Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Uumbaji Unamufunua Mungu Aliye Hai

Uumbaji Unamufunua Mungu Aliye Hai

‘Unastahili, Ee Yehova, Mungu wetu, kupokea utukufu . . . kwa sababu uliumba vitu vyote.’​—UFU. 4:11.

1. Tunaweza kufanya nini ili imani yetu iendelee kuwa nguvu?

 WATU wengi wanasema kwamba wanaamini tu mambo wanayoweza kuona kwa macho yao. Namna gani tunaweza kusaidia watu kama hao wamuamini Yehova? Bila shaka, Biblia inasema kwamba ‘hakuna mwanadamu ambaye amemuona Mungu wakati wowote.’ (Yoh. 1:18) Kwa hiyo basi, tunaweza kufanya nini ili imani yetu katika Yehova, “Mungu asiyeonekana,” iendelee kuwa nguvu? (Kol. 1:15) Jambo la kwanza ni kutambua mafundisho yanayozuia watu kujua ukweli juu ya Yehova. Kisha, tunapaswa kutumia Biblia kwa ufundi ili kupindua mawazo ‘ambayo yameinuliwa kinyume na ujuzi wa Mungu.’​—2 Kor. 10:4, 5.

2, 3. Ni mafundisho gani mawili yanayowazuia watu wasijue ukweli juu ya Mungu?

2 Fundisho moja la uongo ambalo limeenea sana na ambalo linawazuia watu wengi wasijue ukweli juu ya Mungu ni lile fundisho la mageuzi. Fundisho hilo halipatane na Biblia na linawafanya watu wasiwe na tumaini. Kwa kuwa fundisho la mageuzi linaonyesha kwamba vitu vyote vinavyoishi vilijitokeza vyenyewe, hilo linafanya maisha ya wanadamu yasiwe na maana yoyote.

3 Kwa upande mwengine, wale wanaoshikilia sana imani ya dini wanafundisha kwamba ulimwengu, kutia ndani dunia na vitu vyote vinavyoishi juu yake, vimekuwako kumepita tu miaka michache. Pengine wale wanaofundisha fundisho hilo la uongo kuhusu uumbaji wanaheshimu sana Biblia, lakini wanafikiri kwamba Mungu aliumba vitu vyote kwa muda wa siku sita na kila siku ilikuwa na urefu wa saa 24. Pia, wanakataa ushuhuda unaoweza kuaminika ambao sayansi inatoa na unaopinga mawazo yao. Kwa hiyo, mawazo hayo ya uongo kuhusu uumbaji yanazaraulisha Biblia, na yanafanya ionekane kwamba haieleweke na ni yenye makosa. Watu wanaofundisha mawazo hayo wanatukumbusha watu fulani wa wakati wa mitume waliokuwa na bidii kwa ajili ya Mungu “lakini si kulingana na ujuzi sahihi.” (Rom. 10:2) Namna gani basi tunaweza kutumia Neno la Mungu ili kupindua “ngome zenye nguvu,” ni kusema, fundisho la mageuzi na fundisho la uongo juu ya uumbaji? * Tunaweza kufanya hivyo ikiwa tu sisi wenyewe tunajikaza kupata ujuzi wa kweli kuhusu yale ambayo Biblia inafundisha.

IMANI INAPASWA KUTEGEMEA MAMBO YALIYO HAKIKA NA YA KWELI

4. Imani yetu inapaswa kutegemea nini?

4 Biblia inatutia moyo tupendezwe sana na ujuzi. (Met. 10:14) Yehova anapenda imani yetu itegemee mambo yaliyo hakika na ya kweli, wala si filozofia za wanadamu ao desturi za kidini. (Soma Waebrania 11:1.) Ili kuwa na imani yenye nguvu katika Mungu, tunapaswa kwanza kuwa hakika kwamba Yehova iko. (Soma Waebrania 11:6.) Kuchunguza mambo yaliyo hakika na ya kweli na kutumia “nguvu zetu za kufikiri” ndio mambo yanayoweza kutusaidia tuwe na imani hiyo, wala si kufuata mawazo yetu tu.​—Rom. 12:1.

5. Ni sababu gani moja inayoweza kutusadikisha kwamba Mungu iko?

5 Mutume Paulo anatutolea sababu moja inayoweza kutusadikisha kwamba Mungu iko, hata ikiwa hatuwezi kumuona. Yeye aliandika hivi kumuhusu Yehova: ‘Sifa zake ambazo hazionekane, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa, yaani, nguvu zake za milele na Uungu.’ (Rom. 1:20) Namna gani unaweza kumusaidia mutu fulani anayetilia shaka kwamba Mungu iko ili aone ukweli wa maneno ya Paulo yaliyoongozwa na roho ya Mungu? Unaweza kuchunguza mambo yanayofuata ya uumbaji yanayofunua kwamba Muumbaji wetu ni mwenye nguvu na hekima.

UUMBAJI UNAFUNUA NGUVU ZA MUNGU

6, 7. Ngao mbili zinazotulinda zinaonyesha namna gani nguvu za Yehova?

6 Nguvu za Yehova zinaonekana katika ngao mbili zinazotulinda​—angahewa na nguvu za sumaku za dunia. Kwa mufano, angahewa ao hewa inayozunguka dunia, inatufanyia mambo mengi kuliko kututolea tu hewa ya kupumua. Inatulinda pia tusiumizwe na vitu hatari vinavyoanguka kutoka angani. Mawe makubwa yanayoweza kutuumiza yanaungua yanapoingia katika angahewa la dunia na kutokeza miangaza yenye kupendeza katika anga la usiku.

7 Nguvu za sumaku za dunia zinatulinda pia na hatari. Ngao hiyo inaanzia katika sehemu ya ndani sana ya dunia. Ndani katikati ya dunia kuna kitu ambacho sehemu yake ya inje imefanyizwa kwa sehemu kubwa na chuma chenye kuyeyuka. Kitu hicho kinatokeza nguvu kubwa ya sumaku inayotuzunguka na inayofika hata katika anga la mbali. Nguvu za sumaku hiyo zinatulinda tusiumizwe na miale hatari na milipuko inayotoka kwenye jua. Ikiwa nguvu za sumaku hazingekuwa, nguvu nyingi za jua zingeteketeza kila kitu kinachoishi duniani. Lakini, nguvu za sumaku zinameza nguvu za jua na kuzielekeza mahali pengine. Tunaona kwamba nguvu za sumaku ni zenye kufanya kazi tunapoona miangaza yenye kupendeza ya rangi mbalimbali inayoonekana angani karibu na Sehemu ya Mwisho ya Kaskazini na Sehemu ya Mwisho ya Kusini ya dunia. Bila shaka, Yehova iko “hodari katika nguvu.”​—Soma Isaya 40:26.

UUMBAJI UNAFUNUA HEKIMA YA MUNGU

8, 9. Mizunguko inayosaidia vitu viendelee kuishi inaonyesha namna gani hekima ya Yehova?

8 Hekima ya Yehova inaonekana katika mizunguko ao mifumo inayofanya vitu viendelee kuishi duniani. Tuchukue mufano: Wazia kwamba unaishi katika muji wenye kujaa watu na wenye kuzungukwa na ukuta na wakaaji wa muji huo hawana namna ya kupata maji safi kutoka mahali pengine na hawana nafasi pa kutupa uchafu. Kisha tu muda muchache, muji huo unaweza kuwa muchafu sana na watu hawawezi kuendelea kuishi ndani yake. Dunia yetu inafanana na muji huo kwa njia fulani. Dunia yetu ina kiasi fulani cha maji safi, na ni vigumu sana kwetu kutupa uchafu inje ya dunia. Lakini, kizazi baada ya kizazi, mabilioni ya viumbe vinaendelea kuishi katika dunia yetu iliyo kama “muji wenye ukuta.” Sababu gani? Kwa sababu dunia ina uwezo wa ajabu wa kubadili vitu vinavyotusaidia kuendelea kuishi.

9 Fikiria muzunguko wa oksijeni. Mabilioni ya viumbe vinachukua oksijeni ao hewa safi na kutoa kaboni dioksidi ao hewa chafu. Hata hivyo, hakuna siku ambayo oksijeni imekosekana duniani, na angahewa haiyajaa hata siku moja na hewa “chafu,” ao kaboni dioksidi. Sababu gani? Kwa sababu ya mufumo wa ajabu unaoitwa usanidimwanga (photosynthèse). Katika mufumo huo, mimea inakamata kaboni dioksidi, maji, na kuitumia pamoja na mwangaza wa jua na vitu vingine ili kufanyiza oksijeni na vitu vilivyo katika chakula vinavyopatia mwili nguvu vinavyoitwa kabohidrati. Tunakamilisha muzunguko huo tunapochukua oksijeni. Katika njia hiyo, Yehova anatumia mimea ambayo ameumba ili kuwapa ‘watu wote uhai na pumuzi.’ (Mdo. 17:25) Bila shaka, Yehova ana hekima nyingi kabisa!

10, 11. Namna gani kipepeo​-mufalme na kerengende vinaonyesha hekima ya Yehova?

10 Hekima ya Yehova inaonekana pia katika viumbe vingi vinavyoishi kwenye dunia yetu ya ajabu. Inakadiriwa kwamba kuna aina kati ya milioni 2 na milioni 100 ya viumbe duniani. (Soma Zaburi 104:24.) Tuzungumuzie viumbe fulani vinavyoonyesha hekima ya Mungu.

Jicho la kidudu hiki kinachoitwa kerengende linaonyesha hekima ya Mungu; picha imeongezwa ukubwa (Ona fungu la 11)

11 Kipepeo​-mufalme kina ubongo ulio na ukubwa wa chongo ya kalamu. Hata hivyo, kipepeo hicho kinaweza kusafiri kilometre karibu 3 000 kutoka Kanada mupaka musitu fulani huko Meksiko kwa kufuata jua. Ni nini inayosaidia kipepeo hicho kisipotee wakati jua halionekane? Yehova alipatia ubongo wake mudogo uwezo wa kuendelea na safari yake bila kupotea hata kama jua halionekane. Fikiria pia macho ya kidudu kinachoitwa kerengende. Kiumbe hicho kinaona kupitia macho mawili makubwa. Kila jicho la kidudu hicho lina lenzi 30 000. Lenzi ni sehemu ya jicho iliyo kama kioo inayosaidia kuona vizuri. Ubongo wa kerengende ni mudogo sana, hata hivyo, una uwezo wa kuunganisha picha ndogondogo zinazoletwa na lenzi zake na kumuwezesha atambue kitu chochote kinachotembea karibu naye.

12, 13. Ni jambo gani linalokushangaza kuhusu namna ambavyo Yehova ameumba chembe zinazofanyiza mwili wako?

12 Jambo lingine linaloshangaza ni namna Yehova alivyoumba chembe zinazofanyiza miili ya viumbe vyote vinavyoishi. Kwa mufano, mwili wako umefanyizwa na chembe karibu miliare elfu mia moja (ao 100 000 000 000 000). Katika kila chembe munapatikana kitu fulani kidogo chenye kufanana na kamba kinachoitwa ADN (asidi deoksiribonyukilia). ADN inachunga habari zinazohitajiwa ili kutengeneza kila kiungo cha mwili wako.

13 Ni kiasi gani cha habari kinachopatikana katika ADN? Linganisha uwezo wa kuchunga habari wa gramu moja ya ADN na uwezo wa kuchunga habari wa CD. CD inaweza kuchunga habari zote zinazopatikana katika kamusi, jambo hilo linashangaza sana kwa sababu CD ni chombo kidogo tu cha plastiki. Hata hivyo, gramu moja tu ya ADN inaweza kuchunga habari nyingi kuliko habari zinazoweza kuchungwa kwenye CD miliare elfu moja! Kwa njia nyingine, kijiko kidogo cha ADN yenye kukauka kinaweza kuchunga habari zote zinazohitajiwa ili kutengeneza viungo vya watu wote wanaoishi leo mara 350!

14. Mambo fulani ambayo wanasayansi wamevumbua yanakufanya umuone Yehova namna gani?

14 Mufalme Daudi alionyesha kwamba habari zinazohitajiwa ili kufanyiza mwili wa mwanadamu zimeandikwa katika kitabu cha mufano. Alisema hivi kumuhusu Yehova Mungu: “Macho yako yalikiona kiini-tete changu, na katika kitabu chako sehemu zake zote zilikuwa zimeandikwa, kuhusiana na siku ambazo zilifanyizwa na hakukuwako hata moja kati ya hizo.” (Zab. 139:16) Inaeleweka kwamba Daudi alichochewa kumusifu Yehova alipofikiria namna mwili wake ulivyoumbwa. Mambo ambayo wanasayansi wamevumbua katika miaka ya hivi karibuni yanatufanya tumuheshimu Yehova zaidi tunapofikiria namna ambavyo ametuumba. Mambo hayo yanatutolea sababu nyingi za kukubaliana na mutunga​-zaburi aliyeandika hivi kumuhusu Yehova: “Nitakusifu kwa sababu nimeumbwa kwa njia ya ajabu yenye kuogopesha. Kazi zako ni za ajabu, kama vile nafsi yangu inavyojua vema.” (Zab. 139:14) Je, mambo hayo ya uumbaji hayawezi kuwasaidia watu kuona kwamba kuna Mungu aliye hai?

UWASAIDIE WENGINE WAMUTUKUZE MUNGU ALIYE HAI

15, 16. (a) Namna gani vichapo vyetu vimetusaidia tupendezwe zaidi na nguvu za uumbaji za Yehova? (b) Ni habari gani katika sehemu “Kitu Hiki Kilijifanya Chenyewe?” iliyokushangaza wewe?

15 Kwa miaka mingi, gazeti Amuka! limesaidia mamilioni ya watu wajifunze kumuhusu Mungu kupitia vitu ambavyo ameumba. Kwa mufano, gazeti Amuka! la Mwezi wa 9, 2006 lilikuwa na kichwa “Je, Kuna Muumba?” Kusudi la gazeti hilo lilikuwa kuwasaidia wale ambao wamepofushwa na fundisho la mageuzi na fundisho la uongo kuhusu uumbaji. Kuhusu gazeti hilo la pekee, dada mumoja aliandikia Beteli ya Amerika hivi: “Kampanye ya kutolea watu gazeti hilo la pekee ilikuwa nzuri kabisa. Mwanamuke mumoja aliomba magazeti 20. Yeye ni mwalimu wa biolojia na kwa hiyo alitaka kila mwanafunzi wake awe na gazeti hilo.” Ndugu mumoja aliandika hivi: “Nimekuwa nikihubiri tangu mwishoni mwa miaka ya 1940 na sasa ninakaribia umri wa miaka 75, lakini sijafurahia kazi ya kuhubiri kama ninavyoifurahia mwezi huu wa kutolea watu gazeti hili la pekee.”

16 Katika miaka ya hivi karibuni, magazeti mengi ya Amuka! yamekuwa na habari “Kitu Hiki Kilijifanya Chenyewe?” Habari hizo fupi zinazungumuzia ufundi wa ajabu unaoonekana katika uumbaji na zinaonyesha namna ambavyo wanadamu wamejaribu kuiga Muumbaji Mwenye Ufundi. Katika 2010, tulipokea broshua Uhai​—Ulitokana na Muumba? Broshua hiyo ni chombo kingine tunachoweza kutumia ili kuwasaidia wengine wamutukuze Mungu. Picha nzuri na michoro ya kusaidia kufundisha inayopatikana katika broshua hiyo imekusudiwa kutusaidia tupendezwe sana na nguvu za uumbaji za Yehova. Kusudi la maulizo yanayopatikana mwishoni mwa kila sehemu ni kusaidia musomaji afikiri kuhusu habari ambayo amesoma. Je, umejaribu kutumia broshua hiyo katika mahubiri ya nyumba kwa nyumba, ao wakati haukupanga kufanya hivyo?

17, 18. (a) Wazazi, namna gani munaweza kuwasaidia watoto wenu watetee imani yao bila kuogopa? (b) Namna gani mumetumia broshua zinazohusu uumbaji katika ibada yenu ya familia?

17 Wazazi, je, mumechunguza broshua hii yenye picha nzuri pamoja na vijana wenu katika ibada ya familia? Mukifanya hivyo, mutawasaidia wapendezwe zaidi na Mungu wetu aliye hai. Pengine wewe una vijana wanaosoma masomo ya segondere. Wale wanaofundisha mageuzi wanajikaza kuwasadikisha kwamba hakuna Muumbaji. Fundisho la mageuzi linatetewa na wanasayansi, waalimu na katika vitabu, na hata kwenye sinema. Munaweza kuwasaidia vijana wenu wajue namna ya kupinga mafundisho hayo kwa kutumia broshua nyingine, Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai, iliyotolewa pia katika 2010. Kama vile broshua Uhai​—Ulitokana na Muumba?, broshua hiyo inawatia moyo vijana kuboresha ‘uwezo wao wa kufikiri.’ (Met. 2:10, 11) Na inawaonyesha namna ya kuchunguza ikiwa mambo wanayofundishwa kwenye masomo ni ya kweli.

Wazazi, muwatayarishe watoto wenu ili waweze kuitetea imani yao (Ona fungu la 17)

18 Broshua Chanzo cha Uhai imechapishwa ili kuwasaidia wanafunzi wachunguze habari zenye kusisimua zinazosema kwamba wanasayansi wamevumbua “vitu vinavyohakikisha kwamba fundisho la mageuzi ni la kweli.” Broshua hiyo inawatia moyo vijana wachunguze ikiwa habari hizo zinahakikisha kabisa kwamba mwanadamu alitokana na viumbe vidogo​-vidogo. Pia inawafundisha wanafunzi namna ya kujibu wale wanaosema kwamba wanasayansi wamevumbua katika vyumba vyao vya kufanyia utafiti kwamba uzima ulijitokeza wenyewe. Wazazi, ikiwa mutatumia broshua hizo, mutawasaidia sana watoto wenu wasiwe na woga wanapotetea imani yao katika Muumbaji.​—Soma 1 Petro 3:15.

19. Sisi wote tuna pendeleo gani?

19 Kisha kufanya utafiti muzuri, tengenezo la Yehova linatutolea habari za kutusaidia tujifunze mengi kuhusu sifa nzuri za Yehova zinazoonekana katika ulimwengu unaotuzunguka. Habari hizo za kweli zinatuchochea tumusifu Mungu wetu. (Zab. 19:1, 2) Bila shaka, tuna pendeleo nzuri la kumutolea Yehova, Muumbaji wa vitu vyote, heshima na utukufu ambao anastahili!​—1 Tim. 1:17.

^ Ili upate habari zaidi kuhusu namna unavyoweza kufikiri na wale wanaofundisha uongo juu ya uumbaji, soma ukurasa wa 24 mupaka 28 wa broshua Uhai​—Ulitokana na Muumba?