Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Namna ya Kufundisha Watoto Wako Adabu

Namna ya Kufundisha Watoto Wako Adabu

“Nilikuwa ninasikiliza kwa uangalifu mulio wa kila motokari iliyopita. Hiyo ilikuwa mara ya tatu Jordan anafika nyumbani nyuma ya saa tuliyomuwekea. Nilijiuliza, ‘Jordan iko wapi? Alipatwa na shida? Hahangaike hata kwamba tunaogopa?’ Wakati alifika, nilikuwa nimejaa hasira karibu kupasuka.”GEORGE.

“Mutoto wangu mwanamuke alilalamika, na jambo hilo liliniogopesha sana. Nilimuona akiwa mwenye kushika kichwa chake na mwenye kulia. Ndugu yake mukubwa mwenye miaka ine alikuwa amemupiga.”—NICOLE.

“Natalie, mutoto wetu mwanamuke mwenye miaka sita alisema hivi: ‘Sikuiba pete. Niliiokota!’ Macho yake yalikuwa yanaonyesha kwamba hakuwa na kosa. Alipoendelea kukataa tuliumia sana, na tulilia. Tulijua kwamba alikuwa anatudanganya.”—STEPHEN.

IKIWA wewe ni muzazi, je, umekwisha kujisikia kama wazazi hao wanaotajwa hapo juu? Wakati unakutana na hali kama hizo, unajiuliza ikiwa utamufundisha mutoto wako adabu ao hata ikiwa utafanya hivyo namna gani? Ni vibaya kuwafundisha watoto wako adabu?

NIZAMU AO KUFUNDISHA ADABU MAANA YAKE NINI?

Katika Biblia, neno “nizamu” ao kufundisha adabu hakumaanishe tu kutoa malipizi. Neno hilo linamaanisha kwanza muongozo, mafundisho, na marekebisho. Halimaanishe hata kidogo kumutendea mutu vibaya ao kwa ukali.—Methali 4:1, 2.

Kufundisha watoto adabu kunaweza kufananishwa na kazi ya kulima bustani. Mulimaji wa bustani anatayarisha udongo, anatia maji na mbolea kwenye mimea, na analinda mimea ili isiharibiwe na wadudu na magugu (majani yasiyofaa). Mimea inapokomaa, mulimaji huyo anaweza kuombwa kupunguza matawi ya mimea hiyo ili iendelee kukomaa na kunyooka katika njia inayofaa. Anajua kwamba kuchanga kwa uangalifu ufundi mbalimbali kutamusaidia apate mimea yenye afya nzuri. Vilevile, wazazi wanahangaikia watoto wao katika njia nyingi. Lakini wakati fulani wanalazimika kuwafundisha adabu, kufanya hivyo ni kama kupunguza majani ya mimea, kunaweza kurekebisha tabia mbaya mbele ya wakati na kusaidia watoto wao wakomae katika njia inayofaa. Lakini, kupunguza majani kunapaswa kufanywa kwa uangalifu, bila kufanya hivyo mumea unaweza kuharibika. Vilevile, wazazi wanapaswa kufundisha watoto adabu kwa njia ya upendo.

Yehova, Mungu anayezungumuziwa katika Biblia, ni mufano muzuri kwa wazazi katika jambo hilo. Namna anawatia adabu waabudu wake watiifu wa duniani inazaa matunda mazuri na ni yenye kupendeza, hilo linawafanya wafikie ‘kupenda nizamu.’ (Methali 12:1) ‘Wanashika nizamu’ na ‘hawaiache.’ (Methali 4:13) Unaweza kumusaidia mutoto wako akubali nizamu ao kufundishwa adabu kwa kuiga vizuri kabisa mambo matatu ya lazima juu ya namna Mungu anatutia adabu: Mungu anatutia adabu kwa namna (1) yenye upendo, (2) yenye kufaa, na (3) isiyobadilika-badilika.

 KUTIA ADABU KWA NAMNA YENYE UPENDO

Namna ya Mungu ya kutia adabu inategemea upendo na inachochewa na upendo. Biblia inasema hivi: ‘Yeye ambaye Yehova anamupenda, anamukaripia, kama vile baba anavyomukaripia mwana anayemufurahia.’ (Methali 3:12) Zaidi ya hayo, Yehova, ni “mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira.” (Kutoka 34:6) Kwa sababu hiyo, Yehova hawatendee watu vibaya wala kwa ukali, wala hatumie maneno makali, ya kuchambua watu kila wakati, ao maneno ya muzaha yenye kuumiza, mambo hayo yote yanaweza kuumiza “kama kwa upanga unaochoma.”—Methali 12:18.

SIKILIZA

Ni kweli, haiwezekane wazazi waige kabisa-kabisa mufano mukamilifu wa Mungu wa kujizuia. Wakati fulani ni vigumu kuendelea kuonyesha uvumilivu, lakini katika hali ngumu sana, ukumbuke kila mara kwamba malipizi yanayotolewa kwa hasira mara nyingi ni yenye kutesa, yenye kupita mipaka, na hayazae matunda mazuri. Tena, malipizi yanayochochewa na hasira ao kukata tamaa haiko kufundisha watoto adabu kabisa. Malipizi ya namna hiyo ni kukosa kujizuia.

Kwa upande mwengine, unapofundisha watoto adabu kwa njia ya upendo na kujizuia, unaweza kuvuna matunda mazuri. Fikiria namna George na Nicole, wazazi wawili kati ya wazazi waliotajwa kwenye mwanzo wa habari hii, walishugulikia mambo.

SALI

“Mwishowe, wakati Jordan alifika, mimi na bibi yangu tulikuwa tumekasirika sana, lakini tulijizuia tulipokuwa tunasikiliza maelezo yake. Kwa sababu ilikuwa usiku sana, tuliamua kuzungumuzia jambo hilo asubuhi. Tulisali sisi wote pamoja na kuenda kulala. Siku iliyofuata, tulikuwa katika hali nzuri ili kuzungumuzia jambo hilo kwa utulivu na kugusa moyo wa kijana wetu. Alitii mambo tulimukataza na alikubali kuwa na daraka juu ya mwenendo wake. Jambo lenye kufurahisha, tulitambua kwamba kutenda haraka wakati watu wanakasirika hakuzae matunda mazuri. Tulipoamua kusikiliza kwanza, mara nyingi mambo yaliendeka vizuri.”—George.

ZUNGUMUZA

“Nilikasirika sana wakati niliona mutoto wangu mwanaume anamuumiza dada yake bila sababu. Kuliko kutenda mara moja, nilimutuma katika chumba chake, singeweza kuchukua uamuzi wenye hekima kwa sababu nilikuwa na hasira nyingi sana. Kisha, wakati nilitulia, nilimuambia kwa ukali kwamba jeuri haikubalike na nilimuonyesha namna alimuumiza dada yake. Njia hiyo ilitumika vizuri. Alimuomba dada yake musamaha na akamukumbatia.”Nicole.

Kwa kweli, kufundisha adabu kwa namna yenye kufaa kunachochewa na upendo sikuzote, hata wakati inaomba kutoa malipizi.

 KUFUNDISHA ADABU KWA NAMNA YENYE KUFAA

Sikuzote, Yehova anatutia adabu “kwa kiwango kinachofaa.” (Yeremia 30:11; 46:28) Anafikiria hali zote, hata zile zisizokuwa wazi. Namna gani wazazi wanaweza kufanya pia hivyo? Stephen, anayetajwa kwenye mwanzo wa habari hii, anaeleza hivi: “Hata ikiwa tulijisikia kuwa wenye kuumizwa sana moyoni na hatukuelewa sababu gani Natalie aliendelea kukataa kwamba hakuiba pete, tulijaribu kufikiria miaka yake na hali yake ya kukosa ukomavu.”

Robert, bwana ya Nicole, yeye pia alijaribu kufikiria hali zote. Wakati watoto wanajiendesha vibaya, anajiuliza mwenyewe tena na tena maulizo haya: ‘Hii ni mara ya kwanza anafanya hivi ao amezoea kuwa na tabia hii mbaya? Mutoto ni mwenye kuchoka ao hajisikie vizuri? Tabia yake ni alama ya tatizo lingine?’

Wazazi wenye hekima wanajua pia kwamba watoto si watu wazima. Mutume Mukristo Paulo alitambua jambo hilo wakati aliandika hivi: ‘Nilipokuwa mutoto, nilikuwa nikisema kama mutoto, nikifikiri kama mutoto.’ (1 Wakorintho 13:11) Robert anasema hivi: “Jambo moja linalonisaidia kuona mambo kwa njia inayofaa na kuepuka kukasirika kupita mipaka ni kukumbuka mambo nilizoea kufanya nilipokuwa mutoto.”

Ni jambo la maana kuwa na usawaziko katika mambo unayotazamia, na wakati huohuo, kutotetea ao kuachilia mwenendo ao tabia mbaya. Ukifikiria uwezo wa mutoto, mipaka yake, na mambo mengine, utamufundisha adabu bila kupita mipaka na kwa namna yenye kufaa.

KUFUNDISHA ADABU KWA NAMNA ISIYOBADILIKA-BADILIKA

Andiko la Malaki 3:6 linasema hivi: “Mimi ni Yehova; sikubadilika.” Watumishi wa Mungu wanaamini kabisa kweli hiyo na wanajisikia salama kwa kujua hivyo. Watoto pia wana lazima ya usalama unaotokana na kufundishwa adabu kwa namna isiyobadilika-badilika. Ikiwa kanuni zako zinabadilika kwa kutegemea namna unajisikia moyoni, mutoto wako atavurugika na kuvunjika moyo.

Kumbuka kwamba Yesu alisema hivi: “Acheni tu neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo, Siyo yenu, Siyo.” Maneno hayo yanaweza kutumiwa pia juu ya kulea watoto. (Mathayo 5:37) Fikiri kwa uangalifu mbele ya kutoa maonyo yenye hauna nia ya kutimiza. Ikiwa unamuonya mutoto wako kwamba akijiendesha vibaya utamupatia malipizi fulani, usikose kumupatia malipizi hayo.

Mazungumuzo mazuri kati ya wazazi ni jambo la maana ili kufundisha watoto adabu kwa namna isiyobadilika-badilika. Robert anaeleza hivi: “Ikiwa watoto wetu wanajaribu kunifanya nikubali jambo fulani ambalo bibi yangu aliwakataza bila mimi kujua, ninapotambua hivyo, ninabadilisha uamuzi wangu ili nimuunge bibi yangu mukono.” Ikiwa wazazi hawakubaliane juu ya namna ya kushugulikia hali fulani, ni vizuri wazungumuzie jambo hilo kati yao wenyewe na kufikia uamuzi moja.

KUFUNDISHA WATOTO ADABU NI JAMBO LA LAZIMA

Ikiwa unaiga namna Yehova anatia adabu kwa njia yenye upendo, yenye kufaa, na isiyobadilika-badilika, unaweza kuwa hakika kwamba bidii yako itawaletea watoto wako faida. Muongozo wako wenye upendo unaweza kusaidia watoto wako kuwa watu wazima, wenye kuchukua madaraka yao kwa uzito, na wenye kuwa na mipaka. Kama Biblia inavyosema: ‘Mulee muvulana [kijana mudogo mwanaume] kulingana na njia inayomufaa; hata atakapozeeka hatageuka kando na kuiacha.’—Methali 22:6.