Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

 MAZUNGUMUZO YA BIBLIA PAMOJA NA JIRANI

Mashahidi wa Yehova Wanaamini Yesu?

Mashahidi wa Yehova Wanaamini Yesu?

Habari inayofuata ni mufano wa mazungumuzo ambayo Shahidi wa Yehova fulani anaweza kuwa nayo pamoja na jirani yake. Kwa mufano, wazia kwamba Shahidi fulani anayeitwa Antoine anamukuta mwanaume anayeitwa Tim nyumbani kwake.

KUMUAMINI YESU NI KWA LAZIMA

Antoine: Jambo Tim. Ninafurahi kukuona tena.

Tim: Mimi pia ninafurahi kukuona.

Antoine: Ninakuletea magazeti ya mupya ya Munara wa Mulinzi na Amuka! Ninawaza utafurahia kabisa habari zilizo katika magazeti hayo.

Tim: Aksanti. Kwa kweli, ninafurahi kuona unafika leo kwa sababu kuna jambo fulani ninataka kukuuliza.

Antoine: Kweli? Ni jambo gani?

Tim: Siku iliyopita, nilikuwa ninazungumuza na mufanyakazi mwenzangu. Nilimuambia juu ya vichapo ulivyonipatia na namna ni vyenye kupendeza sana. Lakini alisema kwamba singepaswa kuvisoma kwa sababu Mashahidi wa Yehova hawamuamini Yesu. Ni kweli? Nilimuambia kwamba nitakuuliza ulizo hilo siku utakuja tena kunitembelea.

Antoine: Sawa, ninafurahi sana kuona unaniuliza. Unafanya vizuri kuuliza Shahidi wa Yehova kuliko kuuliza mutu mwengine. Ukitaka kujua mambo yenye mutu anaamini, ni vizuri kabisa kumuuliza yeye mwenyewe.

Tim: Na mimi niliona vile.

Antoine: Ukweli ni kwamba, Mashahidi wa Yehova wanaamini kabisa Yesu. Kwa kweli, tunajua kwamba kumuamini Yesu ni jambo la lazima ili kupata wokovu.

Tim: Nilikuwa ninafikiri hivyo, lakini wakati mufanyakazi mwenzangu alisema kwamba ninyi Mashahidi wa Yehova hamuamini Yesu, hilo lilinichochea nipende kujua mengi. Ninawaza hatujazungumuzia jambo hilo hata siku moja.

Antoine: Ninaweza kukuonyesha maandiko fulani ya Biblia yanayokazia ulazima wa kumuamini Yesu? Ni maandiko yenye Mashahidi wa Yehova wanazoea kutumia katika mahubiri.

Tim: Sawa.

Antoine: Ni vizuri tuanze na maneno ya Yesu mwenyewe yaliyo katika andiko la Yohana 14:6. Maneno hayo ni sehemu ya mazungumuzo kati ya Yesu na mumoja wa mitume wake. Tunasoma hivi: ‘Yesu akamuambia: Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna anayekuja kwa Baba ila kupitia kwangu.’ Kulingana na andiko hilo, njia moja tu ya kumuendea Baba ni gani?

Tim: Ni kupitia Yesu.

Antoine: Ni vile kabisa. Na Mashahidi wa Yehova wanaamini sana hivyo. Acha nikuulize hivi: Kulingana na yale unajua juu ya mambo Mungu anataka tufanye, wakati mutu anasali, anapaswa kusali katika jina la nani?

Tim: Katika jina la Yesu.

Antoine: Ninakubaliana na wewe. Na ndiyo maana sala zangu zote ninazitoa katika jina la Yesu. Mashahidi wa Yehova wote wanatoa sala zao katika jina la Yesu.

Tim: Ninafurahi kujua hivyo.

Antoine: Andiko lingine tutachunguza ni Yohana 3:16. Andiko hilo ni la maana sana, ndiyo sababu limeitwa Injili ndogo. Wazo ni kwamba ikiwa ungechukua mambo yote yaliyoandikwa juu ya maisha ya Yesu duniani na utumishi wake na kuyafupisha katika andiko moja, andiko hilo lingekuwa Yohana 3:16. Labda utapenda kulisoma.

 Tim: Sawa. Linasema hivi: ‘Kwa maana Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamutoa Mwana wake muzaliwa-pekee, ili kila mutu anayemuamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.’

Antoine: Aksanti kwa usomaji wako. Hii ndiyo mara ya kwanza unasikia andiko hilo?

Tim: Hapana, nimelisikia mara nyingi kwenye kanisa.

Antoine: Ni andiko linalojulikana sana. Kwa kuchunguza andiko hilo kwa uangalifu, utaona mambo Yesu alisema. Alisema kuwa upendo wa Mungu unawawezesha wanadamu kupata uzima wa milele. Lakini, ili kupata uzima huo, jambo moja tu tunalopaswa kufanya ni gani?

Tim: Kuwa na imani.

Antoine: Ndiyo. Zaidi sana, imani katika Yesu Kristo, Mwana muzaliwa-pekee. Na wazo hilo la kwamba kumuamini Yesu kunatufungulia njia ya kupata uzima wa milele, linazungumuziwa hapa kwenye ukurasa wa 2 wa gazeti hili lenye nilikuletea. Juu ya kusudi la Munara wa Mulinzi, wazo hilo linaonyesha kwamba kati ya mambo mengine, gazeti hili “linatia watu moyo wamuamini Yesu Kristo, ambaye alikufa ili tupate uzima wa milele na ambaye sasa ni Mufalme wa Ufalme wa Mungu.”

Tim: Sawa, ninaelewa kabisa. Hata katika gazeti lenu wenyewe kuna ushuhuda kwamba ninyi Mashahidi wa Yehova munaamini Yesu.

Antoine: Ni vile kabisa.

Tim: Sasa, sababu gani watu wanasema kwamba hamuamini Yesu?

Antoine: Inawezekana kuna sababu nyingi zinazofanya watu waseme hivyo. Katika hali fulani, watu wanasema hivyo kwa sababu tu walisikia wengine wanasema hivyo. Ao inawezekana walifundishwa wazo hilo la uongo na mwalimu wao wa dini.

Tim: Ninawaza hivi: Inawezekana watu fulani wanasema hivyo kwa sababu munajiita Mashahidi wa Yehova, wala si Mashahidi wa Yesu.

Antoine: Hiyo pia inaweza kuwa sababu nyingine.

Tim: Sababu gani munazungumuza sana juu ya Yehova?

“NIMEWAJULISHA JINA LAKO”

Antoine: Sababu moja ni kwamba, tunaamini kuwa ni jambo la maana kutumia jina la pekee la Mungu, Yehova, kama vile Mwana wake Yesu alivyofanya. Ona mambo Yesu alisema alipokuwa akisali kwa Baba yake. Sala hiyo inaandikwa katika Yohana 17:26. Tafazali, unaweza kusoma andiko hilo?

Tim: Sawa, linasema hivi: “Nimewajulisha jina lako nami nitalijulisha, ili upendo ulionipenda nao upate kuwa ndani yao nami katika muungano pamoja nao.”

Antoine: Aksanti kwa usomaji wako. Ona kwamba Yesu alisema kuwa alijulisha jina la Mungu. Unafikiri sababu gani alifanya hivyo?

Tim: Hmm. Sijue vizuri.

Kumuamini Yesu ni jambo la lazima ili kupata wokovu

Antoine: Hakuna shida, labda tunaweza kuchunguza andiko lingine linaloweza kutuelewesha jambo hilo. Ninafikiria andiko la Matendo 2:21. Linasema hivi: ‘Kila mutu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.’ Sasa, niko hakika utakubali kwamba ikiwa kuliitia jina la Yehova ni jambo la lazima ili kupata wokovu, Yesu alijua hivyo bila shaka.

Tim: Ni vile kabisa.

Antoine: Kwa hiyo, wokovu wa wafuasi wake ni sababu moja iliyomufanya Yesu aone kuwa ni lazima wajue jina la Mungu na kulitumia. Na ndiyo sababu moja kubwa kati ya sababu zinazotufanya tuzungumuze sana juu ya Yehova. Tunaona kuwa ni jambo la maana kujulisha jina la pekee la Mungu na kusaidia wengine waliitie jina hilo.

Tim: Lakini hata ikiwa watu hawajue jina la Mungu wala kulitumia moja kwa moja, wanapotaja jina Mungu, wanajua kuwa wanazungumuza juu ya Mungu uleule tu.

Antoine: Hilo linaweza kuwa kweli. Hata hivyo, kwa kutuambia jina lake la pekee, Mungu amefanya iwe vyepesi sana kwetu kumukaribia.

Tim: Unamaanisha nini?

 Antoine: Fikiria jambo hili: Haikuwa lazima kwetu kujua jina la pekee la Musa. Tungemujua tu kuwa mutu aliyegawanya Bahari Nyekundu ao mutu aliyepewa Amri Kumi. Ni vilevile juu ya Noa, sababu gani tujue jina lake? Angeitwa tu mutu aliyejenga safina na kuokoa familia yake na wanyama. Na hata Yesu Kristo angejulikana tu kuwa mutu aliyekuja kutoka mbinguni na kufa kwa ajili ya zambi zetu. Sivyo?

Tim: Ninafikiri hivyo.

Antoine: Lakini Mungu alifanya tujue majina ya pekee ya watu hao. Kujua majina yao ya pekee kunafanya tuone habari zao kuwa za kweli kabisa. Hata ikiwa hatukukutana na Musa, Noa, ao Yesu, hata siku moja, kujua tu majina yao kunatufanya tuwaone kuwa watu walioishi kwelikweli.

Tim: Sijafikiria jambo hilo kwa njia hiyo, lakini ninaelewa!

Antoine: Hiyo ni sababu nyingine inayotufanya sisi Mashahidi wa Yehova tutumie sana jina la pekee la Mungu. Tunapenda kuwasaidia watu waamini kuwa Yehova Mungu ni Mutu anayeishi kwelikweli mwenye wanaweza kukaribia. Wakati uleule, tunakazia sana daraka lenye Yesu anatimiza ili kutusaidia tupate wokovu. Labda tunaweza kusoma andiko lingine moja la kutusadia tuelewe jambo hilo.

Tim: Sawa.

Antoine: Kwenye mwanzo wa mazungumuzo yetu, tulisoma andiko la Yohana 14:6. Kumbuka kwamba Yesu alisema kuwa yeye ni “njia na kweli na uzima.” Turudie nyuma kidogo kwenye Yohana 14:1. Tafazali, unaweza kusoma mambo Yesu alisema katika sehemu ya mwisho ya andiko hilo?

Tim: Sawa. Inasema hivi: “Iweni na imani katika Mungu, iweni na imani pia katika mimi.”

Antoine: Aksanti kwa usomaji wako. Kwa hiyo, unaweza kusema kwamba inaomba mutu achague ikiwa atamuamini Yesu ao Mungu?

Tim: Hapana. Yesu alisema kwamba ni lazima tuwaamini wote wawili.

Antoine: Hiyo ni kweli. Na niko hakika utakubali kuwa haitoshe tu kusema kwamba tunamuamini Mungu na Yesu. Kwa kweli, ni lazima tuishi kwa njia inayoonyesha kuwa tunawaamini.

Tim: Ni vile kabisa.

Antoine: Lakini namna gani mutu anaonyesha kuwa anaamini kabisa Mungu na Yesu? Labda tunaweza kuzungumuzia ulizo hilo siku nyingine. *

Tim: Nitafurahi..

Una ulizo fulani juu ya habari za Biblia lenye umekwisha kujiuliza? Unapenda kujua mengi juu ya mambo Mashahidi wa Yehova wanaamini ao juu ya mambo fulani wanayofanya? Ikiwa jibu ni ndiyo, usisite kuuliza ulizo hilo wakati utakutana na Shahidi wa Yehova. Atafurahi kuzungumuzia mambo hayo pamoja na wewe.

^ fu. 60 Ili kupata habari zingine, soma sura ya 12 ya kitabu Biblia Inafundisha Kabisa Nini? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.