Hamia kwenye habari

Mwonekano wa nje wa ofisi mpya ya utafsiri

FEBRUARI 22, 2023
AFRIKA KUSINI

Ofisi ya Tawi ya Afrika Kusini Yafungua Ofisi ya Utafsiri ya Lugha ya Venda

Ofisi ya Tawi ya Afrika Kusini Yafungua Ofisi ya Utafsiri ya Lugha ya Venda

Desemba 7, 2022, ofisi ya utafsiri (RTO) ya lugha ya Venda ilifunguliwa katika Manispaa ya Makhado, Afrika Kusini. Kuna watafsiri kumi wa muda wote na watafsiri nane wanaofanya kazi baadhi ya siku.

Nchini Afrika Kusini kuna watu milioni 1.2 hivi wanaozungumza lugha ya Venda na nchini Zimbabwe kuna 100,000 wanaozungumza lugha hiyo. Kwa sasa, kuna makutaniko 28 ya lugha ya Venda katika nchi hizo mbili na wahubiri 800 hivi.

Eneo lililonunuliwa kwa ajili ya ofisi ya utafsiri lilikuwa na jengo fulani ambalo lilifanyiwa ukarabati likawa nyumba nne kwa ajili ya makazi. Hata hivyo, jengo jipya lilijengwa kwa ajili ya ofisi zitakazotumiwa katika kazi ya utafsiri. Kisha nyumba nyingine tatu zilizo karibu na hapo zilinunuliwa kwa ajili ya makazi zaidi.

Ofisi ya utafsiri ilijengwa kwa njia inayozingatia hali ya hewa ya eneo hilo. Kwa mfano, Ndugu Jody Palvie, wa Idara ya Usanifu-Majengo na Ujenzi ambaye alikuwa msimamizi wa mradi huo alisema hivi: “Kwa kuwa eneo hili lina joto kali na unyevunyevu, hatukukata miti mikubwa iliyokuwepo kwa sababu inatoa kivuli na pia tulitumia sana vigae vya marumaru na sakafu za saruji iliyong’arishwa kwenye majengo ili yawe na ubaridi.”

Kushoto: Programu ya kiroho ikirekodiwa. Kulia: Watafsiri wa lugha ya Venda wakifanya kazi

Katika eneo hilo, kuna watu wengi wanaozungumza lugha ya Venda na hilo litawapa watafsiri fursa nzuri ya kutumia zaidi lugha hiyo. Mtafsiri mmoja anasema hivi: “Sasa tunaweza kuzungumza na wenyeji kila siku. Kufanya hivyo kunaboresha uwezo wetu wa kutafsiri, na kunatusaidia kutumia maneno ya kawaida ambayo wenyeji wanatumia katika maisha yao ya kila siku.” Mtafsiri mwingine alisema: “Sasa tuko karibu na ndugu na dada wengi wanaozungumza lugha ya Venda ambao wanaweza kutumiwa kwa ajili ya kurekodi video na rekodi za kusikiliza.”

Tunajua kwamba Yehova ataendelea kubariki jitihada za ndugu na dada hawa wenye bidii ya “[kutangaza] sifa za Yehova” miongoni mwa watu wanaozungumza lugha ya Venda.​—Zaburi 145:21.