Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Kweli Mungu Anawahangaikia Wanawake?

Je, Kweli Mungu Anawahangaikia Wanawake?

Je, Kweli Mungu Anawahangaikia Wanawake?

“Zambi ilianzishwa na mwanamuke, na kwa sababu ya mwanamuke sisi wote tunakufa.”​—Maneno hayo yanapatikana katika kitabu cha apokrifa kinachoitwa BUSARA YA SIRA, KILICHOANDIKWA KATIKA MIAKA YA 100 MBELE YA KUZALIWA KWA YESU.

“Ninyi ni mulango wa ibilisi: ni ninyi mulioanza kula tunda la muti uliokatazwa: ni ninyi mulioanza kuvunja sheria ya Mungu . . . Ni ninyi mulioharibu kwa vyepesi mwanaume wa kwanza aliyeumbwa kwa mufano wa Mungu.”—Maneno hayo yaliandikwa na TERTULLIEN, KATIKA KITABU CHAKE (THE APPAREL OF WOMEN), KILICHOANDIKWA KATIKA MIAKA YA 100 KISHA KUZALIWA KWA YESU.

MAANDISHI hayo ya zamani hayatoke katika Biblia. Lakini, kwa miaka mingi yametumiwa ili kutetea wazo la kuwabagua wanawake. Hata leo, watu fulani wanaoshikilia mawazo yao ya kuwabagua wanawake wangali wanataja maandishi ya kidini ili kujitetea; wanasema kama ikiwa wanadamu wanapatwa na matatizo yote haya ni kwa sababu ya wanawake. Je, kweli Mungu ndiye alikusudia wanawake wazarauliwe na kutendewa vibaya na wanaume? Biblia inasema nini juu ya jambo hilo? Acheni tuchunguze.

Je, wanawake walilaaniwa na Mungu?

Jibu ni hapana. Ni “yule nyoka wa zamani, anayeitwa Ibilisi,” ndiye “amelaaniwa” na Mungu. (Ufunuo 12:9; Mwanzo 3:14) Mungu aliposema kama Adamu ‘atamutawala’ bibi yake, hakumaanisha kama sasa wanaume wanapaswa kuanza kuwaonea wanawake. (Mwanzo 3:16) Mungu alikuwa tu ameona mbele ya wakati matokeo mabaya ambayo zambi itawaletea bibi na bwana wa kwanza.

Kwa hiyo, kuwatendea wanawake vibaya ni matokeo ya hali ya zambi ya wanadamu, lakini si mapenzi ya Mungu. Biblia haiunge mukono wazo la kwamba wanawake wanapaswa kuonewa na wanaume ili walipie zambi ya kwanza.​—Waroma 5:12.

Je, Mungu aliwaumba wanawake wakiwa wa hali ya chini kuliko wanaume?

Jibu ni hapana. Andiko la Mwanzo 1:27 linasema hivi: ‘Mungu akamuumba mutu kwa mufano wake, kwa mufano wa Mungu alimuumba; mwanaume na mwanamuke aliwaumba.’ Kwa hiyo, tangu mwanzoni, mwanaume na mwanamuke waliumbwa wakiwa na uwezo wa kuonyesha sifa za Mungu. Hata ikiwa waliumbwa tofauti kimwili na namna kila mumoja wao anavyoona ao kujisikia juu ya jambo fulani, Muumbaji wao aliwapatia wote wawili kazi ileile na walikuwa na haki zilezile mbele yake.​—Mwanzo 1:28-31.

Mbele ya kumuumba Eva, Mungu alisema hivi: ‘Nitamufanyia [Adamu] musaidizi, awe kikamilisho chake.’ (Mwanzo 2:18) Je, neno “kikamilisho” linamaanisha kama mwanamuke alikuwa wa hali ya chini kuliko mwanaume? Hapana, kwa sababu neno hilo la Kiebrania linaweza pia kumaanisha “mwenye kulingana na” ao “musaidizi anayefaa.” Wazia namna muganga mupasuaji na muganga anayemutoboa mutu anesthésie (dawa inayomufanya mugonjwa asisikie maumivu wakati wa upasuaji) wanavyosaidiana. Je, mumoja anaweza kutumika bila mwengine? Haiwezekane hata kidogo! Hata ikiwa ni muganga mupasuaji ndiye anafanya upasuaji, je, hilo linamaanisha kama yeye ndiye wa lazima zaidi? Hapana. Vilevile, Mungu aliumba mwanaume na mwanamuke ili wasaidiane, si kushindana.​—Mwanzo 2:24.

Ni nini kinachoonyesha kama Mungu anawahangaikia wanawake?

Mungu aliona mbele ya wakati namna wanaume wasio wakamilifu wangewatendea wanawake, kwa hiyo alichukua mipango ya kuwalinda wanawake. Mwandikaji Laure Aynard alizungumuzia Sheria ya Musa, ambayo Mungu alitoa katika miaka ya 1500 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu. Katika kitabu chake (La Bible au féminin) alisema hivi: ‘Mara nyingi, agano la Sheria linapozungumuzia mwanamuke, ni juu ya kumutetea.’

Kwa mufano, Sheria iliamuru kuheshimu na kutii baba na mama. (Kutoka 20:12; 21:15, 17) Iliomba pia mwanamuke mwenye mimba alindwe kama inavyofaa. (Kutoka 21:22) Leo pia, Sheria za Mungu zinawalinda wanawake hata kama katika sehemu nyingi za dunia hakuna sheria zinazowalinda. Lakini kuna mambo mengine yanayoonyesha kama Mungu anawahangaikia wanawake.

Sheria Inayoonyesha Mawazo ya Mungu juu ya Wanawake

Sheria ambayo Yehova Mungu aliwapatia Waisraeli iliwasaidia wote, wanaume na wanawake, kuwa vizuri kimwili, kuepuka matatizo ya mwenendo muchafu na wangeweza wote kumukaribia Yehova. Wakati wote ambapo walimusikiliza Yehova na kumutii, taifa lao lilikuwa “juu ya mataifa mengine yote ya dunia.” (Kumbukumbu la Torati 28:1, 2) Namna gani Sheria hiyo iliwasaidia wanawake? Iliwasaidia katika njia zinazofuata.

1. Walikuwa na uhuru. Tofauti na wanawake wa mataifa mengine ya zamani, wanawake Waisraeli walikuwa na uhuru mwingi. Hata ikiwa ni bwana ndiye aliyepewa daraka la kuwa kichwa cha familia, bibi angeweza ‘kufikiria shamba na kulinunua’ na ‘kupanda shamba la mizabibu’ kwa ruhusa ya bwana yake. Mwanamuke aliyekuwa na ufundi wa kusokota na kusuka vitu fulani​-fulani, angeweza hata kufanya biashara yake mwenyewe. (Methali 31:11, 16-19) Wakati wa Sheria ya Musa, wanawake walionwa kuwa watu wazima walio na haki zao za kisheria sawa na wanaume.

Katika Israeli la zamani, wanawake walikuwa pia na uhuru wa kufanya uhusiano wa pekee pamoja na Mungu. Biblia inaonyesha kama Hana alisali kwa Mungu juu ya jambo fulani la kipekee na kwa siri, akafanya naziri kwa Mungu. (1 Samweli 1:11, 24-28) Mwanamuke fulani katika jiji la Shunemu alizoea kumuendea nabii Elisha siku ya Sabato. (2 Wafalme 4:22-25) Mungu aliwafanya wanawake fulani kuwa wajumbe wake, kwa mufano Debora na Hulda. Jambo la kupendeza ni kwamba wanaume wenye kujulikana sana na makuhani walikuwa wanawaendea wanawake hao ili kuwaomba mashauri.​—Waamuzi 4:4-8; 2 Wafalme 22:14-16, 20.

2. Waliruhusiwa kusoma. Kwa sababu wanawake pia waliingizwa katika Agano la Sheria, walialikwa kusikiliza usomaji wa Sheria, na hilo liliwatolea nafasi ya kujifunza. (Kumbukumbu la Torati 31:12; Nehemia 8:2, 8) Wangeweza pia kupata mazoezi ili kushiriki katika sehemu fulani za ibada. Kwa mufano, wanawake fulani walifanya “utumishi uliopangwa” kwenye hema la mikutano, na wengine walichangana na wanaume katika kikundi cha waimbaji.​—Kutoka 38:8; 1 Mambo ya Nyakati 25:5, 6.

Wanawake wengi walikuwa na ujuzi na ufundi uliohitajiwa ili kufanya biashara yenye kuleta faida. (Methali 31:24) Wakati huo, katika desturi za mataifa mengine, ni baba tu ndiye alipaswa kuwafundisha watoto wake wanaume, lakini mama Muisraeli alipaswa pia kuwafundisha watoto wake wanaume mupaka walipokomaa na kuwa watu wazima. (Methali 31:1) Mambo hayo yanaonyesha wazi kama, katika taifa la Israeli la zamani, wanawake walikuwa wenye kusoma.

3. Waliheshimiwa na walionwa kuwa wa lazima. Kati ya zile amri kumi, moja ilisema waziwazi hivi: ‘Muheshimu baba yako na mama yako.’ (Kutoka 20:12) Methali moja ya Mufalme Sulemani mwenye hekima inasema hivi: ‘Mwanangu, sikiliza nizamu ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako.’​—Methali 1:8.

Sheria ilionyesha namna ya kuwaheshimu wanawake; ilikuwa na maagizo madogo-madogo juu ya namna ambavyo watu ambao hawajaoa ao kuolewa walipaswa kujiendesha. (Mambo ya Walawi 18:6, 9; Kumbukumbu la Torati 22:25, 26) Bwana muzuri alipaswa kufikiria bibi yake juu ya hali zinazowafikia wanawake kwa ukawaida na uzaifu wake wa kimwili.​—Mambo ya Walawi 18:19.

4. Walikuwa na haki za kulindwa. Katika Neno lake, Yehova anasema kama yeye ni ‘Baba ya wavulana wasio na baba na muamuzi wa wajane.’ Ni kusema, alikuwa Mulinzi wa wanawake waliofiwa na bwana na watoto waliofiwa na baba. (Zaburi 68:5; Kumbukumbu la Torati 10:17, 18) Kwa mufano, mujane fulani ambaye bwana yake alikuwa mumoja wa wana manabii alikuwa na deni la mutu fulani. Mutu huyo alipomutendea vibaya, Yehova alimusaidia mujane huyo kwa kumuomba nabii Elisha afanye muujiza ili aendelee kuishi na kulinda heshima yake.​—2 Wafalme 4:1-7.

Mbele Waisraeli waingie katika Inchi ya Ahadi, Selofehadi alikufa bila kuwa na mutoto mwanaume. Kwa hiyo, watoto wake wanawake watano walimuomba Musa awapatie sehemu ya udongo katika Inchi ya Ahadi. Yehova aliwapatia hata zaidi ya kile walichoomba. Alimuambia Musa hivi: ‘Uwape miliki ya uriti katikati ya ndugu za baba yao, nawe utaupitisha uriti wa baba yao kwao.’ Kuanzia wakati huo na kuendelea, wanawake katika Israeli wangepata uriti kutoka kwa baba zao na kuachia pia watoto wao uriti huo.​—Hesabu 27:1-8.

Mawazo ya Mungu Juu ya Wanawake Yalieleweka Vibaya

Wakati wa Sheria ya Musa, wanawake walionwa kuwa wa maana na haki zao ziliheshimiwa. Lakini, kuanzia miaka ya 300 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu na kuendelea, desturi za Kigiriki za kusema kama wanawake ni wa hali ya chini kuliko wanaume zilianza kuenea katika dini ya Kiyahudi.​—Soma kisanduku “Ubaguzi wa Wanawake Katika Maandishi ya Zamani.”

Kwa mufano, Hesiod, muandikaji Mugiriki aliyeishi katika miaka ya 700 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, aliwalaumu wanawake kwamba wao ndio chanzo cha matatizo yote yanayowapata watu. Katika kitabu chake (Theogony) alisema kama wanawake ni ‘rangi na kabila hatari inayoishi kati ya wanaume wanaoweza kufa ili kuwaumiza.’ Wazo hilo lilienea sana katika dini ya Kiyahudi mwanzoni mwa miaka ya 100 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu. Talmud (kitabu cha dini ya Kiyahudi) ambayo ilianza kuunganishwa katika miaka ya 100 kisha kuzaliwa kwa Yesu na kuendelea, ilionya wanaume kwa kusema hivi: “Musizungumuze mingi na wanawake, kwa sababu hilo litawaongoza kufanya zambi.”

Katika miaka iliyofuata, wazo hilo la kukosa kutumainia wanawake lilileta matokeo mabaya juu ya namna Wayahudi walivyowatendea. Wakati wa Yesu, wanawake hawakuruhusiwa kuingia katika hekalu, waliingia tu katika Uwanja wa Wanawake. Mambo ya dini yalikuwa tu ya wanaume, na katika Sinagogi, wanawake walitenganishwa na wanaume. Talmud inataja maneno ya mwalimu mumoja wa dini ya Kiyahudi aliyesema hivi: “Yeyote anayemufundisha mutoto wake mwanamuke Torati [Sheria] anamufundisha mambo machafu.” Kwa kuelewa vibaya mawazo ya Mungu, viongozi wa dini ya Kiyahudi waliwachochea wanaume wengi wawazarau wanawake.

Wakati Yesu alikuwa duniani, aliona kama watu wengi walifuata sana desturi za kubagua wanawake. (Mathayo 15:6, 9; 26:7-11) Je, Yesu alifuata pia desturi hizo? Tabia yake na namna yake ya kuwatendea wanawake vinaweza kutufundisha nini? Je, Ukristo wa kweli umewakomboa wanawake? Habari inayofuata itatusaidia kujibu maulizo hayo.

[Sanduku katika ukurasa wa 7]

Ubaguzi wa Wanawake Katika Maandishi ya Zamani

Kuanzia wakati wa mitume na kuendelea, waandikaji kama vile Philo wa Alexandria walianza kutumia filozofia ya Kigiriki ili kufasiria kitabu cha Mwanzo. Kulingana na Philo, zambi ambayo Eva alifanya ni uzinzi, kwa hiyo alihukumiwa na “akapoteza kabisa uhuru wake na hilo lilifanya atawaliwe na mwanaume ambaye alikuwa mwenzake.” Tabia ya kuwazarau wanawake ilijiingiza katika dini ya Kiyahudi na hata katika maandishi ya Mababa wa Kanisa.

Katika kitabu kimoja (Midrash Rabba) cha miaka ya 100, mwalimu fulani wa dini ya Kiyahudi alieleza sababu gani mwanamuke anapaswa kuvaa kitambaa, anasema hivi: “Mwanamuke ni kama mutu ambaye amefanya tendo mbaya na anayesikia watu haya.” Mwanateolojia anayeitwa Tertullien, ambaye maandishi yake yalijulikana sana katika miaka ya 100 kisha kuzaliwa kwa Yesu, alifundisha kama wanawake wanapaswa kutembea huku na huku ‘kama Eva wakiomboleza na kutubu.’ Watu wanajidanganya kwa kuwaza kama mafundisho hayo yanatoka katika Biblia, na yamewachochea wanaume kubagua wanawake.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Eva aliumbwa ili awe musaidizi na kikamilisho cha Adamu

[Picha katika ukurasa wa 6]

Katika Israeli ya zamani wanawake pia walifanya biashara