Hamia kwenye habari

SEPTEMBA 13, 2019
AFRIKA KUSINI

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya Yatolewa Katika Lugha Tatu Kwenye Kusanyiko la Kimataifa Nchini Afrika Kusini

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya Yatolewa Katika Lugha Tatu Kwenye Kusanyiko la Kimataifa Nchini Afrika Kusini

Mnamo Septemba 6, 2019, kwenye kusanyiko la kimataifa la Johannesburg, Afrika Kusini, Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilitolewa katika Kivenda, Kiafrikaan, na Kikhosa, lugha zinazozungumzwa na zaidi ya watu milioni 16. Ndugu Anthony Morris, mshiriki wa Baraza Linaloongoza aliwatangazia wahudhuriaji 36,865 kuhusu kutolewa kwa Biblia hizo katika uwanja wa michezo wa FNB. Wasikilizaji wengine 51,229 waliunganishwa katika maeneo mengine manane kutia ndani nchini Lesotho, Namibia, na Saint Helena.

Mtafsiri mmoja alisema hivi kwa msisimko alipokuwa akizungumzia mambo ya pekee yanayopatikana katika Biblia hizo: “Sisi sote tutaanza kusoma Biblia zetu upya katika lugha inayogusa mioyo yetu!” Mtafsiri mwingine alisema hivi: “Jambo muhimu zaidi ni kwamba [Biblia mpya iliyotolewa] itatusaidia kumkaribia Yehova zaidi kwa sababu inatumia jina la Mungu mara nyingi.”

Vilevile, Biblia hizo zitawasaidia sana akina ndugu katika huduma. Mshiriki mmoja wa kikundi cha watafsiri wa Kixhosa alisema hivi: “Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyorekebishwa itatusaidia katika huduma. Watu watasikia waziwazi kile ambacho Biblia inafundisha bila kuhitaji kuelezewa maana ya kila neno.” Mtafsiri wa Kiafrikaan aliongezea hivi: “Sasa unaweza kusoma tu maandiko na Biblia inajieleza yenyewe.”

Tunashangilia kwamba ndugu zetu wamepata Biblia ambazo ni rahisi kusoma zitakazowasaidia kumkaribia zaidi Mungu wetu.—Yakobo 4:8.