ule wa marafiki wako kunaweza kuwa jambo ngumu, hata lenye kuumiza, kwa vijana. Shetani anawafanya watu wafikiri kwamba kufuatia kazi nzuri katika ulimwengu huu kunaleta furaha, lakini Wakristo wanapaswa kujua kwamba kutosheleza uhitaji wao wa kiroho ndilo jambo linaloweza kuwaletea furaha. Yesu alifundisha kwamba “wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mt. 5:3) Wakristo waliojitoa kwa Mungu wanaishi ili kufanya mapenzi ya Mungu, wala si mapenzi ya Shetani. Wanaifurahia sheria ya Yehova, na wanaitafakari muchana na usiku. (Soma Zaburi 1:1-3.) Hata hivyo, elimu nyingi ya ulimwengu leo haiachie mutumishi wa Yehova wakati wa kutosha ili atafakari na kufanya mambo mengine ya kiroho.

12. Vijana wanapaswa kuchukua uamuzi gani leo?

12 Mukubwa wa kazi anaweza kumutesa Mukristo. Katika barua yake ya kwanza kwa Wakorintho, Paulo aliuliza hivi: ‘Je, uliitwa ukiwa mutumwa?’ Kisha aliwashauri hivi: ‘Usiache hilo likutie wasiwasi; lakini ikiwa unaweza pia kuwa huru, afazali utwae nafasi hiyo.’ (1 Kor. 7:21) Ikiwa mutu alikuwa na bwana anayemutesa, alipaswa kutamani kuwa huru kuliko kuwa mutumwa. Leo, sheria ya inchi nyingi inawaomba vijana wasome mupaka miaka fulani. Kisha miaka hiyo, wanafunzi wanapewa nafasi ya kuamua ikiwa watasoma masomo ya juu ao hapana. Mukristo anaweza kushindwa kufuatia utumishi wa wakati wote ikiwa anaamua kufuatia masomo ya juu ili apate kazi nzuri katika ulimwengu huu.​—Soma 1 Wakorintho 7:23.

Utamutumikia bwana gani?

ELIMU ILIYO NZURI ZAIDI

13. Ni elimu gani ambayo itamuletea mutumishi wa Yehova faida kubwa zaidi?

13 Mutume Paulo aliwaonya Wakristo wa Kolosai hivi: ‘Mujihazari: labda kuna mutu ambaye atawachukua ninyi kama windo lake kupitia falsafa na udanganyifu mutupu kulingana na pokeo la wanadamu, kulingana na mambo ya musingi ya ulimwengu na si kulingana na Kristo.’ (Kol. 2:8) Waalimu wengi leo wanafundisha ‘falsafa na udanganyifu mutupu kulingana na pokeo la wanadamu.’ Masomo ya juu, ambayo inakazia tu mambo hayo, haiwatolee wanafunzi uwezo wa kutosha unaoweza kuwasaidia kupambana na matatizo ya maisha. Lakini, watumishi wa Yehova wanachagua elimu itakayowasaidia waishi maisha mepesi ili wamutumikie Mungu. Wanachukua kwa uzito shauri hili ambalo Paulo alimutolea Timotheo: ‘Kwa hakika, huo ni njia ya kupata faida kubwa, huu ujitoaji​-kimungu pamoja na ujitoshelevu. Kwa hiyo, tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, tutarizika na vitu hivyo.’ (1 Tim. 6:6, 8) Kuliko tu kutafuta kupata vyeti vya masomo ya juu na kufanya majina yao yajulikane, Wakristo wa kweli wanafikiria zaidi kupata “barua za pendekezo,” ni kusema, watu ambao Wakristo wanasaidia ili wawe wanafunzi wa Kristo. Wakristo wanafanya hivyo wanaposhiriki kwa nguvu yao yote katika kazi ya kuhubiri.​—Soma 2 Wakorintho 3:1-3.

14. Kulingana na andiko la Wafilipi 3:8, mutume Paulo aliona namna gani pendeleo lake la kutumikia Mungu na Kristo kama mutumwa?

14 Fikiria mutume Paulo. Alifundishwa na Gamalieli, mwalimu wa Sheria ya Kiyahudi. Elimu ambayo Paulo alipata inaweza kulinganishwa leo na elimu ya masomo ya juu. Lakini, Paulo aliona elimu hiyo namna gani alipoilinganisha na pendeleo lake la kutumikia Mungu na Kristo kama mutumwa? Aliandika hivi: ‘Naviona vitu vyote kuwa hasara kwa sababu ya samani bora zaidi ya kumujua Kristo Yesu Bwana wangu.’ Kisha aliongezea hivi: ‘Kwa sababu yake nimekubali hasara ya vitu vyote nami naviona kuwa takataka nyingi, ili niweze kumupata Kristo.’ (Flp. 3:8) Maneno hayo yanawasaidia vijana Wakristo na wazazi wanaomuogopa Mungu kuchukua uamuzi wenye hekima kuhusu elimu. (Ona picha.)

FAIDIKA NA ELIMU ILIYO NZURI ZAIDI

15, 16. Ni elimu gani ambayo Yehova anatutolea kupitia tengenezo lake, na kusudi la elimu hiyo ni nini?

15 Hali iko namna gani katika masomo mengi ya juu? Mara nyingi waalimu na wanafunzi wa masomo hayo wanapenda kuasi na kuipinga serikali. (Efe. 2:2) Lakini, tengenezo la Yehova linatutolea elimu iliyo nzuri zaidi na katika hali ya utulivu katika kutaniko la Kikristo. Kila mumoja wetu anaweza kufaidika kila juma na Masomo ya Huduma ya Kiteokrasi. Pia, kuna masomo ya pekee kwa ajili ya ndugu mapainia ambao hawajaoa (Masomo ya Biblia kwa Ajili ya Ndugu Wasio na Bibi) na kwa ajili ya bibi na bwana ambao ni mapainia (Masomo ya Biblia kwa Ajili ya Ndugu na Bibi Zao). Elimu hiyo ya kiteokrasi inatusaidia tumutii Bwana wetu wa mbinguni, Yehova.

16 Tunaweza kujifunza mambo mengi katika Index des Publications Watch Tower na CD ya Watchtower Library. Kusudi kubwa la elimu yote hiyo ni kumwabudu Yehova. Inatufundisha namna tunavyoweza kuwasaidia wengine wawe marafiki wa Mungu. (2 Kor. 5:20) Kisha, wale ambao tunafundisha, wataweza kuwasaidia wengine.​—2 Tim. 2:2.

BARAKA AMBAZO MUTUMWA WA YEHOVA ATAPATA

17. Kuchagua elimu iliyo nzuri zaidi kunaleta faida gani?

17 Katika mufano wa Yesu wa talanta, watumwa wawili waaminifu walipongezwa. Na bwana wao aliwaingiza katika shangwe yake kwa kuwatolea madaraka mengine. (Soma Mathayo 25:21, 23.) Kuchagua elimu iliyo nzuri zaidi kunaleta furaha na baraka sasa. Fikiria mufano wa Michael. Kwa kuwa alifanya maendeleo mazuri kwenye masomo, waalimu wake walimualika ili kumutia moyo asome masomo ya juu. Lakini, walishangaa wakati Michael alichagua kujifunza kwa muda mufupi ufundi fulani ambao ungemuwezesha kuwa painia. Je, anasikitikia uamuzi wake? Anasema hivi: “Elimu ya kiteokrasi ambayo nimepata nikiwa painia—na sasa nikiwa muzee wa kutaniko​—imeniletea faida. Baraka na mapendeleo ambayo ninafurahia sasa yanashinda sana feza ambazo ningepata. Ninafurahi kabisa kwa kuwa sikuamua kusoma masomo ya juu.”

18. Ni jambo gani linalokuchochea uchague elimu iliyo nzuri zaidi?

18 Elimu iliyo nzuri zaidi inatufundisha mapenzi ya Mungu na inatusaidia tumutumikie Yehova kama watumwa. Elimu hiyo inatutolea tumaini la ‘kuwekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.’ (Rom. 8:21) Zaidi ya yote, inatufundisha namna tunavyoweza kuonyesha vizuri zaidi kwamba tunamupenda Bwana wetu wa mbinguni, Yehova.​—Kut. 21:5.