Hamia kwenye habari

Jumba la Ufalme la Mersin

JUNI 3, 2016
Uturuki

Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu Imeamuru Uturuki Itambue Majumba ya Ufalme Kuwa “Majengo ya Ibada”

Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu Imeamuru Uturuki Itambue Majumba ya Ufalme Kuwa “Majengo ya Ibada”

Mei 24, 2016, Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu (ECHR) ilitetea haki ya uhuru wa ibada kwa ajili ya dini zenye washiriki wachache nchini Uturuki. Hukumu hiyo ilisema kwamba serikali ilizingatia kupita kiasi sheria yake ya ugawaji wa ardhi ili kuhakikisha kwamba Majumba ya Ufalme hayatambuliwi rasmi kuwa “majengo ya ibada.”

Mahakama hiyo ya Ulaya iligundua kwamba sheria ya ugawaji wa ardhi ya Uturuki inaruhusu majengo makubwa kuonekana kuwa “majengo ya ibada” lakini haikubali majengo yanayotumiwa na dini zenye washiriki wachache kuonekana hivyo. Kwa hiyo, bila sababu za msingi, Uturuki imezuia jitihada za Mashahidi za kuabudu kwa uhuru na hivyo kukiuka Kifungu cha 9 cha Mkataba wa Ulaya wa Haki za Kibinadamu. a Hukumu hiyo ilisema kwamba mamlaka imetumia sheria ya ugawaji wa ardhi “kufanya iwe vigumu, na hata kuzuia, mahitaji ya [ibada] za dini zenye washiriki wachache nchini humo, mojawapo ikiwa ni Mashahidi wa Yehova.”

Sheria ya Ugawaji wa Ardhi Haitoi Nafasi kwa Dini Zenye Washiriki Wachache

Mashahidi wa Yehova wana shirika la dini lililosajiliwa kisheria nchini Uturuki na wamejaribu kwa miaka mingi kuomba serikali iyatambue rasmi Majumba ya Ufalme kuwa ni “majengo ya ibada” chini ya sheria ya ugawaji wa ardhi. Hata hivyo, wenye mamlaka nchini Uturuki wanaendelea kukataa kuyatambua Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova kuwa “majengo ya ibada.”

Kwa kuwa Mashahidi hawajapata mahali maalumu kwa ajili ya ujenzi, Majumba yao yote 25 ya Ufalme nchini Uturuki hayatambuliwi na serikali na hivyo yanaweza kufungwa na wenye mamlaka kwa sababu ya hayapatani na viwango vya sheria ya ugawaji wa ardhi. Tayari wenye mamlaka wamefunga Majumba ya Ufalme yaliyopo Mersin na Akçay katika vipindi tofauti-tofauti vya wakati tangu Agosti 2003. Katika wilaya ya Karşıyaka iliyopo mkoani İzmir, wenye mamlaka wamekataa kulitambua Jumba la Ufalme kuwa ni jengo la ibada. Majumba ya Ufalme ya Mersin na İzmir ndiyo yaliyozungumziwa kwenye hukumu iliyotolewa Mei 24 na Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu.

Kabla ya mwaka wa 2003, sheria ya ugawaji wa ardhi ya Uturuki iliyokuwa na kusudi la kutenga maeneo ya kujenga majengo ya ibada iliandikwa kihususa kwa ajili ya ujenzi wa misikiti. Wakati huo, wenye mamlaka waliwaruhusu Mashahidi wafanye ibada kwenye nyumba za watu. Hata hivyo, ili kukidhi viwango vya Ulaya vya kutokuwa na ubaguzi na uhuru wa dini, Uturuki ilirekebisha Sheria yake ya Ugawaji wa Ardhi Namba 3194 mwaka wa 2003. Mojawapo ya mabadiliko yaliyofanywa ni kuondoa neno “msikiti” kwenye sheria na kuandika “jengo la ibada” na kuziamuru manispaa zitenge maeneo kwa ajili ya majengo ya ibada.

Marekebisho hayo yalipaswa kuzipa nafasi dini zenye washiriki wachache haki ya kujenga na kumiliki majengo ya ibada. Hata hivyo, sheria hiyo ya ugawaji wa ardhi hairuhusu dini kuwa na eneo dogo na hivyo kuashiria kwamba lazima dini iwe na washiriki wengi. Pia, muundo wa jengo unaotajwa katika sheria hiyo umekusudiwa hasa ibada ya Kiislamu.

Kushikilia Sana Sheria Kunazuia Haki ya Kuwa na “Majengo ya Ibada”

Kwa kuongezea, wenye mamlaka wa manispaa hawakutenga maeneo kwa ajili ya ujenzi wa majengo madogo ya ibada na wamekataa maombi ya Mashahidi ya kubadili matumizi ya viwanja. Mashahidi wanapokata rufani kwa sababu ya kukataliwa kwa maombi yao, mahakama kuu na wenye mamlaka wanashikilia sana sheria ya ugawaji wa ardhi na kukataa kutambua Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova kuwa “majengo ya ibada.”

Wenye mamlaka wa manispaa ya Mersin na ya Akçay, walishikilia kupita kiasi sheria hiyo mpya na wakafunga Majumba yote ya Ufalme ya eneo hilo kwa sababu haiyatambui kama “majengo ya ibada.” Mashahidi walipoomba eneo lingine ili wajenge majengo yao ya ibada, wenye mamlaka waliwaambia kwamba hakukuwa na eneo lolote lililotengwa kwa kusudi hilo.

Hali hiyo ya utata inaenea katika nchi nzima ya Uturuki. Inawazuia Mashahidi wa Yehova na vikundi vingine vya dini vyenye washiriki wachache kupata kibali cha kukubalika kwa majengo wanayotumia kwa ajili ya ibada. Kwa sasa, wenye mamlaka katika maeneo 27 katika nchi nzima ya Uturuki wamekataa maombi 46 yaliyofikishwa kwao ili kuyatambua majengo ya ibada ya Mashahidi wa Yehova. Isitoshe, sheria hiyo inafanya makutaniko yasinufaike na mpango unaotolewa kwa dini zilizo na majengo ya ibada yanayotambuliwa wa kusamehewa kodi, malipo ya umeme, na ya maji.

Mashahidi Wakata Rufani kwa ECHR Ili Kupata Msaada

Kabla ya kukata rufani kwenda Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu, Mashahidi wa Yehova walijaribu kushughulikia kesi hiyo katika mahakama za nchi hiyo. Halmashauri ya Nchi, mahakama kuu ya serikali, haijawahi kukubali ombi lolote la kutambua kisheria Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova kuwa jengo la ibada kwa kutegemea sheria ya ugawaji wa ardhi. Mahakama hiyo imebadili maamuzi kadhaa ya mahakama mbalimbali zilizowaunga mkono Mashahidi.

Hivyo, Mashahidi wa Yehova walituma maombi mawili mwaka wa 2010 na 2012 ili yashughulikiwe na Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu wakiiomba mahakama hiyo ichunguze ikiwa Uturuki imekiuka Mkataba wa Ulaya wa Haki za Kibinadamu. Mahakama hiyo ya Ulaya ilishikamana na mkataba wake na kueleza umuhimu wa kuwa na sheria ya ugawaji wa ardhi inayoruhusu dini zenye washiriki wachache kutengewa maeneo ya kujenga majengo ya ibada.

Mahakama hiyo ilisema kwamba “itakuwa vigumu kwa dini zenye washiriki wachache kama vile Mashahidi wa Yehova kutimiza vigezo vilivyopo katika sheria ya ugawaji wa ardhi ili waweze kupata maeneo ya kufanya ibada yao.” Mahakama hiyo ilimalizia kwa kusema hivi: “Mahakama za nchi hiyo hazikufikiria mahitaji ya dini zenye washiriki wachache. . . . Kwa kuwa wana wafuasi wachache, Mashahidi wa Yehova hawahitaji jengo lenye ramani hususa badala yake wanahitaji chumba cha kawaida tu kwa ajili ya kufanya ibada, kukutana, na kufundisha imani yao.”

Uamuzi huo unathibitisha kwamba Uturuki imevuruga ibada ya Mashahidi wa Yehova kwa kutoyatambua Majumba ya Ufalme kuwa “majengo ya ibada.” Ahmet Yorulmaz, msimamizi wa shirika la Mashahidi wa Yehova nchini Uturuki liitwalo Association for Jehovah’s Witnesses in Turkey, alisema hivi: “Tumefurahia sana uamuzi wa Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu. Tunatumaini kwamba serikali ya Uturuki itatambua Majumba ya Ufalme yaliyopo sasa kuwa ni majengo ya ibada na itaagiza wenye mamlaka wa manispaa watumie sheria ya ugawaji wa ardhi ili wakati ujao tuweze kupata maeneo ya kujenga majengo yetu ya ibada. Uturuki itakuwa imepiga hatua muhimu katika kuunga mkono kikamili uhuru wa ibada, ikiwa itatumia uamuzi huu.”

Je, Uturuki Itaondoa Ubaguzi wa Dini?

Katika miaka kumi iliyopita, maendeleo makubwa yamefanywa nchini Uturuki kuhusiana na suala la kuwatambua kisheria Mashahidi wa Yehova. Mwaka 2007, wenye mamlaka nchini Uturuki walisajili shirika la kisheria la Mashahidi wa Yehova b baada ya kukataa kufanya hivyo kwa zaidi ya miaka 70.

Mashahidi wa Yehova wanashukuru kwamba serikali ya Uturuki imechukua hatua kuhakikisha kwamba raia wake wanapata uhuru wa kuabudu. Wanatumaini kwamba uamuzi wa hivi karibuni wa Mahakama ya Ulaya utaichochea Uturuki itetee uhuru wa ibada, jambo linalokaziwa katika Katiba ya Uturuki na pia sheria ya kimataifa. Mashahidi wanatarajia kuona Uturuki ikiunga mkono uamuzi wa Mahakama ya Ulaya kwa kukubali Majumba yao 25 ya Ufalme yatambulike kuwa “majengo ya ibada” na kuwaruhusu wajenge majengo mengine ya ibada wakati ujao.

a Kifungu cha 9 kinakazia haki ya “uhuru wa mawazo, dhamiri na ibada.”

b Shirika la kisheria linalowategemeza Mashahidi wa Yehova nchini Uturuki lilianzishwa Julai 31, 2007.