Hamia kwenye habari

APRILI 24, 2017
JAPANI

Wajitoleaji Mashahidi Warekebisha Nyumba Zaidi ya 300 Baada ya Matetemeko ya Nchi Japani

Wajitoleaji Mashahidi Warekebisha Nyumba Zaidi ya 300 Baada ya Matetemeko ya Nchi Japani

Mashahidi wakirekebisha dari iliyoharibiwa katika nyumba iliyoko Koshi.

EBINA, Japani—Mashahidi wa Yehova nchini Japani walimaliza kazi ya kurekebisha nyumba 348 za waabudu wenzao zilizoharibiwa na matetemeko ya nchi yaliyotokea katika eneo la Kumamoto, Japani, Aprili 14 na 16, 2016. Wajitoleaji 15,000 walishiriki kazi ya ujenzi iliyofanywa kuanzia Julai 2016 hadi Machi 2017.

Ingawa hakuna Mashahidi waliouawa na matetemeko hayo, Mashahidi 119 hivi walikimbia kutoka nyumbani kwao. Mwanzoni, wale waliopoteza makao waliishi kwenye Majumba ya Ufalme 15, ambayo ni maeneo ya ibada ya Mashahidi wa Yehova. Wakati huohuo, wajitoleaji waliondoa vifusi kwenye nyumba za walioathiriwa.

Kikosi cha wajenzi sita wakiweka paa mpya katika nyumba iliyoharibiwa mjini Chimachi.

Kuanzia Julai 25, 2016, Mashahidi waliofanya kazi ya ujenzi walirekebisha nyufa, sakafu, kuta za ndani, paa, na mabomba ya maji katika nyumba zilizoathiriwa na matetemeko hayo. Pia, walibadili milango, madirisha, na viyoyozi.

Watoa msaada wakirekebisha nyumba iliyoharibiwa mjini Mashiki.

Bw. Minoru Kono, ofisa aliyefanya kazi katika Jeshi la Japani, ambaye aliona kazi ya kutoa msaada ya Mashahidi, alisema hivi: “Katika kazi yangu, ni muhimu sana kufanya kazi haraka ili kuokoa uhai. Mashahidi wa Yehova walikuwa na hisi hiyo ya uharaka baada ya tetemeko la Kumamoto, waliharakisha kufika kwenye eneo hilo ili kuwasaidia walioathiriwa. Na Mashahidi walipoanza kazi ya ujenzi, nilishangaa kuona wafanyakazi stadi kutoka kotekote nchini Japani wakisaidia kazi, nilitarajia kuona watu wasio na ustadi wowote. Wajitoleaji Mashahidi wanajitoa kabisa na wanafanya kazi kwa bidii sana.”

Wajitoleaji wa ujenzi wakiondoa vigae vya paa na kuweka vigae vipya huko Kikuchi.

Shahidi akiingiza zege kwenye nyumba iliyoharibiwa, zege hiyo itatumiwa kuimarisha msingi ulioharibiwa wa nyumba iliyoko Uki.

Ichiki Matsunaga, msemaji wa Mashahidi wa Yehova nchini Japani, anasema hivi: “Kwa miezi michache iliyopita, tumekuwa tukifanya kazi ya kurekebisha na kujenga pamoja na maelfu ya wale walioathiriwa na tetemeko la Kumamoto. Msaada ambao waabudu wenzetu wameandaa baada ya msiba huo umetufariji sana na kutupa nguvu.”

Wanahabari Wanaweza Kuwasiliana na:

David A. Semonian, Ofisi ya Habari za Umma, +1-845-524-3000

Japani: Ichiki Matsunaga, +81-46-233-0005