Hamia kwenye habari

Mashahidi wakishiriki kampeni ya pekee huko Osaka (kushoto) na Tokyo (juu na chini kulia)

JULAI 30, 2024
JAPANI

Mashahidi Kutoka Nchi Saba Washiriki Kampeni ya Pekee ya Kuhubiri Huko Osaka na Tokyo, Japani

Mashahidi Kutoka Nchi Saba Washiriki Kampeni ya Pekee ya Kuhubiri Huko Osaka na Tokyo, Japani

Kuanzia Mei 13 hadi Juni 2, 2024, maelfu ya Mashahidi wa Yehova nchini Japani walishiriki katika kampeni ya pekee ya kuhubiri katika maeneo ya mjini ya Osaka na Tokyo, Japani. Kwa kuongezea, Mashahidi wengine 350 hivi walialikwa kutoka Australia, Kanada, Korea Kusini, Marekani, New Zealand, Ufaransa, na Ujerumani ili kuunga mkono kampeni hiyo.

Jumla ya wakaaji wa Osaka na Tokyo ni zaidi ya milioni 15. Wahubiri wenyeji walishirikiana na ndugu na dada wageni katika aina mbalimbali za mahubiri ya umma. Walifurahia kuwa na mazungumzo mengi mazuri na pia walifaulu kuanzisha mafunzo kadhaa ya Biblia.

Dada kutoka Australia akiwa pamoja na dada kutoka Japani wakati wa kampeni hiyo.

Dada mmoja alipokuwa kwenye kigari cha machapisho alisali ili azungumze na mtu ambaye anapendezwa kujifunza Neno la Mungu. Muda mfupi baadaye, mwanamume mmoja alifika hapo na akasema angependa kujifunza mengi zaidi kuhusu Biblia. Kwa kuwa mwanamume huyo alizungumza hasa Kichina, dada huyo alifanya mpango ndugu wa eneo hilo anayezungumza Kichina amtembelee. Mwanamume huyo alihudhuria mkutano wa kutaniko siku mbili tu baada ya mazungumzo hayo.

Dada mmoja alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba, alizungumza na mwanamke ambaye alikubali kutazama video yenye kichwa Kwa Nini Ujifunze Biblia? Baada ya kuitazama, mwanamke huyo alisema, “Nimekuwa nikijiuliza maswali haya ambayo yametajwa katika video hii!” Alikubali kwa uchangamfu kuanza kujifunza Biblia na akahudhuria mkutano uliofuata pamoja na dada yetu.

Ndugu na dada wa Kutaniko la Honmachi huko Osaka wakiwa pamoja na wageni kwenye karamu ya mapokezi kabla ya kuanza kampeni ya pekee ya kuhubiri (SPC)

Kampeni hiyo pia iliandaa fursa nzuri sana kwa ndugu na dada zetu kufurahia ushirika wa undugu wa ulimwenguni pote. Aika, dada mwenye umri wa miaka 20 kutoka Tatsuno, Japani anasema hivi: “Hili ni tukio lisiloweza kusahaulika. Ninamshukuru sana Yehova kwa kuniwezesha kushiriki kampeni hii.” Mzee mmoja mwenyeji anayeitwa Akihiro aliongezea kusema hivi: “Tulitiwa moyo sana kuhubiri na ndugu na dada zetu kutoka nchi nyingine. Jambo hilo lilifanya huduma yetu iwe na shangwe zaidi.”

Tunashukuru sana kwa wajitoleaji wengi sana wenyeji na kutoka nchi nyingine ‘waliojitoa kwa hiari’ kwa ajili ya kampeni hii ya pekee na ambao ‘walipaza sauti wakimsifu Yehova.’​—Zaburi 110:3; Ezra 3:11.